2010–2019
Je, Mimi ni Mtoto wa Mungu?
Aprili 2018


Je, Mimi ni Mtoto wa Mungu?

Ni kwa jinsi gani kila mmoja wetu anaweza kupata uzoefu wa nguvu ya kuwa na uelewa wa utambulisho wetu wa kiungu? Inaanza na kutafuta kumjua Mungu, Baba Yetu.

Hivi majuzi nilishiriki Kanisani pamoja na mama yangu mpendwa katika nyumba yetu kuu ya mikutano lililojengwa kwa mawe. Nilivutiwa na sauti ndogo kutoka katika chumba cha Msingi nilikohudhuria miongo mingi iliyopita, niliingia kule nyuma na kuwatazama viongozi wanaojali wakifundisha mada ya mwaka huu “Mimi ni Mtoto wa Mungu.”1 Nilitabasamu nilipokumbuka walimu wenye subira na upendo ambao wakati wa kuimba kwetu wakati huo, mara nyingi wangenitazama mimi—yule mwana mtundu sana pembeni mwa benchi—karibia kusema, “Je, yeye ni mtoto wa Mungu kweli? Na ni nani amemtuma hapa?”2

Ninamwalika kila mmoja wetu afungue moyo wake kwa Roho Mtakatifu, ambaye “hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu.”3

Maneno ya Rais Boyd K. Packer ni wazi na yenye thamani: “Wewe ni mtoto wa Mungu.” Yeye ni Baba wa roho yako. Kiroho wewe ni wa uzao wa kilodi, mtoto wa Mfalme wa Mbinguni. Uweke ukweli huu akilini mwako, na uushikilie. Haijalishi vizazi vingi katika ukoo wako wa maisha ya sasa, haijalishi utaifa wako au watu unaowawakilisha, nasaba ya roho yako inaweza kuandikwa kwenye mstari mmoja. Wewe ni Mtoto wa Mungu!”4

“Wakati wewe … Utakapomwona Baba Yetu,” Brigham Young alieleza, “utamwona kiumbe ambaye umemfahamu kwa muda mrefu, na atakupokea mikononi Mwake, na utakuwa tayari kumkumbatia na kumbusu.”5

Vita Kuu juu ya Utambulisho wa Kiungu

Musa alijifunza kuhusu urithi wake wa kiungu alipozungumza na Bwana ana kwa ana. Kufuatia tukio hilo, “Shetani akaja kumjaribu,” kwa hila, hata hivyo dhamira mbaya ya kupotosha utambulisho wa Musa, “akisema: Musa mwana wa mtu, niabudu mimi. Na … Musa akamtazama Shetani na akasema: Wewe ni nani? Kwa maana, tazama, mimi ni mwana wa Mungu.6

Vita hii kuu kuhusu utambulisho wa kiungu inaendelea kwa nguvu huku silaha za Shetani zinazoenea zikilenga kuharibu imani yetu katika na ufahamu wetu kuhusu uhusiano baina yetu na Mungu. Tunashukuru, tumebarikiwa kwa ono na uelewa wa wazi wa utambulisho wetu wa kweli tokea mwanzo: “Mungu akasema, Na tumfanye mtu kwa mfano [wetu], kwa sura yetu,”7 na manabii Wake walio hai wanatangaza, “Kila [binadamu] ni mwana au binti mpendwa wa kiroho wa wazazi wa mbinguni, na, kama hivyo, kila mmoja ana asili takatifu na takdiri.”8

Kuja kujua kweli hizi kwa uhakika9 kunatusaidia kushinda majaribu, shida, na mateso ya kila aina.10 Wakati alipoulizwa “Ni jinsi gani tunaweza kuwasaidia wale wanaopambana na [changamoto ya kibinafsi]?” Mtume wa Bwana alifundisha, “Wafundishe utambulisho wao na kusudi lao.”11

“Ufahamu wa Nguvu Zaidi Nilio Nao”

Kweli hizi za nguvu zilikuwa zenye kubadilisha maisha kwa rafiki yangu Jen,12 ambaye akiwa kijana alisababisha ajali kubwa mno ya motokaa. Ingawaje majeraha yake ya kimwili yalikuwa makali, alihisi uchungu mkali kwa sababu yule dereva mwingine alipoteza maisha yake. “Mtu fulani alipoteza mama yake, na ni makosa yangu,” yeye husema. Jen, ambaye siku chache tu alisimama na kukariri, “Sisi ni mabinti wa Baba yetu wa Mbinguni, ambaye anatupenda,”13 sasa aliuliza, “Ni jinsi gani anaweza kunipenda mimi?”

“Uchungu wa kimwili ulipita,” yeye husema, “lakini sikudhani ya kwamba ningeweza kupona kutokana na vidonda vya mchomo wa moyo na vya kiroho.

Ili aweze kuendelea kuishi, Jen alificha hisia zake ndani kabisa, alikaa mbali na kuwa mwenye ganzi. Baada ya mwaka mmoja, wakati aliweza hatimaye kuzungumza kuhusu ajali hiyo, mshauri mwenye msukumo alimtaka aandike maneno haya “Mimi ni Mimi ni mtoto wa Mungu” na kuyasema mara 10 kila siku.

“Kuandika maneno ilikuwa rahisi,” anakumbuka, “lakini sikuweza kuyatamka. … Hilo lilifanya yawe ya kweli, na sikuamini kwa hakika kwamba Mungu alikuwa ananitaka kama mtoto Wake. Ningejikunja na kulia.”

Baada ya miezi kadhaa, Jen hatimaye aliweza kukamilisha kazi hiyo kila siku. “Nililia kwa nafsi yangu yote,” alisema, “nikimuomba Mungu. … Kisha nikaanza kuyaamini maneno yale.” Imani hii ilimruhusu Mwokozi aanze kuiponya nafsi yake iliyojeruhiwa. Kitabu cha Mormoni kilileta faraja na ujasiri katika Upatanisho Wake.14

“Kristo alihisi uchungu wangu, huzuni yangu, hatia yangu,” Jen anatamatisha. “Nilihisi upendo msafi wa Mungu na sikuwa nimewahi kuwa na uzoefu wa nguvu kiasi hicho! Kujua ya kwamba mimi ni mtoto wa Mungu ni ufahamu wa nguvu zaidi nilio nao!”

Kutafuta Kumjua Mungu, Baba Yetu

Akina kaka na akina dada, ni kwa jinsi gani kila mmoja wetu anaweza kupata uzoefu wa nguvu ya kuwa na uelewa wa utambulisho wetu wa kiungu? Inaanza na kutafuta kumjua Mungu, Baba Yetu.15 Rais Russell M. Nelson alishuhudia, “Kitu chenye msukumo kinatokea wakati mtoto wa Mungu anapotaka kujua zaidi kumhusu Yeye na Mwana Wake Mpendwa.”16

Tunapojifunza kumhusu na kumfuata Mwokozi hutusaidia kumjua Baba. “Akiwa … mfano wa [Baba] yake,”17 Yesu alifundisha, “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe, ila lile ambalo amwona Baba analitenda.”18 Kila neno na tendo la Kristo huonyesha asili ya kweli ya Mungu na uhusiano wetu Kwake.19 Mzee Jeffrey R. Holland alifundisha, “Damu ikiwa inamtoka katika kila kinyweleo na kilio cha maumivu mdomoni Mwake, Kristo alimtafuta Yule ambaye daima alikuwa anamtafuta—Baba Yake. ‘Aba,’ Alilia, ‘Baba.’”20

Kama Yesu alivyomtafuta Baba Yake kwa dhati kule Gethsemane, ndivyo kijana Joseph Smith, mwaka wa 1820, kwa sala alimtafuta Mungu katika kile Kisitu Kitakatifu. Baada ya kusoma “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima na aombe dua kwa Mungu,”21 Joseph alienda kusali.

“Nilipiga magoti,” aliandika “na kuanza kutoa matakwa ya moyo wangu kwa Mungu. …

“… Niliona nguzo ya mwanga juu ya kichwa changu. …

“… Nikawaona Viumbe wawili, ambao mng’aro na utukufu wao wapita maelezo yote, wakiwa wamesimama juu yangu angani. Mmoja wao akaniambia, akiniita mimi kwa jina na kusema, huku akimwonyesha yule mwingine—[Joseph,] Huyu ni Mwanangu Mpendwa.Msikilize Yeye!22

Tukifuata mifano ya Mwokozi na Nabii Joseph katika kumtafuta Mungu kwa bidii, tutakuja kuelewa katika njia ya kweli kabisa, kama Jen, kwamba Baba yetu anatujua kwa majina, kwamba sisi ni watoto Wake.

Kwa akina mama, hasa kina mama vijana, ambao mara nyingi wanahisi kushindwa na kana kwamba wamezama majini wakati wakijaribu kulea “kizazi kinzani kwa dhambi,”23 usiwahi kadiria kwa upungufu wajibu wako muhimu katika mpango wa Mungu. Katika nyakati za msongo wa mambo—pengine wakati unapokimbizana na watoto wadogo na harufu ya kitu kilichoungua kutoka jikoni inakujulisha ya kwamba chakula cha jioni ulichotayarisha kwa upendo sasa ni dhabihu ya kuteketezwa kwa moto—jua ya kwamba Mungu hutakasa siku zako za matatizo mengi.24 Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe,”25 kwa amani anakuhakikishia. Tunawaheshimu mnapotimiza matumaini ya Dada Joy D. Jones, ambaye alisema, “Watoto wetu wanastahili kuelewa utambulisho wao wa kiungu.”26

Ninawaalika kila mmoja wetu kumtafuta Mungu na Mwana Wake Mpendwa. “Hakuna popote,” Rais Nelson alivyoelekeza, “kweli hizo zinafundishwa kiufasaha na kwa nguvu kuliko katika Kitabu cha Mormoni.”27 Fungua kurasa zake na ujifunze kwamba Mungu hufanya “vitu vyote kwa ustawi [wetu] na furaha”;28 kwamba Yeye ni “mwenye huruma na neema, si mwepesi wa hasira, mwenye subira na amejaa wema”;29 na kwamba “wote ni sawa kwake [Yeye].”30 Wakati unapohisi kuumizwa, kupotea, kutishwa, kukasirishwa, huzuni, njaa, au kuachwa bila ya matumaini katika shida kubwa maishani31—fungua Kitabu cha Mormoni, na utakuja kujua kwamba “Mungu kamwe hatatuacha. Hajawahi kutuacha, na hatatuacha kamwe. Hawezi kufanya hivyo. Siyo tabia Yake [kufanya hivyo].”32

Kuja kumjua Baba yetu kunabadilisha kila kitu, hasa mioyo yetu, wakati Roho Wake mtulivu anadhihirisha utambulisho wetu wa kweli na thamani yetu kubwa mbele ya macho Yake.33 Mungu hutembea nasi katika njia ya agano tunapomtafuta kupitia teto za sala, kutafuta katika maandiko, na jitihada tiifu.

Utukufu wa Tabia ya Mungu—Ushahidi Wangu

Ninampenda Mungu wa baba zangu,34 “Bwana Mwenyezi Mungu,”35 ambaye hulia nasi katika masikitiko yetu, kwa subira hukosoa uovu wetu, na hufurahia wakati tunapotafuta “kuacha dhambi [zetu] zote ili kumjua [Yeye].”36 Ninamuabudu Yeye, ambaye daima ni “baba wa yatima”37 na mwenza kwa wasio na wenza. Kwa shukrani, ninashuhudia ya kwamba nimepata kumjua Mungu, Baba Yangu, na ninashuhudia ukamilifu, sifa, na “utukufu wa tabia Yake.”38

Kwamba kila mmoja wetu aweze kuelewa kwa kweli na kuthamini “haki ya urithi wa kilodi ”39 kama mtoto wa Mungu kwa kuja kumjua Yeye, “Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo [yeye] aliyemtuma”40 ni sala yangu ya dhati katika jina la Yesu Kristo, amina.