2010–2019
Ukweli wa Mambo Yote
Oktoba 2017


Ukweli wa Vitu Vyote

Kila mmoja wetu ana jukumu la kibinafsi kufanya kinachohitajika ili apate na kuhifadhi ushuhuda thabiti.

Tunakuja usiku wa leo tukiwa na matumaini na imani kwamba kwa namna fulani, tutaondoka tukiwa tumeimarishwa na kubarikiwa na Roho Mtakatifu, ambaye hufundisha ukweli.1 Ni kuhusu uchunguzi wetu wa ukweli ningependa kuzungumzia.

Kama mvulana, nilikuwa na maswali mengi kuhusu Kanisa. Baadhi ya maswali yangu yalikuwa ya dhati. Mengine hayakuwa hivyo na yaliashiria mashaka ya wengine.

Mara nyingi nilijadili maswali yangu pamoja na mama yangu. Nina hakika ya kwamba aliweza kuhisi maswali yangu yalikuwa ya dhati na yalitoka moyoni mwangu. Ninafikiria alisikitishwa na yale maswali ambayo hayakuwa ya dhati sana na kwa kiasi kikubwa ya ubishi. Hata hivyo, kamwe hakuninyamazisha kwa kuwa na maswali. Alinisikiliza na kujaribu kuyajibu. Wakati ambapo alihisi ya kwamba alikuwa amesema yote ambayo aliweza kusema na bado nilikuwa na maswali, alinena hivi: “David, hilo ni swali zuri sana. Ukiwa ungali unatafuta na kusoma na kusali ili upate jibu, kwa nini usifanye yale mambo unayojua kuwa unapaswa kuyafanya na usitende yale mambo unajua haupaswi kufanya? Huu ulikuja kuwa mfumo wa uchunguzi wangu wa ukweli. Kupitia kujifunza, kusali, na kutii amri, niligundua ya kwamba kuna majibu kwa maswali yangu yote muhimu. Pia niligundua ya kwamba kwa maswali fulani, kuendelea kwa imani, subira, na ufunuo inahitajika.2

Mama aliniachia jukumu la kukuza imani na kutafuta majibu. Alijua ya kwamba majibu muhimu yangetokana na kutafuta ukweli jinsi Baba wa Mbinguni alivyoamuru. Alijua ya kwamba nilihitaji kupata ukweli. Alijua ya kwamba nilihitaji kuwa mwaminifu katika maswali yangu na niwe radhi kuwajibikia yale ambayo tayari nayajua kuwa kweli. Alijua ya kwamba nilihitaji kujifunza na kusali na kwamba nilihitaji kuwa na subira kubwa nilipokuwa nikitafuta majibu kutoka kwa Bwana. Nia ya kuwa na subira ni sehemu ya kutafuta ukweli na ni sehemu ya mfano wa Bwana wa kufunua ukweli.3

Baada ya muda, nilikuja kujua ya kwamba mama yangu alikuwa ananifundisha mfano wa Baba wa Mbinguni wa kutafuta ukweli. Imani ilikua, majibu yalianza kuja, na nikakubali mwito wangu wa misheni.

Kulikuja wakati, mapema katika misheni yangu, ambapo nilijua ya kwamba nilihitaji kujua ikiwa Kanisa lilikuwa la kweli na Joseph Smith alikuwa nabii wa Mungu. Nilihisi kile ambacho Rais Thomas S. Monson alionyesha wazi kabisa katika mkutano wetu mkuu uliopita: “Kama hauna ushuhuda imara wa vitu hivi, fanya kile kilicho muhimu kuupata. Ni muhimu kwako kuwa na ushuhuda binafsi katika nyakati hizi ngumu, kwani shuhuda za wengine zitakubeba kwa wakati tu.”4 Nilijua kile kilichokuwa muhimu. Nilihitaji kusoma Kitabu cha Mormoni kwa moyo wa dhati, na kusudi halisi na nimuulize Mungu ikiwa ni kweli.

Sikiliza ahadi hii ya ajabu kutoka kwa Baba yetu wa Mbinguni iliyotolewa kupitia nabii Moroni: “Na mtakapopokea vitu hivi, ningewashauri kwamba mngemuuliza Mungu, Baba wa Milele, katika jina la Kristo, ikiwa vitu hivi si vya kweli; na ikiwa mtauliza na moyo wa kweli, na kusudi halisi, mkiwa na imani katika Kristo, atawaonyesha ukweli wake kwenu, kwa uwezo wa Roho Mtakatifu.”5

Ili nipokee kile kilichokuwa katika Kitabu cha Mormoni, nilihitaji kukisoma. Nilianza kutoka mwanzo wa kitabu na kukisoma kila siku. Wengine hupokea ushuhuda kwa haraka sana. Kwa wengine, itachukuwa muda zaidi na maombi zaidi na inaweza jumuisha kusoma kitabu hiki mara kadhaa. Nilihitaji kukisoma kitabu chote kabla ya kupokea ushuhuda ulioahidiwa. Hata hivyo, Mungu alinionyesha ukweli wake kwa nguvu za Roho Mtakatifu.

Katika jarida langu la misheni, nilielezea furaha yangu kwa kujua ukweli pamoja na mtazamo binafsi kujitolea na kusidi halisi la kutenda kulingana na ukweli ambao nilikuwa nimepokea. Niliandika, “Nimemuahidi Baba yangu wa Mbinguni na mimi mwenyewe kwamba nitafanya juhudi zangu zote, kujitolea asilimia 100 kikamilifu maisha yangu yote, chochote nitakachoombwa, nitatenda, lakini kwa sasa ninayo misheni yangu iliyosalia na nitaifanya misheni kuwa ya fanaka, ile ambayo haitanisikitisha, lakini sio kwa ajili yangu, bali kwa ajili ya Bwana. Ninampenda Bwana, na ninaipenda kazi, na ninaomba tu kwamba hisia hiyo kamwe isinitoke.

Nilikuja kufahamu ya kwamba lishe ya kila mara na juhudi inayoendelea ya kutubu na kutii amri inahitajika ili hisia hiyo kamwe isikutoke. Rais Monson alisema, “Ushuhuda unapaswa kutunzwa vizuri na kuwa hai kwa kuendelea kutii amri za Mungu na sala za kila siku na kujifunza maandiko.”6

Kwa miaka mingi, nimewauliza wamisionari na vijana kote duniani jinsi walianza juhudi zao za kibinafsi za kutafuta ukweli na kupata ushuhuda. Karibu wote, hujibu ya kwamba juhudi zao wenyewe kupata ushuhuda wa kibinafsi zilianza na uamuzi wa kibinafsi wa kusoma Kitabu cha Mormoni kutoka mwanzo na kumuuliza Mungu ikiwa ni cha kweli. Kwa kufanya hivyo, walichagua “kutenda” badala ya “kutendewa”7 na shaka za wengine.

Kujua ukweli, tunahitaji kuishi injili8 na “kujaribu”9 juu ya neno. Tunatahadharishwa tusimpinge Roho wa Bwana.10 Kutubu, pamoja na uamuzi wa kutii amri, ni sehemu muhimu ya kila mtu anapotafuta ukweli.11 Kwa kweli, tunahitaji kuwa radhi “tutaacha” dhambi zetu ili tuweze kujua ukweli.12

Tunaamriwa “tafuteni maarifa, hata kwa kujifunza na pia kwa imani” na “tafuteni … kutoka kwenye vitabu vizuri maneno ya hekima.”13 Kutafuta kwetu kwa ukweli kunapaswa kulenga “vitabu vizuri” na vyazo vizuri. Miongoni mwa yaliyo mazuri ni maandiko na maneno ya manabii walio hai.

Rais Monson ameuliza kila mmoja wetu “afanye [kile] kinachohitajika” kupata na kuhifadhi ushuhuda wa nguvu.14 Ni nini kinahitajika ili ushuhuda wako upate kuwa wa kina na kuimarika? Kila mmoja wetu ana jukumu la kibinafsi kufanya kinachohitajika ili apate na kuhifadhi ushuhuda thabiti.

Tukiweka maagano yetu kwa subira huku “tukifanya [kile] kinachohitajika” kupata majibu kutoka kwa Bwana ni sehemu ya mfumo wa Mungu wa kujifunza ukweli. Hasa wakati ambapo mambo ni magumu, tunaweza hitajika “kutii kwa furaha” na subira kwa mapenzi yote ya Bwana.”15 Kutii maagano kwa subira kunazidisha unyenyekevu wetu, kunaimarisha haja yetu ya kutaka kujua ukweli, na kumruhusu Roho Mtakatifu ili atuongoze [sisi] katika njia za hekima ili [sisi] tupate baraka, mafanikio, na kuhifadhiwa.”16

Mke wangu, Mary, pamoja nami tunaye mtu ambaye tunampenda kwa dhati ambaye amepambana maisha yake yote na mambo fulani ya Kanisa. Anaipenda injili, na analipenda Kanisa lakini bado ana maswali. Ameunganishwa hekaluni, anashiriki kikamilifu Kanisani, anatekeleza miito yake, na ni mama na mke wa ajabu. Kwa kipindi cha miaka mingi, amejaribu kufanya yale mambo aliyojua kuwa ni haki na kuepukana na kutenda yale mambo alijua si sawa. Ameweka maagano yake na kuendelea kutafuta. Wakati mwingine amekuwa na shukrani kushikilia imani ya wengine.

Sio kitambo sana, askofu wake aliomba kumuona pamoja na mumewe. Aliwauliza wakubali jukumu la kuhudumu katika hekalu kama mawakala wa wale waliohitaji maagizo ya hekalu. Mwito huu uliwashangaza, lakini walikubali na kuanza huduma yao katika nyumba ya Bwana. Mwana wao kijana alikuwa hivi karibuni ameshiriki katika utafiti wa historia ya familia na kupata jina la familia la mtu ambaye maagizo ya hekalu hayakuwa yamekamilika. Baada ya muda walihudumu kama mawakala na kutimiza maagizo ya hekalu kwa niaba ya mtu huyu na familia yake. Walipokuwa wamepiga magoti kwenye madhabahu na agizo la kuunganisha kufanyika, huyu mwanamke wa ajabu, mwenye subira ambaye ametafuta kwa muda mrefu alikuwa na tukio la kibinafsi la kiroho ambapo alipata kujua kwamba hekalu na maagizo ambayo yanafanyika ndani yake ni ya kweli na halisi. Alimpigia simu mama yake na kumuelezea juu ya tukio na kusema kwamba huku akiwa angali anayo maswali kadhaa, anajua ya kwamba hekalu ni la kweli, kwamba maagizo ya hekalu ni ya kweli, na kwamba Kanisa ni la kweli. Mama yake alilia kwa shukrani kwa ajili ya Baba wa Mbinguni mwenye upendo, na subira na binti ambaye kwa subira anaendelea kutafuta.

Kuweka maagano kwa subira hulete baraka za mbinguni maishani mwetu.17

Nimepata faraja kubwa katika ahadi ya Bwana kuwa “kwa uwezo wa Roho Mtakatifu mtajua ukweli wa vitu vyote”18 Bila ya kujua kila kitu, tunaweza kujua ukweli. Tunaweza kujua kibinafsi ikiwa Kitabu cha Mormoni ni cha kweli. Kwa kweli, kama Rais Russell M. Nelson alivyofunza adhuhuri ya leo, tunaweza kuhisi kwa kina “katika sehemu ya ndani” ya mioyo yetu [ona Alma 13:27], kwamba Kitabu cha Mormoni bila shaka ni neno la Mungu. Na tunaweza “kuhisi kiundani zaidi kwamba hatutataka kuishi siku moja bila hicho.”19

Tunajua ya kwamba Mungu ni Baba Yetu, anayetupenda; na kwamba Mwana Wake, Yesu Kristo, ni Mwokozi na Mkombozi wetu. Tunaweza kujua ya kwamba uumini katika Kanisa Lake upaswa kuthaminiwa na kwamba kupokea sakramenti kila wiki kutatusaidia sisi pamoja na familia kuwa salama. Tunaweza kujua ya kwamba kupitia maagizo ya hekalu, familia kwa kweli zinaweza kuwa pamoja milele. Tunaweza kujua ya kwamba Upatanisho wa Yesu Kristo na baraka za toba na msamaha ni kweli na halisi. Tunaweza kujua ya kwamba nabii wetu mpendwa, Thomas S. Monson, ni nabii wa Bwana na washauri wake na washiriki wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili ni mitume, manabii, waonaji, na wafunuzi.

Yote haya nayajua kuwa kweli na ninatoa ushahidi wangu katika jina la Yesu Kristo, amina.