2010–2019
Inahitajika: Mikono na Mioyo ya Kuharakisha Kazi
Aprili 2014


Inahitajika: Mikono na Mioyo ya Kuharakisha Kazi

Tunaweza kutoa mikono na moyo wa kuharakisha kazi ya ajabu ya Baba wa Mbinguni.

Dada wapendwa, ni jinsi gani ninawapenda! Baada ya kuangalia ile video maridadi, mliiona mikono yenu wenyewe ikinyooka ili kumsaidia mtu katika ile njia ya agano? Nilikuwa nikifikiria kuhusu msichana wa Msingi aitwaye Brynn ambaye alikuwa na mkono mmoja tu na bado kuutumia mkono huo kuibariki familia yake na rafiki zake—Watakatifu wa Siku za Mwisho na wale wa imani nyingine. Si ni mrembo siyo? Na ninyi pia! Akina dada, tunatoa mikono yetu ili kusaidia na moyo wa kuharakisha kazi ya ajabu ya Baba wa Mbinguni.

Kama vile dada zetu wema katika maandiko, kama vile Hawa, Sara, Mariamu na wengine wengi, walijua wajibu na malengo yao, Brynn anajua yeye ni binti wa Mungu.1 Sisi pia tunaweza kujua urithi wetu wenyewe kama mabinti wa Mungu na kazi muhimu Yeye aliyonayo kwa ajili ya sisi kuifanya.

Mwokozi alifundisha, “Kama mtu atatenda mapenzi yake, atajua mafundisho.”2 Nini tunahitaji kujua na kufanya “ili tuweze kuishi naye siku moja”?3 Tunaweza kujifunza kutoka kwenye historia ya kijana tajiri aliyemwuliza Yesu kile alichopaswa kufanya ili aupate uzima wa milele.

Yesu alimjibu, “Kama ukitaka kuingia katika uzima, zishike amri.”

Kijana akamwuliza Yeye ni amri zipi azishike. Ndipo Yesu akamkumbusha baadhi ya Amri Kumi ambazo sote tunazifahamu.

Kijana akajibu, “Haya yote nimeyashika toka ujana wangu: nimepungukiwa na nini tena?”

Yesu akasema, “Ukitaka kuwa mkamilifu, enenda ukauze ulivyo navyo, na uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni: kisha njoo unifuate.”4

Yesu alimwita ili aweze kufanya kazi Yake—kazi ya ufuasi. Kazi yetu ni hiyo hiyo. Tunatakiwa “kuyaacha mambo ya ulimwengu … kuyashika maagano [yetu], ”5 na kuja kwa Kristo na kumfuata Yeye. Hivyo ndivyo wafanyavyo wafuasi!

Sasa, akina dada, tuache kujipiga wenyewe kwa sababu Mwokozi aliongea na kijana tajiri juu ya kuwa mkamilifu. Neno kamilifu katika mada hii lilitafsiriwa toka kwenye neno la Kigiriki likimaanisha “kamili.” Tunapojitahidi kusonga mbele katika njia ya agano, tunakuwa tumekamilika na kuwa kamili katika maisha haya.

Kama kijana tajiri wakati wa Kristo, wakati mwingine tunajaribiwa kuvunjika moyo au kurudi nyuma kwa sababu huenda tukafikiria tuko peke yetu. Na tu sahihi! Hatuwezi kufanya mambo magumu tunayotakiwa kufanya bila ya msaada. Msaada unakuja kwa kupitia Upatanisho wa Yesu Kristo, mwongozo wa Roho Mtakatifu, kwa mikono ya msaada ya wengine.

Dada mmoja mwema mseja majuzi alishuhudia kwamba kupitia Upatanisho, alipata nguvu ya kutumia mikono yake na moyo wa upendeleo kuwalea watoto wanne ambao dada yake aliwaacha baada ya kufariki kwa ugonjwa wa saratani. Hiyo inakumbusha kitu fulani Mzee Neal A. Maxwell alisema: “Mambo yote rahisi ambayo Kanisa ilibidi lifanye yamefanyika. Kuanzia sasa na kuendelea, kuna kazi kubwa, na ufuasi utajaribiwa katika njia fulani za ajabu.”6 Mmeletwa duniani katika kipindi hiki cha nyakati kwa sababu ninyi ni kina nani na kile mlichoandaliwa kukifanya! Bila kujali nini Shetani atajaribu kutushawishi sisi kufikiria ni akina nani, uhalisi wetu wa kweli ni ule wa mfuasi wa Yesu Kristo.

Mormoni alikuwa mfuasi wa kweli, aliyeishi katika siku ambazo “kila moyo ilishupanzwa, … na hakujakuwa na uovu mkuu kama huu miongoni mwa kizazi cha Lehi.”7 Ungependa kuwa uliishi katika siku hiyo? Na bado Mormoni alitangaza kwa uthabiti, “Tazama, mimi ni mfuasi wa Yesu Kristo, Mwana wa Mungu.”8

Hamumpendi Mormoni? Alijua yeye alikuwa nani na kazi yake ilikuwa nini na hakusumbuliwa na maovu yaliyomzunguka. Hakika, aliuchukulia wito wake kama zawadi.9

Fikiria ni baraka gani kuitwa ili kutoa vipaji vyetu kwa ajili ya ufuasi wa kila siku kwa Bwana, akitangaza kwa maneno na matendo, “Tazama, Mimi ni mfuasi wa Yesu Kristo!

Naipenda hadithi aliyosimuliwa na Rais Boyd K. Packer juu ya dada aliyetii kufuata mwongozo wa nabii wa kuhifadhi chakula. Aliyemdhihaki alipendekeza kwamba kama kutatokea wakati wa shida, viongozi wake wangemuuliza agawe chakula chake kwa wengine. Jibu lake rahisi lenye ukweli lilikuwa, “Angalao nitakuwa na cha kuleta.”10

Ninawapenda wanawake wa Kanisa hili, vijana kwa wazee. Nimeona nguvu zenu. Nimeiona imani yenu. Mna kitu cha kutoa, na mko tayari kukitoa. Mnafanya hivyo bila ya vishindo, au kujitangaza, ikivuta macho kwa Mungu tuyemwabudu na siyo ninyi wenyewe, na bila kufikiria watapata nini.11 Hivyo ndivyo wafanyavyo wafuasi!

Hivi majuzi nilikutana na msichana huko Ufilipino ambaye familia yake haikuwa ikishiriki kamilifu katika Kanisa alipokuwa na miaka 7, tu wakimwacha atembee peke yake katika barabara hatari kwenda kanisani wiki baada ya wiki. Alisema jinsi alivyoamua kubaki kwenye kweli ya maagano yake akiwa na umri wa miaka 14 ili aweze kuwa mwema kuilea familia yake ya baadaye katika nyumba “iliyobarikiwa kwa nguvu na uwezo wa ukuhani.” 12 Njia nzuri ya kuiimarisha nyumba, sasa au baadaye, ni kuyatii maagano, ahadi tulizowekeana sisi wenyewe na kwa Mungu.

Hivyo ndivyo wafanyavyo wafuasi!

Dada mwaminifu wa Kijapani na mume wake walitembelea misheni yetu huko Korea. Hakuweza kuongea Kikorea na alikuwa anaongea Kiingereza kidogo sana, lakini alikuwa na moyo wa kutumia vipaji vyake vya kipekee na mikono ya usaidizi ili kufanya kazi ya Bwana. Hivyo ndivyo wafanyavyo wafuasi! Aliwafundisha wamisionari wetu kufanya origami—mdomo ambao ungefunguka na kufunga. Ndipo akatumia maneno machache ya Kiingereza aliyoyajua kuwafundisha wamisionari “kufungua midomo yao” kufundisha injili—somo ambalo hawatalisahau wala mimi pia.

Piga taswira kichwani kwa dakika moja wewe na mimi tukusimama pamoja na mamilioni ya kina dada na ndugu wengine katika Kanisa Lake, kuenda mbele kwa ujasiri, kufanya kile wafuasi wanafanya---kuhudumu na kupenda kama Mwokozi. Inamaanisha nini kwako kuwa mfuasi wa Yesu Kristo?

Fulana na mashati ya Mormon Helping Hands yamevaliwa na mamia na maelfu ya wafuasi wenye kujitolea wa Yesu Kristo ambao wanapenda nafasi ya kutoa huduma ya muda tu. Lakini kuna njia nyingine ya huduma kama wafuasi tuliojitolea. Fikiria baadhi ya alama za kiroho zisemazo “msaada unahitajika: unaohusiana na kazi ya wokovu:

  • Msaada unahitajika: wazazi kuwaleta watoto wao katika nuru na kweli

  • Msaada unahitajika: mabinti na mwana, dada na kaka, wajomba na shangazi, binamu, na kina babu, na marafiki wa kweli kutumikia kama wanasihi na kutoa mikono ya msaada katika njia ya agano

  • Msaada unahitajika: wale ambao wanasikiliza mnong’ono wa Roho Mtakatifu na kutenda kama juu ya msukumo unaopokea.

  • Msaada unahitajika: wale wanaoishi injili katika njia ndogo na rahisi

  • Msaada unahitajika: wafanyakazi wa historia ya familia na hekalu kuunganisha familia milele

  • Msaada unahitajika: wamissionari na washiriki wa kueneza “habari njema”—injili ya Yesu Kristo

  • Msaada unahitajika: waokozi kuwatafuta wale waliopotea njia

  • Msaada unahitajika: waweka maagano kusimama imara kwaajili ya ukweli na haki

  • Msaada unahitajika: wafuasi wa kweli wa Bwana Yesu Kristo

Miaka iliyopita, Mzee M.. Russell Ballard alitoa wito ulio wazi kwa akina dada wa Kanisa pale aliposema:

“Kati ya sasa na siku atakapokuja tena Bwana, Yeye anahitaji wanawake katika kila familia, katika kila kata, katika kila jamii, katika kila taifa ambalo watakuja mbele kwa haki na kusema kwa maneno yao na matendo yao, “Mimi nipo hapa, nitume mimi.”

“Swali langu ni, ‘Mtakuwa miongoni mwa mmoja wa wanawake hao? ’”13

Ninatumaini kila mmoja wetu anaweza kujibu kwa sauti ya kujiamini “Ndiyo!” Ninafunga kwa maneno ya wimbo wa Msingi:

Sisi ni [mabinti] wa agano tukiwa na zawadi ya kutoa.

Tutafundisha injili kwa njia tunavyoishi.

Kwa kila neno na tendo, tutashuhudia:

Tunaamini, na tunamtumikia Yesu Kristo.14

Kama wafuasi wa kweli, ninatumaini kwamba tutatoa mioyo yetu na mikono yetu ya usaidizi ili kuiharakisha kazi Yake. Haijalishi kama, Brynn, kama tuna mkono mmoja. Haijalishi kama bado sisi si wakamilifu wala kamili. Sisi ni wafuasi tuliojitolea kunyoosha mkono na kusaidiana sisi kwa sisi tukiwa njiani. Udada wetu ulianza kutoka vizazi vya nyuma kwa wale akina dada wenye haki ambao walikuwepo kabla sisi. Kwa pamoja, kama akina dada na katika umoja na manabii waliohai, waonaji na wafunuzi pamoja na funguo za ukuhani zilizorejeshwa, tunaweza kutembea kama kitu kimoja, kama wafuasi tukiwa na moyo na mikono ya kuharakisha kazi ya wokovu. Tunapofanya hivyo, tutakuwa kama Mwokozi. Ninashuhudia katika jina la Yesu Kristo, amina.