2015
Nguvu ya Imani
Aprili 2015


Tunazungumza Kumhusu Kristo

Nguvu ya Imani

Mwandishi anaishi Oregon, Marekani.

Kama Baba wa Mbinguni angetuondolea changamoto zetu kwa sababu tu tumemwomba, Angekuwa anatunyima sisi kujifunza mambo muhimu sana kwa ajili ya wokovu wetu.

Picha
A mother ssitting with her small daughter as the girl colors in a coloring book.

Mwaka mmoja katika chuo, nilikuwa ninafanya mtihani wakati shingo yangu ilianza kuuma. Maumivu hayakupotea wakati wasiwasi wa mtihani ulipopita. Niliwaona madaktari na wataalamu wa matibabu na kujaribu aina mbali mbali za tiba, lakini bado maumivu yaliendelea. Mwaka uliofuata, nilipojitahidi kukabiliana na maumivu haya, nilijitahidi pia kuongeza imani yangu. Nilitumia muda mwingi katika maombi, nilisoma maandiko, na niliomba baraka za ukuhani. Nilihisi kwamba kama tu ningekuwa na imani ya kutosha, ningeponywa.

Yesu Kristo aliwaponya wagonjwa, vipofu, viwete, walio na ukoma—“kulingana na imani [yao]” (Mathayo 9:29). Nilijua alikuwa na nguvu ya kuniponya mimi kama Alivyokuwa amewaponya wengine wengi wakati wa maisha yake duniani. Nilihitimisha, kwa hiyo, kwamba ukosefu wangu wa imani tu ndio ulionizuia kuponywa, hivyo basi niliongeza juhudi zangu. Nilipoendelea na tiba ya mwili, nilisali na kufunga na kusoma na kuamini. Hata hivyo maumivu yangu yaliendelea.

Maandiko yanatufundisha kuwa kwa imani tunaweza kufanya miujiza (ona Mathayo 17:20), lakini bado sikuweza kuondolewa mateso haya madogo. Je, nguvu katika imani yangu ilikuwa wapi? Hatimaye, kimya kimya nilikubali hali yangu, nikapata njia za kukabiliana na maumivu yangu, na nikawa nimetoshelezwa kwa kuweka ufahamu kamili wa imani na uponyaji kwa wakati ujao.

Miaka mingi baadaye nilikuwa ninazungumza na rafiki ambaye alikuwa ameteseka na kichefuchefu kibaya kilichokuwa kimempelekaa hospitalini zaidi ya mara moja wakati wa ujauzito wake wa kwanza. Erin alitaka kuwa na mtoto mwingine, lakini alitishwa na hofu kwamba huenda angepitia maumivu yale yale aliyokuwa amepitia wakati wa ujauzito wake wa kwanza. Aliniambia kuwa alikuwa akifunga na kusali na kwamba aliamini kwamba kweli Baba wa Mbinguni hangemwomba apitie tena kwa mara ya pili.

Tulipokuwa tunazungumza, nilikumbuka maandiko, “Tulia, na ujue kuwa Mimi ni Mungu” (Zaburi 46:10). Nilifikiria kuhusu uzoefu wangu mwenyewe katika kujifunza kutulia katkati ya mateso na nikamuhimiza Erin aendelee kuwa na imani lakini asiifanye imani hiyo itegemee kuwapo ama kutokuwapo kwa kichefuchefu wakati wa ujauzito wake ujao.

Nilipokuwa nikieendelea kujifunza kanuni ya imani, nilifungua hotuba ya Alma juu ya imani ambapo anafundisha kwamba “kama mkiwa na imani mna tumaini katika mambo ambayo hayaonekani, ambayo ni ya kweli” (Alma 32:21).

Nikitafakari maandiko, niligundua kwamba imani haikuwa kile nilichofikiri ilikuwa. Imani, Alma anatufundisha, ni matumaini katika kanuni ya kweli. Kuwa na imani haimaanishi kwamba tunaamini Baba yetu wa Mbinguni daima atatupatia kile tunachoomba wakati tunapokiomba. Kuwa na imani kwamba Kristo angeniponya shingo yangu au Yeye angempa Erin wakati wa ujauzito usio na kichefuchefu si kuwa na imani katika kanuni ya kweli. Hata hivyo, tunaweza kuwa na imani kwamba Kristo ana nguvu za kuponya, kwamba anatujali, kwamba atatuimarisha, na kwamba tukistahimili vyema, tutaweza kustahili uzima wa milele.

Bwana aliahidi, “Chochote utakachoomba kwa imani, ukiamini kwamba utapokea kwa jina la Kristo, utakipokea” (Enoshi 1:15). Naamini nguvu katika ahadi hii ipo katika ushauri wa kuamini “katika jina la Kristo”. Kidahizo katika Kamusi ya Biblia hutufundisha: “Tunasali kwa jina la Kristo wakati mawazo yetu ni mawazo ya Kristo, na matakwa yetu ni matakwa ya Kristo—ikiwa maneno yake yanakaa ndani yetu (Yohana 15:7). Ndipo sisi tunapoomba vitu ambavyo Mungu anaweza kutupatia. Mara nyingi hubaki bila kujibiwa kwa sababu hayako katika jina la Kristo hata kidogo; hayawakilishi kwa njia yoyote mawazo Yake, lakini yanatokana na uchoyo wa moyo wa binadamu.”

Tunapoomba kwa imani kitu ambacho kinalingana na mapenzi ya Mungu, Atatupatia kulingana na hamu zetu. Baba wa Mbinguni anatujua, anatupenda, na anataka kila kitu muhimu kwa ajili yetu ili kurudi katika uwepo wake. Na wakati mwingine hiyo hujumuisha majaribu, matatizo na changamoto (ona 1 Petro 1:7). Kama Baba wa Mbinguni angetuondolea changamoto zetu kwa sababu tu tumemwomba, angekuwa anatunyima sisi kujifunza mambo yaliyo muhimu sana kwa ajili ya wokovu wetu. Sharti tujifunze kuamini katika mpango wa Mungu kwa ajili yetu na kuyaweka mapenzi yetu chini ya mapenzi Yake. Tunapoweka matakwa yetu sambamba na matakwa Yake na kukiri utegemezi wetu kamili juu Yake, tunaweza kustahili kupokea “mwisho wa imani [yetu], hata wokovu wa roho [zetu]” (1 Petro 1:9).