Mkutano Mkuu
Njoo kwa Kristo—Kuishi kama Mtakatifu wa Siku za Mwisho
Mkutano mkuu wa Aprili 2020


Njoo kwa Kristo—Kuishi kama Mtakatifu wa Siku za Mwisho

Tunaweza kufanya mambo magumu na kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo, kwa sababu tunajua ni nani tunayeweza kumuamini.

Asante, Mzee Soares, kwa ushuhuda wako wa kinabii wenye nguvu, wa Kitabu cha Mormoni. Hivi karibuni, nilipata fursa ya kipekee ya kushika ukurasa wa muswada halisi wa Kitabu cha Mormoni. Kwenye ukurasa huu mahususi, kwa mara ya kwanza katika kipindi hiki cha maongozi ya Mungu, maneno haya ya kijasiri ya Nefi yaliandikwa: Nitaenda na kutenda vitu ambavyo Bwana ameamuru, kwani ninajua kwamba Bwana hatoi amri kwa watoto wa watu, isipokuwa awatayarishie njia ya kutimiza kitu ambacho amewaamuru.”1

Picha
Ukurasa wa Muswada halisi wa Kitabu cha Mormoni

Niliposhika ukurasa huu, nilijawa na shukrani kubwa kwa jitihada za kijana huyu wa umri wa miaka 23 Joseph Smith, ambaye alitafsiri Kitabu cha Mormoni kwa “kipawa na nguvu za Mungu.”2 Pia nilijisikia kuwa na shukrani kwa maneno ya kijana Nefi, ambaye aliagizwa kutekeleza kazi ngumu katika kuyapata mabamba ya shaba kutoka kwa Labani.

Nefi alijua kwamba kama ataendelea kubaki amefokasi kwa Bwana, angefanikiwa kutimiza kile ambacho Bwana alimuamuru. Alibakia mwenye kufokasi kwa Mwokozi maisha yake yote ingawa aliteseka kwa majaribu, mateso ya kimwili, na hata kusalitiwa na baadhi ya watu wa karibu wa familia yake.

Nefi alijua ni nani Yeye angeweza kumuamini.3 Muda mfupi baada ya kutamka kwa mshangao, “Ewe mimi mtu mwovu! Ndiyo, moyo wangu unahuzunishwa kwa sababu ya mwili wangu,”4 Nefi alieleza, “Mungu wangu amekuwa tegemeo langu; ameniongoza katika masumbuko yangu nyikani; na amenihifadhi kutoka kilindi kikuu cha maji.”5

Kama wafuasi wa Kristo, hatuna kinga dhidi ya changamoto na majaribu katika maisha yetu. Daima tumetakiwa kufanya mambo magumu ambayo, kama tungejaribu peke yetu, yangekuwa ya kuchosha na pengine yasiyowezekana. Tunapokubali mwaliko wa Mwokozi wa “njoo kwangu,”6 Yeye atatupa msaada, faraja, na amani ambayo ni muhimu, kama Alivyofanya kwa Nefi na Joseph. Hata katika majaribu yetu ya kina, tunaweza kuhisi joto la kumbatio la upendo Wake wakati tunapomwamini Yeye na kuyakubali mapenzi Yake. Tunaweza kupata shangwe iliyowekwa kwa ajili ya wafuasi Wake waaminifu, kwa kuwa “Kristo ni shangwe.”7

Mwaka 2014, wakati nikitumikia misheni, familia yetu ilipata mabadiliko ya matukio ambayo hayakutarajiwa. Wakati tukisafiri kushuka mteremko mkali wa kilima tukiwa juu ya ubao mrefu, mtoto wetu mdogo wa kiume alianguka na kupata majeraha kwenye ubongo yaliyotishia maisha yake. Hali yake ilipozidi kuwa mbaya, madaktari walimkimbiza kwenye upasuaji wa dharura.

Familia yetu ilipiga magoti chini katika chumba kilichokuwa wazi hospitalini hapo, na kumimina mioyo yetu kwa Mungu. Katikati ya wakati huu wa kukanganyikiwa na maumivu, tulijazwa na upendo na amani ya Baba yetu wa Mbinguni.

Hatukujua nini kingetokea baadaye au kama tungeliweza kumuona mtoto wetu akiwa hai tena. Tulijua kinagaubaga kwamba maisha yake yalikuwa mikononi mwa Mungu na matokeo, kwa mtazamo wa milele, yangefanya kazi kwa faida yake na yetu. Kupitia zawadi ya Roho, tulikuwa tumeandaliwa kikamilifu kukubali matokeo yoyote.

Haikuwa rahisi! Ajali ilipelekea kukaa hospitali miezi miwili wakati tukisimamia zaidi ya wamisionari 400. Mtoto wetu alipoteza kiasi kikubwa cha kumbukumbu. Kupona kwake kulijumuisha vipindi virefu na vigumu vya tiba ya mazoezi ya kuzungumza, na ya kimwili. Changamoto zilibakia, lakini baada ya muda tumeshuhudia muujiza.

Tunaelewa kwa uwazi kwamba si kila jaribu tunalokabiliana nalo litakuwa na matokeo tunayoyatamani. Hata hivyo, tunapobaki tumefokasi kwa Kristo, tutahisi amani na kuona miujiza ya Mungu, vyoyote vile itakavyokuwa, katika wakati Wake na katika njia Yake.

Kutakuwa na nyakati ambapo tutakuwa hatuwezi kuona njia yoyote ya hali fulani ya sasa kuisha vyema na tunaweza hata kusema, kama Nefi, “Moyo wangu unahuzunishwa kwa sababu ya mwili wangu.”8 Panaweza pakawa na nyakati ambapo tumaini pekee tulilo nalo ni tumaini katika Yesu Kristo. Ni baraka iliyoje kuwa na tumaini na imani hiyo katika Yeye. Kristo ndiye ambaye daima atatimiza ahadi Zake. Pumziko lake ni la uhakika kwa wote wanaokuja Kwake.9

Viongozi wetu kwa dhati wanatamani sisi sote tuhisi amani na faraja ambayo huja kwa njia ya kuamini katika na kwenye kufokasi katika Mwokozi Yesu Kristo.

Nabii aliye hai, Rais Russel M. Nelson, amekuwa akizungumza ono la Bwana kwa ulimwengu na kwa waumini wa Kanisa la Kristo: “Ujumbe wetu kwa ulimwengu ni rahisi na wa kweli: tunawaalika watoto wote wa Mungu kutoka pande zote mbili za pazia waje kwa Mwokozi wao, wapokee baraka za hekalu takatifu, wawe na furaha ya kudumu, na kustahili uzima wa milele.”10

Mwaliko huu wa “kuja kwa Kristo” una maana maalumu kwa Watakatifu wa Siku za Mwisho.11 Kama Waumini wa Kanisa la Mwokozi, tumefanya maagano na Yeye na tumekuwa wana na mabinti Zake kiroho.12 Pia tumepewa fursa ya kufanya kazi na Bwana katika kuwaalika wengine kuja Kwake.

Tunapofanya kazi na Kristo, kiini cha jitihada zetu za kina kinapaswa kuwa ndani ya nyumba zetu sisi wenyewe. Patakuwa na nyakati ambapo wanafamilia na marafiki zetu wa karibu watakabiliwa na changamoto. Sauti za ulimwengu, na pengine tamaa zao wenyewe, zinaweza kuwasababisha kuhoji ukweli. Tunapaswa kufanya kila tuwezalo kuwasaidia kuhisi vyote upendo wa Mwokozi na upendo wetu. Ninakumbushwa juu ya mstari wa maandiko ambao umekuwa wimbo wetu pendwa “Pendaneni,” ambao unatufundisha, “Kwa hili … watu wajue kwamba … ninyi ni wanafunzi wangu, kama mnapendana.”13

Katika upendo wetu kwa wale wanaohoji ukweli, adui wa furaha yote anaweza kujaribu kutufanya tujisikie kwamba tunawasaliti wale tunaowapenda ikiwa sisi wenyewe tunaendelea kuishi utimilifu wa injili na kufundisha ukweli wake.

Uwezo wetu wa kuwasaidia wengine kuja kwa Kristo au kurudi kwa Kristo kwa sehemu kubwa utaamuliwa na mfano tunaouonesha kupitia msimamo wetu wenyewe wa kubaki kwenye njia ya agano.

Kama hamu yetu ya kweli ni kuwaokoa wale tuwapendao, sisi wenyewe lazima tubaki imara kwa Kristo kwa kulikumbatia Kanisa Lake na utimilifu wa injili Yake.

Tukirudi katika hadithi ya Nefi, tunajua kwamba matakwa ya Nefi ya kuamini katika Bwana yalishawishiwa sana na hulka ya wazazi wake ya kuamini katika Bwana na mfano wao wa kushika maagano. Hili linaoneshwa vizuri sana katika ono la Lehi la mti wa uzima. Baada ya kula tunda tamu na la shangwe la mti, Lehi “alitupa macho [yake] hapa na pale, ili pengine [yeye] aione familia [yake].”14 Alimwona Saria, Samu, na Nefi wamesimama “kama hawajui wanapoenda.”15 Lehi kisha akaeleza, “Niliwapungia mkono; na pia kwa sauti kubwa nikawaambia wanikaribie, na wale tunda.”16 Tafadhali kumbuka kwamba Lehi hakuondoka kwenye mti wa uzima. Alibaki kiroho na Bwana na akaialika familia yake kuja pale yeye alipokuwepo ili wale tunda.

Mjaribu angewashawishi baadhi kuiacha furaha ya injili kwa kutenganisha mafundisho ya Kristo kutoka Kanisa Lake. Angetutaka sisi kuamini kwamba tunaweza kubakia imara kwenye njia ya agano sisi wenyewe, kwa njia yetu wenyewe ya kiroho, mbali na Kanisa la Bwana.

Katika siku hizi za mwisho, Kanisa la Kristo lilirejeshwa ili kuwasaidia watoto wa agano wa Kristo kubaki katika njia Yake ya agano.

Katika Mafundisho na Maagano tunasoma, “Tazama, hili ni fundisho langu—yeyote atubuye na kuja kwangu, huyo ndiye kanisa langu.”17

Kupitia Kanisa la Kristo, tunaimarishwa kupitia uzoefu wetu kama jumuiya ya Watakatifu. Tunaisikia sauti Yake kupitia manabii Wake, waonaji, na wafunuzi. Muhimu zaidi, kupitia Kanisa Lake tunapewa baraka zote muhimu za Upatanisho wa Kristo ambazo zinaweza kutambulika tu kwa njia ya kushiriki katika ibada takatifu.

Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho ni Kanisa la Kristo duniani, lililorejeshwa katika siku hizi za mwisho kwa ajili ya kuwanufaisha watoto wote wa Mungu.

Ninatoa ushahidi kwamba tunapokuja kwa Kristo na kuishi kama Watakatifu wa Siku za Mwisho, tutabarikiwa kwa ongezeko la upendo Wake, shangwe Yake, na amani Yake. Kama Nefi, tunaweza kufanya mambo magumu na kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo, kwa sababu tunajua ni nani tunayeweza kumuamini.18 Kristo ni nuru yetu, uzima wetu, na wokovu wetu.19 Katika Jina la Yesu Kristo, amina.