2023
Kuipeleka Injili Kongo
Desemba 2023


Kihistoria

Kuipeleka Injili Kongo

Mwanzoni mwa miaka ya 1960, watu waliokuwa wakiishi katika nchi ijulikanayo leo kama Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (iliyojulikana kama Zaïre toka 1971 mpaka 1997) walianza kuwasiliana na makao makuu ya Kanisa. Ingawa Kanisa halikuwepo katika nchi hiyo, wawakilishi wa Kanisa walituma vitabu na kuwatia moyo wale waliokuwa wakituma barua. Wengi wao walianza kufundisha injili na kuanzisha mikusanyiko isiyo maalumu. Katika kujibu jitihada hizi, viongozi wa Kanisa walituma wawakilishi kuanzisha kujulikana rasmi kuanzia mwaka 1979 na kuendelea mpaka katikati ya miaka ya 1980.

Wakati huo huo, wahamiaji wengi wa Kongo walijiunga na Kanisa huko Ulaya na Marekani. Mbuyi Nkitabungi alibatizwa huko Ubelgiji mnamo 1980, akahudumu kama mmisionari huko Uingereza, na kisha alipata msukumo kurejea nyumbani mnamo 1985. “Moja ya malengo mema ni kujenga … Sayuni katika ardhi ya Zaïre,” aliyaandikia makao makuu ya Kanisa. “Ninajua kuna angalau waumini wachache kwenye nchi yangu ambao wanasubiri fursa hiyo.… Niambieni kila kitu ninachotakiwa kufanya.”

Nkitabungi aliwekwa kwenye mawasiliano na waumini wengine wa huko Kinshasa, ambao walikutana katika nyumba ya Mike na Katie Bowcutt, wanandoa kutoka Amerika. Kama Nkitabungi, waumini wengi walikuwa Watakatifu wa Kikongo ambao walijiunga na kanisa wakiwa nje ya nchi. Kwa sababu Kanisa lilikuwa bado halitambuliki kisheria, waumini hawakufanya vikao vya umma. Hata hivyo, kundi kwa haraka liliongezeka kuzidi makazi ya akina Bowcutts na kuhamishia mikutano yao katika gereji ya Nkitabungi.

Mnamo Februari 1986 rais wa nchi aliahidi wakati wa matangazo yaliyofanywa na televisheni ya taifa kwamba angelipatia Kanisa utambulisho wa kisheria, na punde waumini walianza kufundisha injili wazi wazi. Katika mwezi huo huo, Ralph na Jean Hutchings, wamisionari wa kwanza kuitwa Zaïre, walifika na kukuta kundi lililokuwa likiongezeka huko Kinshasa. Utambulisho kisheria ulitolewa rasmi mwezi Aprili na kufikia Juni 1987 Kanisa lilikuwa likikua kwa kasi huko Zaïre mpaka misheni ikaanzishwa, Ralph Hutchings akiwa Rais.

Wamisionari pia waliifikia mikusanyiko isiyo maalumu karibu na Lubumbashi. Ingawa mabadiliko yalikuwa magumu kwa baadhi, kituo kingine cha kukutania kilianzishwa. Kati ya Mei na Julai 1987, watu 170 walibatizwa. Baadhi walisafiri umbali wa kilometa 30 (maili 186) kutoka Pweto, Kolwezi na Likasi kuhudhuria Kanisa.

Wakati Elie Monga mwenye miaka 21 kutoka Kolwezi aliposoma Kitabu cha Mormoni mnamo 1987, alivutiwa. “Nilihisi kwa dhati,” akisimulia baadaye, “kwamba hicho ndicho nilichokihitaji.” Monga alisafiri kilometa 300 hadi Lubumbashi ili kukutana na wamisionari. Baada ya somo moja tu, aliamua kubatizwa. Baada ya ubatizo wake, kwa kutiwa moyo na wamisionari, alifanya mikutano ya Shule ya Jumapili katika makazi yake. “Tulianza kukusanyika na kuwafundisha rafiki zetu [na familia],” anasema, “tukiwaletea ujumbe wa tumaini kupitia injili iliyorejeshwa.” Kundi kubwa punde lilikuwa likikutana katika nyumba ya Monga. Wakati huduma ya ubatizo wa kwanza huko Kolwezi ilipofanyika mwaka uliofuatia, ilimchukua Monga masaa matatu na nusu kuwabatiza waongofu 82 walioikubali injili. Ilikuwa ni moja ya mafanikio kati ya mengi: mnamo mwaka 1990, miaka minne tu baada ya Kanisa kutambuliwa na serikali, matawi na wilaya vilikuwa vikishamiri huko Kinshasa, Lubumbashi na majiji mengine mengi nchini kote.