2010–2019
Kushinda Ulimwengu
Aprili 2017


Kushinda Ulimwengu

Kushinda ulimwengu si tukio moja la ajabu katika maisha, lakini ni maisha yenye matukio yanayoelezea milele yote.

Miaka mingi iliyopita, Rais David O. McKay alielezea kuhusu tukio njema aliloona alipokuwa akisafiri kwa mashua kuelekea Samoa. Baada ya kushikwa na usingizi, “aliona katika maono kitu kitukufu sana. Kwa umbali,” alisema, “Niliona mji mzuri mweupe. … Miti yenye matunda matamu … na maua yaliyochanuka kamili kila mahali. … Mkusanyiko mkubwa wa watu ulikuwa unakaribia mji. Kila mmoja alivaa vazi refu jeupe. … papo hapo mawazo yangu … yaliangazia juu ya kiongozi wao, na ingawa ningeweza kuona tu umbo la mwili wake  … , nilimtambua mara moja kama Mwokozi wangu! … Mng’aro wa uso wake [ulikuwa] mtukufu. … Amani iliyomzunguka … ilikuwa ya kiungu!”

Rais McKay aliendelea, “mji … ulikuwa wake … Mji wa Milele; na wale waliomfuata walipaswa kuishi kule kwa amani na furaha ya milele.”

Rais McKay alishanga, “[Ni] kina nani? [Hawa watu ni kina nani?]

Anaelezea kile kilichofanyika baadaye:

“Kana kwamba Mwokozi alisoma mawazo yangu, alijibu kwa kuelekeza kwenye [maneno] katika nusu duara … yaliyoonekana juu ya [watu], … yaliyoandikwa kwa dhahabu … :

“‘Hawa Ni Wale Walioshinda Ulimwengu—

“Wale Ambao Wamezaliwa Upya Kwa Kweli!’”1

Kwa miongo kadhaa, nimeyakumbuka maneno hayo: “Hawa ni wale walioshinda ulimwengu.”

Baraka ambazo Bwana amewaahidi wale ambao wameshinda ulimwengu ni za ajabu. “Watavikwa mavazi meupe … na [kutajwa katika] kitabu cha uzima.” Bwana “atayakiri [majina yao] mbele za Baba, na mbele ya malaika Zake.”2 “Kila mmoja atakuwa na “sehemu katika ufufuo wa kwanza,”3 kupokea uzima wa milele,4 wala “kutotoka humo tena”5 kutoka kwa uwepo wa Mungu.

Je, inawezekana kushinda ulimwengu na kupokea baraka hizi? Ndio, kweli

Upendo kwa Mwokozi

Wale walioshinda ulimwengu wanakuwa na upendo mkuu kwa Bwana wetu na Mwokozi, Yesu Kristo.

Kuzaliwa Kwake kwa kiungu, maisha yake makamilifu Upatanisho Wake usio na mwisho huko Gethsemane na Golgotha, ulihakikisha Ufufuo wa kila mmoja wetu. Kupitia kwa toba yetu ya dhati, Yeye pekee Anaweza kutusafisha kutokana na dhambi zetu, kuturuhusu kurudi katika uwepo wa Mungu. “Sisi twampenda kwa maana yeye alitupenda sisi kwanza.”6

Yesu alisema, “Jipeni moyo; mimi nimeushinda ulimwengu.”7

Baadaye Aliongeza, “ninawaambia, kuwa nataka kwamba muushinde ulimwengu.”8

Kushinda ulimwengu si tukio moja la ajabu katika maisha, lakini ni maisha yenye matukio yanayoelezea milele yote.

Inaweza kuanza kama vile mtoto anavyojifunza kuomba na kuimba kwa heshima, “Najaribu kuwa kama Yesu.”9 Inaendelea jinsi mtu anavyosoma maisha ya Mwokozi katika Agano Jipya na kutafakari uwezo wa Upatanisho wa Mwokozi katika Kitabu cha Mormoni.

Kuomba, kutubu, kumfuata Mwokozi, na kupokea neema Yake hutupeleka kwenye ufahamu bora wa kuwepo kwetu hapa na ni nini tutaweza kuwa.

Alma anaelezea kwa njia hii: “Mabadiliko makuu yakafanyika katika mioyo yao, na wakajinyenyekeza na kuweka tumaini lao katika Mungu wa kweli na anayeishi … [kuwa] waaminifu hadi mwisho.”10

Wale ambao wameshinda ulimwengu wanajua kwamba watawajibika kwa Baba yao wa Mbinguni. Kubadilika na kutubu dhambi zetu kwa dhati si kizuizi tena lakini ni ukombozi, kwa kuwa “dhambi [ziwe] nyekundu … [zitakuwa] nyeupe kama theluji.”11

Kuwajibika kwa Mungu

Wale wa ulimwengu wana ugumu wa kuwajibika kwa Mungu—kama mtoto anayesherekea nyumbani mwa wazazi wake wakiwa wamesafiri nje ya mji, kufurahia vitu vya kawaida, kukataa kufikiria juu ya madhara wakati wazazi watakaporudi masaa 24 baadaye. 

Ulimwengu unapenda sana kujihusisha na mtu wa kawaida kuliko kumbadilisha.

Kushinda ulimwengu sio uvamizi wa kimataifa lakini vita vya faragha, vya binafsi, vinavyohitaji kupambana mkono kwa mkono na maadui zetu wa ndani.

Kushinda Ulimwengu unamaanisha kuthamini Amri kuu: “Mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote,na kwa roho yako yote, na kwa akili zako zote.”12

Mwandishi Mkristo C. S. Lewis alielezea kwa njia hii: “Kristo anasema ‘Nipe Yote. Sitaki muda wako mwingi na pesa zako nyingi na kazi zako nyingi: Nakutaka Wewe.’”13

Kushinda ulimwengu ni kuweka ahadi zetu kwa Mungu—ahadi zetu za ubatizo na maagano ya hekalu na kiapo chetu cha uaminifu kwa mwenzi wetu wa milele. Kushinda ulimwengu kunatuongoza kwa unyenyekevu kwenye meza ya sakramenti kila wiki, tukiomba msamaha na kuahidi “kumkumbuka na kushika amri zake” ili kwamba “daima tuwe na Roho wake kuwa na [sisi].”14

Upendo wetu kwa ajili ya siku ya Sabato hauna mwisho wakati milango ya Kanisa imefungwa nyuma yetu, lakini badala yake hufungua milango kwa siku nzuri ya kupumzika, kusoma, kuomba, na kufikia familia na wengine ambao wanahitaji usikivu wetu. Badala ya kusikia nafuu wakati mkutano wa kanisa unapokwisha, kwa matumaini ya kupata televisheni haraka kabla mchezo wa mpira kuanza, mawazo yetu yanabakia juu ya Mwokozi na siku Yake tukufu.

Ulimwengu umevutiwa na mbubujiko mwingi wa sauti za kuvutia na kutongoza.15

Kushinda ulimwengu ni kutegemea sauti moja ambayo inaonya, inafariji, kuelimisha, na huleta amani “si kama ulimwengu utoavyo.”16

Kutokuwa na ubinafsi

Kushinda ulimwengu humaanisha kujigeuza nje, kukumbuka amri ya pili17: “Atakaye kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu.”18 Furaha ya mwenzi wetu ni muhimu sana kuliko burudani yetu wenyewe. Kusaidia watoto wetu kumpenda Mungu na kuweka amri Zake ni kipaumbele cha msingi. Kwa hiari tunashiriki baraka zetu za dunia kupitia zaka, matoleo ya mfungo, na kutoa kwa wale wanaohitaji. Kuweka antena zetu za kiroho zikielekea mbinguni, Bwana hutuongoza kwa wale tunaweza kusaidia.

Ulimwengu hujenga dunia karibu naye, kutangaza wazi: “Nione ikilinganishwa na jirani yangu! Tazama kilicho changu! Angalia jinsi nilivyo muhimu!

Ulimwengu unahudhika kwa haraka, haupendelei, na unadai, hupenda pongezi za umati wa watu, wakati kushinda ulimwengu huleta unyenyekevu, uelewa, uvumilivu, na huruma kwa wale walio tofauti na wewe mwenyewe.

Usalama katika Manabii

Kushinda ulimwengu daima itamaanisha kwamba tutakuwa na baadhi ya imani ambayo inadharauliwa na ulimwengu. Mwokozi alisema:

“Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia.

“Kama mgekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake.”19

Rais Russell M. Monson alisema asubuhi ya leo, “Wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo wako radhi kusimama, kusema, na kuwa tofauti na watu wa ulimwengu.”20

Mfuasi wa Kristo hapati wasiwasi ikiwa maoni juu ya imani yake hajapokea pendwa 1,000 au hata maoni ya kirafiki.

Kushinda ulimwengu ni kutojihusisha na miunganisho wa mtandaoni na kujihusisha zaidi na miunganisho wetu wa mbinguni na Mungu.

Katika kushinda ulimwengu, Mungu Anatupatia usalama tunapofuata mwongozo kutoka kwa manabii na mitume Wake walio hai.

Picha
Rais Monson akiongea

Rais Thomas  S. Monson alisema: “Ulimwengu unaweza kuwa … na changamoto. … [Tunapoenda hekaluni], … Tutaweza kustahimili kila jaribio na kushinda kila majaribu. … Tutajengwa upya na kuimarishwa.”21

Kwa majaribu yanayoongezeka, uharibifu, na upotovu, ulimwengu hujaribu kumdanganya yule mwaminifu ili kupuuza uzoefu muhimu wa kiroho wa maisha ya mtu aliyopitia, kuelezea kama udanganyifu wa kijinga.

Kushinda ulimwengu ni kukumbuka, hata tunapohisi kukata tamaa, wakati tulipohisi upendo wa Mwokozi. Mzee Neal A. Maxwell alielezea mojawapo ya matukio haya kwa njia hii: “Mimi nilikuwa nimebarikiwa, na nilijua kwamba Mungu alijua kwamba mimi nilijua kwamba nimebarikiwa.”22 Ingawa tunaweza kuhisi kusahaulika kwa muda, hatuwezi kusahau.

Kushinda ulimwengu haimaanishi kwamba tuishi maisha ya watawa, yaliyolindwa kutokana na ukosefu wa usawa na ugumu wa maisha. Badala yake, hupanua mtazamo mpana wa imani, kutuvuta kwa Mwokozi na ahadi Zake.

Ingawaje ukamilifu haujakamilika katika maisha haya, kushinda ulimwengu kunaweka matumaini yetu hai kwamba siku moja sisi “tutasimama mbele ya [Mkombozi wetu]; [Na] kuona uso wake kwa furaha,”23 na kusikia sauti yake: “Njoni, mliobarikiwa na Baba yangu, urithini ufalme mliowekewa tayari.”24

Mfano wa Mzee Bruce D. Porter

Mnamo Desemba 28 wa mwaka huu uliopita, mpendwa rafiki yetu na Kiongozi mkuu mwenye Mamlaka, Mzee Bruce D. Porter, alikamilisha maisha yake ya duniani. Alikuwa na umri wa miaka 64.

Nilikutana na Bruce mara ya kwanza tulipokuwa wanafunzi pale kwenye Chuo Kikuu cha Brigham Young. Alikuwa mmoja wa wale bora na werevu zaidi. Baada ya kupokea shahada yake ya udaktari ya kuzingatia mambo ya Urusi kutoka kwa Chuo Kikuu cha Harvard, kufikiria na kuandika kwa Bruce kulimletea umaarufu ambao ungemharibu, lakini utajiri na sifa za ulimwengu hazikuwahi kuziba maono yake.25 Uaminifu wake ulikuwa kwa Mwokozi Wake, Yesu Kristo; kwa mchumba wake wa milele, Susan; kwa watoto wake na wajukuu wake.

Picha
Mzee Porter na familia yake changa

Bruce alizaliwa na kasoro ya figo. Alifanyiwa upasuaji, lakini baada ya muda figo zake ziliendelea kudhoofika.

Muda mfupi baada ya mwito wa Bruce kama Kiongozi Mkuu mwenye Mamlaka mnamo 1995, tulihudumu pamoja na familia zetu huko Frankfurt, Ujerumani, ambapo kazi yake ilihusiana na Urusi na Ulaya Mashariki

Maisha ya Mzee Porter yalibadilika kwa kasi mnamo mwaka wa 1997 wakati figo yake na afya ilipoanza kudhoofika. Familia ya Porter ikarudi Mjini Salt Lake.

Wakati wa miaka yake ya 22 ya huduma katika Sabini, Bruce alilazwa hospitalini mara kadhaa, ikiwemo upasuaji mara 10. Madaktari walimwambia Susan mara mbili kwamba Bruce hataishi kupita usiku, lakini aliishi.

Bruce alifanyiwa usafishaji wa damu yake kwa zaidi ya miaka 12 ya huduma yake kama Kiongozi Mkuu mwenye Mamlaka. Kwa muda mrefu wa wakati huo, usafishaji wa damu ulichukua jioni tano kwa wiki kwa masaa manne kwa kila matibabu ili aweze kutumika wito wake wakati wa mchana na kutekeleza majukumu ya mkutano mkuu mwishoni mwa wiki. Wakati afya yake ilipokosa kupata afueni baada ya baraka nyingi za ukuhani, Bruce alishangazwa, lakini alijua katika ambaye aliyemwamini.26

Mnamo 2010, Bruce alipokea figo kutoka kwa mwanawe David. Wakati huu, mwili wake haukukataa kiungo hiki. Ilikuwa muujiza kuleta afya upya, hatimaye kumruhusu yeye na Susan kurudi sehemu yake aipendayo ya Urusi katika Urais wa Eneo.

Picha
Mzee na Dada Porter huko Urusi

Mnamo Desemba 26, 2016, baada ya kupambana na maambukizi ya kuendelea katika hospitali Mjini Salt Lake, aliomba madaktari waondoke chumbani. Bruce alimwambia Susan “kwamba alijua kwa njia ya Roho kwamba hakuna chochote madaktari wangefanya ambacho kingeokoa maisha yake. Alijua … kwamba Baba wa Mbinguni angempeleka nyumbani. Alijawa na amani.”27

Mnamo Desemba 28, Bruce alirudi nyumbani kwa familia yake. Masaa machache baadaye, akiwa amezungukwa na wapendwa wake, kwa amani alirudi nyumbani kwake mbinguni.

Picha
Mchoro wa Mzee Bruce D. Porter

Miaka mingi iliyopita, Bruce Porter aliandikia watoto wake maneno haya:

“Ushuhuda nilio nao wa ukweli na upendo wa Yesu Kristo umekuwa dira ya maisha yangu. … Ni ushuhuda msafi, wa kuchoma wa Roho kwamba Yeye yu hai, kwamba Yeye ni Mkombozi wangu na Rafiki katika kila wakati wa haja.”28

“Changamoto yetu … ni kuja kumjua [Mwokozi], na kupitia kwa imani katika yeye kushinda majaribu na vishawishi vya ulimwengu huu.”29

“Acha tuwe waaminifu na wa kweli, kuamini Kwake Yeye.”30

Bruce Douglas Porter alishinda ulimwengu.

Hebu kila mmoja wetu ajaribu kwa bidii katika juhudi zetu ili kushinda ulimwengu, si kutetea makosa makubwa lakini kuwa na subira na mitelezo midogo midogo na mianguko, kwa shauku kuongeza kasi yetu na kwa ukarimu kuwasaidia wengine. Unapoamini kikamilifu katika Mwokozi, nakuahidi baraka za amani kuu katika maisha haya na uhakikisho mkubwa wa maisha yako ya milele, katika jina la Yesu Kristo, amina