2010–2019
Je, tunamwamini Yeye? Ugumu ni Mzuri
Oktoba 2017


Je, Tunamwamini Yeye? Ugumu ni Mzuri

Bila kujali suala hili, ugumu unaweza kuwa mzuri kwa wale ambao watasonga mbele kwa imani na kumwamini Bwana na mpango Wake.

Kabla ya kuanza, kama mmoja anayetuwasilisha sisi wote tulioathiriwa na maangamizi ya tufani na mtetemeko ya hivi karibuni, ninatoa shukrani zangu za moyoni kwa watu wote wa Helping Hands na waratibu wao, ambao walitupatia msaada na tumaini.

Mnamo Oktoba 2006, nilitoa hotuba yangu ya kwanza kwenye mkutano mkuu. Nilihisi ujumbe muhimu kwa Kanisa kote duniani ilijumuisha dai kuwa “Bwana ana imani nasi!”

Hakika anatuamini kwa njia nyingi sana. Ametupa injili ya Yesu Kristo, na katika hiki kipindi cha maongozi, ukamilifu wake. Anatuamini sisi na mamlaka ya ukuhani Wake kamili pamoja na funguo kwa matumizi sahihi. Kwa uwezo huo, tunaweza kubariki, kuhudumu, kupokea ibada, na kuweka maagano. Anatuamini na Kanisa Lake la urejesho, pamoja na hekalu takatifu. Anawaamini watumishi Wake na nguvu za kuunganisha—kufunga duniani na kuweza kufunga mbinguni! Na hata ametuamini sisi kuwa wazazi wa duniani, walimu, na watunzaji wa watoto Wake.

Baada ya miaka hii ya huduma ya Uongozi Mkuu katika sehemu nyingi za ulimwengu, ninatangaza kwa ukweli kabisa; Anatuamini sisi.

Sasa swali kwa ajili ya mkutano huu ni “Je, tunamwamini Yeye?”

Je, tunamwamini Yeye?

Rais Thomas S. Monson mara nyingi ametukumbusha sisi “kumwamini Bwana kwa moyo wako wote; na usiegemee ufahamu wako binafsi.

“Katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako.

“Usiwe mwenye hekima machoni pako” (Mithali 3:5–7).

Je, tunaziamini amri Zake kuwa za manufaa kwetu? Viongozi wake, japo siyo wakamilifu, kutuongoza sisi vizuri? Ahadi zake kuwa za kweli? Tunaamini kwamba Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo wanatujua sisi na wanataka kutusaidia? Hata katikati ya majaribu, changamoto, na nyakati ngumu, bado tunamwamini Yeye?

Nikiangalia nyuma, nilijifunza baadhi ya masomo mazuri katika kipindi cha kigumu—nikiwa kijana, nikiwa misheni, nikianza kazi mpya, nikijaribu kutimiza wito wangu, kulea familia kubwa, au nikihangaika kujitegemea. Inaonekana wazi kwamba ugumu ni mzuri!

Ugumu ni Mzuri

Ugumu hutufanya kuwa shupavu, hutunyenyekeza, na hutupa nafasi ya kujidhihirisha wenyewe. Wapendwa wetu watangulizii wa mikokoteni walikuja kumjua Mungu katika upeo wa mateso yao. Kwa nini ilichukua sura mbili kwa Nefi na ndugu zake kupata mabamba ya shaba na aya tatu pekee kuandika juu ya familia ya Ishmaili ijiunge nao kwenda nyikani? (ona 1 Nefi 34; 7:3–5). Inaonekana Bwana alitaka kumuimarisha Nefi kupitia mateso ya kuyapata mabamba.

Vitu vigumu katika maisha yetu havipaswi kutushangaza. Mojawapo ya maagano ya mwanzo tuliyoweka na Bwana ni kuishi sheria ya dhabihu. Dhabihu kwa ufafanuzi inahusisha kutoa kitu cha kutamanisha. Kwa uzoefu tunaona ni gharama ndogo kulipa kulinganisha na baraka zinazofuata. Chini ya maelekezo ya Joseph Smith ilisemekana kwamba, “Dini ambayo haihitaji dhabihu ya vitu vyote haina nguvu ya kutosha kuzaa imani muhimu katika maisha na wokovu.”1

Washiriki wa Uungu si wageni kwa mambo magumu. Mungu Baba alimtoa dhabihu Mwanawe wa Pekee kwenye mateso makali ya Upatanisho, yakiwemo kifo cha kusulubiwa. Maandiko yanasema Yesu Kristo alijifunza “kutii kwa mateso hayo yaliyompata” (Waebrania 5:8). Aliteseka kwa hiari Yake uchungu wa Upatanisho. Roho Mtakatifu lazima awe na uvumilivu ili kuhamasisha, kutuonya, na kutuongoza, kwa wakati mwingine kupuuzwa, kutafsiriwa tofauti, au kusahaulika.

Sehemu ya Mpango

Ugumu ni sehemu ya mpango wa injili. Mojawapo ya malengo ya maisha haya kwetu ni kujaribiwa (ona Ibrahimu 3:25). Wachache wameteseka sana pasi kustahili kuliko watu wa Alma. Walikimbia kutoka kwa Mfalme muovu Nuhu, tu kuwa watumwa wa Walamani. Kupitia hayo majaribu, Bwana aliwafundisha kwamba Anawarudi watu Wake na kujaribu uvumilivu wao na imani yao (Mosia 23:21).

Wakati wa siku za hatari katika Jela ya Liberty, Bwana alimfundisha Joseph Smith “kuvumilia vyema” (M&M 121:8) na aliahidi kwamba kama atafanya hivyo, “mambo haya yote yatakupa wewe uzoefu, na yatakuwa kwa faida yako” (M&M 122:7).

Rais Thomas S. Monson ameomba, “Natuweze daima kuchagua yaliyo magumu ya haki, badala ya yaliyo rahisi ya makosa.”2 Kuhusu mahekalu yetu, alisema kuwa “hakuna dhabihu iliyo kubwa mno, hakuna deni nzito sana, hakuna mahangaiko magumu sana, ili kupata baraka za [hekalu]”3

Katika ulimwengu wa asili, ugumu ni sehemu ya mzunguko wa maisha. Ni vigumu kwa kifaranga kuangua kutoka nje ya shayiri yake. Lakini wakati mtu anapojaribu kufanya iwe rahisi, kifaranga hakipati nguvu ya kuweza kuishi. Kwa namna hiyo, mapambano ya kipepeo kuepuka kifukofuko huimarisha maisha ambayo ataishi.

Kupitia mifano hii, tunaona kwamba ugumu ni kisiobadilika! Sisi wote tunazo changamoto. Kigeugeu ni mjibizo wetu wa ugumu.

Wakati fulani baadhi ya watu wa Kitabu cha Mormoni walipata “mateso makubwa” na “huzuni kubwa.”(Helamani 3:34). Je, walijibu vipi? “Walifunga na kuomba kila wakati, na wakapokea nguvu zaidi na zaidi katika unyenyekevu wao, na wakawa imara zaidi na imara katika imani ya Kristo, hadi nafsi zao zikajazwa na shangwe na faraja” (Helamani 3:35). “Kwa sababu ya muda mrefu wa vita kati ya Wanefi na Walamani wengi wamekuwa na roho ngumu, … na wengi walilainishwa kwa sababu ya mateso yao, kiasi kwamba walijinyenyekeza mbele ya Mungu” (Alma 62:41).

Kila mmoja wetu anachagua mjibizo wetu kwa ugumu.

Kuwa Mwangalifu na Urahisi

Kabla ya wito huu nilikuwa mshauri wa fedha huko Houston, Texas. Kazi yangu zaidi ilikuwa na mamilionea ambao wanamiliki biashara zao wenyewe. Karibu wote walianzisha biashara zao zilizofanikiwa wakiwa hawana kitu bali kupitia kazi ngumu.Kitu cha kusikitisha kwangu ilikuwa kuwasikia baadhi yao wakisema kwamba walitaka iwe rahisi kwa watoto wao. Hawakutaka watoto wao kutaabika kama walivyotaabika. Kwa maneno mengine, walitaka kuwaepusha watoto wao kila kitu kilichowafanya wafanikiwe.

Kwa upande mwingine, tunaijua familia ambayo ilichukua njia tofauti. Wazazi walivutiwa na uzoefu wa J. C. Penney ambaye baba yake alimwambia yeye alipofikisha miaka nane alikuwa ajitegemee kifedha. Walikuja na toleo lao wenyewe: watoto wao wanapohitimu kutoka shule ya sekondari, walikuwa wajitegemee kifedha—kwa ajili ya elimu zaidi (chuo, chuo kikuu) na kwa ajili ya mahitaji yao ya kifedha (kujitegemea kweli) (ona M&M 83:4). Kwa furaha, watoto walijibu kwa busara. Wote wamemaliza chuo, na baadhi pia wamemaliza elimu ya juu—wote kwa kujitegemea wenyewe. Haikuwa rahisi, lakini walifanya hivyo. Walifanya hivyo kupitia kazi ngumu na imani.

Imani ya Kumwamini Yeye

Swali, “Je, tunamwamini Yeye? linaweza kusema vizuri, “Je, sisi tuna imani ya kumwamini Yeye?

Je, tuna imani ya kuamini ahadi zake kuhusiana na zaka kwamba asilimia 90 ya nyongeza yetu pamoja na msaada wa Bwana tupo vizuri kuliko asilimia 100 tukijitegemea wenyewe?

Je, tuna imani ya kutosha kuamini kwamba Atatutembelea katika shida zetu (ona Mosia 24:14), kwamba Atashindana na wale wanaoshindana nasi (ona Isaya 49:25; 2 Nephi 6:17), na kwamba atatakasa mateso yetu kwa faida yetu? (Ona 2 Nefi 2:2).

Tutaonyesha imani yetu ili kutii amri ili aweze kutubariki sisi kimwili na kiroho? Na tutaendelea na wema hadi mwisho ili kwamba aweze kutupokea katika uwepo Wake? (ona Mosia 2:41).

Ndugu na dada, tunaweza kuwa na imani ya kumwamini Yeye! Anahitaji kilicho bora kwetu (ona Musa 1:39). Atayajibu maombi yetu (ona M&M 112:10). Atatimiza ahadi Zake (ona M&M 1:38). Ana uwezo wa kutimiza ahadi hizo (ona Alma 37:16). Yeye anajua kila kitu!. Na muhimu zaidi, Anajua nini kizuri (ona Isaya 55:8–9).

Dunia Hatari

Ulimwengu wetu leo ni mgumu. Tuna uovu unaoenea, ufisadi katika kila taifa, ugaidi kufika hata mahali salama, mdororo wa uchumi, ukosefu wa ajira, magonjwa, maafa ya asili, vita vya wenyewe kwa wenyewe, viongozi dhalimu, na alkadhalika. Tunatakiwa kufanya nini? Tunakimbia au tunapigana? Kipi sahihi? Chaguo lolote linaweza kuwa hatari. Ilikuwa hatari kwa George Washington na majeshi yake kupigana lakini piakwa watangulizi wahenga wetu kukimbia. Ilikuwa hatari kwa Nelson Mandela kupigania uhuru. Imesemekana kwamba ili uovu utawale, ni lazima watu wema wasifanye chochote.4

Usiogope!

Kwa lolote tufanyalo, hatutakiwi kuamua wala kutenda kwa roho wa woga. Hakika, “Mungu hakutupa Roho ya uwoga” (2 Timotheo 1:7). (Je, unagundua kuwa dhana ya “usiogope” imesisitizwa kote katika maandiko?) Bwana amenifunza mimi kwamba kukata tamaa na woga ni zana za adui.Jibu la Bwana katika nyakati ngumu ni kusonga mbele kwa imani.

Ni nini Kigumu?

Kila mmoja wetu anaweza kuwa na wazo tofauti kuhusu nini kigumu. Wengine wanafikiria ni vigumu kulipa zaka wakati kuna shida ya hela. Viongozi wakati mwingine wanaona vigumu kutarajia maskini kulipa zaka. Inaweza kuwa vigumu kwa baadhi yetu kusonga mbele kwa imani kuoa/kuolewa au kuwa na familia.Kuna wale wanaoona vigumu “kutosheka [na] vitu ambavyo Bwana amewapatia [wao]” (Alma 29:3). Inaweza kuwa vigumu kutosheka na wito wetu wa sasa (ona Alma 29:6). Nidhamu ya Kanisa inaweza kuonekana ngumu sana, lakini kwa baadhi inaashiria mwanzo wa mchakato wa toba ya kweli.

Bila kujali suala hili, ugumu unaweza kuwa mzuri kwa wale ambao watasonga mbele kwa imani na kumwamini Bwana na mpango Wake.

Ushahidi Wangu

Ndugu zangu na dada zangu, ninatoa ushahidi kwamba viongozi hawa walioketi nyuma yangu wameitwa na Mungu. Matamanio yao ni kumtumikia Bwana vizuri na kusaidia kuanzisha injili katika mioyo yetu. Ninawapenda na kuwakubali.

Ninampenda Mwokozi wetu, Yesu Kristo. Ninashangaa kwamba Yeye alimpenda Baba na sisi na kuwa Mwokozi na Mkombozi wetu, na kwa kufanya hivyo alipaswa kuteseka hivyo kumsababisha “kutetemeka kwa sababu ya maumivu, na kutokwa damu katika kila kinyweleo, na kuteseka mwili wote na roho” (M&M 19:18). Hata hivyo akikabiliwa na matarajio haya mabaya na muhimu kwake, alimwambia Baba, “walakini si mapenzi yangu, bali yako yatendeke” (Luka 22:42). Ninashukuru kwa maneno ya malaika: “Hayupo hapa, kwani amefufuka” (Mathayo 28:6).

Mfano wake hakika ni “njia, kweli na uzima” (Yohana 14:6). Ni kwa kufuata mfano huo tunaweza kupata “amani katika ulimwengu huu na uzima wa milele katika ulimwengu ujao” (M&M 59:23). Wakati ninapokuwa nimefuata mfano Wake na kutumia mafundisho Yake, nimejifunza mwenyewe kwamba kila mojawapo wa “baraka Zake kuu zaidi na za thamani” (2 Petro 1:4) ni kweli.

Matamanio yangu makubwa ni kusimama na Mormoni kama mfuasi wa kweli ya Yesu Kristo (ona 3 Nefi 5:13) ili siku moja nisikie kutoka kwa mdomo Wake, “Vema, mtumishi mwema na mwaminifu” (Mathayo 25:21). Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Ona Lectures on Faith (1985), 69.

  2. Thomas S. Monson, “Choices,” Liahona, May 2016, 86.

  3. Thomas S. Monson, “The Holy Temple—a Beacon to the World,” Liahona, May 2011, 92.

  4. Ona John Stuart Mill, Inaugural Address: Delivered to the University of St. Andrews, Feb. 1, 1867 (1867), 36.