2023
Kujitegemea Kunatuimarisha Sisi
Agosti 2023


“Kujitegemea Kunatuimarisha Sisi,” Liahona, Agosti 2023

Ujumbe wa Kila Mwezi wa Gazeti la Liahona, Agosti 2023

Kujitegemea Kunatuimarisha Sisi

Picha
watu wawili wakiosha vyombo

Kujitegemea kunamaanisha kwamba tunaweza kukidhi mahitaji yetu wenyewe na ya familia zetu. Tunapojitegemea, tunaweza pia kumtumikia Bwana na kuwajali wengine vyema zaidi. Lakini kujitegemea haimaanishi kwamba tunahitaji kukabiliana na changamoto zetu peke yetu. Tunaweza kuomba msaada kutoka kwa marafiki, familia, washiriki wa kata au tawi, na wataalamu tunapohitaji msaada huo.

Kanuni za Kujitegemea

Kuwa mwenye kujitegemea kunahitaji elimu, utii, na bidii. Tunafanya kila tuwezalo kujijali wenyewe, na tunaweza kuwaomba wengine msaada wakati inapohitajika. Hata hivyo, ili kuwa mwenye kujitegemea kikamilifu, lazima pia tujifunze kuwa na imani katika Yesu Kristo. Kisha tunapofanya kazi ili kujisaidia wenyewe, Yeye atatuimarisha.

Picha
mikono miwili iliyokunjwa

Kujitegemea Kiroho

Tunaweza kujenga kujitegemea kwetu kiroho kwa kufanya kazi ili kuimarisha ushuhuda wetu wa Yesu Kristo. Tunafanya hivyo wakati tunapoomba, kujifunza maandiko, kuhudhuria kanisani, kutii amri, na kufanya mambo mengine ambayo yanatuleta karibu na Kristo. Kujua kwamba Yeye yuko tayari kutusaidia itatupa imani ya kubaki imara hata wakati maisha yanapokuwa magumu.

Kujitegemea Kimwili

Kujitegemea kimwili hujumuisha kuwa na uwezo wa kukidhi mahitaji yetu ya kimwili sisi wenyewe na ya familia yetu. Hii hujumuisha chakula, makazi, afya, na mahitaji mengine. Tunafanya hivyo kwa kupata elimu nzuri, kujifunza au kukuza ujuzi unaohitajika, kufanya kazi kwa bidii, kutumia muda wetu kwa busara, na kusimamia pesa zetu vizuri.

Picha
wanawake watatu wakitembea pamoja

Kujitegemea Kihisia

Kijitegemea kihisia ni uwezo wa kukabiliana na changamoto za kihisia kwa ujasiri na imani. Sote tuna changamoto na vikwazo. Shukrani kwa injili, tunajua tunaweza kuchagua jinsi ya kukabiliana nazo. Kujibu kwa imani katika Bwana huongeza uwezo wetu wa kukabiliana na shida zingine kwa matumaini zaidi.

Elimu

Tunapaswa kujifunza kila wakati. Mungu anataka tuelimishe akili zetu na tuboreshe ujuzi wetu katika maisha haya yote na katika siku zijazo. Kadiri tunavyojifunza zaidi, ndivyo tunavyoweza kuwa na ushawishi bora kwa wema na kujikimu sisi wenyewe, familia yetu, na wale walio na uhitaji.

Picha
mvulana akiwa amebeba begi

Baraka za Kujitegemea

Manabii wamefundisha kwamba tunapoboresha kujitegemea kwetu, tutabarikiwa na tumaini kubwa na amani. Tutaweza kuzisaidia familia zetu na wengine wenye uhitaji. Na tutabarikiwa kwa fursa zaidi na uwezo wa kuendelea kusonga mbele.

Nyenzo za Kanisa

Kigingi chako kinaweza kutoa vikundi vya kujitegemea. Hivi vinaweza kukufundisha kanuni za kujitegemea na ujuzi kama vile kusimamia pesa zako au kupata kazi bora. Unaweza kupata nyenzo husika katika Maktaba ya Injili. Chagua “Books and Lessons” na kisha “Self-Reliance.”