2010–2019
Mtazamo wa Milele wa Injili
Aprili 2015


Mtazamo wa Milele wa Injili

Kwa maamuzi ambayo yanaathiri umilele, kuwa na mtazamo wa injili ni muhimu.

Katika ufunuo uliotolewa kwa Musa, tunaambiwa malengo yaliyotolewa na Baba yetu wa Mbinguni: “Kwani tazama, hii ndiyo kazi yangu na utukufu wangu – kuleta kutokufa na uzima wa milele wa mwanadamu.”1 Kulingana na kauli hiyo, hamu ya Baba wa Mbinguni ni kumpa kila mtu nafasi ya kupata furaha kamilifu. Mafunuo ya Siku za mwisho yanaonyesha kwamba Baba yetu wa Mbinguni aliweka mpango mzuri kwa watoto Wake wote, mpango maalum ili tuweze kurudi kuishi Naye.

Kuulewa mpango huu wa furaha kunatupa sisi mtazamo wa milele na kutusaidia kuthamini kwa dhati amri, ibada, maagano, na majaribu na dhiki.

Kanuni moja muhimu inatoka kwa Alma: “Kwani hivyo Mungu aliwapa amri, baada ya kuwafahamisha mpango wa ukombozi.”2

Inafurahisha kuona mfuatano katika mchakato wa mafundisho. Baba yetu wa Mbinguni kwanza aliwafundisha Adamu na Hawa mpango wa ukombozi, na kisha Akawapa amri.

Huu ni ukweli muhimu. Kuulewa mpango kutawasaidia watu kutii amri, kufanya maamuzi mazuri, na kuwa na hamasa sahihi.

Kwa kipindi nilichotumikia katika Kanisa, nimeona kujitolea na wema wa waumini wa Kanisa katika nchi mbalimbali, ambazo nyingine zina matatizo ya kisiasa, kijamii, au kiuchumi. Kipengele kimoja cha kawaida ambacho nimekiona mara nyingi kwa hawa waumini wema ni mtazamo wao wa umilele. Mtazamo wa milele wa injili unatuongoza kujua sehemu ambayo tunayoshikilia katika mpango wa Mungu, kukubali ugumu na maendeleo kupitia kwao, kufanya maamuzi, na kulenga maisha yetu katika uwezo wetu wa kiuungu.

Mtazamo ni njia tunayoona mambo pale tunapoyaona kwa umbali fulani, na kutuwezesha kuthamini thamani yake halisi.

Ni kama kuwa katika msitu na kuwa na mti mbele yetu. Pengine turudi nyuma kidogo, hatutaweza kutathimini jinsi msitu ulivyo. Niliwahi kutembelea Jangwa la Amazon huko Leticia, Colombia, karibu na mipaka ya Brazil na Peru. Sikuweza kutathimini ukubwa wake hadi pale nilipopita juu yake na kupata mtazamo mzuri.

Watoto wetu walipokuwa wadogo, walikuwa wanaangalia televisheni chaneli ya watoto ambayo ilikuwa na kipindi kilichoitwa What Do You See? Skrini ilikuwa ikionyesha kwa karibu kitu fulani, na watoto walitakiwa wabahatishe kilikuwa kitu gani huku picha ikipanuka pole pole. Mara picha yote ilipoonekana, ungeweza kutaja kwa urahisi alikuwa paka, mmea, tunda, nk.

Ninakumbuka kwamba wakati fulani walikuwa wanaangalia kipindi hicho na kilionyesha kitu kwa karibu ambacho kilionekana vibaya kwao, hata kutia kinyaa, lakini fokasi ilipotanuka, waligundua kwamba ilikuwa pizza ya kutamanisha. Kisha wakaniambia, “Baba, tunaomba utununulie kama ile!” Baada ya kuelewa kilikuwa nini, kitu ambacho kwanza hakikuwafurahisha kikaishia kuwa kitu kilichowavutia sana.

Ngoja nielezee tukio lingine. Nyumbani kwetu watoto wetu walipenda mchezo fumbo wa kupanga vipande upate picha kamili. Huenda sisi wote tulipata nafasi ya kuchezea fumbo. Mafumbo mengine yanatengenezwa kwa vipande vidogo vidogo. Nakumbuka kwamba mmoja wa watoto wetu (sitatoa jina lake ili asitambulike) alikuwa analenga kwenye kipande kimoja kimoja, na kimoja kilipokuwa hakikai sehemu aliyotarajia kingekaa, alikuwa anashikwa na hasira na kufikiri kilikuwa hakifai na kutaka kukitupa. Mwishowe akajua jinsi ya kuunganisha fumbo pale alipoelewa kwamba kila kipande kilikuwa na sehemu yake katika picha ya mwisho, hata pale ambapo hakujua wapi kinakaa kwa wakati fulani.

Hii ni njia mojawapo ya kukamilisha mpango wa Bwana. Hatuna sababu ya kujihangaisha na kila kipande peke yake bali kujaribu kuileta picha nzima kwenye fokasi, tukifikiria jinsi ya matokeo ya mwisho yatakavyokuwa. Bwana anajua ni wapi kila kipande kinakwenda ili kutosheleza mchoro. Amri zote zina umuhimu wa milele katika muktadha wa mpango mkuu wa furaha.

Ni muhimu sana kutofanya uamuzi wa milele toka kwenye mtazamo wa kidunia. Kwani uamuzi ambao utaathiri umilele, kuwa na mtazamo wa injili ni muhimu.

Mzee Neal A. Maxwell alifundisha: “Japokuwa tumekita nanga katika tumaini kuu na la hatima, baadhi ya matumaini yetu ya mbinu ni tofauti. Tunaweza kutumaini kuongezewa mshahara, miadi maalumu, ushindi wa uchaguzi, au kuwa na nyumba kubwa---vitu ambavyo vinawezekana au haviwezekani. Imani katika mpango wa Baba unatupa sisi uvumilivu dhidi ya kuvunjika kwa matumaini ya karibu kama hayo. Tumaini linatufanya sisi ‘tujihusishe kwa bidii’ kwenye mambo mazuri hata kama inaonekana hayafikiwi (ona M&M 58:27).”3

Bila kuwa na mtazamo wa milele, au kuupoteza, kunaweza kutuongoza kuwa na mtazamo wa kidunia kama ilivyo kwa kiwango binafsi na kufanya maamuzi yasiyowiana na mapenzi ya Mungu.

Kitabu cha Mormoni kinataja tabia ambazo Nefi alikuwa nazo na tabia za Lamani na Lamueli. Wote waliteseka mateso mengi na matatizo magumu, hata hivyo, tabia zao dhidi ya matatizo zilikuwa tofauti. Nefi alisema, “Na baraka kuu za Bwana zilikuwa nasi, kwamba wakati tulipokula nyama mbichi huko nyikani, wake zetu walipata maziwa ya kutosha ya kunyonyesha watoto wao, na walikuwa na nguvu, ndio, hata kwamba wanaume, na wakaanza kusafiri bila kunung’unika.”4

Lamani na Lamueli, kwa upande mwingine, walilalamika sana. “Na hivyo ndivyo Lamani na Lemueli, wakiwa wakubwa, walivyonung’unika dhidi ya baba yao. Na walinung’unika kwa sababu hawakujua matendo ya yule Mungu aliyewaumba.”5 Bila kujua au bila kujali, “matendo ya … Mungu” ni njia mojawapo ya kukosa mtazamo wa milele, na kunung’unika ni moja ya dalili. Hata hivyo Lamani na Lemueli walishuhudia miujiza mingi wakiwa pamoja na Nefi, walilalamika, wakisema: “Na tumezunguka nyikani kwa hii miaka mingi; na wanawake wetu wamefanya kazi ya kuchosha, wakiwa wajawazito, na wamezaa watoto nyikani na kuteseka kwa vitu vyote, ila kifo tu; na ingekuwa vyema wafe kabla ya kutoka Yerusalemu badala ya kuteseka na haya masumbuko.”6

Hizo ndiyo ilikuwa mitazamo miwili tofauti kabisa, japokuwa shida na masumbuko waliyokabiliana nayo yalikuwa yale yale. Pamoja na hivyo mitazamo yao ilikuwa tofauti.

Rais Spencer W. Kimball aliandika yafuatayo: “Kama tukiyaangalia maisha haya kuwa ndio maisha pekee, hivyo maumivu, huzuni, na maisha mafupi yangekuwa majanga. Lakini tukiyaangalia maisha kama kitu cha milele yakianzia mbali tangu maisha kabla kuzaliwa na kuendelea milele baada ya kifo wakati ujao, basi matukio yote yatawekwa kwenye mtazamo sahihi.”7

Mzee David B. Haight aliongelea juu ya mchongaji sanamu Michelangelo kuelezea umuhimu wa kuona kila kitu katika mtazamo halisi: “Wakati mchongaji alipokuwa akichonga kipande cha marumaru, mvulana alikuja kila siku kumwangalia kimyakimya. Wakati sanamu ya David ilipoonekana toka kwenye lile jiwe, ikiwa imekamilika ili dunia ishangae, mvulana akamwuliza Michelangelo, ‘Ulijuaje kuwa alikuwa humo ndani?’”8

Mtazamo ambao mchongaji aliuona ni kwamba jiwe la marumaru ulikuwa tofauti kuliko na ule wa yule mvulana aliyekuwa akimwangalia pindi akifanyakazi. Ono la mwanasanaa la uwezekano uliomo ndani ya jiwe unamruhusu kutengeneza kazi ya sanaa.

Bwana anajua kile Anachotaka kukikamilisha kwa kila mmoja wetu. Anajua aina ya marekebisho Anayotaka kuyafanikisha katika maisha yetu, na hatuna haki ya kumshauri Yeye. Mawazo Yake yapo juu kuliko mawazo yetu.9

Ninashuhudia kwamba tunaye Baba wa Mbinguni mwenye upendo, mwenye haki, na mwenye huruma ambaye ameandaa mpango kwa ajili ya uzima wetu wa milele. Ninashuhudia kwamba Yesu Kristo ni Mwanawe na Mwokozi wa ulimwengu. Ninajua kwamba Rais Thomas S. Monson ni nabii wa Mungu. Ninasema mambo haya katika jina la Yesu Kristo, amina.