2010–2019
Mpangilio wa Amani
Aprili 2016


Mpangilio wa Amani

Amani ambayo sote tunatafuta inatubidi kutenda—kwa kujifunza kutoka kwa Yesu Kristo, kwa kusikiliza maneno Yake, na kwa kuenenda Naye.

Miaka michache iliyopita, binti yetu na mkwe wetu waliombwa kwa pamoja kufundisha darasa la Msingi la wavulana watano wa umri wa miaka minne. Binti yetu alikuwa mwalimu na mkwe wetu alikuwa mtekeleza sheria, wakifanya kwa juhudi kulifanya darasa liwe na utulivu, katikati ya vurugu mara kwa mara ili kufundisha kanuni za injili kwa watoto.

Wakati wa kipindi kimoja kigumu, baada ya maonyo kadhaa kwa wavulana wadogo wenye nguvu, mkwe wetu alimsindikiza mtoto wa miaka minne nje ya darasa. Walipofika nje ya darasa, na kabla ya kuongea na yule mtoto juu ya tabia yake na akihitaji kuwatafuta wazazi wake, yule mtoto akamsimamisha mkwe wetu kabla hajasema neno na, akiwa amenyosha mikono juu hewani na akiwa na hisia kali, aliropoka, “Wakati mwingine ni vigumu kwangu kufikiria kuhusu Yesu!”

Katika safari yetu ya duniani, licha ya jinsi safari yetu ya mwisho unavyokusudiwa kuwa ya utukufu na licha ya jinsi safari unavyoweza kudhibitishwa kuwa yenye msisimko, sisi sote tutakuwa kwenye majaribu na huzuni humo njiani. Mzeer Joseph B. Wirthlin alifundisha: “Uso wa gurudumu la huzuni hatimaye unamwelekea kila mmoja wetu. Wakati mmoja au mwingine, kila mmoja lazima apitie huzuni. Hakuna aliyeachiwa.”1 “Bwana katika busara Zake hamkingi yeyote kutokana na huzuni au majonzi.”2 Hata hivyo, uwezo wetu wa kusafiri kwenye njia hii kwa amani, kwa sehemu kubwa, itategemea kama sisi tuna wakati mgumu kufikiria juu ya Kristo.

Amani ya akili, amani ya dhamira, na amani ya moyo haviamuliwi na uwezo wetu wa kuepuka majaribu, huzuni, au maumivu ya moyo. Licha ya maombi yetu ya dhati, si kila dhoruba itabadilisha mwelekeo, si kila udhaifu utaponywa, na hatuwezi kuelewa kila mafundisho, kanuni, au tabia zilizofundishwa na manabii, waonaji, na wafunuzi. Hata hivyo, tumeahidiwa amani—kwa masharti yaliyoambatanishwa.

Katika Injili ya Yohana, Mwokozi alifundisha kwamba bila kujali mateso ya maisha, tunaweza kuwa na furaha; tunaweza kutumaini, na hatuhitaji kuogopa, kwa sababu Alisema, “Katika mimi mpate kuwa na amani.”3 Imani katika Yesu Kristo na dhabihu Yake ya upatanisho ni, na daima itakuwa, kanuni ya kwanza ya injili na msingi ambao tumaini letu kwa ajili ya “amani katika ulimwengu huu, na uzima wa milele katika ulimwengu ujao” imejengwa.4

Katika kutusaidia kutafuta amani katikati ya changamoto za maisha, tumepewa utaratibu rahisi wa kuweka mawazo yetu kwa Mwokozi, ambaye alisema: “Jifunze kwangu, na sikiliza maneno yangu; enenda katika unyenyekevu wa Roho wangu, na utapata amani kwangu. Mimi ni Yesu Kristo.”5

Jifunze, sikiliza, na enenda—hatua tatu zenye ahadi.

Hatua ya Kwanza: “Jifunze Kunihusu”

Katika Isaya tunasoma, “Na mataifa wengi watakwenda na kusema, Njooni, twendeni juu mlimani kwa Bwana, nyumbani kwa Mungu wa Yakobo; naye atatufundisha njia zake.”6

Katika ongezeko kubwa la mahekalu hapa duniani, tunajifunza juu ya Yesu Kristo na wajibu Wake katika mpango wa Baba kama Mwumbaji wa ulimwengu, kama Mwokozi na Mkombozi wetu, na ndiye chanzo cha amani yetu.

Rais Thomas S. Monson alielezea: Dunia inaweza kuwa yenye changamoto na mahali pagumu kuishi. … Wewe na mimi tunapoenda katika nyumba takatifu za Mungu, tunapokumbuka maagano tunayofanya mle, tutaweza hata zaidi kustahamili kila mateso na kushinda kila jaribio. Katika mahala hapa patakatifu tutapata amani.”7

Wakati wa mkutano wa kigingi nikiwa ninahudumu huko Amerika ya Kusini, nilikutana na wenza ambao walikuwa wanaomboleza kifo cha hivi majuzi cha mwana wao mchanga.

Ilikuwa wakati wa mahojiano ya mkutano ambapo kwanza nilikutana na Kaka Tumiri na kujua kuhusu kufiwa kwake. Tukiwa tunaongea, alishiriki kwamba siyo tu kwamba alikuwa na huzuni ya kifo cha mtoto wake lakini kwamba alikuwa amefadhaishwa na wazo la kutoweza kumwona tena kamwe. Alielezea kwamba, kama waumini wapya wa Kanisa, waliweka akiba ya pesa za kutosha kuhudhuria hekalu, kabla ya kuzaliwa kwa mvulana wao mdogo, na waliunganisha kama wenza na kwa binti zao wawili. Kisha akaelezea jinsi walivyokuwa wakiweka akiba kwa ajili ya kurudi tena hekaluni lakini hawakuweza kwenda na mvulana wao mdogo ili kuunganishwa naye pia.

Baada ya kugundua uwezekano wa kutoelewa, nilimwelezea kwamba hakika atamwona tena mwana wake, kama ataendelea kuwa mwaminifu, kwa sababu ibada ya kufunganisha imemwunganisha yeye na mke wake na binti zake pia ilitosha kumwunganisha mwanae pia, ambaye alizaliwa katika agano.

Kisha akaniomba kama nitakubali kuongea na mke wake, ambaye alikuwa na huzuni kwa kipindi cha wiki mbili baada ya kifo cha mwana wake.

Jumapili mchana, baada ya mkutano, nilikutana na Dada Tumiri na kumwelezea mafundisho haya matakatifu kwake pia. Akiwa bado na maumivu ya msiba, lakini sasa akiwa na matumaini, na machozi aliuliza,“Je, nitaweza kumshika mtoto wangu kwenye mikono yangu? Ni wangu kweli, milele?” Nilimhakikishia kwamba akitii maagano yake, nguvu za kuunganishwa zipatikanazo hekaluni, kwa sababu ya mamlaka ya Yesu Kristo, hakika yatamuwezesha kuwa tena na mwana wake na kumpakata mikononi mwake.

Dada Tumiri, akiwa amevunjika moyo kwa kifo cha mwana wake, aliondoka kwenye mkutano akiwa na machozi ya furaha na alijazwa na imani kwa sababu ya ibada takatifu za hekalu, zilizowezeshwa na Mwokozi na Mkombozi wetu.

Kila wakati tunapohudhuria hekalu—katika yote tunayoyasikia, tenda na kusema; katika kila ibada tunayohudhuria; na katika kila agano tunaloweka—tunaelekezwa kwa Yesu Kristo. Tunahisi amani tunaposikia maneno Yake na kujifunza kwa mfano Wake. Rais Hinckley alifundisha, “Enendeni katika nyumba ya Bwana na kule muhisi Roho Wake na kuongea Naye, na mtajua amani ambayo haiwezi kupatikana sehemu nyingine yeyote.”8

Hatua ya Pili: “Sikilizeni Maneno Yangu”

“Iwe kwa maneno yangu mwenyewe au maneno ya watumishi wangu, yote ni sawa.”9 Kutoka kwa siku ya Adamu hadi wakati wa nabii aliyepo, Thomas Spencer Monson, Bwana amenena kupitia kwa wawakilishi wake wenye mamlaka. Wale wanaochagua kusikiliza na kutii maneno ya Bwana, yakitolewa kupitia manabii Wake, watapata usalama na amani.

Katika Kitabu cha Mormoni tunapata mifano mingi ya umuhimu wa kufuata ushauri wa kinabii na kusimama na nabii, pamoja na somo la kujifunza toka kwenye ono la Lehi la mti wa uzima, linalopatikana kwenye 1 Nefi sura ya 8. Kamwe hapajawahi kuwa na wakati ambapo jengo kubwa na pana limfurika au makelele yanayotoka kupitia madirisha yake kuwa potovu zaidi, yenye kufanya mzaha, na ya kutatanisha kuliko ilivyo katika siku zetu. Katika aya hii tunasoma juu ya makundi mawili ya watu na majibizo wao kwa kelele toka kwenye jengo.

Picha
Ndoto ya Lehi

Kuanzia mstari wa 26, tunasoma:

“Na pia nikatupa macho yangu hapa na pale, na nikaona, kwenye ng’ambo nyingine ya mto wa maji, jengo kubwa na pana. …

“Na lilikuwa limejaa watu, … na walikuwa na tabia ya kufanya mzahaa na kuwaonyesha kwa vidole vyao wale ambao walikuwa wanakuja … na kula matunda.

“Na baada ya kuonja matunda waliaibika, kwa sababu ya wale waliokuwa wakiwadharau; na wakaingia katika njia zilizokataliwa na wakapotea.”10

Katika mstari wa 33 tunasoma juu ya wengine ambao walikuwa na mjibizo tofauti kwa wale waliokuwa wakidhihaki kutoka kwenye jengo. Nabii Lehi anaelezea kwamba kwenye lile jengo “walitufanyia ishara za madharau kwa vidole vyao mimi na wale ambao walikuwa wanakula matunda; lakini hatukuwasikiza.”11

Tofauti kubwa kati ya wale walioona aibu, wakaanguka, na wakapotea na wale ambao hawakusikia kejeli kutoka kwenye jengo na kusimama na nabii inapatikana kwenye vishazi viwili: kwanza, “baada ya wao kuonja, na pili, “wale ambao walikuwa wanakula.

Kundi la kwanza lilifika kwenye mti, likasimama kwa muda na nabii, lakini walionja tunda tu. Kwa kutoendelea kula, waliruhusu makelele toka kwenye jengo kuwaathiri, kuwafanya watoweke toka kwa nabii na kwenda kwenye njia isiyo sahihi, ambako walipotea.

Tofauti na wale walioonja na kuzurura walikuwepo wale walioendelea kula tunda. Hawa watu walipuuza makelele kutoka kwenye jengo, walisimama na nabii, na kufurahia usalama na amani. Kujitoa kwetu kwa Bwana na watumishi Wake hakuwezekani kuwa sharti la muda. Ikiwa hivyo, tunajiweka wenyewe katika hatari kwa wale wanaotaka kuiangamiza amani yetu. Tunapomsikiliza Bwana kupitia kwa watumishi Wake wenye mamlaka, tunasimama mahali patakatifu na hatuwezi kuondolewa.

Mwovu anatoa suluhisho bandia ambalo linaweza kuonekana kutoa majibu lakini hutupeleka mbali zaidi na imani tunayoihitaji. Yeye hutoa mazigazi ambayo yana muonekano wa uhalali na usalama lakini hatimaye, kama jengo kubwa na pana, litaanguka, na kuharibu wote ambao hutafuta amani ndani ya kuta zake.

Kweli inapatikana kwenye wimbo wa msingi: “Maneno ya nabii: Zitii Amri. Katika hii kuna usalama na amani.12

Hatua ya Tatu: “Enendeni katika Upole wa Roho Yangu”

Licha ya umbali tunaoweza kupotea kutoka kwenye njia, Mwokozi anatualika kurudi na kutembea pamoja Naye. Mwaliko huu wa kutembea na Yesu Kristo ni mwaliko wa kumsindikiza kwenda Gethsemane na kutoka Gethsemane kwenda Kalivari na kutoka Kaivari kwenda kwenye Bustani ya Kaburi. Ni mwaliko wa kuangalia na kutumia dhabihu kubwa ya upatanisho, ambao humfikia mtu binafsi na hauna kikomo. Ni mwaliko wa kutubu, kuja karibu na nguvu Zake za uponyaji, na kupata upendo Wake, kwa mikono iliyonyoshwa. Ni mwaliko wa kuwa na amani.

Picha
Sisi tumealikwa kutembea pamoja Naye.

Sote tumehisi, wakati fulani katika maisha yetu, maumivu na moyo kuuma kulikotokana na dhambi na kosa, kwani “kama tunasema kwamba hatuna dhambi, tunajidanganya wenyewe, na ukweli haupo nasi.”13 Hata hivyo, “japo una madoa makubwa ya dhambi,” tunapotumia Upatanisho wa Yesu Kristo na kutembea pamoja Naye kupitia toba ya kweli, “utakuwa weupe kama theluji.”14

Picha
Tumealikwa Kutubu.

Alma Mdogo alilazimika kukabiliana na dhambi zake wakati alipotembelewa na malaika wa Bwana. Alielezea uzoefu wake kwa maneno haya:

“Roho yangu iliteseka kwa kiasi kikubwa sana na kuadhibiwa kwa dhambi zangu zote.

“… Ndio, niliona kwamba nimeasi dhidi ya Mungu wangu, na kwamba sikuwa nimetii amri zake.”15

Hata jinsi dhambi zake zilivyokuwa kubwa, na katikati ya tatizo hili, aliendelea:

“Nilikumbuka pia nikisikia baba yangu akitoa unabii kwa watu kuhusu kuja kwa mmoja aitwaye Yesu Kristo, Mwana wa Mungu, kulipia dhambi za ulimwengu.

“… Nililia ndani ya moyo wangu: Ee Yesu, wewe Mwana wa Mungu, nihurumie.”16

“Na haikuwa, mpaka nilipomlilia Bwana Yesu Kristo kwa huruma, ndipo nikapata kusamehewa dhambi zangu. Lakini tazama, nilimlilia na nikapata amani ndani ya roho yangu.17

Kama Alma, sisi pia tutapata amani katika nafsi yetu pale tutakapotembea na Yesu Kristo, kutubu dhambi zetu, na kutumia nguvu Zake za uponyaji katika maisha yetu.

Amani ambayo wote tunaitaka inahitaji zaidi ya kutamani. Inatubidi kutenda—kwa kujifunza kuhusu Yeye, kwa kusikiliza maneno Yake, na kwa kuenenda Naye. Huenda tusiwe na uwezo wa kuzuia yale yanayotutokea sisi, lakini tunaweza kudhibiti jinsi tunavyoutumia mpango wa amani ambao Bwana ameutoa—mpango unaofanya rahisi kufikiria mara nyingi kuhusu Yesu.

Picha
Tunaweza kutumia mpangilio wa Mwokozi.

Ninashuhudia kwamba Yesu Kristo ndiye “njia, kweli, na uzima”18 na kwamba ni kupitia Kwake pekee tunaweza kupata amani ya kweli katika maisha haya na ya milele katika ulimwengu ujao. Katika jina la Yesu Kristo, amina