2010–2019
Mbali, Bali Pamoja
Oktoba 2017


Mbali, Bali Pamoja

Kanisani, licha ya tofauti zetu, Bwana anatutarajia kuwa kitu kimoja

Mnamo Juni 1994, nilikuwa nikiendesha gari kwa hamu nikirejea nyumbani kutoka kazini ili kutazama Runinga timu yetu ya soka ikicheza kwenye Kombe la Dunia. Mara baada ya kuanza safari yangu, niliona mtu kwa mbali kando ya barabara aliyekuwa akienda kwa kasi kwenye kiti chake cha magurudumu, ambacho niliona kimerembeshwa kwa bendera yetu ya Brazili. Nilijua papo kwamba alikuwa akienda nyumbani kutazama mechi!

Njia zetu zilipokutana, macho yetu yakakutana, na kwa sehemu ya sekunde, nilihisi kwa nguvu kuunganishwa na yule mtu! Tulikuwa tukienda katika mielekeo tofauti, hatukujuana, na tulikuwa na tofauti bayana ya kijamii na kimwili, lakini hamu yetu ya soka na upendo kwa nchi yetu ulitufanya kuhisi kuwa moja kwa wakati huo! Sijamuona mtu huyu tangu wakati huo, bali leo, miongo mingi baadaye, ningali ninaona yale macho na kuhisi muunganisho wa nguvu na yule mtu. Kwani, tulishinda mchezo huo na Kombe la Dunia mwaka huo!

Kanisani, licha ya tofauti zetu, Bwana anatutarajia kuwa kitu kimoja! Alisema kwenye Mafundisho na Maagano “muwe na umoja; na kama hamna umoja ninyi siyo wangu.”1

Sisi wote tunapoingia katika jumba la mikutano kuabudu kama kikundi, tunapaswa kuacha tofauti zetu nyuma, ikijumuisha bari, hali za kijamii, maegemeo ya kisiasa, na mafanikio yetu ya kielimu na ya kikazi na badala yake kuzingatia malengo yetu ya kiroho. Pamoja tunaimba nyimbo, tunatafakari kuhusu maagano sawa wakati wa sakramenti, na kwa pamoja tunasema “amina” inayosikika baada ya hotuba, masomo na maombi—kumaanisha kuwa kwa pamoja tunakubaliana na yale yaliyoshirikiwa.

Mambo haya tunayofanya kwa pamoja yanatusaidia kujenga hisia imara ya umoja katika mkusanyiko.

Hata hivyo, kile kinachoamua, kuimarisha au kuangamiza umoja wetu ni jinsi tunavyotenda tukiwa mbali na waumini wetu wa Kanisa. Kama sote tujuavyo, ni jambo lisiloepukika na la kawaida kwamba hatimaye tutazungumza kuhusu kila mmoja.

Ikitegemea kile tunachochagua kusema kumhusu mwingine, maneno yetu yatafanya“mioyo yao ifumwe pamoja kwa umoja,”2 kama vile Alma alivyofundisha wale aliowabatiza katika Maji ya Mormoni, au yatamomonyoa upendo, imani na nia njema ambayo inafaa kuwepo kati yetu.

Kuna maoni ambayo kwa ufiche huangamiza umoja, kama vile “ Ndiyo, yeye ni askofu mwema, ah, lakini ungemwona wakati alipokuwa mvulana!”

Aina ya kujenga ya hili inaweza kuwa “Askofu ni mwema, na amekomaa sana kwa ukomavu na busara kwa miaka hii.”

Mara nyingi tunapachika watu vitambulisho vya kudumu kwa kusema kitu kama “Rais wetu wa Muungano wa Usaidizi wa Kina Mama ameshapotea, ni mkaidi sana!” Kinyume na hayo, tunaweza kusema, “Rais wa Muungano wa Usaidizi wa Kina Mama hajakuwa anaweza kubadilika kwa urahisi; pengine anapitia changamoto fulani!”Acha tumsaidie na kumuunga mkono!”

Akina kaka na kina dada, hatuna haki ya kumsawirisha mtu yeyote, ikijumuisha kutoka miongoni mwa marafiki wa Kanisa, kama bidhaa baya! Badala yake, maneno yetu kuhusu binadamu wenzetu yanafaa kuonyesha imani yetu kwake Yesu Kristo na Upatanisho Wake, na kwamba ndani Yake na kwa kupitia Kwake, tunaweza kila mara kubadilika na kuwa bora!

Wengine huanza kukosoa na kugawanyika kutoka kwa viongozi wa Kanisa na waumini kuhusu vitu vidogo mno.

Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa mtu aliyeitwa Simonds Ryder, aliyekuwa muumini wa Kanisa mnamo 1831. Baada ya kusoma ufunuo kumhusu, alishangaa kuona kwamba jina lake likiwa limeandikwa vibaya Rider likiwa na herufi ibadala ya kuwa na herufi y. Jibu lake kwa tukio hili lilichangia yeye kumshuku nabii na hatimaye kulipelekea kumtesa Joseph Smith na kuanguka kutoka katika Kanisa.3

Inawezekana kuwa sote tunapata kukosolewa na viongozi wetu wa kidini, ambayo itakuwa tathmini kuhusu jinsi tulivyoungana nao.

Nilikuwa umri wa miaka 11 tu, lakini naweza kukumbuka kwamba miaka 44 iliyopita, jumba la mikutano ambapo familia yetu ilihudhuria kanisa lilihitaji urekebisho mkuu. Kabla ya mradi huo kuanza, kulikuwa na mkutano ambapo viongozi wenyeji na viongozi wa eneo walijadili jinsi waumini wangeshiriki kwa kazi ile. Baba yangu, ambaye awali alikuwa amesimamia kitengo hicho kwa miaka, alieleza hisia kwa nguvu kwamba kazi hii ifanywe na mkandarasi badala ya watu wasio na ustadi.

Si tu kwamba maoni yake yalikataliwa, bali tulisikia kwamba alikashifiwa vikali na kwa umma wakati huo. Sasa, huyu alikuwa mtu aliyejitolea kwa Kanisa na pia mstaafu wa Vita Vikuu vya II vya Dunia huko Uropa, aliyezoea kupinga na kupigania kile alichokiamini. Mtu angeshangaa kuhusu mjibizo wake baada ya tukio hili. Je, angeedelea kushikilia maoni yake na kuendelea kupinga uamuzi uliofanywa tayari?

Tulikuwa tumeona familia katika kata yetu zilizokuwa zimefifia katika injili na kuacha kuhudhuria mikutano kwa sababu hawakuweza kuwa wa mojawapo ya wale waliokuwa wakiongoza. Mimi mwenyewe pia nilishuhudia wengi wa marafiki zangu kutoka kwenye Msingi wakikosa kuwa waaminifu katika ujana wao kwa sababu wazazi wao waliona makosa katika wale waliokuwa ndani ya Kanisa.

Baba yangu, hata hivyo, aliamua kuwa na umoja na Watakatifu wenzetu. Na siku chache baadaye, wakati waumini wa kata walipokuwa wakikusanyika ili kusaidia kwenye ujenzi, “alialika” familia yetu kumfuata kwenda kwenye jumba la mikutano ambapo tungejitolea kusaidia kwa njia yoyote ile.

Nilighadhabika. Nihisi kumuuliza, “Baba, kwa nini tunaenda kusaidia ujenzi ikiwa ulipinga wauumini kuufanya?” Lakini taswira kwenye uso ilinizuia kufanya hivyo. Nilitaka iwe vyema wakati wa kuweka wakfu tena, Basi, kwa bahati nzuri, niliamua kunyamaza tu na kwenda kutoa msaada katika ujenzi!

Baba hakupata kuona kanisa jipya, kwa vile aliaga dunia kabla ya kumalizika kwa kazi hii. Lakini sisi kwenye familia, tukiongozwa na mama yetu, tuliendelea kufanya sehemu yetu hadi ilipokamilika, na hiyo ilituweka katika umoja baba yangu, pamoja na waumini wa Kanisa, na viongozi wetu, na muhimu zaidi, na Bwana!

Muda mfupi baada ya matukio Yake ya uchungu mwingi Gethsemane, wakati Yesu alipokuwa akiomba kwa Baba kwa ajili ya Mitume Wake na sisi wote, Watakatifu, Alisema “Wote wawe na umoja; kama wewe, Baba, ulivyo ndani yangu, nami ndani yako.4

Akina ndugu na dada, ninashuhudia kwamba tunapoamua kuwa na umoja na waumini na viongozi wa kanisa—sote tukiwa tumekusanyika pamoja na hasa tukiwa mbali—tutahisi pia kuunganishwa kikamilifu na Baba yetu wa Mbinguni na Mwokozi. Katika jina la Yesu Kristo, amina.