2010–2019
Kesho Bwana Atafanya Miujiza miongoni Mwenu
Aprili 2016


Kesho Bwana Atafanya Miujiza miongoni Mwenu

Endelea kupenda. Endelea kujaribu. Endelea na uaminifu. Endelea kuamini. Endelea kukua. Mbingu zinakushangilia leo, kesho, milele.

Ndugu na kina dada, je mnatambua—mnafahamu hata kidogo au mna fununu yoyote—jinsi sisi tunawapenda? Kwa saa 10 ninyi mtatazama, mkitazama uso mmoja kwenye mimbari hii mmoja baada ya mwingine, lakini kwa saa 10, sisi tuliokaa nyumba ya mimbari, tunawatazama ninyi. Mnatuchangamsha hata kwenye kitovu cha nafsi zetu, iwe ni 21,000 katika Kituo cha Mikutano, ama umati katika majumba ya mikutano na makanisani, ama mamilioni mkiwa nyumbani kote ulimwenguni, labda mmekusanyika karibu na skrini ya kompyuta ya familia. Hapa mpo, kule mpo, saa baada saa, katika mavazi yenu maridadi ya Sabato, mkiwa nadhifu. Mkiimba na kusali. Mkisikiliza na mkiamini. Ninyi ni muuijiza katika Kanisa hili. Tunawapenda.

Ni mkutano mzuri jinsi gani ambao tumekuwa nao. Tumebarikiwa na uwepo wa Rais Thomas S. Monson na jumbe za kinabii. Rais, tunakupenda, tunakuombea, tunakushukuru, na juu ya haya yote, tunakukubali. Tunashukuru kwa kufundishwa wewe na washauri wako wa ajabu na viongozi wengi sana wanaume kwa wanawake. Tumesikia muziki usio na kifani. Tumeombewa kwa dharura na kusihiwa. Hakika Roho wa Bwana amekuwa kwa wingi. Ni wikiendi nyenye maongozi jinsi gani katika kila njia.

Sasa, mimi naona shida kadhaa. Moja ni ukweli kwamba mimi ndiye mtu pekee niliyesimama kati yenu na barafu mnayokuwa nayo tayari kwa ajili ya kufunga mkutano mkuu. Ile shida ingine ni kile kilichopo katika picha niliyoiona majuzi katika Intaneti.

Picha
Dinosau akiwafukuza watoto

Naomba msamaha kwa watoto wote ambao kwa sasa wanajificha chini ya sofa, lakini ukweli wa mambo ni kwamba hakuna mmoja wetu anayetaka kesho kuharibu hisia nzuri tulizozipata wikiendi hii. Tunataka kushikilia hisia za kiroho tulizozipata na mafundisho mazuri tuliyoyasikia. Lakini haiepukiki kwamba baada ya muda wa mbinguni katika maisha yetu, sisi, inabidi, turudi duniani, kumsemo tu, ambako wakati mwingine matatizo mengine yanatukabili tena.

Mtunzi wa Waebrania alituonya juu ya hayo pale aliposema, “Kumbukeni yaliyotokea siku zile za kwanza mlipoangaziwa mwanga, ninyi mlistahimili mateso.”1 Mwanga huo wa awali unaweza kuja kwa njia nyingi, na unaweza kuja kwetu sisi wote. Hakika kila mmisionari ambaye amewahi kuhudumu mara akagundua kwamba maisha ya utumishi hayakuwa sawa na yale ya kwenye chuo cha mafunzo ya umisionari. Hata kwetu sisi pia baada ya kuondoka katika kipindi kitamu cha hekalu au hasa kumalizia sehemu ya mkutano wa kiroho wa sakramenti.

Kumbuka kwamba Musa alishuka toka kwenye tukio la kipekee la Mlima Sinai, aliwakuta watu wake “wamejiharibu wenyewe” na “wakageuka ghafla.”2 Pale walikuwa kwenye chini ya mlima, kwa bidii wakitengeneza dama wa dhahabu ili wamwabudu, muda ule ule ambao Yehova, katika kilele cha mlima, alikuwa akimwambia Musa, “Usiwe na miungu wengine ila mimi,” na “Usijifanyie sanamu yeyote ya kuchonga.”3 Musa hakuwa na furaha na kundi lake la Waisraeli lililokuwa likiyumbayumba siku ile!

Wakati wa utumishi Wake duniani, Yesu aliwachukua Petro, Yakobo na Yohana kwenda kwenye Mlima wa Kugeuka Sura, ambako, maandiko yanasema, “Uso wake ukang’aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru.”4 Mbingu zikafunguka, manabii wakale wakaja, na Mungu Baba akanena.

Baada ya tukio hili la kiselestia, Yesu alikuja kupata nini chini ya mlima? Sawa, kwanza alikuta mabishano miongoni mwa wafuasi wake na maadui zao juu ya baraka shinde iliyotolewa kwa kijana mdogo. Kisha Yeye akajaribu kuwashawishi wale Kumi na Wawili—bila mafanikio, yamkini—kwamba muda mfupi angetolewa kwa watawala ambao wangemuua. Kisha mtu mmoja akamkumbusha Yeye kodi Yake iliyotakiwa kulipwa, ambayo ililipwa mara moja. Kisha Yeye aliwakemea baadhi ya ndugu kwa sababu walikuwa wakibishana kuhusu nani angekuwa mkuu zaidi katika ufalme Wake. Haya yote yalimfanya aseme, “Enyi kizazi kisicho na imani, … Nitakaa nanyi mpaka lini?”5 Alikuwa na nafasi ya kuuliza swali hilo zaidi ya mara moja wakati wa huduma Yake. Haishangazi Yeye alitamani maombi ya upweke kwenye vilele vya milima!

Baada ya kutambua kwamba sisi wote yatupasa kuja chini kutoka kwa matukio ya kileleni kuja kwenye maisha ya kawaida, naomba kutoa faraja hii wakati mkutano mkuu unahitimishwa.

Kwanza katika yote, kama katika siku zetu za usoni unaweza kuona mapungufu si tu kwa wale walio karibu nawe lakini pia kuona mambo katika maisha yako mwenyewe ambayo bado hayalingani na jumbe ulizozisikia wikiendi hii, usifadhaike na wala usikate tamaa. Injili, Kanisa, na mikusanyiko hii ya kila mwaka inakusudia kutoa tumaini na maongozi. Inakusudiwa kutoa tumaini na msukumo, na siyo kukatisha tamaa. Adui pekee, adui wetu sisi sote, angejaribu kutushawishi kwamba maadili yaliyoainishwa kwenye mkutano mkuu yanafadhaisha na si ya kweli, kwamba watu hawaendelei, kwamba hakuna hata mmoja awezaye kuendelea. Na kwa nini Luciferi atoe kauli kama hiyo? Kwa sababu anajua yeye hawezi kuendelea, kwamba yeye hawezi kusonga mbele, kwamba hata mwisho wa ulimwengu yeye hataweza kamwe kuwa na siku za usoni angavu. Ni mtu mwenye huzuni mkubwa aliyefungwa kwa kamba za milele, na anawataka ninyi muwe na huzuni pia. Vyema, usinaswe na hilo. Pamoja na zawadi ya Upatanisho na nguvu za mbinguni kutusaidia, sisi tunaweza kuendelea, na kitu kizuri kuhusu injili ni kwamba tunapata tuzo kwa ajili ya kujaribu, hata kama hatufanikiwi kila mara.

Palipokuwa na mabishano katika Kanisa la kale kuhusu nani aliyestahili baraka za mbinguni na nani hakustahili, Bwana alimwambia Nabii Joseph Smith, “Kwani amini nawaambia, [vipawa vya Mungu] hutolewa kwa manufaa ya wale ambao hunipenda Mimi na hushika … amri zangu, na [kwa wale] watafutao kufanya haya.”6 Lo, nasi wote tunashukuru “na … kutamani kufanya hivyo”! Hiyo imekuwa ni kuokoa maisha kwa sababu wakati mwingine hilo ndilo tunaloweza kutoa! Tunapata kiasi cha faraja katika ukweli kwamba kama Mungu angewatuza tu waaminifu, Asingekuwa na orodha kubwa ya mgawo.

Hivyo tafadhali kumbuka kesho, na siku zote baada ya hapo, kwamba Bwana huwabariki wale ambao wanataka kuendelea, ambao wanakubali haja ya amri na kujaribu kuzitii, wanaothamini tabia za Kristo na kujaribu kwa uwezo wao wote kuzipata. Kama unajikwaa katika hiyo njia, kila mtu hujikwaa; mwite Mwokozi akusaidie, na endelea kusonga mbele. Kama unaanguka, omba nguvu Zake. Itana kama vile Alma, “Ewe Yesu, … nihurumie.”7 Yeye atakusaidie kusimama tena. Yeye atakusaidia kutubu, kujirekebisha, kusahihisha chochote unachohitaji kusahihisha, na endelea kusonga mbele. Punde utapata mafanikio unayotaka.

“Kama vile unavyotaka kutoka kwangu na hivyo ndivyo itakavyokuwa kwako,” Bwana amesema.

“Weka imani yako katika Roho yule ambaye huongoza kufanya mema—ndiyo, kufanya haki, kutembea kwa unyenyekevu, kuhukumu kwa haki. …

“… [Ndipo] mambo yote ambayo unahitaji kutoka kwangu [katika] haki, … utapokea.8

Ninayapenda mafundisho hayo! Yanasema tena kwamba tutabarikiwa kwa ajili ya matumainio yetu ya kutenda mema, hata pale tunapojaribu kufanya hivyo. Na inatukumbusha kwamba kustahili baraka hizo, lazima tuhakikishe tunazikubali dhidi ya nyingine: lazima tutende kwa haki, kamwe tusirazini, na kamwe tusionee; tutembee kwa unyenyekevu, kamwe bila kiburi, kamwe bila jeuri; tuhukumu kwa haki, kamwe bila ubinafsi, kamwe bila uovu.

Akina kaka na dada, amri kuu ya kwanza zaidi ya zote za milele ni kumpenda Mungu kwa moyo wetu wote, uwezo, akili, na nguvu—hiyo ndiyo amri kuu ya kwanza. Lakini ukweli mkuu wa kwanza wa milele yote ni kwamba Mungu anatupenda sisi kwa moyo Wake wote, nguvu, akili na uwezo. Upendo huo ni jiwe la msingi wa milele, na linapaswa kuwa jiwe la msingi wa maisha ya kila siku. Kwa kweli ni kwa uhakika huo ukituchoma katika nafsi zetu ndipo tunaweza kuwa na tumaini la kuendelea kujaribu kujiboresha, kuendelea kuomba msamaha kwa ajili ya dhambi zetu, na kuendelea kutenda wema kwa jirani zetu.

Rais George Q. Cannon aliwahi kufundisha: “Bila kujali ukubwa wa majaribu, umaarufu wetu, ukubwa wa shida, [Mungu] hatatuacha. Hajawahi kutuacha, na hatatuacha kamwe. Hawezi kufanya hivyo. Siyo tabia Yake [kufanya hivyo] … Yeye atasimama [daima] karibu nasi. Tunaweza kupitia kwenye tanuru la moto; tunaweza kupitia kwenye kina kirefu; lakini hatutashindwa wala kuzidiwa. Tutayashinda majaribu na matatizo haya yote tukiwa bora na wasafi kutokana nayo.”9

Sasa, uchaji Mungu huu ukipiga mwangwi kwa kudumu katika maisha yetu, umejidhihirisha kwa usafi na kikamilifu katika maisha, kifo, na Upatanisho wa Bwana Yesu Kristo, tunaweza kuepuka matokeo yote ya dhambi na ujinga—wetu wenyewe au wa wengine—kwa njia yoyote iwezayo kuja kwetu katika maisha ya kila siku. Kama tunautoa moyo wetu kwa Mungu, ikiwa tunampenda Bwana Yesu Kristo, ikiwa tutafanya vyema tuwezavyo kushika injili, basi kesho—na kila siku—itaendelea kuwa ya ajabu, hata kama hatutambui hivyo kila wakati. Kwa nini? Kwa sababu Baba yetu wa Mbinguni anataka iwe hivyo! Anataka kutubariki. Uzima wa milele wenye kutosheleza, utele ndiyo hasa dhamira Yake ya mpango wa huruma kwa ajili ya watoto Wake! Ni mpango unaotegemea ukweli “kwamba vitu vyote vinafanyakazi pamoja kwa mazuri kwa wale wampendao Mungu.”10 Kwa hivyo endelea kupenda. Endelea kujaribu. Endelea na uaminifu. Endelea kuamini. Endelea kukua. Mbingu zinakushangilia leo, kesho, milele.

“Kwani wewe hujajua? hujasikia?” Isaya alilia.

“[Mungu] huwapa nguvu walioanguka, na kwa wale wasio na nguvu huwaongezea. …

“… Wale wanaomsubiri [Yeye] watarejesha nguvu zao; watakuwa na mabawa kama tai. …

“Kwani … Bwana … Mungu atashika mikono [yao] ya kulia, akiwaambia [wao], Msiogope; nitawasaidieni.”11

Ndugu na dada, naomba Baba wa Mbinguni mwenye upendo atubariki kesho ili tukumbuke tulivyojisikia leo. Na Yeye atubariki tujitahidi kwa uvumilivu na kwa bidii kwa yale tuliyoyasikia yakihubiriwa katika wikiendi hii ya mkutano mkuu, tukijua kwamba upendo Wake mkuu na msaada usio na kikomo utakuwa pamoja nasi tunapopata shida—hapana, atakuwa nasi hususani tunapojitahidi.

Kama viwango vinaonekana kuwa juu na maboresho binafsi yanayohitajika siku za usoni zinaonekana kuwa hayawezekani, mkumbuke hamasa ya Yoshua kwa watu wake walipokumbana na siku za usoni ngumu. “Jitakaseni wenyewe,” alisema, “kwani kesho Bwana atafanya miujiza miongoni mwenu.”12 Nami natangaza ahadi hiyo hiyo. Ndiyo ahadi ya mkutano mkuu huu. Ndiyo ahadi ya Kanisa hili. Ndiyo ahadi ya Yule ambaye hutenda miujiza hiyo, ambaye Yeye Mwenyewe ni “Mshauri wa Ajabu, Mwenyezi Mungu, … Mfalme wa Amani”13 Juu Yake mimi natoa ushahidi. Juu Yake mimi ni shahidi. Na Kwake mkutano mkuu huu unasimama kama ushuhuda wa kazi Yake inayoendelea katika hizi siku kuu za mwisho. Katika jina la Yesu Kristo, amina.