2010–2019
Kukaa katika Mungu na Kuziba Ufa
Oktoba 2017


Kukaa katika Mungu na Kuziba Ufa

Kristo ana uwezo wa kutuleta katika jumuiko la upendo kwa Baba na baina yetu.

Tunahitaji kila siku kuzidisha elimu yetu na utiifu kwa Baba wa Mbinguni. Uhusiano wetu na Yeye ni wa Milele. Sisi ni watoto Wake wapendwa na hiyo haitabadilika. Tutaweza kukubali kwa moyo mkunjufu mwaliko Wake kumkaribia na kisha kufurahia baraka Anazotaka kutupatia katika maisha haya na katika ulimwengu ujao?

Bwana alisema kwa Israeli ya kale na Anasema kwetu, “Ndio, Niliwapenda ninyi na upendo wa milele: kwa hiyo kwa upendo mkarimu nimewaleta.”1 Kama asemavyo Baba, Yeye pia alitwambia, “Wewe utakaa ndani Yangu, Nami ndani yako; kwa hiyo tembea Nami”2 Je, tunamwamini vya kutosha kukaa Naye na kutembea pamoja Naye?

Tupo hapa katika dunia hii kujifunza na kukua, na kujifunza na kukua ambako ni muhimu sana kutakuja kutokana na uunganisho wetu wa agano kwa Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo. Kutokana na uhusiano wetu wa uaminifu na Wao huja maarifa ya kiuungu, upendo, nguvu, na uwezo mkubwa wa kutumikia.

“Tumezungukwa na jukumu la kujifunza vyote ambavyo Mungu amefunua kumhusu Yeye mwenyewe.”3 Lazima tuelewe kwamba Mungu Baba alimwelekeza Mwanawe, Yesu Kristo, kuumba dunia kwa ajili ya kukua kwetu, kwamba Baba wa Mbinguni alimtoa Mwanawe kulipa matakwa ya haki kwa ajili ya wokovu wetu, na kwamba nguvu za ukuhani za Baba na Kanisa la kweli la Mwana pamoja na maagizo muhimu yalirejeshwa kwa ajili ya baraka zetu. Unaweza hisi kiasi cha upendo unaokuja kupitia haya maandalizi Yao kwa ajili ya shangwe na kukua kwetu? Tunapaswa kujua kwamba mpango wa wokovu wa Baba wa Mbinguni ni kwamba tunatii sheria na maagizo ya injili na basi kupata uzima wa milele na hivyo kuwa kama Mungu Alivyo.4 Hii ni furaha ya kweli na ya kudumu Baba wa Mbinguni anatupatia. Hakuna furaha nyingine ya kweli na ya kudumu.

Changamoto zinaweza kutuvuta kutoka katika njia hii ya furaha. Tunaweza kupoteza muunganiko wetu na Mungu wa uaminifu kama majaribu yatatupeleka katika vurugu badala ya kutupeleka katika magoti yetu.

Kipande hiki rahisi cha ufahamu kinatulazimu kuchunga baadhi ya vipaumbele:

Baadhi ya vitu ni vya msingi, baadhi si vya msingi.

Vitu vichache vinadumu, lakini vitu vingi havitadumu.5

Kina dada, ni nini kilicho na maana kwenu? Ni nini kilinachodumu kwenu? Kitu chenye thamani ya kudumu kwa Baba ni kwamba tunajifunza kumhusu Yeye, tunajinyenyekeza, na kukua katika kumtii kupitia uzoefu wa dunia. Anatuhitaji tubadilishe ubinafsi wetu kuwa huduma na hofu zetu kuwa imani. Hizi mada za kudumu zinaweza kututia majaribuni hata kwenye kiini chetu.

Ni sasa, tukiwa na mapungufu ya kidunia, kwamba Baba anatuomba kupenda wakati kupenda ni kitu kigumu sana, kutumika wakati kutumikia inashindikana, kusamehe wakati kusamehe ni kitu kinachotanua nafsi. Kivipi? Tunaweza kufanya vipi? Tunafikia kwa bidii msaada wa Baba wa Mbinguni, katika jina la Kristo, na kufanya vitu kwa njia Yake badala ya mapenzi yetu binafsi kwa majivuno.

Picha
Mtungi wa maji

Niligundua kiburi changu wakati Rais Ezra Taft Benson aliongelea kusafisha chombo cha ndani6 Nilijichukulia binafsi kama mtungi. Ningewezaje kutoa mabaki ya majivuno kutoka katika mtungi? Kujilazimisha binafsi kuwa mnyenyekevu na kujifanya kuwapenda wengine ni unafiki, na uongo na kwa kifupi haifai. Dhambi na kiburi chetu huleta ufa—au mwanya—kati yetu na kisima cha upendo wote, Baba yetu wa Mbinguni.

Ni upatanisho wa Mwokozi tu unaoweza kutusafisha dhambi zetu na kuziba mwanya au ufa.

Tunahitaji kuzungukwa na mikono ya upendo na mwongozo wa Baba yetu wa Mbinguni, na hivyo tunaweka mapenzi Yake kwanza kwa moyo uliyopondeka tukiomba kwamba Kristo atamwaga mito yenye maji ya kutakasa katika mtungi wetu. Kwa mara ya kwanza inaweza kuja tone kwa tone, lakini tanapofuta, tunapoomba na kutii, itakuja kwa wingi. Haya maji ya uhai yataanza kutujaza, na kwa kukingwa na upendo Wake, tunaweza toa mtungi wa nafsi yetu na kushiriki vilivyomo na wengine wenye kiu cha kuponywa, matumaini, na kujaliwa. Kadiri chombo chetu kinavyokuwa safi, mahusiano yetu ya kidunia yanaanza kupona.

Kuachana na ajenda zetu binafsi kunahitajika ili kutoa nafasi kwa mipango ya Mungu. Mwokozi, Ambaye huongea kwa niaba ya Baba, anatusihi, “Sogeeni karibu nami na mimi nitasogea karibu na nyinyi.”7 Kusogea karibu na Baba kunaweza kumaanisha kujifunza kweli Zake kupitia maandiko, kufuata ushauri wa kinabii, na kujitahidi kufanya mapenzi Yake kiukamilifu zaidi.

Je, tunaelewa kwamba Kristo ana uwezo wa kutuleta katika jumuiko la upendo kwa Baba na baina yetu? Yeye, kwa uweza wa Roho Mtakatifu, anaweza kutupa umaizi unaohitajika katika mahusiano.

Mwalimu wa Msingi aliniambia kuhusu uzoefu wa nguvu katika darasa lake la wavulana wa umri wa miaka 11. Mmoja kati yao ambaye nitamwita Jimmy alikuwa si mwanafunzi anayeshirikiana darasani. Jumapili moja, mwalimu alipata maono kuweka kando somo lake na kusema kwa nini alimpenda Jimmy. Aliongelea shukrani zake na imani yake kwa huyu kijana mdogo. Halafu mwalimu akawaomba wana darasa kumuambia Jimmy kitu ambacho walikipendelea kuhusiana na Jimmy. Wakati wana darasa, mmoja mmoja, wakimwambia Jimmy kwa nini alikuwa mtu maalum kwao,kijana aliinamisha kichwa chake na machozi yalianza kutiririka usoni kwake. Huyu mwalimu na darasa walijenga daraja katika moyo mpweke wa Jimmy. Upendo rahisi, ulikioneshwa kwa dhati, hutoa tumaini na thamani kwa wengine.Ninaita hii “kuziba ufa au mwanya”

Pengine maisha yetu katika ulimwengu uliopita, yaliweka shauku ya ukweli, upendo wa kudumu hapa duniani. Tumeumbwa na Mungu kutoa upendo na kupendwa, na upendo mkubwa zaidi huja wakati tu wamoja na Mungu. Kitabu cha Mormoni kinatualika “kupatana na [Mungu] kupitia upatanisho wa Kristo.”18

Isaya aliongea kuhusu wale wanaoishi kwa uaminifu sheria ya mfungo na hivyo kuwa kuziba ufa kwa vizazi vyao. Ndiyo wale ambao Isaya ameahidi, “watapajenga mahali palipokuwa ukiwa.”9 Katika namna hiyo hiyo, Mwokozi aliziba ufa au mwanya kati yetu na Baba wa Mbinguni. Yeye, kupitia upatanisho Wake, hutufungulia njia ya kushiriki nguvu za upendo wa Mungu na kwa kisha tuweze kurekebisha “mahali palipo ukiwa” katika maisha yetu binafsi. Kuponya mwanya wa mhemko baina yetu kunahitaji ukubali wetu wa upendo wa Mungu ukiambatana na kuondoa ubinafsi wetu na tabia za woga.

Usiku mmoja unaokumbukwa, ndugu na mimi tulitofautiana kuhusu suala la kisiasa. Kwa haraka na umakini alishambulia maoni yangu, akinikosoa tukiwa karibu kabisa na wanafamilia. Nilijihisi mjinga na nisiyejua—na labda nilikuwa hivyo. Usiku ule nilipopiga magoti kusali, niliharakisha kumueleza Baba wa Mbinguni jinsi gani huyu ndugu alikuwa mbishi. Niliongea tena na tena. Labda niliacha muda mfupi kulalamika, na Roho Mtakatifu alikuwa na nafasi kupata usikivu wangu—kwa sababu, nilishangaa, nilipojisika tena nikisema, “Yamkini Unanihitaji nimpende.” Mpende? Niliendelea kusali, nikisema kitu kama hiki, “Ni jinsi gani naweza kumpenda? Sifikirii kama hata ninampenda. Moyo wangu ni mgumu na hisia zangu zimeumizwa. Siwezi kufanya Hivyo.

Halafu, hakika kwa msaada wa Roho, Nilikuwa na wazo jipya niliposema, “Lakini Unampenda, Baba wa Mbinguni. Unaweza nipatia kiasi cha upendo Wako kwake—ili nimpende yeye pia?” Hisia zangu ngumu zililainika, moyo wangu ukaanza kubadilika na nikaanza kumuona mtu huyu katika njia tofauti. Nilianza kuhisi thamani yake halisi ambayo Baba wa Mbinguni aliona. Isaya anaandika, “Bwana atakapofunga mapigo ya watu wake, na kuliponya pigo la jeraha yao.”10

Baada ya muda, mwanya kati yetu ulizibwa kwa uzuri kabisa. Lakini hata kama hakukubali moyo wangu ulibadilika, nilijifunza kuwa Baba wa Mbinguni atatusaidia kupenda hata wale tunaofikiri hawapendeki kama tutaomba msaada Wake. Upatanisho wa Mwokozi ni mfereji wa mtiririko wa upendo daima kutoka kwa Baba wa Mbinguni. Lazima tuchague kukaa katika upendo huu ili kuwa na upendo kwa wote.

Tukitoa moyo wetu kwa Baba na Mwana, tunabadilisha dunia yetu—hata kama hali zinazotuzunguka hazijabadilika. Tunamkaribia Baba wa Mbinguni na kuhisi ukubali Wake ororo wa jitihada zetu za kuwa wafuasi wa kweli wa Kristo. Utambuzi wetu, kujiamini, na imani huongezeka.

Mormoni anatuambia tuombe kwa nguvu zetu zote za moyo kwa ajili ya upendo huu na tutakirimiwa juu yetu kutoka kwenye chanzo—Baba wa Mbinguni.11 Ni hapo tu ndipo tunaweza kuwa warekebishaji wa ufa katika mahusiano ya kidunia.

Upendo wa milele wa Baba yetu hutufikia, kuturudisha katika utukufu Wake na shangwe. Alimtoa Mwanawe wa Pekee, Yesu Kristo, kuziba ufa ambao umeachia kati yetu na Yeye. Muungano na Baba wa Mbinguni ni kiini cha upendo wa kudumu na dhumuni la milele. Lazima tufanye uunganisho Naye sasa kujifunza ni kitu kipi cha muhimu zaidi, kupenda kama Apendavyo na kukua na kuwa kama Yeye. Nashuhudia uhusiano mwaminifu na Baba wa Mbinguni na Mwokozi ni wa muhimu milele Kwao na kwetu. Katika jina la Yesu Kristo, amina