2010–2019
Jione Mwenyewe Hekaluni
Aprili 2016


Jione Mwenyewe Hekaluni

Ndugu na dada, ninaomba kwamba kila mmoja wetu aweze kumstahi Mwokozi na kufanya mabadiliko ili tujione katika mahekalu Yake matakatifu.

Kuanzishwa kwa mpango wa Bwana wa wokovu katika kipindi hiki cha utimilifu wa nyakati ni karibu zaidi ya ufahamu.1 Hili linadhihirishwa na tangazo la Rais Thomas S. Monson’s la mahekalu 4 mapya katika kikao hiki. Wakati Rais Monson alipewa mwito kama Mtume mwaka wa 1963, kulikuwepo na mahekalu 12 yaliyokuwa yakitumika kote ulimwenguni.2 Baada ya kuwekwa wakfu kwa Hekalu la Provo City Center, sasa kunayo 150, na kutakuwepo na 177 wakati mahekalu yote yaliyotangazwa yatawekwa wakfu. Hii ni sababu yetu sisi ya kufurahi kwa unyenyekevu.

Miaka mia moja na themanini iliyopita, siku sawa na hii, Aprili 3, 1836, ono kubwa lilifunguliwa kwake Nabii Joseph Smith na Oliver Cowdery katika Hekalu la Kirtland. Hili lilifanyika wiki moja tu baada ya hekalu hilo kuwekwa wakfu. Katika ono hili walimuona Bwana akiwa amesimama kwenye jukwaa la mimbari katika hekalu. Miongoni mwa mambo mengine, Mwokozi alitangaza:

“Na acha mioyo ya watu wangu wote ifurahi, ambao, kwa nguvu zao, wameijenga nyumba hii kwa ajili ya jina langu.

“Kwani tazama, nimeikubali nyumba hii, na jina langu litakuwa humu; nami nitajionyesha kwa watu wangu kwa rehema katika nyumba hii.”3

Wakati wa tukio hilo takatifu, manabii wa kale wakatokea, ikiwa ni pamoja na Eliya, ambaye ambaye alitoa funguo muhimu katika maagizo ya hekalu.

Tuna kiwango fulani cha hisia ya furaha inayoendelea kule Quito, Ecuador; Harare, Zimbabwe; Belém, Brazil; na Lima, Peru, miongoni mwa washiriki na wamisionari, kulingana na yaliyotendeka kule Bangkok, Thailand, mwaka mmoja uliopita wakati hekalu ilipotangazwa. Dada Shelly Senior, mke wa aliyekuwa-rais wa Misheni ya Thailand Bangkok, David Senior, alituma barua pepe kwa familia na marafiki kusema kwamba baada ya kumsikiliza Rais Monson akitangaza hekalu hilo, kulikuwa na “masaa 12 bila usingizi na machozi mengi ya furaha.” Waliwapigia wasaidizi wao wa misheni saa 5:30 za usiku na kuwajulisha. Wasaidizi waliwapigia simu wamisionari wote. Ripoti ilirudishwa kwamba “misheni nzima ilikuwa macho katikati mwa usiku wakirukaruka vitandani mwao.” Dada Senior kwa ucheshi aliwashauri familia na marafiki, “Tafadhali msije mkafahamisha Idara ya Umisionari!”4

Mujibizo wa dhati wa kiroho wa waumini katika Thailand pia ulikuwa wa nguvu sawia. Nina uhakika kwamba kumekuwepo na matayarisho ya kiroho katika mioyo na nyumbani na madhihirisho kutoka mbinguni kuwatayarisha Watakatifu katika hizi sehemu ambapo mahekalu haya mapya yaliyotangazwa yatakuwa.

Picha
Wasichana Wathai wakiwa na kioo ambacho kimeandikwa, “Jione Mwenyewe Hekaluni.”

Dada Senior, kule Thailand, alikuwa vioo maalum vya mkono vilivyotengenezwa kwa mafundisho yake ya kibinafsi, hasa na kina dada. Kulikuwa na hekalu lililochorwa kwenye kioo na maandishi, “Jione Mwenyewe Hekaluni.” Watu walipotazama kwenye kioo, walijiona hekaluni. Ndugu na dada Senior waliwafundisha wachunguzi na waumini kujiona wakiwa hekaluni na kufanya mabadiliko yanayohitajika na matayarisho ya kiroho ili kuweza kufikia lengo hili.

Changamoto yangu asubuhi hii ni kwa kila mmoja wetu, popote tunapoishi, tujioneni wenyewe hekaluni. Rais Monson amesema: “Hadi wakati ambapo utaingia katika nyumba ya Bwana na kupokea baraka zote ambazo zinakusubiri kule, ungali haujapokea kila kitu ambacho Kanisa linaweza kutoa. Muhimu zaidi na baraka za kilele za uumini katika Kanisa ni zile baraka ambazo tunapokea katika mahekalu ya Mungu.”5

Licha ya ukosefu wa haki duniani siku hizi, tunaishi katika wakati mtakatifu. Manabii, wenye mioyo ya upendo na matumaini, wameeleza siku zetu kwa karne nyingi.6

Nabii Joseph Smith, akinukuu Obadia7 katika Agano la Kale na 1 Petro8 katika Agano Jipya, alikiri mpango mkubwa wa Mungu kwa kufanya kuwepo na ubatizo kwa ajili ya wafu na kuturuhusu sisi kuwa waokozi Mlimani Sayuni.9

Bwana amefanikisha watu wetu na kutoa rasilimali na mwongozo wa kinabii ili tuweze kuwa jasiri katika kutekeleza majukumu yetu ya hekalu kwa wote walio hai na wafu.

Kwa sababu ya injili ya urejesho ya Yesu Kristo, tunaelewa madhumuni ya maisha, mpango wa wokovu wa Baba kwa watoto Wake, dhabihu ya Mwokozi ya ukombozi, na jukumu la familia la muhimu zaidi katika mpangilio wa mbinguni.10

Mchanganyiko wa kuongezeka kwa idadi ya mahekalu na maendeleo ya kiteknolojia katika kutimiza majukumu yetu matakatifu ya historia ya familia kwa mababu zetu inafanya wakati huu kuwa wenye baraka zaidi katika historia yote. Ninafurahia katika uaminifu wa ajabu wa vijana wetu katika kuorodhesha na kutafuta mababu zao na kisha kufanya kazi ya ubatizo na uthibitisho katika hekalu. Katika hali halisi ninyi ni miongoni mwa waokoaji waliotabiriwa kewenye Mlima Sayuni.

Ni Namna Gani Tunaweza Kujitayarisha Kwa Ajili ya Kwenda Hekaluni?

Tunajua kwamba haki na utakaso ni viungo muhimu katika kujiyatayarisha kwa ajili ya kwenda hekaluni.

Katika Mafundisho na Maagano sehemu ya 97, inasema, “Na alimradi watu wangu wakinijengea nyumba katika jina la Bwana, na ikiwa hawataruhusu kitu chochote kichafu kuingia ndani yake, ili isichafuliwe, utukufu wangu utatulia juu yake.”11

Hadi mwaka wa 1891 Rais wa Kanisa alitia sahihi kwenye kila sifu ya hekalu ili kulinda utakatifu wa hekalu. Jukumu hili lilipewa maaskofu na marais wa vigingi.

Ni hamu yetu kubwa kwamba waumini wa Kanisa wataishi kuwa wastahiki wa sifu ya hekalu. Tafadhali usione hekalu kama lengo lililo mbali na pengine lisiloweza kufikiwa. Wakishirikiana na askofu, waumini wengi wanaweza kutimiza mahitaji yote ya haki ikilinganishwa katika muda mfupi sana ikiwa wana azmio la kuhitimu na kutubu makosa kikamilifu. Hii ni pamoja na kuwa tayari kujisamehe sisi wenyewe na sio kulenga kasoro zetu au dhambi kama zinazotukosesha kamwe kuhitimu kuingia katika hekalu takatifu.

Upatanisho wa Mwokozi ulitimizwa kwa ajili ya watoto wote wa Mungu. Dhabihu Yake ya ukombozi inatosheleza mahitaji ya haki kwa wale wote ambao kwa kweli wametubu. Maandiko yanaelezea haya katika mtindo wa kupendeza zaidi:

“Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji.”12

“Sitazikumbuka [hizo] tena.”13

Tunawahakikishia kwamba kuishi kulingana na kanuni kutawaletea nyinyi na familia zenu furaha, kuridhika, na amani.14 Waumini, wakubwa kwa vijana15 huthibitisha binafsi ustahiki wao wakati wanapojibu maswali ya sifu ya hekalu. Mahitaji muhimu ni kuzidisha ushuhuda wetu kuhusu Mungu Baba; Mwana Wake, Yesu Kristo; na Urejesho wa injili Yake na kupata huduma ya Roho Mtakatifu.

Baraka za Hekalu ni Nyingi Sana

Baraka za msingi za hekalu ni maagizo ya kuinuliwa. Mpango wa injili unahusu kuinuliwa na, ni pamoja na kufanya na kushika maagano matakatifu na Mungu. Isipokuwa ubatizo na uthibitisho, maagizo na maagano haya hutendeka na kupokelewa hekaluni kwa walio hai. Kwa wafu, maagizo yote ya wokozi na maagano hupokelewa hekaluni.

Brigham Young alifundisha, “Hakuna jambo hata moja ambalo Bwana angeweza kufanya kwa ajili ya wokovu wa familia ya binadamu ambalo amekosa kufanya; … kila jambo linaloweza kutimizwa kwa wokovu wao, limetimizwa katika na kwa Mwokozi.”16

Viongozi wa Kanisa huandaa vigingi, kata, jamii, vikundi saidizi vya Kanisa, misheni, na kadhalika katika makanisa yetu na mjengo mengine. Bwana huandaa familia za milele tu mahekaluni.

Ni wazi kwamba wale walio na mioyo iliyovunjika na roho zilizopondeka ambao kwa kweli wametubu dhambi zao wanakubalika kikamilifu kwake Bwana katika nyumba Yake takatifu.17 Tunajua “Mungu hana mapendeleo kwa watu.”18 Kitu kimoja miongoni mwa vitu vya thamani kubwa ninachokipenda kuhusu hekalu ni kwamba miongoni mwa wale wanaohudhuria hakuna tofauti za kimali, cheo, au wadhifa wa aina yoyote. Sisi sote tuko sawa mbele ya Mungu. Kila mtu anavalia nguo nyeupe kumaanisha kwamba sisi ni watu safi na wenye haki.19 Kila mmoja huketi upande kwa upande na hamu mioyoni mwao kuwa wana na mabinti wastahiki wa Baba wa Mbinguni mwenye upendo.

Picha
Chumba cha kufunganishwa cha hekalu

Hebu fikiria, kote ulimwenguni wanawake na wanaume wanaweza kupitia “maagizo na maagano matakatifu yanayopatikana katika mahekalu matakatifu … na kurudi katika uwepo wa Mungu na … na kunganishwa milele.”20 Wanafanya haya katika chumba kitakatifu cha kufunganisha kinachopatikana kwa waumini wote wastahiki hekaluni. Baada ya wao kufanya maagano haya, wanaweza, “kujiona hekaluni” kwenye vioo vinavyoangaliana ana kwa ana. “Pamoja vioo vya hekalu huonyesha mbele na nyuma picha zinazoonekana kufululizika hadi milele.”21 Picha hizi hutusaidia kutafakari wazazi, kina babu, na vizazi vilivyopita. Vinatusaidia kutambua maagano matakatifu ambayo hutuunganisha na vizazi vyote vijavyo. Hili ni muhimu mno, na huanza wakati unapojiona hekaluni.

Picha
Vioo katika chumba cha kufunganishwa cha hekalu

Rais Howard W. Hunter alitushauri “zingatia mafundisho makuu yaliyomo katika sala kuu ya kuweka wakfu Hekalu la Kirtland, sala ambayo Nabii Joseph Smith alipewa kwa kupitia ufunuo. Ni sala ambayo inazidi kujibiwa juu ya kila mmoja wetu binafsi, juu yetu kama familia, na juu yetu kama binadamu kwa sababu ya nguvu za ukuhani ambazo Bwana ametupa tutumie katika mahekalu Yake matakatifu.”22 Tutafanya vyema kujifunza sehemu ya 109 ya Mafundisho na Maagano na kufuata ushauri wa Rais Hunter “kuanzisha hekalu la Bwana kama ishara kuu ya uumini [wetu].”23

Hekaluni pia ni mahala pa kukimbilia, kutoa shukrani, na kuelewa, kwamba [sisi] tunaweza kukamilishwa …na “katika mambo yote yahusuyo ufalme wa Mungu juu ya dunia.”24 Maishani mwangu pamekuwa mahali pa utulivu na amani katika dunia ambayo kwa kweli iko katika vurugu.25 Ni ajabu kuacha shida za dunia kando katika yale mazingira takatifu.

Mara nyingi hekaluni, na tunapofanya utafiti wa historia ya familia, huwa tunahisi misukumo na kuwa na hisia kutoka kwake Roho Mtakatifu.26 Mara nyingine hekaluni, pazia kati yetu na wale walio huo upande mwingine huwa nyembamba mno. Huwa tunapata usaidizi wa ziada katika juhudi zetu za kuwa wokozi kwenye Mliman Sayuni.

Miaka kadhaa iliyopita hekaluni kule Amerika ya Kati, mke wa mmoja wa aliye sasa Kiongozi Mkuu Mwenye Mamlaka aliyestaafu alimsaidia baba, mama, na watoto wao kupokea maagano ya milele katika chumba cha kufunganisha ambako vioo vya hekaluni vipo. Walipokuwa wakimalizia na wakiwa wanatazama vioo vile, aligundua kulikuwepo na sura kwenye kioo ambayo haikuwepo chumbani. Alimwuliza mama na akaja kujua kwamba binti yake alikuwa ameaga na hivyo basi hakuwepo. Kisha binti aliyeaga alishirikishwa kupitia mwakilishi katika agizo hilo takatifu.27 Usije ukadhalilisha usaidizi unaotolewa mahekaluni kutoka ule upande mwingine wa pazia.

Tafadhalini mfahamu namna gani kwa bidii tunatamani kwamba kila mtu afanye mabadiliko yoyote yanayohitajika kuhitimu kuingia hekaluni. Kwa maombi fanya mapitio ya mahali ulipo maishani, utafute uongozi wa Roho, na uzungumze na askofu wako kuhusu wewe kujitayarisha kwenda hekaluni. Rais Thomas S. Monson amesema, “Hakuna lengo muhimu zaidi kwako kushighulikia kuliko kuwa mstahiki kuingia hekaluni.”28

Mwokozi ni “Jiwe Kuu Lisilohamishika la Pembeni la Imani Yetu na Kanisa Lake”

Nilipata nafasi ya kushiriki na Rais Henry B. Eyring katika kuweka wakfu tena kwa Hekalu la Suva Fiji miezi miwili iliyopita. Ilikuwa tukio maalum, na takatifu. Ujasiri wa Rais Eyring na misukumo ya nguvu ya kiroho iliruhusu kuweka wakfu tena kuendelea huku kukiwepo na kimbunga kibaya zaidi ambacho kimewahi rekodiwa katika Nusu Tufe ya Kusini Ulinzi wa kimwili na kiroho ulitolewa kwa vijana, wamisionari, na waumini.29 Mkono wa Bwana ulionekana wazi wazi. Kuweka wakfu tena kwa Hekalu la Fiji Suva kulikuwa kimbilio kutokana na dhoruba. Mara nyingi tunapopitia shida za maisha, tunashuhudia mkono wa Bwana katika kutupa ulinzi wa milele.

Kuwekwa wakfu kwa awali kwa Hekalu la Fiji Suva ilikuwa tarehe 18 Juni , 2000, kulikuwa pia kwa ajabu. Wakati hekalu lilikaribia kumalizika, wabunge walitekwa nyara na kundi la waasi. Jijini Suva, Fiji, kuliporwa na kuchomwa. Jeshi ilitangaza sheria ya kijeshi.

Kama Rais wa Eneo, niliandamana na wale marais wanne wa kigingi kule Fiji na kukutana na wakuu wa majeshi katika kambi ya Queen Elizabeth. Baada ya kueleza mapendekezo yetu ya kuweka wakfu, walituunga mkono lakini walikuwa na wasiwasi kuhusu usalama wa Rais Gordon B. Hinckley. Walipendekeza shughuli ya kuweka wakfu ndogo bila shughuli zozote nje ya hekalu, kama vile sherehe ya jiwe la pembeni. Walisisitiza kwamba yeyote ambaye angekuwepo nje ya hekalu kuna uwezekano angekuwa angelengwa na vurugu.

Rais Hinckley aliidhinisha kikao kidogo cha kuweka wakfu kukiwa tu na urais mpya wa hekalu na viongozi wachache wa mitaa; wengine hawakuwa wamealikwa kwa sababu ya hatari zilizokuwepo. Hata hivyo, kwa msisitizo alisema, “Ikiwa tutaweka wakfu hekalu, tutakuwa na sherehe ya jiwe la kona kwa sababu Yesu Kristo ni jiwe la kona, na hili ni Kanisa lake.

Wakati ambapo kweli tulienda nje kwa sherehe ya jiwe la kona, hapakuwepo na watu wasio waumini wa kanisa, watoto, wanahabari, au watu wengine. Lakini nabii mwaminifu alionyesha ahadi yake yenye ujasiri na isiyoyumbayumba.

Baadaye Rais Hinckley, akizungumza kumhusu Mwokozi, alisema: “Hakuna yeyote aliye sawa Naye. “Kamwe hakujakuwepo. “Kamwe hakutakuwepo. Shukrani kwa Mungu kwa ajili ya zawadi ya Mwana Wake Mpendwa, ambaye aliutoa uzima Wake kwamba sisi tuweze kuishi na ambaye ni jiwe la pembeni, lisilohamishika la imani yetu na Kanisa Lake.”30

Ndugu na dada, ninaomba kwamba kila mmoja wetu aweze kumstahi Mwokozi na kufanya mabadiliko ili “tujione katika mahekalu Yake matakatifu.” Katika kufanya hivyo, tunaweza kutekeleza mipango Yake takatifu na kujitayarisha pamoja na familia zetu kwa baraka zote Bwana na Kanisa Lake linaweza kutoa katika maisha ya sasa na ya milele. Ninatoa ushuhuda wangu wa hakika kwamba Mwokozi yu hai. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona Mafundisho na Maagano 112:30–32.

  2. Hekalu la 12, Hekalu la London England, liliwekwa wakfu Septemba 7, 1958.

  3. Mafundisho na Maagano 110:6–7.

  4. Shelly Senior, barua pepe, Apr. 6, 2015.

  5. Thomas S. Monson, “The Holy Temple—a Beacon to the World,”Liahona,May 2011, 93.

  6. Ona Isaya 2:2.

  7. Ona Obadia 1:21.

  8. Ona 1 Petro 4:6.

  9. Ona Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith (2007), 409.

  10. Ona Teachings of Presidents of the Church: Wilford Woodruff (2004), 177, 192–93.

  11. Mafundisho na Maagano 97:15; ona pia mstari wa 17.

  12. Isaya 1:18.

  13. Yeremia 31:34.

  14. Ona Mafundisho na Maagano 59:23.

  15. Zaidi ya sifu inayashikiliwa na watu wazima waliopata endaumenti, sifu ya matumizi ya muda kwa ubatizo wa wafu inaweza kutolewa kwa vijana na watu wazima ambao hawajapata endaumenti walio wastahiki. Sifu zote mbili zinahitaji sahihi ya anayepokea akidhibitisha ustahiki wake mwenyewe. Sifu ya matumizi ya muda ni halali kwa muda wa mwaka mmoja na inatoa nafasi kwa uaskofu kujadili na kila mtu ustahiki wao kila mwaka.

  16. Teachings of Presidents of the Church: Brigham Young (1997), 32.

  17. Ona Mafundisho na Maagano 58:42.

  18. Matendo 10:34; ona pia Moroni 8:12; Mafundisho na Maagano 1:35; 38:16.

  19. Ona Mafundisho na Maagano 100:16.

  20. “The Family: A Proclamation to the World,” Liahona, Nov. 2010, 129.

  21. Gerrit W. Gong, “Vioo vya Hekalu vya Milele: A Testimony of Family,” Liahona, Nov. 2010, 37.

  22. Teachings of the Presidents of the Church: Howard W. Hunter (2015), 183.

  23. Teachings: Howard W. Hunter, 178.

  24. Ona Mafundisho na Maagano 97:13–14.

  25. Ona Mafundisho na Maagano 45:26–27.

  26. Tunarejelea kila mara haya kama Roho ya Eliya. Rais Russell M. Nelson amefundisha kwamba Roho ya Eliya ni “dhihirisho la Roho Mtakatifu akishuhudia hali takatifu ya familia” (“Nyakati Mpya ya Mavuno,” Ensign, Mei 1998, 34).

  27. Imeshirikiwa kwa Idhini.

  28. Thomas S. Monson, “Hekalu Takatifu—Kioleza kwa Dunia,” 93.

  29. Wamisionari na vijana walioletwa kutoka visiwa vya nje walipewa makazi katika shule salama za Kanisa na majengo ya Kanisa na walikuwa salama kutokana na madhara mabaya ya Kimbunga Winston.

  30. Gordon B. Hinckley, “Mawe ya Kona Manne ya Imani Liahona, Feb. 2004, 4–5.