2022
Uumbaji
Januari/Februari 2022


Njoo, Unifuate

Uumbaji

Mwanzo 1–2; Musa 2–3; Ibrahimu 4–5

Picha
earth with sun and moon

Dunia iliumbwa na Yesu Kristo chini ya maelekezo ya Baba wa Mbinguni ili kwamba tuweze kuwa na mahali pa kuishi, kujifunza na kutumia haki yetu ya kujiamulia kufanya chaguzi nzuri (ona Ibrahimu 3:24–26).

“Nabii Joseph Smith alifundisha kwamba kuumba … haimaanishi kuumba kutokana na kitu ambacho hakipo, inamaanisha kupangilia, sawasawa na vile ambavyo mwanadamu angepangilia vifaa na kujenga merikebu.”1 Neno la Kiebrania la “umba” humaanisha kuipa muundo, mtindo, mpangilio na umbo (ona Mwanzo 1:1; Ibrahimu 3:24).

Rais Russell M. Nelson alieleza kwamba “Uumbaji halisi wenyewe uliwekwa kwenye hatua kupitia vipindi vilivyopangwa vya wakati,” siyo siku za kalenda. “Iwe viliitwa siku, wakati, au miaka, kila kipindi [cha Uumbaji] kilikuwa kipindi kati ya matukio mawili yaliyotambulika—mgawanyiko wa umilele.”2

Siku ya Kwanza: Nuru na Giza

“Mungu akasema, Iwe nuru,” “akatenga nuru na giza,”akaiita nuru Mchana, na giza akaliita Usiku (ona Mwanzo 1:3–5).

Siku ya Pili: Maji na Mbingu

Mungu aliyatenga maji na mbingu. “Mungu, akasema: Na liwe anga katikati ya maji. … Na Mungu akaliita anga Mbingu.” (Ona Mwanzo 1:6–8.)

Siku ya Tatu: Bahari na Dunia

“Mungu akapaita pale pakavu Nchi; na … makusanyiko ya maji akayaita Bahari ” (Mwanzo 1:10). Dunia kisha ilikuwa tayari kwa ajili ya maisha ya mimea (ona Mwanzo 1:11–12).

Siku ya Nne: Jua na Majira

Mungu alifanya jua, mwezi na nyota “ili itenge kati ya mchana na usiku”; nayo “iwe ndiyo dalili na majira na siku na miaka” (ona Mwanzo 1:14–16).

Siku ya Tano: Viumbe Hai

Mungu aliumba “kila kiumbe chenye uhai kiendacho” (Mwanzo 1:21). Viumbe hawa waliamriwa kuongezeka na kuijaza dunia na bahari (ona Mwanzo 1:22).

Siku ya Sita: Adamu na Hawa

Uumbaji wa Mungu wa maisha uliendelea kwa “mnyama wa kufugwa wa dunia,” navyo “vitambaavyo,” na “wanyama wa mwitu” (Ibrahimu 4:24–25). Kisha alimuumba Adamu na Hawa “katika mfano wa mwili wake yeye mwenyewe” (Musa 6:9) na aliwaamuru “kuzaa, kuijaza nchi, na kuitiisha; … na kutawala kila kiumbe chenye uhai” (Mwanzo 1:28).

Siku ya Saba: Siku ya Mapumziko

Baada ya kukamilisha kazi Yake, Mungu alipumzika siku ya saba. “Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya” (Mwanzo 2:3).

Mungu baadaye aliamuru kwamba “tuikumbuke siku ya sabato na kuitakasa” (Kutoka 20:8).

Tunaweza kuitakasa siku ya Sabato kwa kutenga muda kuhudhuria kanisani, kupokea sakramenti na kumkumbuka Mwokozi. Bwana alifundisha, “Kwani amini hii ndiyo siku iliyoteuliwa kwako kupumzika kutokana na kazi zako, na utoe dhabihu zako za shukrani kwa Aliye Juu sana” (Mafundisho na Maagano 59:10).

Katika siku ya Sabato, “mawazo yetu, matendo, na mwenendo ni ishara tunayompa Mungu na kielelezo cha upendo wetu Kwake.”3

Muhtasari

  1. Mahubiri ya Joseph Smith, yaliyotolewa mnamo Apr. 7, 1844, katika History, 1838–1856, juzuu E-1 [1 Julai 1843–30 Aprili 1844], ukurasa wa 1973, josephsmithpapers.org.

  2. Russell M. Nelson, “Uumbaji,” Liahona, Julai 2000, 103.

  3. David A. Bednar, “Ahadi Nyingi Kuu na za Thamani,” Liahona, Nov. 2017, 92; ona pia Russell M. Nelson, “Sabato ni ya Furaha,” Liahona, Mei 2015, 130.