2010–2019
Ndio,Tunaweza na Tutashinda!
Aprili 2015


Ndio,Tunaweza na Tutashinda!

Ni sharti tushikilie zaidi kabisa ushuhuda wetu wa injili ya Yesu Kristo. Kisha tutaweza kushinda vita vya kila siku dhidi ya uovu.

Ndugu wapenzi nimenyenyekezwa na heshima niliyopata ya kuzungumza nanyi, mnaoshikilia ukuhani wa Mungu popote katika Kanisa leo

Rais Thomas S. Monson wakati mmoja alisema:

“Wakati mwingine, ulimwengu unaweza kuwa sehemu ya kutisha ambayo tunaweza kuishi. Viwango vya uadilifu wa jamii vinaonekana kupunguka kwa haraka vya kutisha. Hakuna---awe kijana au mzee au mtu wa makamo anayeweza kukwepa kuwa wazi kwa vitu hivyo ambavyo vinaweza kutudhuru na kutuharibu.

“… Lakini hatuhitaji kukata tama … tunapigana vita dhidi ya dhambi … Ni vita tunavyoweza na tutashinda. Baba yetu wa Mbinguni ametupa vifaa tunavyohitaji ili kufanya hivyo.”1

Sisi sote, vijana na wazee, tunakabiliwa kila siku na vita vilivyotajwa na Rais Monson. Adui na malaika wake wanajaribu kutuvuta. Kusudi lao ni kutushawishi tuchepuke kutoka kwa maagano ambayo tumeyafanya na Bwana, na kutusababishia kusahau kuhusu urithi wetu wa milele. Wao wanajua vizuri mpango wa Baba yetu wa Mbinguni kwa ajili ya watoto Wake, kwani walikuwa pamoja nasi katika lile Baraza kuu Mbinguni wakati yote yaliwasilishwa. Wanajaribu kutumia udhaifu na kasoro zetu, kutudanganya kwa “ukungu wa giza…, ambao unapofusha macho, na kufanya migumu mioyo ya wanadamu, na kuwaongoza mbali kwenye barabara pana, ili waangamie na wawe wamepotea.”2

Licha ya upinzani tunaokabiliana nao, kama Rais Monson alivyofundisha, hivi ni vita ambavyo tunaweza, na tutashinda. Bwana anaamini uwezo wetu na ushupavu wetu wa kufanya hivyo.

Maandiko yana mifano mingi ya wale ambao wameshinda vita vyao, hata wakati wa hali ya uhasama mwingi. Moja wapo ya mifani hii ni Kapteni Moroni katika Kitabu cha Mormoni. Kijana huyu wa ajabu alikuwa na ujasiri wa kulinda ukweli katika wakati ambao kulikuwa na mifarakano, na vita, ambavyo vilihatarisha kuharibu taifa zima la Wanefi. Ingawa alikuwa mwenye akili sana katika kutekeleza wajibu wake, Moroni alibaki mnyenyekevu. Hii na zile sifa zingine zilimfanya chombo cha ajabu mikononi mwa Mungu kwa wakati ule. Nabii Alma alitangaza kwamba kama watu wote wangekuwa kama Moroni, “Nguvu zenyewe za jahanamu zingekuwa zimetikiswa milele; [na] ibilisi asingeweza kamwe kuwa na nguvu juu ya mioyo ya wanadamu.”3 Sifa zote za Moroni zilianzia kutokana na imani yake kubwa katika Mungu na Bwana Yesu Kristo4 na uamuzi imara wa kufuata sauti ya Mungu na manabii Wake.5

Kitaswira, sisi sote tunahitaji kujibadilisha leo tuwe aina ya Kapteni Moroni wa kisasa ili tuweze kushinda vita dhidi ya ushawishi wa uovu katika maisha yetu. Ninamjua Shemasi kijana mwaminifu sana aliyejibadilisha kuwa Kapteni Moroni wa kisasa. Kadri amejaribu kufuata ushauri wa wazazi wake na viongozi wa Kanisa imani yake na azma yake vimejaribiwa kila siku, hata kwenye umri wake mdogo. Yeye aliniambia siku moja alishangazwa na hali ngumu na isiyoridhisha---rafiki zake walikuwa wakitumia simu zao za rununu kuangalia picha za ngono. Katika wakati uleule, kijana huyu ilibidi aamue nini kilikuwa muhimu---umaarufu wake au wema wao. Ndani ya sekunde chache zilizofuata, alijawa na ujasiri na aliwaambia marafiki zake kwamba kile walichokuwa wanakifanya hakikuwa sahihi. Hata hivyo, aliwaambia kwamba hawana budi kuacha kile walichokuwa wanafanya au watatawaliwa nacho. Karibu wanafunzi wenzake wote walidhihaki ushauri wake, wakisema kwamba ilikuwa sehemu ya maisha na kwamba hapakuwa na ubaya wowote ndani yake. Hata hivyo palikuwa na mmoja miongoni mwao aliyesikilia ushauri wa kijana yule na akaamua kuacha kile alichokuwa anafanya.

Mfano wa Shemasi huyu ulikuwa na ushawishi chanya kwa angalau mmoja wa wanafunzi wenza. Bila shaka, yeye na rafiki yake walifanyiwa mzaha na kushutumiwa kwa sababu ya uamuzi ule. Kwa upande mwingine, walikuwa wamefuata onyo dogo la Alma kwa watu wake wakati aliposema, “tokeni nyie nje ya uovu, na muwe mliojitenga, na msiguse vitu vyao visivyo safi.”6

Kijitabu Kwa Nguvu za Vijana kina ushauri kutoka kwa Urais wa Kwanza kwa vijana wa Kanisa: “Unawajibika kwa maamuzi unayofanya. Mungu anakujua wewe na atakusaidia ufanye maamuzi mazuri, hata kama familia yako na marafiki wanatumia haki yao ya kujiamulia katika njia ambazo sio sahihi. Kuweni na ujasiri wa kusimama imara katika kutii mapenzi ya Mungu, hata kama unasimama peke yako. Unapofanya hivi, unaweka mfano kwa wengine kufuata.”7

Vita ya mema dhidi ya uovu vitaendelea katika maisha yetu yote, kwa kuwa nia ya adui ni kuwafanya watu wote wawe na huzuni kama yeye. Shetani na malaika zake watajaribu kutuchanganya mawazo yetu na kudai madaraka ya kuongoza kwa kutushawishi tutende dhambi. Kama wanaweza, watapotosha yote yaliyo mema. Hata hivyo, ni muhimu kuelewa kwamba watakuwa tu na nguvu juu yetu kama tutaruhusu.

Maandiko pia yana mifano kadha ya hao ambao walitoa ruhusa hiyo kwa adui na matokeo yake wakachanganyikiwa na hata kuangamia kama Nehori, Korihori, na Sheremu. Tunahitaji kufahamu hatari hii. Hatuwezi kuruhusu sisi wenyewe tuchanganyikiwe na ujumbe unaopendwa ambao ni rahisi sana kukubalika na ulimwengu na ambao unapingana na mafundisho na kanuni za kweli za injili ya Yesu Kristo. Ujumbe mwingi wa ulimwengu hauwakilishi chochote zaidi ya jaribu la kuhalalisha jamii yetu kutenda dhambi.Tunahitaji kukumbuka hilo, mwishowe, wote watasimama mbele ya Kristo kuhukumiwa kwa vitendo vyao, kama ni vizuri au ni viovu.8 Wakati tunapokabiliwa na ujumbe huu wa ulimwengu, ujasiri mkubwa na elimu thabiti ya mpango wa Baba yetu wa Mbinguni utahitajika ili kuchagua kilicho sahihi.

Sisi wote tunaweza kupokea nguvu ya kuchagua kilicho sahihi kama tutamtafuta Bwana na kuweka tumaini na imani yetu Kwake. Lakini, kama maandiko yanavyofundisha, tunahitaji kuwa na “moyo mnyoofu” na “nia thabiti.” Kisha Bwana, katika huruma yake ya milele, “atadhihirisha ukweli kwetu kwa nguvu za Roho Mtakatifu. Na kwa nguvu za Roho Mtakatifu utaweza kujua ukweli wa vitu vyote.”9

Elimu hii tuliyopata kupitia Roho Mtakatifu sio kitu zaidi ya ushuhuda wetu, ambao unaongeza imani yetu na uamuzi wa kufuata mafundisho ya injili ya urejesho katika siku hizi za mwisho, bila kujali ujumbe unaopendwa tunaosikia kutoka ulimwenguni. Ushuhuda wetu sharti uwe ngao yetu ya kutulinda dhidi ya mishale ya moto ya adui katika majaribu yake kutushambulia.10 Utatuongoza salama kupita kwenye giza na machafuko ambayo yapo katika ulimwengu leo.11

Nilijifunza kanuni hii wakati nilipohudumia kama mmisionari kijana. Mwenza wangu nami tulikuwa tunahudumia katika tawi dogo sana la kanisa la mbali sana.Tulijaribu kuzugumza na kila mtu katika jiji. Walitupokea vizuri sana, lakini walipenda kujadiliana kuhusu maandiko na wakatuomba ushahidi usiokanushika kuhusu ukweli wa kile tulichokuwa tunafundisha.

Ninakumbuka kwamba kila wakati mwenza wangu nami tulipojaribu kuthibitisha kitu fulani kwa watu, Roho wa Mungu alituacha na tulijisikia tumepotea kabisa na kuchanganyikiwa. Tulihisi kulazimika kwa nguvu zaidi kuoanisha ushuhuda wetu na kweli za injili tulizokuwa tunafundisha. Kutoka wakati huo, nakumbuka kwamba tulipotoa ushuhuda kwa moyo wetu wote, nguvu ya kimya ya kuthibitisha, zikija kutoka kwa Roho Mtakatifu, zikajaza chumba na hapakuwa na njia kwao kuchanganyikiwa, au kukaidi kile tulichokuwa tunafundisha.Nilijifunza kwamba hakuna nguvu za uovu zilizopo ambazo zina uwezo wa kuchanganya, kudanganya,au kuchepusha nguvu za ushuhuda wa kweli wa mwanafunzi wa kweli waYesu Kristo.

Wakati Mwokozi Mwenyewe alipofundisha, adui alitamani kutupepeta kama ngano, asababishe sisi kupoteza uwezo wetu wa kushawishi ulimwengu moja kwa moja.12

Ndugu wapendwa, kwa sababu ya mawimbi ya kiwewe na wasiwasi kuenea ulimwenguni kote leo, ni sharti tushikilie kwa uthabiti ushuhuda wetu wa injili ya Yesu Kristo. Ndipo uwezo wetu wa kulinda ukweli na haki utaongezeka kwa nguvu. Tunashinda vita vya kila siku dhidi ya uovu, na kuliko kushindwa na changamoto za maisha, tutawashawishi wengine kuishi kufuatana na viwango vya Bwana.

Ninawaalikeni nyote mtafute usalama katika mafundisho yanayopatikana katika maandiko. Kapteni Moroni alioanisha imani yake katika Mungu na ushuhuda wake wa ukweli kwenye elimu na busara vinavyopatikana katika maandiko. Kwa njia hii, aliamini kwamba atapokea baraka za Mungu na angepata ushindi mara nyingi, kitu ambacho ndicho, kwa hakika, kilitokea.

Ninawaalikeni nyote mtafute usalama katika maneno ya busara ya manabii wetu wa sasa. Rais Thomas S. Monson alisema: “Sisi tuliotawazwa kwenye ukuhani wa Mungu tunaweza kuleta mabandiliko. Wakati tunapodumisha usafi wetu binafsi na kuheshimu ukuhani wetu, tunakuwa mifano ya haki kwa wengine kufuata … [nasi] kusaidia kuuangaza ulimwengu unaozidi kuwa giza.”13

Ninawaalika nyote kuamini katika ustahili na nguvu za Upatanisho wa Yesu Kristo. Kupitia dhabihu Yake ya upatanisho, tunaweza kupata ujasiri wa kushinda vita vyote vya wakati wetu, hata wakati wa matatizo yetu, changamoto, na majaribu. Na tutumaini katika upendo Wake na uwezo wa kutuokoa. Kristo Mwenyewe alisema:

“Mimi ni njia,ukweli, na uzima:hakuna mtu ajae kwa Baba, bali kwa kupitia kwangu.”14

“Mimi ni nuru ya ulimwengu: yule ambae ananifuata mimi hatatembea gizani, bali atapata nuru ya uzima.”15

“Mambo haya nimesema kwenu, ili ndani yangu muweze kupata amani. Katika ulimwengu mtapata taabu: bali muwe na furaha kuu; Nimeushinda ulimwengu.”16

Ninatoa ushuhuda wa ukweli wa mambo haya katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.