2022
Kutafuta Njia ya Furaha
Januari/Februari 2022


Kutafuta Njia ya Furaha

Tunaweza kukuza watoto waadilifu, wenye tumaini popote pale ulimwenguni ikiwa wana msingi imara katika Mwokozi.

Picha
African family praying

Picha na Jim Lillywhite

Miaka mingi iliyopita, baadhi ya binamu zangu wadogo walipangiwa kufanya mradi wa huduma kwenye shamba la Babu yetu Crozier Kimball. Kama malipo, waliahidiwa keki nzuri ya Bibi Clara1 iliyotengenezwa nyumbani.

Wakati walipokamilisha majukumu yao, walielekea jikoni kwa ajili ya zawadi yao. Babu, hata hivyo, aliziba mlango wa jikoni. Binamu yangu Kathy Galloway, ambaye alikuwa na takriban miaka 14 wakati huo, anakumbuka kwamba babu aliketi kwenye meza ya piano na kuwaalika akina binamu kuketi sakafuni. Aliwashukuru kwa kazi yao kubwa na kisha akasema kuwa alikuwa na jambo la muhimu la kushiriki kabla hawajala keki.

“Kutakuwa na wakati katika maisha yenu ambapo mtatakiwa kujua na kutenda juu ya kile ninachotaka kushiriki nanyi,” alisema.

Alielezea kwamba babu yake, Heber C. Kimball (1801–68) pamoja na mababu wengine watangulizi walikabiliwa na changamoto ngumu ya kimwili. Babu alisema watangulizi kwa haraka walijifunza kwamba ili kusalimika, walipaswa kufanya kazi pamoja na kupendana na kutumikiana kila mmoja.

“Huu ni moja ya urithi mkubwa waliowaachia ninyi!” alisema wakati machozi yakianza kutiririka mashavuni mwake.

“Katika wito wangu kama patriaki na kama babu yenu, wakati ninapotazama siku za nyuma, … moyo wangu unaumia kwa ajili yenu,” alisema. “Mtakabiliwa na changamoto za kihisia na kiroho ambazo wengi wa mababu zenu watangulizi kamwe hawangeweza kuzifikiria.”

Isipokuwa kizazi kichanga kiheshimu urithi mkuu wa upendo na huduma ya watangulizi, aliongeza, “wengi wenu mtashindwa kwa sababu hamtaweza kusalimika ninyi wenyewe.”

Kisha, kwa muunganiko wa roho na roho, Babu Kimball alihitimisha: “tunahitajiana. Katika kuongezea kwenye kushiriki shuhuda zetu za injili kwa kila mmoja, wajibu wetu ni kupendana na kutumikiana na kuimarishana na kustawishana na kuungana mkono na kuidhinishana, … hususani katika familia yetu. Tafadhali kumbukeni kuwa katika siku za mwisho, kusalimika kwenu hasa kunaweza kutegemea utayari wenu wa kufanya kazi pamoja na kupendana na kutumikiana. Sasa, twendeni tukale keki!”

Tunamuhitaji Kila Mmoja.

Picha
group of people in India

Picha na Wendy Gibbs Keeler

Kama vile ilivyooneshwa kwa vurugu za ulimwengu ambazo zinatuzunguka na kama vile Babu Crozier Kimball alivyoona yajayo, tunahitajiana. Tunahitaji familia zenye upendo, akidi na Vikundi vya Usaidizi vilivyojaa huduma na matawi, kata na vigingi vyenye kutoa usaidizi.

“Mungu anatutaka sisi tufanye kazi kwa pamoja na kusaidiana,” Rais Nelson amesema. “Hiyo ndiyo sababu Anatuleta duniani katika familia na kutuweka kwenye kata na vigingi. Hiyo ndiyo sababu Anatutaka tutumikiane na kuhudumiana. Hiyo ndiyo sababu Anatutaka tuishi katika ulimwengu lakini sio kuwa wa ulimwengu. Tunaweza kutimiza mengi zaidi pamoja kuliko tunavyoweza kipekee.”2

Maisha katika hali yetu ya pili ni magumu. Kwa sababu ya Anguko la Adamu na Hawa, tunakabiliana na miiba na michongoma na majaribu. Uzoefu wa namna hiyo ni sehemu ya mpango wa furaha, lakini tunasaidiana kuepuka dhoruba za maisha.

Kama vile Adamu na Hawa, ambao “walitolewa katika bustani ya Edeni” (Mwanzo 3:23), sisi tumetolewa kutoka nyumbani kwetu pa maandalizi kabla ya maisha ya duniani kuja kwenye dunia hii iliyoanguka. Na kama vile Adamu na Hawa, tunafurahi katika ufahamu wetu wa mpango wa Mungu kwa ajili ya watoto Wake:

“Na katika siku ile Adamu alipombariki Mungu naye akajawa na Roho Mtakatifu, na akaanza kutoa unabii kuhusu familia zote za dunia, akisema: Na libarikiwe jina la Mungu, kwani kwa sababu ya uvunjaji wangu wa sheria macho yangu yamefunguliwa, na katika maisha haya nitakuwa na shangwe, na tena katika mwili nitamwona Mungu.

“Naye Hawa, mke wake, alisikia mambo haya yote na akafurahi, akisema: Kama isingelikuwa kwa uvunjaji wetu wa sheria kamwe tusingelikuwa na uzao, na kamwe tusingelijua mema na maovu, na shangwe ya ukombozi wetu, na uzima wa milele ambao Mungu huutoa kwa wote walio watiifu” (Musa 5:10–11; ona pia 2 Nefi 2:25).

“Sehemu ya Lengo Lake Takatifu”

Kuleta “kutokufa kwetu na uzima wa milele” ndiyo “kazi na … utukufu” wa Baba yetu (Musa 1:39). “Sisi ni,” kama Rais Nelson alivyofundisha, “sehemu ya lengo Lake takatifu.”3

Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili umetangaza kwamba kama wana na mabinti wa kiroho katika maisha kabla ya kuja duniani “tulimjua na kumwabudu Mungu kama Baba [yetu] wa Milele na kukubali mpango Wake ambao ungewezesha watoto Wake kupokea mwili na kupata uzoefu wa dunia ili kukua kwa ukamilifu na hatimaye kutambua maisha yao matakatifu kama warithi wa maisha ya milele.”4 Na Rais Dallin H. Oaks, Mshauri wa Kwanza katika Urais wa Kwanza, hivi karibuni alifundisha, “Chini ya mpango wa Baba yetu wa Mbinguni, [Yesu Kristo] ‘aliumba mbingu na dunia’ (Mafundisho na Maagano 14:9) ili kwamba kila mmoja wetu aweze kupitia maisha ya duniani yaliyo muhimu katika kutafuta hatima yetu ya kiungu.”5

Maandiko pamoja na manabii wa siku za mwisho wanaweka wazi jukumu muhimu ambalo miili yetu hutimiza katika mpango wa Mungu. Hatima yetu ni kurudi kwenye uwepo Wake tukiwa na miili iliyofufuka, iliyoinuliwa na kuishi kama familia milele.

“Uhusiano wetu na watu wengine, uwezo wetu wa kugundua na kutenda kufuatana na ukweli, na uwezo wetu wa kutii kanuni na ibada za injili ya Yesu Kristo zinakuzwa kupitia maumbile ya kimwili,” alisema Mzee David A. Bednar wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili. “Katika shule ya maisha ya duniani, tunapata uzoefu wa huruma, upendo, upole, furaha, huzuni, masikitiko, maumivu, na hata changamoto za mapungufu ya kimwili katika njia ambazo zinatutayarisha kwa ajili ya maisha ya milele.”6

Fundisha kuhusu Kristo

Picha
a family sitting around a table

Katika siku hizi za hofu na wasiwasi, ufahamu wa mpango wa furaha ni muhimu kwa ajili ya kusalimika kwetu kiroho. Lakini hatuwezi kutarajia ulimwengu uwastawishe watoto wetu kwa kanuni za furaha ya milele. Kama wazazi, tunahitaji kuwafunza watoto wetu kuhusu asili yao ya kiungu na hatima ya kiungu.

Tunaanza kwa kuwasaidia kujenga ushuhuda wa Yesu Kristo na Upatanisho Wake, ambavyo ni muhimu kwenye mpango wa wokovu. Ninaamini tunaweza kukuza watoto waadilifu, wenye tumaini popote ulimwenguni ikiwa tutakuwa na msingi imara katika Mwokozi.

Katika jioni ya nyumbani, wakati wa sala ya familia na kujifunza maandiko kifamilia, kupitia shughuli na tamaduni za familia na hata nyakati za masahihisho, “tunazungumza kuhusu Kristo, tunafurahia katika Kristo, tunahubiri kuhusu Kristo, tunatoa unabii kumhusu Kristo, … ili watoto wetu waweze kujua ni chanzo gani wanaweza kutafuta kwa ajili ya msamaha wa dhambi zao” (2 Nefi 25:26).3

Tunawasaidia watoto wetu waelewe kwamba katika mpango wa wokovu, toba ni “mtaala wa maisha yote”7 ambao huleta tumaini na uponyaji wakati inapoondoa mzigo nafsini na kuangaza wakati ujao.

Wakati watoto wetu wanapojenga imani katika Upatanisho wa Kristo, watakuja kuelewa kwamba yote kamwe hayajapotea na kwamba Bwana anawangojea kwa mikono iliyokunjuliwa. Tunawasaidia waelewe kwamba “chochote ambacho lazima [tuache] nyuma ili kuifuata njia ya nyumbani [kwetu] mbinguni siku moja kitaonekana kama si dhabihu kabisa.”8

Kusanya Watoto wa Mungu

Hatufikii hatima yetu ya kiungu peke yetu. Kama Watakatifu wa Siku za Mwisho, tuna wajibu maalum wa kuwaalika wengine katika safari yetu ya nyumbani kwetu mbinguni. Ulimwengu unahitaji Watakatifu wa Siku za Mwisho ambao wako radhi kuruhusu nuru ya Urejesho iangaze kupitia shuhuda zao, mifano na utayari wao wa kushiriki injili. Tunapoangaza, tunakusanya.

“Tunapozungumza kuhusu kukusanyika,,” alisema Rais Nelson “kiurahisi tunamaanisha ukweli huu muhimu: Kila mmoja wa watoto wa Baba yetu wa Mbinguni, katika pande zote za pazia, anastahili kusikia ujumbe wa injili ya urejesho ya Yesu Kristo. Wanajiamulia wao wenyewe ikiwa wanataka kujua zaidi.”9

Na kwa hiyo kama jinsi Babu Crozier alivyoshauri, tunashiriki shuhuda zetu za injili ya Yesu Kristo. Tunapenda na kuhudumu, kuimarisha na kustawisha na kuwaunga mkono na kuwaidhinisha wapendwa wetu na jirani zetu.

Tunapowasaidia wengine kwenye njia ya kuelekea hatima yao ya kiungu, tunajisaidia wenyewe kwenye njia hiyohiyo, “kupokewa katika ufalme wa Baba kutotoka tena, lakini kuishi na Mungu milele mbinguni” (3 Nefi 28:40).

Muhtasari

  1. Baada ya mke wa kwanza wa Babu Crozier Kimball, Mary Lenora Roberts kufariki, alimuoa Clara, binamu wa mke wake wa kwanza. Watoto walimwita “Shangazi Clara.” Wajukuu walimwita “Bibi.”

  2. Russell M. Nelson, “Ni Kipi Tunajifunza na Kamwe Hatuwezi Kusahau,” Liahona, Mei 2021, 79.

  3. Russell M. Nelson, “Mwili Wako: Zawadi Tukufu ya Kuthamini,” Liahona, Aug. 2019, 50.

  4. “Familia: Tangazo kwa Ulimwengu,” ChurchofJesusChrist.org.

  5. Dallin H. Oaks, “Ni kipi Mwokozi Wetu Amefanya kwa Ajili Yetu?,” Liahona, Mei 2021, 77.

  6. David A. Bednar, “Tunaamini katika Kuwa Wasafi,” Liahona,, Mei 2013, 41.

  7. Lynn G. Robbins, “Hata Saba mara Sabini,” Liahona, Mei 2018, 22.

  8. José A. Teixeira, “Kumbuka Njia Yako ya Kurudi Nyumbani,” Liahona, Mei 2021, 94.

  9. Russell M. Nelson, “Tumaini la Israeli” (mkutano wa ibada wa vijana ulimwenguni kote, Juni 3, 2018), HopeofIsrael.ChurchofJesusChrist.org.