2010–2019
Wabebe Mizigo Yao kwa Urahisi
Aprili 2014


Wabebe Mizigo Yao kwa Urahisi

Mizigo ya kipekee katika maisha yetu inatusaidia sisi kutegemea wema, rehema, na neema za Masiya Mtakatifu.

Nina rafiki mpendwa ambaye, katika miaka yake ya mwanzo ya ndoa yake, alijithibitishia yeye na familia yake kuwa walihitaji gari kubwa inayoendesha kwa magurudumu manne aina ya pikapu. Mkewe alikuwa na hakika kwamba hakuhitaji ila tu alitaka gari jipya. Mazungumzo ya kiutani kati ya mume huyu na mke yalianzisha wao kufikiria faida na hasara ya ununuzi huu.

“Mpenzi, tunahitaji gari inayoendesha kwa magurudumu manne”

Mke aliuliza,”Kwa nini unafikiri tunahitaji gari jipya?”

Mume alijibu swali lake na kile aliamini ni jibu kamili. “Vipi kama tungehitaji maziwa kwa ajili ya watoto katika dhoruba kali, na njia pekee ningeweza kufika kwenye duka la vyakula ni kwa pikapu?”

Mkewe alijibu kwa tabasamu, “Kama tutanunua gari jipya, hatutakuwa na pesa ya maziwa–sasa kwa nini tuwe na wasiwasi kuhusu kufika kwenye duka katika dharura!”

Kwa muda waliendelea kushauriana pamoja na mwishowe waliamua kupata gari. Muda mfupi baada ya kupata gari jipya, rafiki yangu alitaka kuonyesha jinsi gani gari lilikuwa muhimu na kuthibitisha sababu zake za kutaka kulinunua. Kwa hiyo aliamua angekata na kubeba mzigo wa kuni kwa ajili ya nyumbani kwao. Ilikuwa wakati wa mwaka wa majira ya kupukutika kwa majani, na theluji imekwisha anguka katika milima ambako alitaka kutafuta kuni. Alipokuwa anaendesha akipanda sehemu ya mlima, theluji polepole ikawa inaongezeka kina. Rafiki yangu aligundua hali ya utelezi ya barabara ilileta hatari, lakini kwa ujasiri mkubwa katika gari jipya, aliendelea.

Cha kusikitisha, rafiki yangu alikwenda mbali zaidi kwenye barabara yenye theluji. Alipokuwa akiendesha gari nje ya barabara kwenye sehemu alipokusudia kukata miti, alikwama. Magurudumu yote manne kwenye gari jipya yalizunguka katika theluji.Tayari aligundua kwamba hakujua afanye nini ili ajinasue kutoka hali hii ya hatari. Aliona aibu na kuwa na wasiwasi.

Rafiki yangu aliamua, “Sasa, sitaweza kukaa tu hapa.”Aliteremka kutoka kwenye gari na kuanza kukata miti. Aliijaza kabisa sehemu ya nyuma ya gari na mzigo mzito. Na kisha rafiki yangu akidhamiria angejaribu kuendesha kutoka kwenye theluji mara moja zaidi. Alipoingiza gia kwenye pikapu na kutia moto, alianza kwenda mbele. Polepole gari lilitoka nje ya theluji na kurudi kwenye barabara. Hatimaye alikuwa huru kurudi nyumbani, akiwa na furaha na mtu aliye mnyenyekevu.

Mizigo Yetu Binafsi

Ninaomba msaada wa Roho Mtakatifu ninaposisitiza masomo muhimu ambayo yanaweza kufundishwa kutoka hadithi hii kuhusu rafiki yangu, gari, na miti. Ilikuwa ni mzigo. Ilikuwa ni mzigo wa miti ambao ulitoa mburuzo muhimu kwake yeye kutoka kwenye theluji na kurudi tena barabarani, na kuendelea mbele. Ilikuwa ni barabara iliyomwezesha kurudi kwenye familia yake na nyumbani kwake.

Kila moja wetu pia hubeba mzigo. Mzigo wetu binafsi ndani yake mna mahitaji na fursa, wajibu na faida kubwa, mateso na baraka, na hiari, na vikwazo. Maswali mawili ya mwongozo yanaweza kuwa ya msaada kila baada ya kipindi fulani na kimaombi kukadiria mzigo wetu: “Je mzigo ninaoubeba unatoa mburuzo wa kiroho ambao utaniwezesha kwenda mbele pamoja na imani katika Kristo kwenye njia nyembamba iliyosonga na kukwepa kukwama? Je, mzigo ninaoubeba unaleta mburuzo wa kutosha kiroho ili hatimaye niweze kurudi nyumbani kwa Baba wa Mbinguni?”

Wakati mwingine kimakosa tunaweza kuamini kwamba furaha ni kutokuwa na mzigo. Lakini kubeba mzigo ni muhimu na sehemu maalumu ya mpango wa furaha. Kwa sababu mizigo yetu binafsi inahitaji kuzalisha mburuzo wa Kiroho, tunahitaji kuwa waangalifu tusije tukabeba kila mahali katika maisha yetu vitu vingi vizuri lakini visivyo muhimu kwamba tunachanganyikiwa na kuchepushwa kutoka vitu ambavyo kwa kweli ni vya muhimu sana.

Nguvu ya Kuimarisha ya Upatanisho.

Mwokozi alisema:

“Njooni kwangu, nyie nyote msumbukao na wenye kulemewa na mizigo, nami nitawapumzisha”

“Jitieni nira yangu, mjifunze kwangu kwa kuwa mimi ni mpole na mnyenyekevu wa moyo; nanyi mtapata raha nafsini mwenu.”

“Kwa maana nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi” (Mathayo 11:28–30).

Nira ni boriti ya mbao, kwa kawaida hutumika kati ya maksai wawili au wanyama wengine ambayo inawawezesha kwa pamoja kuvuta mzigo. Nira inawaweka wanyama bega kwa bega ili waweze kutembea pamoja ili kukamilisha kazi.

Fikiria mwaliko wa kibinafsi wa kipekee wa Bwana “Jitieni nira yangu.” Kufanya na kuweka maagano matakatifu yanatutia nira kwa, na, pamoja na Bwana Yesu Kristo. Kimsingi, Mwokozi anatuashiri tumtegemee kuvuta pamoja Naye, hata kama juhudi zetu haziko sawa na haziwezi kulinganishwa na Zake. Na tunapomwamini na kuvuta mzigo wetu pamoja Naye wakati wa safari ya maisha ya duniani kwa kweli nira yake ni laini, na mzigo Wake ni mwepesi.

Hatupo, na kamwe hatuhitaji kuwa peke yetu. Tunaweza kwenda kwa haraka katika maisha yetu ya kila siku kwa msaada wa mbinguni. Kupitia kwa Upatanisho wa Mwokozi tunaweza kupokea uwezo na “nguvu kushinda zetu wenyewe” (“Lord I would Follow Thee, Hymns, no. 220). Kama Bwana alivyotangaza,“Kwa hiyo, endeleeni na safari yenu na mioyo yenu ifurahi; kwani tazameni, na lo, Mimi nipo pamoja nanyi hadi mwisho” (M&M 100:12).

Fikiria mfano katika Kitabu cha Mormoni wakati Amuloni alipokuwa akimtesa Alma na watu wake. Sauti ya Bwana ilikuja kwa wafuasi hawa katika mateso yao: “lnueni vichwa vyenu na msherehekee, kwani ninajua agano ambalo mlinifanyia; na nitaagana na watu wangu na kuwakomboa kutoka utumwani” (Mosia 24:13).

Kumbuka umuhimu wa maagano ya ahadi ya ukombozi. Maagano yanayopokelewa na kuheshimiwa kwa uadilifu na ibada kufanywa na mamlaka sahihi ya ukuhani ni muhimu kwa kupokea baraka zote zilizofanywa zipatikane kupitia kwa Upatanisho wa Yesu Kristo. Kwani katika ibada za ukuhani, nguvu za kiungu zinaonyeshwa kwa wanaume na wanawake katika mwili, ikijumuishwa baraka za Upatanisho (ona M&M 84:20–21).

Kumbuka kauli ya Mwokozi “Kwani nira yangu ni laini, na mzigo wangu ni mwepesi(Mathayo 11:30) tunapofikiria aya ifuatayo katika maelezo ya Alma na watu wake.

“Na pia nitawapunguzia mizigo ambayo imewekwa mabegani mwenu, hata kwamba hamtaisikia kamwe migongoni mwenu” (Mosia 24:14).

Wengi wetu tunadhani maandiko haya yanapendekeza kwamba mzigo ghafla na kwa kudumu utaondolewa mbali. Mstari unaofuata, hata hivyo, unaelezea jinsi mzigo ulivyolainishwa.

“Na sasa ikawa kwamba mizigo ambayo ilikuwa wamewekewa Alma na ndugu zake ilipunguzwa; ndio, Bwana aliwapatia nguvu kwamba wabebe mizigo yao kwa urahisi, na walinyenyekea kwa furaha na subira kwa mapenzi ya Bwana” (Mosia 24:15; mkazo umeongezwa).

Changamoto na matatizo hayakuondolewa mara moja kutoka kwa watu. Lakini Alma na watu wake walitiwa nguvu, na ongezeko la uwezo wao ulifanya mizigo kuwa miepesi. Watu hawa wema waliwezeshwa kupitia Upatanisho kutenda kama mawakala (ona M&M 58:26–29) na matokeo ya hali zao. Na “katika nguvu za Bwana” (Maneno ya Mormoni 1:14; Mosia 9:17; 10:10; Alma 20:4), Alma na watu wake walielekezwa kwenye usalama katika nchi ya Zarahemla.

Sio tu Upatanisho wa Yesu Kristo unaoshinda matokeo ya Anguko la Adamu na kufanya uwezekano wa msamaha wa dhambi na makosa yetu binafsi, bali upatanisho Wake pia unatuwezesha kufanya mema na kuwa wema zaidi katika njia ambazo zimenyooka mbele zaidi ya uwezo wetu wa maisha ya duniani.Wengi kati yetu tunajua kwamba tunapofanya mambo vibaya na tunahitaji msaada kushinda matokeo ya dhambi katika maisha yetu, Mwokozi amefanya iwezekane kwetu sisi kuwa wasafi kupitia nguvu Zake za ukombozi’ Lakini sisi pia tunaelewa kwamba Upatanisho ni kwa wanaume na wanawake waaminifu ambao ni watiifu, wanaostahili, na wenye dhamira na wanaojitahidi kuwa wema zaidi kuhudumu kwa uaminifu zaidi? Nashangaa kama tunashindwa kukiri kikamilifu kipengele hiki cha uimarishwaji katika maisha yetu na kimakosa kuamini ni lazima tubebe mzigo wetu peke yetu—kipitia ujasiri tu, utashi, na nidhamu, na pamoja na uwezo wetu mdogo uliodhahiri.

Ni kitu kimoja kujua kwamba Yesu Kristo alikuja duniani kufa kwa ajili yetu. Lakini tunatakiwa pia kushukuru kwamba Bwana anatamani, kupitia kwa Upatanisho Wake na kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, kutuchangamsha —sio tu kutuongoza bali pia kutuimarisha na kutuponya.

Mwokozi Husaidia Watu Wake

Alma anaelezea kwa nini na jinsi gani Mwokozi anaweza kutuwezesha.

“Na atakwenda, na kuteseka maumivu na masumbuko na majaribio ya kila aina; na hii kwamba neno litimizwe ambalo linasema atabeba maumivu na magonjwa ya watu wake.

Na atajichukulia kifo, ili afungue kamba za kifo ambazo zinafunga watu wake; na atajichukulia unyonge wao, ili moyo wake ujae rehema, kulingana na mwili, ili ajue kulingana na mwili jinsi ya kuwasaidia watu wake kulingana na unyonge wao” (Alma 7:11–12).

Ndivyo, Mwokozi ameteseka sio tu kwa dhambi zetu na maovu yetu---lakini pia kwa maumivu yetu ya kimwili na machungu, udhaifu na mapungufu yetu, hofu zetu na kukatishwa tamaa, masikitiko yetu, na kuvunjwa moyo, majuto yetu na toba, kufa kwetu moyo na kukata tamaa, udhalimu na uovu unaotupata, mihemko ya kuhuzunisha inayotuzonga.

Hakuna maumivu ya kimwili, hakuna kidonda cha kiroho, hakuna maumivu makali ya nafsi au ya moyo, hakuna unyonge au udhaifu wewe au mimi unaotupata katika maisha ya duniani ambao Mwokozi hakuwa na uzoefu nao kwanza. Katika wakati wa hudhaifu tunaweza kutoa sauti, “Hakuna anayejua vile ilivyo. Hakuna anayeelewa.”Lakini Mwana wa Mungu anajua vizuri na kuelewa, kwani alihisi na kubeba mizigo yetu binafsi. Na kwa sababu ya dhabihu yake isiyo na mwisho na ya milele (ona Alma 34:14), Yeye ana uwezo kamili wa kuhisi maono ya mwingine, na anaweza kutunyooshea mkono wake wa huruma. Anaweza kunyoosha, kugusa, kusaidia, kuponya, na kutuimarisha tuwe zaidi ya tunavyoweza kuwa na kutusaidia kufanya yale ambayo tusingeweza kufanya tukitegemea tu uwezo wetu. Hakika, nira Yake ni laini na mzigo Wake ni mwepesi.

Mwaliko, Ahadi, na Ushuhuda

Ninakualika ujifunze, usali, utafakari, na ujitahidi kujifunza zaidi kuhusu Upatanisho wa Mwokozi unapopima mzigo wako binafsi. Mambo mengi kuhusu Upatanisho hatuwezi kuyaelewa kirahisi kwa akili zetu za binadamu. Lakini vipengele vingi vya Upatanisho tunaweza na tunahitaji kuvielewa.

Kwa rafiki yangu, mzigo wa miti ulileta mburuzo wa kuokoa maisha. Gari tupu halikuweza kutembea kupita kwenye theluji, ingawa lilikuwa limetayarishwa na magurudumu manne yanayoendesha. Mzigo mzito ulikuwa muhimu kuleta mburuzo.

Ilikuwa ni mzigo. Ilikuwa ni mzigo ambao ulitoa mburuzo ambao ulimwezesha rafiki yangu kujikwamua, na kurudi barabarani, kuendelea mbele na kurudi kwa familia yake.

Mizigo ya kipekee katika maisha ya kila mmoja wetu inatusaidia kutumaini juu ya wema, rehema, na neema ya Masiya Mtakatifu (ona 2 Nefi 2:8). Ninashuhudia na kuahidi kuwa Mwokozi atatusaidia kubeba mizigo yetu kwa urahisi (ona Mosia 24:15).. Tunapofungwa nira pamoja naye kupitia maagano matakatifu na kupokea nguvu inayowezesha ya Upatanisho Wake katika maisha yetu, tutaongeza kutafuta kuelewa na kuishi kilingana na mapenzi Yake. Na pia sisi tutasali kwa ajili ya nguvu za kujifunza kutoka kwazo, kubadilika, au kukubali hali zetu kuliko kusali bila kusita kwa hali zetu zibadilishwe kulingana na mapenzi yetu. Tutakuwa mawakala wa kutenda wala si vitu vya kutendewa (ona 2 Nefi 2:14). Tutabarikiwa na mburuzo wa Kiroho.

Na kila mmoja wetu tufanye na kuwa wema zaidi kupitia Upatanisho wa Mwokozi. Leo ni Aprili 6. Sisi tunajua kwa ufunuo kwamba leo ndiyo tarehe halisi na sahihi ya kuzaliwa kwa Mwokozi. Aprili 6 pia ndiyo siku ambayo Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho lilianzishwa. (Ona D&C 20:1; Harold B. Lee, “Strengthen the Stakes of Zion,” Ensign, July 1973, 2; Spencer W. Kimball, “Remarks and Dedication of the Fayette, New York, Buildings,” Ensign, May 1980, 54; Discourses of President Gordon B. Hinckley, Volume 1: 1995–1999 [2005], 409.) Katika siku hii maalum ya Sabato takatifu, ninatangaza ushuhuda wangu kwamba Yesu Kristo ni Mkombozi wetu. Yeye yu hai na anatusafisha, anaponya, anatuongoza, anatulinda, na anatuimarisha. Kwa mambo haya nashuhudia kwa furaha katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.