Maandiko Matakatifu
Musa 4


Mlango wa 4

(Juni–Oktoba 1830)

Jinsi Shetani alivyokuja kuwa ibilisi—Anamjaribu Hawa—Adamu na Hawa wanaanguka, na mauti yaingia ulimwenguni.

1 Na Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia Musa, nikisema: Kwamba Shetani, ambaye wewe ulimwamuru katika jina la Mwanangu wa Pekee, ni yeye yule aliyekuwepo tangu mwanzo, na aliyekuja mbele yangu, akisema—Tazama, niko hapa, nitume mimi, nitakuwa mwanao, nami nitawakomboa wanadamu wote, ili hata nafsi moja isipotee, na hakika nitatenda hivyo; kwa sababu hiyo nipe mimi heshima yako.

2 Walakini, tazama, Mwanangu Mpendwa, ambaye alikuwa Mpendwa na Mteule tangu mwanzo, aliniambia—Baba, mapenzi yako na yatimizwe, na utukufu uwe wako milele na milele.

3 Kwa hiyo, kwa sababu yule Shetani aliasi dhidi yangu, na akatafuta kuangamiza haki ya mtu ya kujiamulia, ambayo Mimi, Bwana Mungu, nimempa, na pia, kwamba alinitaka nimpe yeye uwezo wangu mwenyewe, kwa uwezo wa Mwanangu wa Pekee, nikamfanya atupwe chini;

4 Naye akawa Shetani, ndiyo, hata ibilisi, baba wa uwongo wote, ili kudanganya na kuwapofusha watu, na kuwaongoza utumwani kadiri apendavyo, hata wengi kadiri wasivyosikia sauti yangu.

5 Na sasa nyoka alikuwa mwenye hila kuliko wanyama wote wa mwituni ambao Mimi, Bwana Mungu, niliwaumba.

6 Na Shetani aliwekwa katika moyo wa nyoka, (kwa maana alikwisha wadanganya wengi upande wake,) na pia alitafuta kumlaghai Hawa, kwa maana hakujua mawazo ya Mungu, kwa jinsi hiyo alitafuta kuuangamiza ulimwengu.

7 Na akamwambia mwanamke: Ndiyo, Mungu amesema—Msile matunda ya kila mti wa bustani? (Naye alisema kwa kinywa cha yule nyoka.)

8 Naye mwanamke akamwambia yule nyoka: Twaweza kula matunda ya miti ya bustani;

9 Bali tunda la mti unaouona katikati ya bustani, Mungu kasema—Msile, wala msiliguse, msije mkafa;

10 Naye nyoka akamwambia mwanamke: Hakika hamtakufa;

11 Kwa maana Mungu ajua kuwa katika siku mtakayo kula matunda yake, ndipo macho yenu yatafunguka, nanyi mtakuwa kama miungu, mkijua mema na maovu.

12 Na mwanamke alipoona kuwa mti ni mzuri kwa chakula, na kwamba ulikuwa wenye kupendeza machoni, na mti wa kutamanika kwa kumfanya kuwa mwenye hekima, akachuma tunda lake, na akala, na pia akampa mume wake, naye akala.

13 Na macho yao wote wawili yakafunguka, nao wakajua ya kuwa wako uchi. Nao wakajishonea majani ya mtini na wakajifanyia mavazi.

14 Na wakasikia sauti ya Bwana Mungu, walipokuwa wakitembea katika bustani, wakati wa jua kupunga; na Adamu na mkewe walienda wakajificha wao wenyewe kutoka katika uwepo wa Mungu kati ya miti ya bustani.

15 Na Mimi, Bwana Mungu, nikamwita Adamu, na nikamwambia: Umeenda wapi?

16 Naye akasema: Nalisikia sauti yako bustanini, nami nikaogopa, kwa sababu nilijiona kuwa niko uchi, na nikajificha.

17 Na Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia Adamu: Nani aliyekuambia ya kuwa u uchi? Je, wewe umekula tunda la mti ule niliokuamuru usile, kama hivyo ndivyo hakika utakufa?

18 Naye mwanadamu akasema: Mwanamke uliyenipa, na kuamuru kwamba aambatane nami, alinipa tunda la ule mti nami nikala.

19 Na Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia mwanamke: Ni kitu gani hiki ulichokifanya? Na mwanamke akasema: Nyoka alinidanganya, nami nikala.

20 Na Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia nyoka: Kwa sababu wewe umefanya haya utalaaniwa kuliko wanyama wote wafugwao, na kuliko wanyama wote wa kondeni; kwa tumbo lako utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako;

21 Nami nitaweka uadui kati yako wewe na mwanamke, kati ya uzao wako na uzao wake; naye atakuponda kichwa chako, nawe utamponda kisigino chake.

22 Na kwa mwanamke, Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia: Hakika nitakuzidishia uchungu wako na kuzaa kwako. Kwa uchungu utazaa watoto, na tamaa yako itakuwa kwa mume wako, naye atakutawala.

23 Na kwa Adamu, Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia: Kwa sababu umeisikiliza sauti ya mke wako, na umekula tunda la mti ambao nilikuamuru wewe, nikisema—Usiyale; ardhi imelaaniwa kwa ajili yako; kwa uchungu utakula mazao yake siku zote za maisha yako.

24 Michongoma pia, na miiba itakuzalia, nawe utakula mboga za kondeni.

25 Kwa jasho la uso wako utakula mkate, hata utakapoirudia ardhi—kwa kuwa hakika utakufa—kwa maana kutoka hiyo wewe ulitwaliwa: kwa maana u mavumbi wewe, nawe mavumbini utarudi.

26 Na Adamu akaliita jina la mke wake Hawa, kwa sababu yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai; kwani hivyo ndivyo Mimi, Bwana Mungu, nilivyomwita wa kwanza kati ya wanawake wote, ambao ni wengi.

27 Kwa Adamu, na pia kwa mke wake, Mimi, Bwana Mungu, niliwafanyia mavazi ya ngozi, na nikawavika.

28 Na Mimi, Bwana Mungu, nikamwambia Mwanangu wa Pekee: Tazama, mtu huyu amekuwa kama mmoja wetu kwa kujua mema na maovu; na sasa asije akanyoosha mkono wake na kutwaa tunda la mti wa uzima, na akala na akaishi milele,

29 Kwa hiyo Mimi, Bwana Mungu, nitamfukuza kutoka Bustani ya Edeni, ili akailime ardhi ambayo katika hiyo alitwaliwa;

30 Kwa maana kama vile Mimi, Bwana Mungu, niishivyo, vivyo hivyo maneno yangu hayatarudi bure, kwa maana jinsi vile yatokavyo kinywani mwangu ni lazima yatimizwe.

31 Hivyo nikamfukuza huyo mtu, na kumweka mashariki ya Bustani ya Edeni, makerubi na upanga wa moto, uliogeuka huko na huko kuilinda njia ya mti wa uzima.

32 (Na haya ndiyo maneno niliyoyanena kwa Musa mtumishi wangu, nayo ni ya kweli hata kama vile nilivyotaka; nayo nimeyanena kwako. Angalia usiyaonyeshe kwa mtu yeyote, hata nitakapokuamuru, isipokuwa kwa wale wenye kuamini. Amina.)