2018
Hatua ya Kwanza Kuelekea Toba
Oktoba 2018


Vijana Wakubwa

Hatua ya Kwanza Kuelekea Toba

Mwandishi anaishi Ouest, Haiti.

Nilihisi giza likizangaa maishani mwangu. Kisha nikatambua ninahitaji kuongea na askofu wangu.

Picha
man praying, thinking of Christ

Kielelezo na Joshua Dennis

Ninakumbuka kuchagua tarehe yangu ya ubatizo nikiwa na wamisionari. Waliniuliza kama nilikuwa tayari kuweka agano hili na Baba yetu wa Mbinguni. Bila hata kufikiria kuhusu hili na kwa moyo wenye shangwe, nilisema, “Ndiyo!” Nilitaka kukubali zawadi maalum ambayo Baba yangu wa Mbinguni alikuwa amenipa, na nilijua kwamba nisingekuwa na furaha bila Mwokozi maishani mwangu. Lakini sikuwa na uhakika wa nini kilicho mbele yangu.

Hatimaye, siku kubwa ilifika. Ilikuwa isiyosahaulika, na nilikuwa na furaha sana.

Siku za Kiza

Baada ya ubatizo wangu na uthibitisho, mara moja siku zilionekana kuwa na kiza. Nilikuwa nikishughulikia mambo mbalimbali ya kifamilia, na nilikuwa nikihangaika kutii sheria zote za Mungu. Sikujua nini cha kufanya, na nilitaka kukata tamaa ya kila kitu. Ilionekana kama hakuna aliyenielewa.

Nilikuwa mara zote nikipenda kusoma Kitabu cha Mormoni, lakini kwa wakati huo nilikiweka pembeni. Siku moja, wakati nikiwa nyumbani peke yangu, nilihisi uzuri wa Roho akinitia msukumo kusoma Kitabu cha Mormoni. Nilisali kwanza, nikitaka kupata jibu ambalo lingeleta furaha katika sumbuko langu. Moja kwa moja nilifungua Alma mlango wa 5. Mstari wa 27 unaosema: “Mmetembea, na mkijiweka bila lawama mbele ya Mungu? Mngesema, kama mngeitwa kufariki wakati huu, ndani yenu, kwamba mlikuwa wanyenyekevu wa kutosha? Kwamba mavazi yenu yameoshwa na kufanywa meupe kwa damu ya Kristo, ambaye atakuja kuwakomboa watu wake kutokana na dhambi zao?”

Hatimaye, nilihisi kuguswa na maneno haya. Nilijua kwamba nilihitaji kutubu, kwa hivyo niliweka miadi ya kumuona askofu wangu. Nilikuwa mwoga, lakini nilijilazimisha kwenda na kumwona.

Kuelewa Ahadi ya Mungu

Wakati nilipofika katika ofisi ya askofu, nilijihisi mwenye hatia kwamba nilitaka kugeuka na kuondoka. Lakini nilisali kupata ujasiri wa kusema kila kitu ambacho nilihitaji kusema. Askofu alinikaribisha ofisini kwake, na kisha akasali ili kupokea msaada wa Mungu. Aliongea na mimi kama vile nilikuwa mwanaye akionyesha upendo wake kwangu kupitia maneno yake. Alinipa ushauri na kuniomba kufanya baadhi ya vitu ili kwamba nipokee msamaha wa Mungu na kisha kurudi tena na kuonana naye.

Nilikuwa na furaha sana kwa fursa hii. Nilifuata ushauri wake na hatimaye nilikuja kuelewa ahadi ya Mungu ya msamaha kwa Alma: “na kama ataungama dhambi zake mbele yako na mimi, na atubu kwa moyo wake kwa kweli, utamsamehe, na pia nitamsamehe” (Mosia 26:29). Baada ya kutubu kwa dhati, nilijua kwamba Mungu alinisamehe. Hatimaye niliweza kuhisi upendo wa Baba wa Mbinguni katika moyo wangu, na kiza kikatoweka. Nilikuwa mwenye furaha na kujivunia.

Askofu Yupo Kwa ajili ya Kusaidia

Askofu ni mwakilishi wa Bwana kwenye kata. Jua kwamba yuko kwa ajili ya kukusaidia kupata furaha ya kweli ambayo Mungu ameitunza kwa ajili yako. Mwamini. Kama una matatizo au unahitaji kutubu, mtafute. Atakusaidia.

Najua wakati mwingine si rahisi kwenda na kumwona. Lakini kama Rais Lorenzo Snow (1814–1901) alivyofafanua kuhusu mpango wa milele wa Baba yetu wa Mbinguni: “Nina thubutu kusema kwamba katika ulimwengu wa roho wa [maisha kabla ya maisha ya duniani], wakati ilipopendekezwa kwetu … kupita katika uzoefu ambao sasa tunaupitia, haikuwa jambo la kupendeza na kukubalika kwa pamoja. … Bado hakuna shaka kwamba tuliona na kuelewa barabara huko kwamba, ili kutimiza kuinuliwa kwetu na utukufu, huu ulikuwa uzoefu wa lazima. Aliendelea kwa kusema, “tulikuwa tayari kukubaliana na mapenzi ya Mungu, na kwa hivyo tuko hapa” (Teachings of the Presidents of the Church: Lorenzo Snow [2012], 110).

Toba ni sehemu ya kukubaliana na mapenzi ya Mungu. Kwa hivyo badala ya kumwogopa askofu, mfanye kuwa rafiki yako. Aliteuliwa na Mungu, na anaweza kukusaidia kutubu na kuponya nafsi yako kupitia kumjia Yesu Kristo. Bwana anataka kutusaidia, lakini tunahitaji kuchukua ile hatua ya kwanza kuelekea toba. Kwa njia hiyo tunaweza kuona ahadi katika Isaya 1:18 ikitimizwa: “Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji.” Na kwa hilo, askofu yupo pale ili kusaidia.

Ninashuhudia kwamba Mungu anaishi na kwamba Yesu Kristo ni Mwokozi wetu. Wote wanatupenda sana!