2010–2019
Geukia Kitabu, Mgeukie Bwana
Oktoba 2016


Geukia Kitabu, Mgeukie Bwana

Je, unaweza kuona Kitabu cha Mormoni kama jiwe lako la tao, kitovu cha nguvu yako ya kiroho?

Mary Elizabeth Rollins

Katika mawazo yangu, ninawafikiria nyinyi kizazi kinachoinuka mnaotazama au kusikiliza kikao hiki cha mkutano mkuu mahali fulani katika ulimwengu. Ningependa kushiriki hadithi ya kweli na nyinyi, hadithi ambayo inaweza kuwa mfano na somo. Inaweza kuwaonyesha jinsi ya kusogea karibu na Bwana na kupata uwezo mkubwa wa kukinza majaribu.

Hii ni hadithi ya msichana mdogo, anayeishi huko New York, ambaye kabla ya umri wa miaka mitatu alipoteza baba yake wakati mashua yake ilizama kwenye ziwa kubwa. Yeye, mama yake, kaka, na dada mdogo walihamia mji mpya katika jimbo lingine ili kuishi na shangazi na mjomba wake. Muda fulani baada ya familia hiyo kuwasili, wamisionari na washiriki wa dini iliopangwa upya walifika mjini mwao na habari ya tukufu ya Urejesho wa injili. Walielezea hadithi ya ajabu ya malaika akipeana rekodi ya kale kwa kijana mmoja jina lake Joseph Smith, rekodi ambayo alikuwa ametafsiri kwa uwezo wa Mungu. Wawili kati ya wageni hao, Oliver Cowdery na John Whitmer, kwa kweli walikuwa wameona kurasa za chuma zilizochongwa za rekodi za kale kwa macho yao wenyewe, na Whitmer akashuhudia kwamba aliweza kuyashika mabamba za dhahabu katika mikono yake mwenyewe. Rekodi hii ilikuwa imechapishwa hivi majuzi, na ndugu Whitmer alikuja pamoja na kitabu. Jina la kitabu, bila shaka, lilikuwa Kitabu cha Mormoni

Wakati Mary mwenye umri wa miaka 12 aliposikia wamisionari wakizungumza kuhusu kitabu, alikuwa na hisia maalum katika moyo wake. Ijapokuwa Kitabu cha Mormoni kilikuwa kizito na kurasa nyingi, Mary alitamani kukisoma. Wakati Ndugu Whitmer alipoondoka, alitoa nakala moja ya thamani ya kitabu hicho kwa Ndugu Isaac Morley, ambaye alikuwa rafiki wa mjomba wa Mary na kiongozi katika kanisa jipya.

Mary alirekodi baadaye: “Nilikwenda nyumbani mwa [Ndugu Morley] … na nikaomba kukiona Kitabu hicho; [Yeye] alikiweka katika mkono wangu, [na] nilipokuwa nikikitazama, nilihisi tamaa ya kama kukisoma, ambapo sikuweza kujizuia kumuuliza kuniruhusu kuipeleka nyumbani kukisoma … Alisema … Hakuwa amepata muda wa kusoma sura ndani yake mwenyewe, na lakini wachache wa ndugu walikuwa wameiona, lakini nilisihi kwa bidii, hatimaye alisema, ‘mtoto, kama utaleta kitabu hiki nyumbani kabla ya kifungua kinywa kesho asubuhi, unaweza kukichukua.’”

Picha
Mary Elizabeth Rollins akisoma

Mary alikimbia nyumbani na kukaa karibu usiku wote akisoma. Asubuhi iliofuata aliporudisha kitabu, Ndugu Morley alisema, “Nadhani hukusoma mengi ndani yake” na “Siamini unaweza kuniambia neno moja juu yake.” Maria alisimama wima na kukariri kutoka kwa kumbukumbu mstari wa kwanza wa Kitabu cha Mormoni. Kisha alimwambia hadithi ya nabii Nefi. Mary baadaye aliandika, “aliniangalia kwa mshangao, akasema, ‘mtoto, peleka kitabu hiki nyumbani na umalize kukisoma, naweza kusubiri.’”

Muda mfupi baadaye, Mary alimaliza kusoma kitabu na alikuwa mtu wa kwanza katika mji wake kusoma kitabu chote. Alijua ni kweli na kwamba kilitoka kwa Baba wa Mbinguni. Alipogeukia kitabu, alimgeukia Bwana.

Mwezi mmoja baadaye, mgeni maalum alikuja nyumbani kwao. Hii ndio kile Mary aliandika kuhusu tukio lake la ajabu siku hiyo: “Wakati [Joseph Smith] aliniona alinitazama sana. … Baada ya dakika moja au mbili  …alinipa baraka kubwa … na kunifanyia zawadi ya kitabu, na kusema kwamba atampatia Ndugu Morley nyingine [nakala]. … Sisi sote tulihisi kwamba alikuwa mtu wa Mungu, kwa maana alizungumza na uwezo, na kama mmoja aliye na mamlaka.”

Msichana huyu mdogo, Mary Elizabeth Rollins, aliona miujiza mengine mengi katika maisha yake na daima aliweka ushuhuda wake wa Kitabu cha Mormoni.1 Hadithi hii ina maana maalum kwangu kwa sababu yeye ni shangazi yangu mkuu wa nne. Kupitia kwa mfano wa Mary, pamoja na matukio mengine katika maisha yangu, nimejifunza kwamba mtu kamwe si kijana sana kutafuta na kupokea ushuhuda wa kibinafsi wa Kitabu cha Mormoni.

Jiwe la Tao la Ushuhuda Wako

Kuna somo binafsi kwa ajili yenu katika hadithi ya Mary. Kila mmoja wenu wavulana, wasichana, na watoto mnaweza kuwa na hisia sawa na zake. Unaposoma Kitabu cha Mormoni na kuomba kwa hamu ya kujua ni kweli, wewe pia unaweza kupokea hisia hiyo hiyo katika moyo wako ambayo Mary alipokea. Unaweza kupata pia kwamba unaposimama na kushuhudia kuhusu Kitabu cha Mormoni, utahisi roho ile ile ya uthibitisho. Roho Mtakatifu atazungumza na moyo wako. Unaweza pia kuhisi roho hiyo hiyo ya uthibitisho unapowasikia wengine wakishiriki ushuhuda wao wa Kitabu cha Mormoni. Kila moja ya shuhuda hizi za kiroho zinaweza kufanya Kitabu cha Mormoni kuwa jiwe la tao la ushuhuda wako.

Acha nieleze. Nabii Joseph Smith, ambaye alitafsiri Kitabu cha Mormoni kwa “kipawa na nguvu za Mungu,” alielezea Kitabu cha Mormoni kuwa “ndicho kitabu sahihi duniani, na ndilo jiwe la tao la dini yetu.”2

Tangu uchapisho wa kwanza wa Kitabu cha Mormoni mnamo 1830, zaidi ya nakala milioni 174 zimechapishwa katika lugha 110 tofauti, kuthibitisha kwamba Kitabu cha Mormoni bado ndicho jiwe la tao la dini yetu. Lakini hii ina maana gani kwa kila mmoja wenu?

Picha
Jiwe la tao ndio kitovu hasa

Katika suala la usanifu, jiwe la tao ni kipengele kikuu katika lango la tao. Ni jiwe lenye umbo wa kabari pale katika kitovu na sehemu ya juu ya tao. Ni mojawapo ya mawe muhimu zaidi kwa sababu huimarisha pande za tao, ili kuzuia kubomoka. Na ni muundo wa kimsingi unaohakikisha lango, au njia ya chini, inapitika.

Picha
Jiwe la tao katika tao

Katika suala la injili, ni kipawa na baraka kutoka kwa Bwana kwamba jiwe la tao la dini yetu, ni kitu kinachoonekana na kushikika kama Kitabu cha Mormoni na kwamba unaweza kukishikilia na kukisoma. Je, unaweza kuona Kitabu cha Mormoni kama jiwe lako la tao, kitovu cha nguvu yako ya kiroho?

Rais Ezra Taft Benson alifafanua juu ya mafundisho hayo ya Joseph Smith. Alisema: “Kuna njia tatu ambazo kwazo Kitabu cha Mormoni ni jiwe la kiungo la tao la dini yetu. Ndio jiwe la kiungo la tao katika ushahidi wetu wa Kristo. Ndio jiwe la kiungo la tao la mafundisho yetu. Ni jiwe la kiungo la tao la ushuhuda wetu.

Rais Benson alifundisha zaidi: “Kitabu cha Mormoni hutufundisha ukweli [na] hutoa ushahuda wa Kristo … Lakini kuna kitu kingine zaidi. Kuna uwezo katika kitabu hiki ambao utatiririka katika maisha yako wakati utaanza kujifunza kitabu hiki kwa bidii. Utapata uwezo mkuu wa kushinda majaribu … Utapata uwezo wa kukaa katika njia iliyosonga na nyembamba.”3

Ushuhuda Wangu Binafsi

Kwangu, Kitabu cha Mormoni kilikuwa jiwe la kiungo la teo la ushuhuda wangu kwa miaka kadha na kupitia kwa uzoefu kadha. Uzoefu moja wa nguvu katika kutengeneza ushuhuda wangu ulitokea nilipokuwa mmisionari kijana nikihudumu katika eneo langu la kwanza la: Kumamoto, Japan. Mimi na mwenzangu tulikuwa tukitembelea nyumba hadi nyumba. Nilikutana na bibi ambaye kwa ukarimu alitukaribisha kwenye lango la nyumba yake, iitwayo genkan kwa Kijapani. Alitupatia kinywaji baridi katika siku yenye joto. Nilikuwa sijawa Japan kwa muda mrefu sana, na hiyo majuzi nilikuwa nimekamilisha kusoma Kitabu cha Mormoni na nilikuwa nikisali ili kujua kwa hakika kwamba kilikuwa kweli.

Kwa sababu ya ugeni wangu Japani, sikuweza kuzungumza Kijapani vizuri sana. Kwa kweli, sidhani mwanamke huyu alielewa mengi ya yale niliyokuwa nikisema. Nilianza kumfundisha kuhusu Kitabu cha Mormoni, nikielezea jinsi Joseph Smith alipokea kutoka kwa malaika rekodi za kitambo zilizochorwa katika mabamba na jinsi alivyozitafsiri kwa uwezo wa Mungu.

Niliposhiriki naye ushuhuda wangu kwamba Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu na ushahidi mwingine wa Yesu Kristo, nilipokea hisia ya nguvu, ikifuatana na hisia changamfu ya faraja na utulivu ndani ya kifua changu, ambayo maandiko inaeleza kama “moyo wako[uwakao] ndani yako.”4 Hisia hii ilinithibitishia kwa njia ya nguvu kwamba Kitabu cha Mormoni kweli ni neno la Mungu. Wakati huo, hisia zangu zilikuwa kali sana kiasi kwamba machozi yalitoka machoni mwangu nilipoongea na huyu bibi Mjapani. Sijawahi kusahau hisia maalum ya siku hiyo.

Ushuhuda Wako Binafsi

Kila mmoja wenu pia anaweza kupokea ushuhuda binafsi wa kitabu hiki! Je, mnatambua kwamba Kitabu cha Mormoni kiliandikwa kwa ajili yenu—na kwa siku yenu? Kitabu hiki ni moja ya baraka ya kuishi katika kile tunachokiita maongozi ya Mungu wa nyakati jalivu. Ingawa Kitabu cha Mormoni kiliandikwa na waandishi wa kale wenye maongozo—wengi ambao walikuwa manabii—wao na watu wa siku zao hawakuwa na faida ya kumiliki kitabu kizima. Sasa unapata kwa urahisi rekodi takatifu karibu nawe ambayo manabii, makuhani, na wafalme walithamini, kukumbatia na kuhifadhi! Una faida ya kushikilia katika mikono yako Kitabu cha Mormoni chote. Cha kushangaza, Moroni, nabii mmoja wa Kitabu cha Mormoni, aliona siku yetu—siku yako. Hata alikuona, kwa maono, mamia ya miaka iliyopita! Moroni aliandika:

“Tazama, Bwana amenionyesha vitu vikubwa na vya ajabu kuhusu  … siku ile ambayo vitu hivi” kumaanisha Kitabu cha Mormoni “kitatokea mbele miongoni mwenu.

“Tazama, ninawazungumzia kama vile mko hapa, lakini hamko. Lakini tazama, Yesu Kristo amenionyesha nyinyi kwangu, na ninajua yale mnayofanya.”5

Ili kusaidia Kitabu cha Mormoni kuwa jiwe la kiungo la tao la ushuhuda wako, nakupatia changamoto. Hivi karibuni nilijifunza kwamba katika nchi nyingi duniani, vijana hutumia wastani wa saa karibu saba kwa siku kuangalia TV, kompyuta, na simu za rununu.6 Ukiwa na hili akilini, unaweza kuleta mabadiliko kidogo? Je, unaweza kubadili baadhi ya muda wa kutazama—hasa ule uliyotolewa kwa vyombo vya habari vya kijamii, Intaneti, michezo, au televisheni, na kusoma Kitabu cha Mormoni? Ikiwa utafiti nilioelezea si sahihi, unaweza kupata wakati kwa urahisi wa masomo ya kila siku ya Kitabu cha Mormoni hata kama ni kwa dakika 10 tu kwa siku. Unapojifunza kwa njia ambayo itakuruhusu kukifurahia na kukielewa—iwe kwenye kifaa chako au katika njia ya kitabu. Rais Russell M. Nelson hivi karibuni alionya, “Sisi hatupaswi kamwe kufanya kusoma Kitabu cha Mormoni kuonekana kama wajibu wa kutaabisha, kama vile kugugumia dawa chungu inayofaa kumwezwa upesi na kisha kuweka tiki hilo limetimia.”7

Picha
Kijana Akisoma Kitabu cha Mormoni
Picha
Mtoto Akisoma Kitabu cha Mormoni

Kwa wengine wenu watoto wadogo, mnaweza kukisoma pamoja na mzazi, mzazi mkuu, au mpendwa. Kama sura, aya, au sehemu inakuwa vigumu kiasi ya kuondoa tamaa yako ya kusoma, songa mbele kwa nyingine na nyingine. Nakuona ukifuata mfano wa Mary. Nakuona ukipata muda na mahali tulivu pa kusoma Kitabu cha Mormoni. Nakuona ukigundua majibu, ukihisi uongozi, na kupata ushuhuda wako mwenyewe wa Kitabu cha Mormoni na ushuhuda wa Yesu Kristo. Unapogeukia kitabu hiki, Unamgeukia Bwana.

Picha
Kugeukia kitabu hiki

Utajibwaga katika vifungu vya kitabu hiki chenye thamani na kukutana na Mwokozi wako mpendwa, Bwana Yesu Kristo, karibu katika kila ukurasa. Inakadiriwa kuwa hali fulani ya jina Lake linatumika wastani wa mara moja kila aya ya 1.7.8 Hata Kristo mwenyewe alishuhudia ukweli wake katika hizi siku za mwisho, na kusema, “na kama vile Bwana wenu na Mungu wenu aishivyo ni kweli.”9

Ninashukuru kwa mwaliko na ahadi ambayo Bwana ametoa kupitia nabii Moroni kwa kila mmoja wenu—na kwa kila mtu anayesoma Kitabu cha Mormoni. Nakamilisha kwa kusoma mwaliko huu na ahadi na kuongeza ushahidi wangu: “Na mtakapopokea vitu hivi, ningewashauri kwamba mngemwuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la [Yesu] Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli; na ikiwa mtauliza na moyo wa kweli, na kusudi halisi, mkiwa na imani katika Kristo, atawaonyesha ukweli wake kwenu, kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.”10

Natoa ushuhuda wa Urejesho wa injili katika siku hizi za mwisho na wa Kitabu cha Mormoni kama ushahidi wa kuonekana wa Urejesho. Kama vile maneno ya kitabu hiki yalimwongoza msichana mwenye umri wa miaka 12 kukumbatia Kanisa lililorejeshwa la Yesu Kristo karibu karne mbili zilizopita, kweli ambazo utapata pale ndani zitakuinua na kukuongoza katika njia hiyo hiyo. Zitaimarisha imani yako, kujaza nafsi yako na mwanga, na kukuandaa kwa ajili ya siku zijazo ambayo hauna uwezo wa kufahamu.

Ndani ya kurasa za kitabu, utagundua upendo usio na mwisho na neema ya Mungu isiyoeleweka. Unapojitahidi kufuata mafundisho unayoyapata hapo, furaha yako itaongezeka, uelewa wako utaongezeka, na majibu unayotafuta kwa changamoto nyingi zinazoletwa na maisha zitafunguliwa kwenu. Unapogeukia kitabu hiki, Unamgeukia Bwana. Kitabu cha Mormoni ni neno lililofunuliwa la Mungu. Kwa haya ninashuhudia kwa moyo na nafsi yangu, katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona “Mary Elizabeth Rollins Lightner,” Utah Genealogical and Historical Magazine, July 1926, 193–95.

  2. Utangulizi wa Kitabu cha Mormoni

  3. Ezra Taft Benson, “The Book of Mormon—Keystone of Our Religion,” Ensign, Nov. 1986, 5, 7.

  4. Mafundisho na Maagano 9:8.

  5. Mormoni 8:34–35.

  6. Ona American Academy of Pediatrics, “Media and Children,” aap.org.

  7. Russell M. Nelson, “Strengthen the Shepherds” (address given at the general conference leadership meetings, Sept.  28, 2016).

  8. Ona Susan Easton Black, Finding Christ through the Book of Mormon (1987), 16–18.

  9. Mafundisho na Maagano 17:6.

  10. Moroni 10:4; ona pia mistari 3, 5.