Mkutano Mkuu
Kumwona Zaidi Yesu Kristo Katika Maisha Yetu
mkutano mkuu wa Oktoba 2022


Kumwona Zaidi Yesu Kristo Katika Maisha Yetu

Mwokozi anatualika tuyaone maisha yetu kupitia Yeye ili tuweze kumwona zaidi katika maisha yetu.

Akina kaka na akina dada, jinsi gani nimenyenyekezwa kusimama mbele yenu asubuhi ya leo. Ninaunganisha moyo wangu na yenu katika shukrani kupata kukusanyika, popote mlipo ulimwenguni kote, ili kusikia jumbe kutoka kwa manabii, mitume, waonaji, wafunuzi na viongozi katika ufalme wa Mungu. Kwa mfano tunakuwa kama watu wa siku za Mfalme Benjamini, tukipiga hema zetu na milango yetu ikifunguliwa na kuelekezwa kwa nabii wa Mungu duniani,1 Rais Russell M. Nelson.

Nimekuwa na upeo hafifu wa kuona kwa muda mrefu kadiri niwezavyo kukumbuka na siku zote nimehitaji usaidizi wa lenzi ili kurekebisha uoni wangu. Ninapofumbua macho yangu kila asubuhi, ulimwengu unaonekana kukanganya sana. Kila kitu kiko nje ya fokasi, kina chembechembe na kimeharibika. Hata mume wangu kipenzi anafanana zaidi na picha ya dhahania kuliko umbo pendwa na lenye kufariji ambalo ni uhalisia wake! Hitaji langu la kawaida, kabla sijafanya jambo lingine lolote mwanzoni mwa siku yangu, ni kufikia miwani yangu ili inisaidie kuelewa mazingira yangu na kufurahia uzoefu mzuri zaidi pale inaponisaidia kupita siku nzima.

Kwa miaka mingi, nimekuja kutambua kwamba tabia hii inaonesha utegemezi wangu wa kila siku kwa vitu viwili: kwanza, chombo ambacho hunisaidia kufafanua, kufokasi na kupata msingi wa ulimwengu unaonizunguka; na pili, hitaji la mwongozo unaoonekana ili kuendelea kunielekeza katika mwelekeo sahihi. Mazoezi haya rahisi, ya kila siku yanaonesha kwangu angalizo muhimu kuhusu uhusiano wetu na Mwokozi wetu, Yesu Kristo.

Kwenye maisha yetu ambayo mara nyingi yamejaa maswali, wasiwasi, shinikizo na fursa, upendo wa Mwokozi wetu kwetu sisi binafsi na kama watoto Wake wa agano, na pia mafundisho na sheria Zake, ni nyenzo za kila siku ambazo tunaweza kuzitegemea ili kuwa “nuru ambayo hung’ara, … ikiangaza macho [yetu] [na] kuhuisha ufahamu [wetu].”2 Tunapotafuta baraka za Roho katika maisha yetu, tutaweza, kama Yakobo alivyofundisha, kuona “vitu vilivyo, na … vile vitu vitavyokuwa.”3

Kama watoto wa agano wa Mungu, tumebarikiwa kwa njia ya kipekee kwa wingi wa zana zilizoteuliwa na Mungu ili kuboresha uoni wetu wa kiroho. Maneno na mafundisho ya Yesu Kristo kama yalivyoandikwa katika maandiko na jumbe kutoka kwa manabii Wake wateule na Roho Wake zinazopokelewa kupitia maombi ya kila siku, mahudhurio ya kila mara hekaluni na kupitia ibada ya kila wiki ya sakramenti vinaweza kusaidia kurejesha amani na kutoa zawadi muhimu ya utambuzi ambayo huleta nuru ya Kristo na ufahamu Wake kwenye nyanja za maisha yetu na katika ulimwengu ambao unaweza kuwa na mawingu. Mwokozi anaweza pia kuwa dira yetu na rubani wetu tunapopita katika maji tulivu na misukosuko ya maisha. Anaweza kubainisha wazi njia sahihi inayotuongoza kwenye hatma yetu ya milele. Kwa hivyo, Yeye angetaka tuone nini na wapi Angetaka twende?

Nabii wetu mpendwa amefundisha kwamba “fokasi yetu lazima ielekezwe kwa Mwokozi na injili Yake” na kwamba lazima “tujitahidi kumtegemea Yeye katika kila wazo.”4 Rais Nelson pia ameahidi kuwa “hakuna kinachomwalika Roho zaidi ya kukita fokasi yako juu ya Yesu Kristo. … Yeye atakuelekeza na kukuongoza wewe katika maisha yako binafsi ikiwa utatenga muda kwa ajili Yake katika maisha yako—kila siku ipitayo.”5 Marafiki, Yesu Kristo ndiye vyote dhumuni la fokasi yetu na kusudi la hatma yetu. Ili kutusaidia kubaki thabiti na kuelekea katika njia sahihi, Mwokozi anatualika tuyaone maisha yetu kupitia Yeye ili tumwone Yeye zaidi katika maisha yetu. Nimekuja kujifunza zaidi kuhusu mwaliko huu maalum kupitia kujifunza kwangu Agano la Kale.

Sheria ya Musa ilitolewa kwa Waisraeli wa kale kama injili ya matayarisho, iliyokusudiwa kuwatayarisha watu kwa ajili ya uhusiano wa agano la juu zaidi na Mungu kupitia Yesu Kristo.6 Sheria, yenye ishara nyingi zikielekeza waumini “kutarajia ujio” na Upatanisho wa Yesu Kristo,7 ilikusudiwa kuwasaidia watu wa Israeli kufokasi kwa Mwokozi kwa kutumia imani katika Yeye, dhabihu Yake na sheria na amri Zake maishani mwao8—ikiwa na lengo la kuwaleta kwenye ufahamu mkubwa zaidi wa Mkombozi wao.

Kama vile sisi leo, watu wa kale wa Mungu walialikwa wayaone maisha yao Kupitia Yeye ili waweze kumwona Yeye zaidi katika maisha yao. Lakini wakati wa huduma ya Mwokozi, Waisraeli walikuwa wamepoteza upeo wa kumwona Kristo katika utii wao, wakimweka kando na kuongeza kwenye sheria mazoea ambayo hayakuruhusiwa ambayo hayakuwa na mafunzo yenye ishara zinazoelekeza kwenye chanzo cha kweli na cha pekee cha wokovu na ukombozi wao—Yesu Kristo.9

Ulimwengu wa kila siku wa Waisraeli ulikuwa wenye mkanganyiko na wenye mashaka. Wana wa Israeli, katika hali hii, waliamini kwamba mazoea na taratibu za sheria zilikuwa njia ya wokovu binafsi na kwa sehemu zilipunguza sheria ya Musa kwa seti za itifaki zilizowekwa kutawala maisha ya raia.10 Hii ilimhitaji Mwokozi kurejesha fokasi na ufafanuzi kwenye injili Yake.

Hatimaye sehemu kubwa ya Waisraeli walikataa ujumbe Wake, hata kufikia hatua ya kumshitaki Mwokozi—Yeye ambaye aliwapa sheria na kutangaza kwamba Yeye alikuwa “sheria na nuru”11—kwa kuivunja. Na bado Yesu katika Mahubiri yake ya Mlimani, akizungumza juu ya sheria ya Musa, alitangaza, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii: sikuja kutangua, bali kutimiliza.”12 Kisha Mwokozi, kupitia Upatanisho Wake wa milele, alihitimisha kanuni, mipangilio na desturi za sherehe zilizozingatiwa na watu wa Israeli wakati huo. Dhabihu yake ya mwisho ilipelekea kuhama kutoka dhabihu za kuteketezwa hadi kutoa kwetu “moyo uliovunjika na roho iliyopondeka,”13 kutoka kwenye ibada ya dhabihu hadi ibada ya sakramenti.

Rais M. Russell Ballard, akifundisha juu ya mada hiyo alisema, “Katika utambuzi, dhabihu ilibadilika kutoka kwenye matoleo kuwa mtoaji.”14 Tunapoleta matoleo yetu kwa Mwokozi, tunaalikwa kumwona zaidi Yesu Kristo katika maisha yetu, pale tunapowasilisha mapenzi yetu Kwake kwa unyenyekevu katika kutambua na kuelewa utiifu Wake mkamilifu kwa mapenzi ya Baba. Tunapoelekeza macho yetu kwa Yesu Kristo, tunatambua na tunaelewa kwamba Yeye ndiye chanzo pekee na njia pekee ya kupokea msamaha na ukombozi, hata kwenye uzima wa milele na kuinuliwa.

Kama mfuasi wa mwanzo wa injili, nilikutana na wengi ambao waliona na kushuhudia mabadiliko katika tabia, desturi na chaguzi zangu baada ya kujiunga na Kanisa. Walikuwa na shauku ya kutaka kujua “kwa nini” ya kile walichokuwa wanakiona—kwa nini nilichagua kubatizwa na kujiunga na mkusanyiko huu wa waumini, hata Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, kwa nini najiepusha na mazoea fulani siku ya Sabato, kwa nini mimi ni mwaminifu katika kutii Neno la Hekima, kwa nini ninasoma Kitabu cha Mormoni, kwa nini ninaamini na kuingiza mafundisho ya manabii na mitume wa siku za leo kwenye maisha yangu, kwa nini ninahudhuria mikutano ya Kanisa ya kila wiki, kwa nini ninawaalika wengine “waje na kuona, waje na kusaidia,waje na kubakia,”15” na “waje na kuwa wa mahala hapa.”16

Wakati huo, maswali hayo yalionekana kama mzigo na, niwe muwazi, nyakati zingine kama mashtaka. Lakini nilipokuwa nikikabiliana na uchunguzi wa watu, nilikuja kugundua kwamba uchunguzi wao ulikuwa, kwa hakika, mwaliko wangu wa kwanza wa kuchukua na kuvaa lenzi za kiroho ili kufafanua, kufokasi na kuimarisha kile kilichochochea ufuasi wangu kwenye mazoea na viwango vya injili. Nini kilikuwa chanzo cha ushuhuda wangu? Je, nilikuwa nikitekeleza tu “maonyesho ya nje” bila kuruhusu mazoea hayo kuunganika na sheria za Mungu za “kutia nguvu imani [yangu] katika Kristo,”17 au kubainisha ufahamu kwamba Yesu Kristo ndiye chanzo pekee cha nguvu katika utii wangu?

Kupitia juhudi kubwa ya kumwangalia Yeye na kwa ajili ya Yesu Kristo katika kila wazo na tendo langu, macho yangu yalitiwa nuru, na ufahamu wangu ulihuishwa kutambua kwamba Yesu Kristo alikuwa akiniita “nije” Kwake.18 Kuanzia msimu huu wa mapema wa ufuasi katika ujana wangu, ninaweza kukumbuka mwaliko uliotolewa kwangu na wamisionari kujiunga nao walipokuwa wakifundisha injili kwa kundi la wasichana wadogo wa umri wangu. Jioni moja, nikiwa nimeketi katika nyumba ya familia ya mmoja wa wasichana hawa, swali lao la dhati la “kwa nini ninaamini” lilichoma moyo wangu, na kuniruhusu kuwashuhudia kwa ufahamu wa kina juu ya ono la Bwana kuhusu motisha za kiroho za ufuasi wangu na imesafisha ushuhuda wangu wa kusonga mbele.

Nilijifunza wakati huo, kama nijuavyo sasa, kwamba Mwokozi wetu, Yesu Kristo, anaelekeza miguu yetu kwenye nyumba za mikutano kila wiki ili kushiriki sakramenti Yake, kwenye nyumba ya Bwana kufanya maagano Naye, kwenye maandiko na mafundisho ya manabii ili kujifunza Maneno yake. Anaelekeza vinywa vyetu kushuhudia juu Yake, mikono yetu kuinua na kuhudumu kama vile ambavyo Yeye angeinua na kuhudumu, macho yetu kuuona ulimwengu na kila mmoja kama Yeye anavyoona—“vitu vilivyo, na … vile vitu vitakavyokuwa.”19 Na tunapomruhusu Yeye atuelekeze katika mambo yote, tunapokea ushuhuda kwamba “vitu vyote vinaonyesha kwamba kuna Mungu,”20 kwa sababu pale tunapomtafuta tutampata21—kila siku ipitayo. Juu ya hili ninashuhudia katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.