2010–2019
Ufufuo wa Yesu Kristo
Aprili 2014


Ufufuo wa Yesu Kristo

Yesu wa Nazareti ndiye Mkombozi aliyefufuka, na mimi nashuhudia yale yote yanayofuatia kutokana tendo la Ufufuo Wake.

Hali chungu ya kushindwa na kukata tamaa iliwakumba wanafunzi Wake wakati Yesu alipoteseka na kufa juu ya msalaba na mwili wake kuwekwa bila uhai kaburini. Licha ya kile Mwokozi alisema kila mara juu ya kifo Chake na baadaye kufufuka tena, bado hawakuelewa. Alasiri ya giza ya Kusulubiwa Kwake, hata hivyo, ilifuatiwa mara tu na asubuhi yenye furaha ya Ufufuo Wake. Lakini furaha hiyo ilikuja tu wakati wanafunzi walipokuwa mashahidi wa Ufufuo, hata tamko la malaika kwamba alikuwa Amefufuka mara ya kwanza halikueleweka – ilikuwa ni kitu cha kipekee kabisa.

Mariamu Magdalene na wanawake wengine wachache waaminifu walikuja mapema kaburini mwa Mwokozi Jumapili hiyo asubuhi, wakileta yale manukato na marhamu ili kukamilisha upako wakati mwili wa Bwana ulipowekwa kwa haraka katika kaburi kabla ya kukaribia Sabato. Katika asubuhi hii ya asubuhi zote, walikaribishwa na kaburi wazi, jiwe la kufunika likiwa limeviringishwa mbali, na malaika wawili ambao walitangaza:

“Kwa nini mnamtafuta aliye hai miongoni mwa wafu?

“Hayupo hapa, bali amefufuka. Kumbukeni alivyosema nanyi wakati alipokuwa bado Galilaya

“Akisema, Imempasa Mwana wa Adamu kutiwa mikononi mwa wenye dhambi, na kusulibiwa, na kufufuka siku ya tatu.”1

“Njoni, mpatazame mahali Bwana alipolazwa.

“Nanyi nendeni upesi, mkawaambie wanafunzi wake, Amefufuka kutoka wafu.”2

Kama alivyoambiwa na malaika, Mariamu Magdalene alichungulia kaburini, lakini inaonekana yote yaliobakia akilini mwake ni kwamba mwili wa Bwana ulikuwa umeondolewa. Kwa haraka alienda kuripoti kwa Mitume, na kuwapata Petro na Yohana akawaambia, “Wamemwondoa Bwana kaburini, wala hatujui walikomweka.”3 Petro na Yohana walikimbilia mahali pale na kuthibitisha kuwa ni kweli kaburi lilikuwa tupu, wakiona “vitambaa vya sanda vimelala …na ile leso iliyokuwako kichwani pake, ... imezongwa-zongwa mbali mahali pa peke yake.”4 Yohana inaonekana ndiye wa kwanza kuelewa ujumbe wa ajabu wa ufufuo. Anaandika kwamba “aliona na kuamini,” ilihali wengine kwa uhakika, “hawakufahamu bado andiko, ya kwamba [Yesu] lazima afufuke.”5

Petro na Yohana waliondoka, lakini Mariamu alibakia nyuma bado katika maombolezo. Wakati huo huo malaika walikuwa wamerudi na kumwambia kwa upole, “Mama, unalilia nini? Akawaambia, Kwa sababu wamemwondoa Bwana wangu, wala mimi sijui walikomweka.”6 Wakati huo huo Yesu aliyefufuka sasa akiwa amesimama nyuma yake akasema, “Mama, unalilia nini? Unamtafuta nani? Naye, huku akidhania ya kuwa ni mtunza bustani, akamwambia, Bwana, ikiwa umemchukua wewe, uniambie ulipomweka, nami nitamwondoa.”7

Mzee James E. Talmage aliandika: “Alikuwa ni Yesu ambaye alizungumza naye, Bwana wake mpendwa, ingawa yeye hakujua. Neno moja kutoka kwa midomo yake iliyo hai ilibadilisha huzuni wake mchungu kuwa furaha kuu. ‘Yesu akamwambia, Mariamu.’ Sauti, toni, tamko lafudhi aliyokuwa amesikia na kupenda katika siku za awali lilimtia moyo kutoka kwenye kina cha kukata tamaa ambako alikuwa amezama. Aligeuka, na kumwona Bwana. Katika hali ya furaha alinyoosha mikono yake ili kumkumbatia, akitamka tu neno la uzuri na la heshima, ‘Raboni,’ yaani Mwalimu wangu.”8

Na hivyo, mwanamke huyu aliyebarikiwa alikuwa binadamu wa kwanza kuona na kuzungumza na Kristo aliyefufuka. Baadaye siku hiyo hiyo Yeye alimtokea Petro katika au karibu na Yerusalemu;9 kwa wanafunzi wawili katika barabara ya Emau;10 na wakati wa jioni kwa 10 ya Mitume na wengine, kujitokeza ghafla kati yao, akisema, “Tazameni mikono yangu na miguu yangu, ya kuwa ni mimi mwenyewe. Nishikenishikeni, mwone; kwa kuwa roho haina mwili na mifupa kama mnavyoniona mimi kuwa nayo.”11 Kisha kuwashawishi zaidi “walipokuwa hawajaamini kwa furaha, huku wakistaajabu,”12 Alikula samaki wa kuokwa na asali mbele yao.13 Baadaye Aliwafundisha, “Nanyi mtakuwa mashahidi wangu katika Yerusalemu, na katika Uyahudi wote, na Samaria, na hata mwisho wa nchi.”14

Zaidi ya shahidi hizi zilizothibitishwa katika Yerusalemu, tuna huduma isiyo na kifani ya Bwana aliyefufuka kwa wakazi wa kale wa ulimwengu wa Magharibi. Katika nchi ya Bountiful, Alishuka kutoka mbinguni na kualika umati uliokusanyika, wengine 2,500, kuja mbele moja moja mpaka wote walipoenda, wakisukuma mikono yao kwenye upande Wake na kuhisi alama za misumari katika mikono Yake na katika miguu Yake. .15

“Na wakati walipokuwa wameenda wote na wameshuhudia wenyewe, walipaza sauti kwa pamoja, wakisema:

“Hosana! libarikiwe jina la Mungu Aliye Juu Sana! Na waliinama chini miguuni mwa Yesu, na kumwabudu.”16

Ufufuo wa Kristo unaonyesha kwamba uwepo Wake ni huru na wa milele. “Maana kama vile Baba alivyo na uzima nafsini mwake, vivyo hivyo alimpa na Mwana kuwa na uzima nafsini mwake.”17 Yesu alisema:

“Kwa hiyo Baba anipenda, kwa sababu nautoa uhai wangu ili niutwae tena.

“Hakuna mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, na ninao uwezo wa kuutwaa tena.”18

Mwokozi hategemei chakula au maji au oksijeni au kitu kingine chochote, nguvu, au mtu kwa ajili ya maisha. Wote kama Bwana na Masiya, Yeye ndiye Mkubwa, Mungu binafsi aliye hai.19 Yeye ndiye tu na Atakayekuwa.

Kupitia kwa Upatanisho na Ufufuo Wake, Yesu Kristo ameshinda masuala yote ya Anguko. Kifo cha kimwili kitakuwa cha muda, na hata kifo cha kiroho kina mwisho, katika hayo wote wanarudi katika uwepo wa Mungu, angalau kwa muda, ili kuhukumiwa. Tunaweza kuwa na imani halisi na matumaini katika uwezo Wake ili kushinda yote, na kutupa uzima wa milele.

“Maana kwa kuwa mauti ililetwa na mtu, kadhalika na ufufuo wa wafu uliletwa na mtu.

“Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.”20

Kwa maneno ya Mzee Neal A. Maxwell: “Ushindi wa Kristo juu ya kifo ulimaliza matatizo ya binadamu. Sasa kuna matatizo binafsi tu, na kutoka kwa hayo pia tunaweza kuokolewa kwa kufuata mafundisho ya yule aliyetuokoa kutokana na kufa.”21

Baada ya kutosheleza madai ya haki, Kristo sasa anaingia katika nafasi ya haki; au tunaweza kusema, Yeye ni haki, kama vile Yeye ni Upendo.22 Kadhalika, kando na kuwa Mungu mkamilifu, Yeye ni Mungu kamili na mwenye huruma.23 Hivyo Mwokozi hufanya mambo yote kuwa sawa. Hakuna dhuluma katika maisha haya ambayo inadumu, hata kifo, kwa kuwa Yeye anarejesha uhai tena. Hakuna, jeraha, ulemavu, usaliti, au matumizi mabaya yanayopita bila malipo mwishowe kwa sababu ya haki Yake ya mwisho na huruma.

Kwa ishara hiyo hiyo, sisi sote tunawajibika Kwake kwa maisha yetu, chaguo zetu, na matendo yetu, hata mawazo yetu. Kwa sababu Yeye alitukomboa kutoka kwenye Anguko, maisha yetu haswa ni Yake. Alitangaza:

“Tazama, nimewapatia injili yangu, na hii ndiyo injili ambayo nimewapatia---kwamba nilikuja kwenye ulimwengu kufanya mapenzi ya Baba, kwa sababu alinituma.

“Na baba yangu alinituma ili nipate kuinuliwa juu kwenye msalaba; na baada ya kuinuliwa juu kwenye msalaba, kwamba ningeleta watu wote kwangu, kwamba kama nilivyoinuliwa juu na watu, hata hivyo watu wainuliwe juu na Baba, kusimama mbele yangu, na kuhukumiwa kwa vitendo vyao.”24

Fikiria kwa muda mfupi umuhimu wa Ufufuo katika kutatua mara moja na mwisho utambulisho wa kweli wa Yesu wa Nazareti na mashindano makubwa ya falsafa na maswali ya maisha. Kama Yesu alifufuka kwa kweli, yafuatia kwamba yeye ni kiumbe cha milele. Hakuna kiumbe yeyote aliye na uwezo ndani yake kuweza kufufuka tena baada ya kufa. Kwa sababu alifufuka, Yesu hawezi kuwa tu seremala, mwalimu, rabi, au nabii. Kwa sababu alifufuka, Yesu ilibidi awe Mungu, hata Mwana wa Pekee wa Baba.

Kwa hiyo, kile alichofundisha ni kweli; Mungu hawezi kusema uwongo.25

Kwa hiyo, Yeye alikuwa Muumbaji wa dunia, kama Alivyosema.26

Kwa hiyo, mbinguni na kuzimu ni vya kweli, kama Yeye Alivyofundisha.27

Kwa hiyo, kuna ulimwengu wa roho ambao Alitembelea baada ya kifo Chake.28

Kwa hiyo, Atakuja tena jinsi malaika walivyosema,29 na kutawala binafsi juu ya nchi.”30

Kwa hiyo, kuna ufufuo na hukumu ya mwisho kwa wote.31

Kutokana na hali halisi ya Ufufuo wa Kristo, shaka juu ya kuweza yote, kujua yote, na ukarimu wa Mungu Baba---ambaye alitoa Mwanawe wa pekee kwa ajili ya ukombozi wa ulimwengu hazina msingi. Shaka juu ya maana na madhumuni ya maisha hazina msingi. Yesu Kristo kwa kweli ndiye jina tu au njia ambayo wokovu unaweza kuja kwa wanadamu. Neema ya Kristo, ni halisi, inayostahili, msamaha na utakaso kwa mwenye dhambi aliyetubu. Imani kweli ni zaidi ya mawazo au uvumbuzi kisaikolojia. Kuna ukweli wa milele na wa ulimwengu wote, na kuna malengo na viwango vya maadili visivyobadilika kama ilivyofundishwa Naye.

Iwapo uhalisi wa Ufufuo wa Kristo, toba ya ukiukaji wowote wa sheria na amri Zake inawezekana na nisuala la dharura. Miujiza ya Mwokozi ilikuwa ya kweli, kama ilivyo ahadi Yake kwa wanafunzi Wake kwamba waweze kufanya hivyo, na hata matendo makuu zaidi.32 Ukuhani Wake hakika ni nguvu halisi ambayo “huihudumia injili na hushikilia ufunguo wa siri za Ufalme, hata ufunguo wa ufahamu wa Mungu. Kwa hiyo, katika ibada hizo, nguvu za uumungu hujidhihirisha.”33 Kutokana na hali halisi ya ufufuo wa Kristo, kifo sio mwisho wetu, na ingawa minyoo ya ngozi huharibu miili yetu, lakini katika miili [yetu] [sisi] tutamwona Mungu.”34

Rais Thomas S. Monson anaelezea kuhusu Robert Blatchford, ambaye miaka 100 iliyopita “katika kitabu chake God and My Neighbor, alishambulia kwa nguvu imani za Kikristo zilizokubaliwa, kama vile Mungu, Kristo, sala, na uzima wa milele. Alisema kwa ujasiri, ‘Ninadai kuthibitisha kila kitu nilichoweka kuthibitisha kikamilifu na kwa uhakika kwamba hakuna Mkristo, hata awe mkubwa au mwenye uwezo kiasi gani, anaweza kujibu hoja yangu au kutikisa kesi yangu.’ Alijizingira mwenyewe na ukuta wa nadharia ya kushuku. Kisha jambo la kushangaza likatokea. Ukuta wake ghafla ukavunjika ukawa mavumbi. … Polepole alianza kuhisi njia yake kurudi kwa imani aliobeza na kudharau. Ni nini kilichosababisha mabadiliko haya makubwa katika mtazamo wake? Mke wake [alikuwa] amefariki. Kwa moyo uliovunjika, aliingia chumbani ulipowekwa mwili wake. Alitazama tena uso alioupenda sana. Kutoka nje, alimwambia rafiki: ‘Ni yeye, na hali si yeye. Kila kitu kimebadilika. Kitu ambacho kilikuwa hapo kabla kimeondolewa. Yeye si sawa. Ni nini kinaweza kuwa kimeondoka ikiwa si nafsi?’”35

Je, kwa kweli Bwana alikufa na kufufuka tena? Ndiyo. “Kanuni za msingi za dini yetu ni ushahidi wa Mitume na Manabii, kuhusu Yesu Kristo, kwamba alikufa, akazikwa, na akafufuka siku ya tatu, na kupaa mbinguni; na mambo mengine yote ambayo yanahusiana na dini yetu ni tu viambatisho.”36

Kama vile kuzaliwa kwa Yesu kuliotabiriwa kulikaribia, kulikuwa na wale miongoni mwa Wanefi na Walamani wa kale walioamini, ingawa wengi walikuwa na shaka. Hatimaye, ishara ya kuzaliwa Kwake iliwasili---mchana na usiku na mchana bila giza---na wote walijua.37 Hata hivyo leo, baadhi wanaamini katika ufufuo halisi wa Kristo, na wengi wanashuku au hawaamini. Lakini wengine wanajua. Hatimaye, wote watauona na wote watajua; kwa kweli, “Kila goti litapigwa, na kila ulimi utakiri mbele yake.”38

Hadi wakati huo, naamini mashahidi wengi wa ufufuo wa Mwokozi ambao uzoefu na ushahidi wao unapatikana katika Agano Jipya---Petro na wenzake wa Kumi na Wawili na mpendwa, msafi Mariamu wa Magdala, miongoni mwa wengine. Naamini shuhuda zinazopatikana katika Kitabu cha Mormoni---za Mtume Nefi, pamoja na watu wasiojulikana katika nchi Bountiful, miongoni zingine. Na naamini ushuhuda wa Joseph Smith na Sidney Rigdon ambao, kufuatia shuhuda zingine nyingi, walitoa ushuhuda wa ajabu wa kipindi hiki cha mwisho ‘kwamba yu hai! Kwani tulimwona.”39 Chini ya mtazamo wa jicho Lake lote la kuona, nasimama mwenyewe kama shahidi kwamba Yesu wa Nazareti ni Mkombozi Aliyefufuka, na nashuhudia juu yote yatakayofuata kutokana na tendo la Ufufuo Wake. Muweze kupokea imani na faraja wa ushuhuda huo, ninaomba katika jina la Yesu Kristo, amina.