2010–2019
Kwa Ajili Yake
Oktoba 2018


Kwa Ajili Yake

Kujua nani na kwa nini katika kutumikia wengine kunatusaidia kuelewa kwamba onyesho kuu la upendo ni uaminifu kwa Mungu.

Katika usiku huu wa kihistoria, ninatoa upendo wangu na shukrani kwa kila mmoja wenu, dada zangu wapendwa. Haijalishi umri wetu, mahali, au hali, tunakusanyika usiku huu katika umoja, katika nguvu, katika lengo, na katika ushuhuda kwamba tunapendwa na kuongozwa na Baba yetu wa Mbinguni; Mwokozi wetu, Yesu Kristo; na nabii wetu anayeishi, Rais Russell M. Nelson.

Kama wanandoa vijana, mimi na mume wangu tuliitwa na askofu wetu kutembelea na kuhudumia familia ambayo haikuwa imekuja kanisani kwa miaka mingi. Bila kusita tulikubali jukumu na kwenda nyumbani kwao siku chache baadaye. Ilikuwa wazi mara moja kwetu kwamba hawakutaka wageni kutoka Kanisani.

Hivyo kwenye matembezi yetu yaliyofuata, tuliwaendea na sahani ya biskuti, kwa ujasiri kwamba biskuti za chokoleti zingelainisha mioyo yao. Hazikulainisha. Wanandoa walizungumza nasi kupitia kisitiri cha mlango, ikifanya hili liwe wazi zaidi kwamba hatukukaribishwa. Lakini tulipokuwa tukirudi nyumbani, tulikuwa na uhakika wa kuridhisha mafanikio yangeweza kufikiwa kama tungewapelekea Zawadi za Kaukau za Mchele kama mbadala.

Upungufu wetu wa ono la kiroho ulifanya juhudi za ziada zilizoshindikana kuwa za kuvunja moyo. Kukataliwa kamwe hakuleti raha. Baada ya muda tulianza kujiuliza wenyewe, “kwa nini tunafanya hili? Lengo letu ni lipi?

Mzee Carl B. Cook alitoa wazo hili: “Kuhudumu katika Kanisa … kunaweza kuwa changamoto kama tukiombwa kufanya kitu ambacho kinatutisha, kama tunachoka kutumikia, au kama tunaitwa kufanya kitu ambacho hatukupata kuona mwanzo kuwa kinavutia .”1 Tulikuwa kwenye uzoefu wa ukweli wa maneno ya Mzee Cook wakati tulipoamua tulipaswa kutafuta maelekezo kutoka kwa Mtu mwenye maono makubwa kuliko yetu.

Hivyo, baada ya sala na kujifunza kwa uaminifu, tulipokea jibu la kwa nini ya huduma yetu. Tulikuwa na badiliko katika uelewa wetu, badiliko la moyo, kwa kweli uzoefu wa ufunuo.2 Tulipotafuta maelekezo kutoka kwenye maandiko, Bwana alitufundisha jinsi ya kufanya mchakato wa kuwahudumia wengine kuwa rahisi na wa maana zaidi. Huu ni mstari tuliosoma ambao ulibadili mioyo yetu na mbinu yetu: “Nawe mpende Bwana Mungu wako kwa moyo wako wote, na kwa uwezo wako wote, na kwa akili zako zote, na kwa nguvu zako zote; na katika jina la Yesu Kristo utamtumikia yeye.”3 Japo mstari huu ulikuwa unajulikana sana, ulionekana kuzungumza nasi katika njia mpya na ya muhimu.

Tuligundua kwamba tulikuwa tukijaribu kwa uaminifu kuhudumia familia hii na kumtumikia askofu wetu, lakini tulipaswa kujiuliza kama kweli tulihudumu kwa sababu ya upendo kwa Bwana. Mfalme Benyamini aliweka wazi tofauti hii wakati aliposema, “Tazama, nawaambia kwamba kwa sababu niliwaambia kuwa nimewatumikia maishani mwangu, sitamani kujivuna, kwani nimekuwa tu katika utumishi wa Mungu.”4

Hivyo nani hasa Mfalme Benyamini alikuwa akimtumikia? Baba wa Mbinguni na Mwokozi. Kujua nani na kwa nini katika kutumikia wengine kunatusaidia kuelewa kwamba onyesho kuu la upendo ni uaminifu kwa Mungu.

Pale lengo letu lilipobadilika taratibu, ndivyo zilivyokuwa sala zetu. Tulianza kutazamia matembezi yetu na familia hii pendwa kwa sababu ya upendo wetu kwa Bwana.5 Tulikuwa tukifanya hivyo kwa ajili Yake. Yeye alifanya mahangaiko kuwa si mahangaiko tena. Baada ya miezi mingi ya kusimama nje ya mlango, familia ilianza kutukaribisha ndani. Hatimaye, tulikuwa na sala za mara kwa mara na mijadala ororo ya injili pamoja. Urafiki wa muda mrefu ukajengeka. Tulikuwa tukimuabudu na kumpenda Yeye kwa kuwapenda watoto Wake.

Je, unaweza kukumbuka nyuma wakati kwa upendo uliponyosha mkono kwa juhudi za dhati kumsaidia mtu mwenye uhitaji na kuhisi kwamba juhudi zako hazikuonekana au pengine hazikushukuriwa au hata kukataliwa? Katika saa ile, je, ulitilia shaka thamani ya huduma yako? Kama ndivyo, acha maneno ya Mfalme Benyamini yachukue nafasi ya mashaka yako na hata maumivu yako: mnamtumikia tu Mungu wenu.”6

Badala ya kujenga chuki, tunaweza kujenga, kupitia huduma, uhusiano mkamilifu zaidi na Baba wa Mbinguni. Upendo na uaminifu wetu Kwake huchochea hitaji la utambuzi au shukrani na kuruhusu upendo Wake kutiririka kwetu na kupitia kwetu.

Wakati mwingine tunaweza mwanzo tukakuhudumu kama sehemu ya wajibu au sharti, lakini hata huduma hiyo inaweza kutupelekea kuvuta kitu kikubwa ndani yetu, ikituongoza kutumikia katika “njia bora zaidi”7—kama ilivyo katika mwaliko wa Rais Nelson wa mbinu “mpya”, takatifu ya kuwatunza na kuwahudumia wengine.”8

Tunapolenga kwenye yote ambayo Mungu ametutendea, huduma yetu hutiririka kutoka kwenye moyo wa shukrani. Tunapoacha kujihangaisha kuhusu huduma yetu kutukuza sisi, badala yake tunatambua kwamba lengo la huduma yetu litakuwa kumweka Mungu kwanza.9

Rais M. Russell Ballard alifundisha, “Ni pale tu tunapompenda Mungu na Kristo kwa mioyo yetu yote, nafsi, na akili ndipo tunapoweza kushiriki upendo huu na jirani zetu kupitia matendo ya ukarimu na huduma.”10

Ya kwanza kati ya Amri Kumi inakumbusha hekima hii takatifu: “Mimi ni Bwana Mungu wako. … Usiwe na miungu mingine ila mimi.”11 Uwepo wa amri hii hutusaidia kuelewa kwamba kama tutamuweka Yeye kama kipaumbele chetu kikuu, kila kitu chochote hatimaye kitafanikiwa—hata huduma yetu kwa wengine. Wakati Yeye anapochukua nafasi ya kwanza katika maisha yetu kwa uchaguzi wetu wa uangalifu, ndipo anapoweza kubariki matendo yetu kwa manufaa yetu na kwa manufaa ya wengine.

Bwana alishauri, “Nitegemeeni katika kila wazo.”12 Na kila wiki tunafanya agano la kutenda hilo tu—“daima kumkumbuka.”13 Je, lengo hilo la kiungu linaweza kutumika katika kila tunachokifanya? Je, kutenda hata kazi ya mikono kunaweza kuwa fursa ya kuonyesha upendo wetu na uaminifu Kwake? Ninaamini kunaweza na kutakuwa.

Tunaweza kufanya kila kipengele kwenye orodha yetu ya mambo ya kufanya kuwa njia ya kumtukuza. Tunaweza kuona kila kazi kama heshima na fursa ya kumtumikia Yeye, hata kama tuko katikati ya muda wa mwisho, majukumu, au nepi chafu.

Kama Amoni alivyosema, “Ndio, najua kwamba mimi si kitu; kulingana na nguvu zangu mimi ni mlegevu; kwa hivyo sitaweza kujivuna mwenyewe, lakini nitajivuna katika Mungu wangu, kwani kwa nguvu zake naweza kufanya vitu vyote.”14

Wakati kumtumikia Mungu kunapokuwa kipaumbele chetu kikuu katika maisha, tunapoteza nafsi zetu, na kwa wakati upasao, tunaziona.15

Mwokozi alifundisha kanuni hii kwa urahisi na unyoofu: “Kwa hivyo acha nuru yenu iangaze mbele ya hawa watu, ili wapate kuyaona matendo yenu, na kumtukuza Baba yenu aliye mbinguni.”16

Naomba nishiriki nanyi baadhi ya maneno ya hekima yaliyopatikana kwenye ukuta wa nyumba ya yatima huko Calcutta, India: “Kama wewe ni mkarimu, watu wanaweza kukutuhumu kwa ubinafsi, nia zilizofichika. Kuwa mkarimu vyovyote vile. Kile ulichokijenga kwa miaka, mtu anaweza kukibomoa kwa usiku mmoja. Jenga vyovyote vile. Mazuri unayofanya leo, watu mara nyingi watayasahau kesho. Fanya mema vyovyote vile. Upe ulimwengu kizuri ulichonacho, na yawezekana kamwe kisiwe cha kutosha. Upe ulimwengu kizuri ulichonacho vyovyote vile. Unaona, kwenye uchanganuzi wa mwisho, ni kati yako wewe na Mungu wako … vyovyote vile.”17

Akina dada, daima ni kati yetu na Bwana. Kama Rais James E. Faust alivyosema: “‘Ni nini hitaji kuu zaidi ulimwenguni?’ … ‘Je, si hitaji kuu zaidi ulimwenguni kote kwa kila mtu ni kuwa na uhusiano endelevu, binafsi, hai, wa kila siku, na Mwokozi?’ Kuwa na uhusiano kama huo kutafungua utakatifu ndani yetu, na hakuna kinachoweza kuleta tofauti kubwa katika maisha yetu kama tunapokuja kujua na kuelewa uhusiano wetu mtakatifu na Mungu.”18

Vivyo hivyo, Alma alielezea kwa kijana wake, “Ndio, acha vitendo vyako vyote viwe kwa Bwana, na popote uendapo acha iwe kwa Bwana; ndio, acha fikira zako zote zielekezwe kwa Bwana; ndio, acha mapenzi ya moyo wako yaelekezwe kwa Bwana milele.”19

Na Rais Russell M. Nelson kadhalika ametufundisha, “Wakati tunapotambua Upatanisho Wake wa hiari, dhabihu yoyote ya upande wetu inakuwa imefunikwa kabisa na hisia kuu ya shukrani kwa fursa ya kumtumikia Yeye.”20

Akina dada, ninashuhudia kwamba wakati Yesu Kristo, kupitia nguvu ya Upatanisho Wake, anapofanya kazi juu yetu na ndani yetu, Yeye huanza kufanya kazi kupitia sisi ili kuwabariki wengine. Tunawatumikia wao, lakini tunafanya hivyo kwa kumpenda na kumtumikia Yeye. Tunakuwa kile maandiko yanachoelezea: “Kila mwanaume [na mwanamke] akitafuta ustawi wa jirani yake, na kufanya mambo yote kwa ajili ya utukufu wa Mungu.”21

Pengine askofu wetu alijua hilo lilikuwa somo mimi na mume wangu tungejifunza kutokana na juhudi zile za mwanzo na zenye malengo mazuri, lakini zisizo kamilifu za kuhudumu kwa wana na mabinti wapendwa wa Mungu. Ninatoa ushahidi wangu binafsi na wa uhakika wa wema na upendo Anaoshiriki nasi hata pale tunapojitahidi kutumikia kwa ajili Yake. Katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.