2010–2019
Ombi kwa Dada zangu
Oktoba 2015


Ombi kwa Dada zangu

Tunahitaji nguvu yenu, uongofu wenu, kusadiki kwenu, uwezo wenu wa kuongoza, busara yenu, na sauti zenu.

Wapendwa Wazee Rasband, Stevenson, na Renlund, sisi, Ndugu zenu, tunawakaribisheni kwenye Akidi ya Mitume Kumi na Wawili. Tunamshukuru Mungu kwa mafunuo ambayo Yeye hutoa kwa nabii Wake, Rais Thomas S. Monson.

Akina kaka na dada, wakati tulipokutana katika mkutano mkuu miezi sita iliyopita, hakuna kati yetu aliyetarajia mabadiliko yanayokuja ambayo yatavuta upendo wa Kanisa zima. Mzee L. Tom Perry alitoa ujumbe wenye nguvu sana kuhusu nafasi isiyozibika ya ndoa na familia iliyoko katika ule mpango wa Bwana. Tulistushwa siku chache tu baadaye, wakati tulipoambiwa kuhusu saratani ambayo muda mfupi baadaye ingemwondoa kutoka kwetu.

Ingawa afya ya Rais Boyd K. Packer imekuwa ikidhoofika, yeye aliendelea kwa ujasiri “kupiga hatua” katika kazi ya Bwana. Alikuwa mdhaifu Aprili iliyopita, bado alikuwa ameamua kutangaza ushahidi wake ilimradi alikuwa na pumzi. Halafu, siku 34 tu baada ya Mzee Perry kuaga, Rais Packer pia alikanyaga upande mwingine wa pazia.

Tulimkosa Mzee Richard G. Scott kwenye mkutano wetu mkuu uliopita, lakini tulitafakari ushahidi wa nguvu wa Mwokozi alioutoa katika mikutano mingi iliyopita. Na siku 12 tu zilizopita, Mzee Scott aliitwa nyumbani na akaungane pamoja na kipenzi chake Jeanene.

Nilipata fursa ya kuwa pamoja na hawa Ndugu wote wakati wa siku zao za mwisho, ikijumuisha kuungana na wana familia wa karibu wa Rais Packer na wa Mzee Scott kabla tu ya kufariki kwao. Imekuwa vigumu kwangu kuamini kwamba hawa marafiki zangu wapendwa watatu, watumishi adhimu wa Bwana, wameondoka ghafla. Nawakosa zaidi ya ninavyoweza kusema.

Ninapotafakari juu ya haya matokeo yasiyotarajiwa, mojawapo ya mawazo ambayo yamedumu pamoja nami ni kwamba niliona katika hawa wake wajane. Kilichoganda akilini mwangu ni taswira tulivu za Dada Donna Smith Packer na Dada Barbara Dayton Perry kando ya vitanda vya waume zao, wote wawili ni wanawake waliojawa na upendo, ukweli, na imani halisi.

Wakati Dada Packer alipokuwa amekaa karibu na mumewe katika saa zake za mwisho, alionyesha imani ile ambayo inapita uelewa wote.1 Ingawa alielewa kwamba mwenza wake mpendwa wa takribani miaka 70 ataondoka hivi punde, alionyesha utulivu wa mwanamke aliyejawa na imani. Alionekana kama malaika, kama alivyokuwa akionekana katika hii picha yao katika siku ya kuweka wakfu hekalu la Brigham city.

Picha
Rais na Dada Packer katika Hekalu la Brigham City Utah

Niliona upendo wa aina hiyo hiyo na imani ikitoka kwa Dada Perry. Moyo wake wa upendo kwa wote mumewe na Bwana ulikuwa dhahiri, na uligusa hisia zangu kwa kina.

Picha
Mzee na Dada Perry

Mwanzo hadi mwisho wa masaa ya mwisho ya waume zao, na kuendelea mpaka siku ya leo, hawa wanawake jasiri wameonyesha nguvu na uhodari ambao wanawake wanaoshika maagano daima huonyesha.2 Itakuwa haiwezekani kupima uzoefu ambao wanawake kama hawa wanao, sio tu kwa familia lakini katika Kanisa la Bwana, kama wake, akina mama, na akina bibi; kama akina Dada na mashangazi; kama walimu na viongozi; na hususani kama mifano na walinzi wa dhati wa imani.3

Hii imekuwa kweli katika kila kipindi cha injili tangu siku za Adamu na Hawa. Bado wanawake wa kipindi hiki ni tofauti na wanawake wa vipindi vingine, kwa sababu kipindi hiki ni tofauti na vingine.4 Tofauti hii huleta yote fursa na uwajibikaji.

Picha
Picha ya Rais Kimball

Miaka thelathini na sita iliyopita, mwaka wa 1979, Rais Spencer  W. Kimball alitoa unabii mzito kuhusu nguvu ambayo wanawake wanaoshika -maagano watakuwa nayo juu ya siku za baadaye za Kanisa la Bwana. Yeye alitabiri: “Wingi wa ukuaji mkubwa ambao unakuja kwenye Kanisa katika siku za mwisho utakuja kwa sababu wengi wa wanawake wema wa ulimwengu …watavutwa kuja katika Kanisa kwa idadi kubwa. Hii itatokea kwa kiasi kwamba wanawake wa Kanisa wataonyesha uadilifu na ufasaha katika maisha yao na kwa kiasi kwamba wanawake wa Kanisa wanaonekana dhahiri na tofauti—katika njia za furaha—tofauti na wanawake wa ulimwengu.”5

Wapendwa dada zangu, nyinyi mlio washirika wetu muhimu wakati huu wa kumalizia tukio, siku ile Rais Kimball aliyoiona ni leo. Nyinyi ndiyo wanawake aliowaona! Maadili yenu, nuru, upendo, elimu, ujasiri, tabia, imani, na maisha ya haki vitawavuta wanawake wema wa ulimwengu, pamoja na familia zao, kuja katika Kanisa kwa wingi wa kipekee!6

Sisi, ndugu zenu, tunahitaji nguvu zenu, wongofu wenu, kusadiki kwenu, uwezo wenu wa kuongoza, busara zenu na sauti zenu. Ufalme wa Mungu si kamili na hauwezi kukamilika bila wanawake wanaofanya maagano matakatifu, na kuyashika, wanawake wamaoweza kusema kwa uwezo na mamlaka ya Mungu!7

Rais Boyd K.Packer alitangaza :

“Tunahitaji wanawake waliojipanga na wanawake wanaoweza kupanga. Tunahitaji wanawake wenye uwezo wa utendaji wanaoweza kupanga na kuelekeza na kusimamia; wanawake wanaoweza kufundisha, wanawake wanaoweza kutoa hoja bila woga. ...

“Tunahitaji wanawake wenye karama ya kutambua wanaoweza kuona mielekeo katika ulimwengu na kugundua ile ambayo, hata kama inapendwa, siyo makini ama ni hatari.”8

Leo, wacha niongeze kwamba tunahitaji wanawake wanaojua jinsi ya kufanya mambo muhimu yatendeke kwa imani yao na ambao ni walinzi jasiri wa uadilifu na familia katika ulimwengu uliojaa dhambi. Tunahitaji wanawake waliojitolea kulea watoto wa Mungu kwenye njia ya agano kuelekea kuinuliwa; wanawake ambao wanajua jinsi ya kupokea ufunuo binafsi, wanaoelewa uwezo na amani ya endaumenti ya hekalu; wanawake wanaojua jinsi ya kuomba nguvu za mbinguni kulinda na kuimarisha watoto na familia; wanawake wanaofundisha bila woga.

Katika maisha yangu yote, nimebarikiwa na wanawake kama hawa. Mke wangu mwenda zake, Dantzel, alikuwa kama wanawake hawa. Daima nitamshukuru kwa uwezo aliokuwa nao wa kubadilisha maisha yangu katika sura zote za maisha yangu, pamoja na juhudi zangu ikijumuisha kuasisi upasuaji wazi wa moyo.

Miaka hamsini na nane iliyopita, niliombwa kumfanyia upasuaji msichana mdogo, aliyekuwa mgonjwa wa moyo tangu kuzaliwa kwake. Kaka yake mkubwa alikufa hapo nyuma kwa hali kama hii. Wazazi wake walinisihi niwasaidie. Sikuwa na uhakika kuhusu matokeo lakini niliapa kufanya yote yaliyo katika uwezo wangu kumwokoa. Licha ya juhudi zangu, mtoto alikufa. Baadaye, wazazi wale wale walimleta mtoto wao wa kike mwingine kwangu, wakati huo akiwa na miezi 16 tu, pia amezaliwa na moyo wenye hitilafu. Tena, kwa maombi yao, nilifanya upasuaji. Mtoto huyu pia alikufa. Huku kufiwa kwa mara ya tatu kwenye kuvunja moyo katika familia moja kulinitengua mimi.

Nilirudi nyumbani nikiwa na huzuni mkubwa. Nilijitupa juu ya sakafu ya chumba cha kupumzika na kulia usiku mzima. Dantzel alikaa pembeni mwangu, akisikiliza nilipokuwa narudia kutangaza kwamba kamwe sitafanya upasuaji mwingine wa moyo. Kisha, karibu saa 11:00 za asubuhi, Dantzel alinitazama na kwa upendo akauliza, “umemaliza kulia? Basi nenda kavae. Rudi kwenye maabara. Nenda kafanye kazi! Unahitaji kujifunza zaidi. Kama ukiacha sasa, wengine watatakiwa kujifunza kwa jitihada kubwa kile ambacho wewe tayari unakijua.”

Ee, jinsi gani nilihitaji ono la mke wangu, ujasiri na uvumilivu na upendo! Nilirudi kufanya kazi na kujifunza zaidi. Kama isingekuwa msukumo wenye maongozi wa Dantzel, ni singeendelea na upasuaji wa moyo na nisingekuwa nimejitayarisha kufanya upasuaji mwaka 1972 ambao uliokoa maisha ya Rais Spencer W. Kimball.9

Akina Dada, mnaelewa mapana na marefu ya ushawishi wenu wakati mnazungumza vitu hivi ambavyo vinakuja kwenye mioyo yenu kama yalivyoelekezwa na Roho? Rais wa kigingi mzuri sana alinieleza kuhusu baraza la kigingi ambapo walikuwa wanapambana na changamoto ngumu. Wakati mmoja, alitambua kwamba rais wa Msingi wa kigingi alikuwa hajasema, kwa hiyo alimwuliza kama alikuwa na wazo lolote . “Sawa, kwa kweli ninalo,” alisema na kisha akaendelea kuelezea wazo ambalo lilibadili mwelekeo wote wa mkutano. Rais wa kigingi aliendelea, “Alipokuwa anasema, Roho alishuhudia kwangu kwamba ametoa sauti kwa ufunuo tuliokuwa tunatafuta kama baraza.”

Wapendwa dada zangu, mwito wowote ulio nao, hali yoyote uliyomo, tunahitaji mawazo yenu, utambuzi wenu, na msukumo wenu. Tunawataka mseme bila woga na mseme wazi katika mabaraza ya kata na kigingi. Tunamtaka kila dada aliyeolewa kusema kama mchangiaji na mwenza kamili10 mnapoungana pamoja na waume zenu katika kuongoza familia zenu. Walioolewa na wasioolewa, nyinyi akina dada mna uwezo tofauti na uwezo wa kipekee kuhisi kitu haraka mmepokea kama zawadi kutoka kwa Mungu. Sisi ndugu hatuwezi kunakili ushawishi wenu wa kipekee.

Tunajua kwamba kitendo cha kufikia mwisho wa uumbaji wote kilikuwa ni kuumbwa kwa mwanamke!11 Tunahutaji uwezo wenu!

Mashambulizi dhidi ya Kanisa, mafundisho yake, na desturi yetu ya maisha yataongezeka. Kwa sababu hii, tunahitaji wanawake ambao wana msingi wa mwamba wa kuelewa mafundisho ya Kristo na ambao watatumia uelewa huo kufundisha na kusaidia kuinua kizazi cha kupinga dhambi.12 Tunahitaji wanawake ambao wanaweza kutambua udanganyifu wa hali zote. Tunahitaji wanawake wanaojua jinsi ya kutumia uwezo wa Mungu ambao anaweka upatikane kwa washika agano na ambao huonyesha imani zao kwa matumaini na hisani. Tunahitaji wanawake walio na ujasiri na ufunuo wa Mama yetu Hawa.

Wapendwa dada zangu, hakuna chenye maana sana kwa maisha yenu ya milele zaidi ya wongofu wenu binafsi. Ni wanawake waongofu, washika maagano ambao maisha yao ya uadilifu yatasimama wazi kwa kuongezeka katika ulimwengu unaodhoofika na ambao wataonekana hivyo dhahiri na tofauti katika njia za furaha kubwa.

Kwa hiyo leo, ninawasihi dada zangu wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho mjitokeze mbele! Mchukue sehemu yenu adilifu na inayohitajika katika nyumba zenu, katika jumuia zenu, na katika ufalme wa Mungu—zaidi ya ambavyo mmewahi kufanya hapo mapema. Ninawasihi mtimize utabiri wa Rais Kimball. Na ninawaahidi katika jina la Yesu Kristo kwamba mtakapofanya hivyo, Roho Mtakatifu atakuza ushawishi wenu katika njia haijawahi kutokea!

Ninatoa ushahidi wa uhalisi wa Bwana Yesu Kristo na ukombozi Wake, upatanisho, na uwezo Wake wa kutakasa. Na kama mmoja wa Mitume Wake, nawakushukuru, dada zangu wapendwa, na nawabariki muinuke kwenye kimo chenu kamili, kukamilisha kipimo cha uumbaji wenu, tunapotembea bega kwa bega katika kazi hii takatifu. Kwa pamoja tutasaidia kuuandaa ulimwengu kwa Ujio wa Pili wa Bwana. Kwa haya nashuhudia, kama kaka yenu, katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona Wafilipi 4:7.

  2. Hii ujumuisha machozi—katika kutii amri ya kuomboleza kwa wale tunaowapenda wanapohitimu kutoka kwa maisha haya (ona Mafundisho na Maagano 42:45).

  3. Ona ushawishi wa Rebeka kwa Isaka na mwana wao Yakobo katika Mwanzo 27:46; 28:1–4..

  4. Ona Joseph Fielding Smith, Answers to Gospel Questions, comp. Joseph Fielding Smith Jr., 5 vols. (1957–66), 4:166. Muhtasari Vipindi vyote vya awali vilikuwa vya sehemu awamu ndogo ya ulimwengu na iliishia na ukengeufu. Kinyume, kipindi hiki si cha eneo au wakati fulani. Kitajaza ulimwengu na kuunganika na Ujio wa Pili wa Bwana.

  5. Teachings of Presidents of the Church: Spencer W. Kimball (2006), 222–23.

  6. Nilipozaliwa, kulikuwa na waumini wachache kushinda 600,000 wa Kanisa. Leo kuna zaidi ya milioni 15. Idadi hiyo itaendelea kuongezeka.

  7. Rais Joseph Fielding Smith aliwaambia kina dada wa Muungano wa Usaidizi wa Kina Mama, ”Mnaweza kusema kwa mamlaka, kwa sababu Bwana amewaweka mamlaka juu yao.” Alisema pia kwamba Muungano wa Usaidizi wa Kina Mama ”umepatiwa nguvu na mamlaka kufanya mambo mengi makuu. Kazi ambayo wanafanya inafanywa kwa mamlaka takatifu” (“Relief Society—an Aid to the Priesthood,” Relief Society Magazine, Jan. 1959, 4, 5). Dondoo hizi zilitolewa na Mzee Dallin H. Oaks katika hotuba ya mkutano mkuu, “The Keys and Authority of the Priesthood,” Liahona, May 2014, 51.

  8. Boyd K. Packer, “The Relief Society,” Ensign, Nov. 1978, 8; ona pia M. Russell Ballard, Counseling with Our Councils: Learning to Minister Together in the Church and in the Family (1997), 93.

  9. Ona Spencer J. Condie, Russell M. Nelson: Father, Surgeon, Apostle (2003), 146, 153–56. Muhtasari Katika 1964 Rais Kimball alitawazwa kama rais wa kigingi na kunibariki kwamba idadi ya vifo ingepunguka katika juhudi zangu za uanzilishi wa upasuaji wa mifereji ya moyo. Tusijue basi kwamba miaka minane baadaye, ningemfanyia upasuaji Rais Kimball ambao ulijumuisha kubadilisha mfereji wa moyo wake uliokuwa na hitilafu.

  10. ”Wakati tunaongea juu ya ndoa kama muungano, acha tuongea juu ya ndoa kama muungano kamili. Hatutaki wanawake wetu WSM wawe wenzi kimya ama wenzi wasio na uwezo katika hiyo kazi ya milele! Tafadhalini muwe wenzi wachangiaji na wenzikamili” (Spencer W. Kimball, “Privileges and Responsibilities of Sisters,” Ensign, Nov. 1978, 106).

  11. ”Madhumuni yote ya ulimwengu na yale yote yalikuwa katika ulimwengu yatakuwa bure bila mwanamke—jiwe la pembeni la tao la ukuhani” (Russell M. Nelson, “Lessons from Eve,” Ensign, Nov. 1987, 87). ”Hawa akawa kiumbe cha mwisho cha Mungu, jumuisha kuu la kazi ya maajabu ambayo ilikuwa imetangulia” (Gordon B. Hinckley, “The Women in Our Lives,” Liahona, Nov. 2004, 83).

  12. Ona Russell M. Nelson, “Children of the Covenant,” Ensign, May 1995, 33.