Maandiko Matakatifu
Mosia 14


Mlango wa 14

Isaya huzungumza kuhusu Masiya—Manyanyaso na mateso ya Masiya yanafafanuliwa—Anatoa nafsi Yake kama malipo ya dhambi na kutetea wanaovunja sheria—Linganisha Isaya 53. Karibia mwaka 148 K.K.

1 Ndiyo, si hata Isaya anasema: Ni nani ambaye ameamini ujumbe wetu, na ni kwa nani mkono wa Bwana umefunuliwa?

2 Kwani atakua mbele yake kama mmea mwororo, na kama mzizi kutoka nchi kavu; hana umbo nzuri wala urembo; na tutakapomuona hana urembo wa kutuvutia.

3 Amechukiwa na kukataliwa na watu; mtu wa huzuni, na aliyezoea huzuni; na tukaficha nyuso zetu kutoka kwake; alichukiwa, na hatukumheshimu.

4 Kwa hakika amechukua ghamu zetu, na kubeba huzuni zetu; na tulimdhania kuwa amepigwa, na Mungu, na kuteswa.

5 Lakini alijeruhiwa kwa makosa yetu, alichubuliwa kwa maovu yetu; adhabu ya amani yetu ilikuwa juu yake; na kwa mapigo yake tunaponywa.

6 Sisi sote, kama kondoo, tumepotea; kila mmoja wetu amegeukia njia yake; na Bwana amemwekea maovu yetu sisi sote.

7 Alidhulumiwa, na aliteswa, lakini hakufungua kinywa chake; yeye analetwa kama mwanakondoo machinjoni, na kama vile kondoo ni bubu mbele ya wanaokata manyoya yake hakufungua kinywa chake.

8 Alichukuliwa kutoka gerezani na kutoka kwenye hukumu; na ni nani atatangaza uzazi wake? Kwani aliondolewa kutoka nchi ya wanaoishi; kwa makosa ya watu wangu alipigwa.

9 Na kaburi lake lilikuwa pamoja na waovu, na matajiri kifoni mwake; kwa sababu hakuwa ametenda uovu wowote, wala hapakuwa na uwongo wowote kinywani mwake.

10 Lakini Bwana alipendezwa kumchubua; amemhuzunisha; utakapotoa nafsi yake kuwa dhabihu ya dhambi ataona uzao wake, ataongeza siku zake, na mapenzi ya Bwana yatafanikiwa mkononi mwake.

11 Ataona taabu ya nafsi yake, na kuridhika; kwa maarifa yake mtumishi wangu mwenye haki atawafanya wengi kuwa wenye haki; kwani atayachukua maovu yao.

12 Kwa hivyo nitamgawia sehemu pamoja na wakuu, na atagawanya nyara pamoja na mashujaa; kwa sababu ametoa nafsi yake hata kufa; na akahesabiwa na wenye dhambi; na alibeba dhambi za wengi, na kuwatetea wenye dhambi.