Mkutano Mkuu
Furaha na Milele
mkutano mkuu wa Oktoba 2022


Furaha na Milele

Shangwe ya kweli, ya kudumu na umilele pamoja na wale tuwapendao ndio kiini hasa cha mpango wa furaha wa Mungu.

Marafiki, akina kaka na dada wapendwa, je, unakumbuka kuamini, au kutaka kuamini, katika kuwa na furaha daima?

Maisha huanza. Kisha “tunakua.” Mahusiano yanakuwa magumu. Ulimwengu huu una kelele, wenye msongamano, usumbufu, wenye kujifanya na kujidai. Lakini bado, katika “kiini cha moyo wetu,”1 tunaamini, au tunataka kuamini, mahali fulani, kwa namna fulani, furaha milele ni kitu halisi na kinawezekana.

“Furaha na milele” sio mambo ya kufikirika ya hadithi za kale. Shangwe ya kweli, ya kudumu na umilele pamoja na wale tuwapendao ndio kiini hasa cha mpango wa furaha wa Mungu. Njia yake iliyotayarishwa kwa upendo inaweza kufanya safari yetu ya milele kuwa yenye furaha na milele.

Tunayo mengi ya kufurahia na kuwa na shukrani kwayo. Na bado, hakuna kati yetu aliye mkamilifu, wala familia yoyote. Mahusiano yetu hujumuisha upendo, ujamaa na utu lakini mara nyingi pia msuguano, kuumizwa, wakati mwingine maumivu makali.

“Kwa kuwa kama katika Adamu wote wanakufa, kadhalika na katika Kristo wote watahuishwa.”2 Kuhuishwa katika Yesu Kristo hujumuisha kutokufa—zawadi Yake ya ufufuo wetu wa kimwili. Tunapoishi kwa imani na utiifu, kuhuishwa katika Kristo kunaweza pia kujumuisha uzima wa milele wenye furaha tele pamoja na Mungu na wale tunaowapenda.

Kwa njia ya ajabu, nabii wa Bwana anatusogeza karibu na Mwokozi wetu, ikijumuisha kupitia ibada na maagano matakatifu ya hekaluni kuwa karibu nasi katika sehemu nyingi zaidi. Tunayo fursa na kipawa kikubwa cha kugundua uelewa mpya wa kiroho, kupenda, kutubu, na kusameheana sisi kwa sisi na familia zetu, sasa na milele.

Kwa ruhusa, ninashiriki matukio mawili matakatifu yaliyosimuliwa na marafiki kuhusu Yesu Kristo kuunganisha familia kwa kuponya hata uchungu wa vizazi.3 “Usio na mwisho na wa milele,”4 “wenye nguvu kuliko kamba za kifo,”5 Upatanisho wa Yesu Kristo unaweza kutusaidia kuleta amani katika maisha yetu ya kale na tumaini kwa yale yajayo.

Walipojiunga na Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, rafiki yangu na mume wake walijifunza kwa furaha uhusiano wa kifamilia hauhitaji kuwa “mpaka kifo kitakapowatenganisha.” Katika nyumba ya Bwana, familia zinaweza kuwa milele (kuunganishwa).

Lakini rafiki yangu hakutaka kuunganishwa kwa baba yake. “Hakuwa mume mzuri kwa mama yangu. Hakuwa baba mzuri kwa watoto wake,” alisema. “Baba yangu itabidi asubiri. Sina hamu yoyote ya kumfanyia kazi ya hekaluni na kuunganishwa naye milele yote.”

Kwa mwaka, alifunga, akaomba, alizungumza mengi na Bwana juu ya baba yake. Hatimaye, alikuwa tayari. Kazi ya hekalu ya baba yake ilikamilika. Baadaye, alisema, “Nikiwa usingizini baba yangu alinitokea katika ndoto, akiwa amevaa mavazi meupe. Alikuwa amebadilika. Alisema ‘Niangalie mimi. Niko msafi kabisa. Asante kwa kufanya kazi kwa ajili yangu katika hekalu.’” Baba yake akaongeza, “Simama na urudi hekaluni; kaka yako anangojea kubatizwa.”

Rafiki yangu anasema, “Mababu zangu na wale ambao wamekufa wanangojea kwa hamu kazi yao kufanywa.”

“Kwangu mimi,” anasema, “hekalu ni mahali pa uponyaji, kujifunza na kutambua Upatanisho wa Yesu Kristo.”

Uzoefu wa pili. Rafiki mwingine alitafiti kwa bidii historia ya familia yake. Alitaka kumtambua baba wa babu yake.

Mapema asubuhi moja, rafiki yangu alisema alihisi uwepo wa kiroho wa mwanaume katika chumba chake. Mwanaume huyo alitaka atambulike na kujulikana katika familia yake. Mwanaume huyo alijuta kwa kosa ambalo sasa alikuwa ametubu. Mwanaume huyo alimsaidia rafiki yangu kutambua kwamba rafiki yangu hakuwa na uhusiano wa vinasaba na mtu ambaye rafiki yangu alifikiri ni baba wa babu yake. “Kwa maneno mengine,” rafiki yangu alisema,“nilikuwa nimemgundua baba wa babu yangu na nikagundua kuwa hakuwa mtu ambaye rekodi za familia yetu zilisema alikuwa babu yetu.”

Mahusiano yake ya kifamilia yalifafanua, rafiki yangu alisema, “Ninahisi huru, nina amani. Inaleta tofauti kujua familia yangu ni ipi.” Rafiki yangu anawaza, “Tawi lililopinda haimaanishi mti mbaya. Jinsi tunavyokuja katika ulimwengu huu sio muhimu kuliko wakati tunapouacha.”

Maandiko matakatifu na uzoefu mtakatifu wa uponyaji wa kibinafsi na amani, ikijumuisha na wale walio hai katika ulimwengu wa roho, vinasisitiza kanuni tano za mafundisho.

Kwanza: Muhimu katika mpango wa Mungu wa ukombozi na furaha, Yesu Kristo, kupitia Upatanisho Wake, anaahidi kuunganisha roho na mwili wetu, “tusitengane tena, ili tupate utimilifu wa shangwe.”6

Pili: Upatanisho—upatanisho katika Kristo—unakuja tunapotumia imani na kuzaa matunda yapasayo toba.7 Kama katika hali ya kufa, vivyo hivyo katika kutokufa. Ibada za hekaluni zenyewe hazitubadilishi sisi au wale walio katika ulimwengu wa roho. Lakini ibada hizi takatifu huwezesha maagano ya kutakasa pamoja na Bwana, ambayo yanaweza kuleta upatanifu pamoja Naye na kila mmoja.

Furaha yetu hujaa tunapohisi neema na msamaha wa Yesu Kristo kwetu. Na tunapotoa muujiza wa neema na msamaha Wake kwa kila mmoja wetu, rehema tunayopokea na rehema tunayotoa zinaweza kusaidia kubadili dhuluma za maisha kuwa za haki.

Tatu: Mungu anatujua na kutupenda kikamilifu. “Mungu hadhihakiwi,”9 wala Yeye hawezi kudanganywa. Kwa rehema kamilifu na haki, Yeye huwakumbatia katika mikono Yake ya usalama wanyenyekevu na wenye kutubu.

Katika Hekalu la Kirtland, Nabii Joseph Smith alimwoona kwenye ono kaka yake Alvin katika ufalme wa selestia. Nabii Joseph alistaajabu, kwa vile Alvin alikufa kabla ya kupokea ibada ya okozi ya ubatizo.10 Kwa faraja, Bwana alieleza kwa nini: Bwana “atatuhukumu [sisi] kulingana na matendo [yetu], kulingana na mapenzi ya mioyo [yetu].”11 Nafsi zetu zinashuhudia kazi zetu na matamanio yetu.

Kwa shukrani, tunajua walio hai na “wafu wanaotubu watakombolewa, kwa njia ya utii kwa ibada za nyumba ya Mungu”12 na Upatanisho wa Kristo. Katika ulimwengu wa roho, hata wale walio katika dhambi na makosa wanayo nafasi ya kutubu.13

Kinyume chake, wale wanaochagua uovu kwa makusudi, wanaoghairi toba kwa kudhamiria, au ambao kwa njia yoyote iliyokusudiwa au ya kujua wanavunja amri wakipanga toba rahisi watahukumiwa na Mungu na “kumbukumbu nzuri ya hatia [yao] yote.”14 Hatuwezi kufanya dhambi kwa kudhamiria siku ya Jumamosi, kisha kutarajia msamaha wa moja kwa moja kwa kushiriki sakramenti siku ya Jumapili. Kwa wamisionari au wengine wanaosema kumfuata Roho kunamaanisha kutotii viwango vya misheni au amri, tafadhali kumbuka kwamba kutii viwango vya misheni na amri humwalika Roho. Hatupaswi hata mmoja wetu kughairi toba. Baraka za toba huanza tunapoanza kutubu.

Nne: Bwana hutupatia fursa takatifu ya kuwa zaidi kama Yeye tunapotoa ibada okozi za hekaluni kwa niaba ambazo wengine wanahitaji lakini hawawezi kujifanyia wao wenyewe. Tunakuwa wakamilifu zaidi na kukamilishwa15 tunapokuwa “waokozi … juu ya Mlima Sayuni.”16 Tunapowahudumia wengine, Roho Mtakatifu wa Ahadi anaweza kuidhinisha ibada na kuwatakasa wote mtoaji na mpokeaji. Mtoaji na mpokeaji wote wanaweza kufanya na kuimarisha maagano ya kubadilisha, na baada ya muda kupokea baraka zilizoahidiwa kwa Ibrahimu, Isaka na Yakobo.

Hatimaye, tano: Kama Kanuni ya Dhahabu17 inafundisha, ulinganifu wa utakaso katika toba na msamaha hutualika kila mmoja wetu kuwapa wengine kile ambacho sisi wenyewe tunahitaji na kutamani.

Wakati mwingine nia yetu ya kumsamehe mtu mwingine inawawezesha wao na sisi kuamini kwamba tunaweza kutubu na kusamehewa. Wakati fulani nia ya kutubu na uwezo wa kusamehe huja kwa nyakati tofauti. Mwokozi wetu ni Mpatanishi wetu pamoja na Mungu, lakini Yeye pia hutusaidia kutuleta kwetu sisi wenyewe na kwa kila mmoja wetu pale tunaposonga Kwake. Hasa wakati uchungu na maumivu ni makubwa, kurekebisha mahusiano yetu na kuponya mioyo yetu ni vigumu, labda haiwezekani kwetu sisi wenyewe. Lakini mbingu inaweza kutupa nguvu na hekima zaidi ya ile tuliyonayo ili kujua wakati wa kungojea na jinsi ya kuachilia.

Hatuko peke yetu tunapogundua kuwa hatupo peke yetu. Mwokozi wetu daima anaelewa.18 Kwa msaada wa Mwokozi wetu, tunaweza kukabidhi kiburi chetu, maumivu yetu, dhambi zetu kwa Mungu. Tunaweza kuhisi tu tunapoanza, tunakuwa wakamilifu zaidi tunapomwamini Yeye kufanya mahusiano yetu kuwa kamili.

Bwana, ambaye anaona na kuelewa kikamilifu, husamehe amtakaye; sisi (tukiwa si wakamilifu) tunapaswa kusamehe wote. Tunapokuja kwa Mwokozi wetu, tunajitazama wenyewe kwa kiwango kidogo. Tunahukumu kidogo na kusamehe zaidi. Kutumainia fadhili, rehema na neema Zake19 kunaweza kutuweka huru kutokana na ugomvi, hasira, unyanyasaji, kutelekezwa, ukosefu wa haki, na changamoto za kimwili na kiakili ambazo wakati mwingine huja na mwili katika ulimwengu huu wa kufa. Furaha milele haimaanishi kuwa kila uhusiano utakuwa wa furaha milele. Lakini miaka elfu moja ya milenia ambapo Shetani atafungwa20 inaweza kutupa wakati unaohitajika na njia za kushangaza za kupenda, kuelewa, na kutatua mambo, tunapojitayarisha kwa umilele.

Tunaona uhusiano wa mbinguni katika kila mmoja wetu21 Kazi na utukufu wa Mungu ni pamoja na kuleta furaha milele.22 Uzima wa milele na kuinuliwa ni kumjua Mungu na Yesu Kristo hivyo, kwa uwezo wa kiungu, mahali Wao wako ndipo nasi tutakuwako.23

Wapendwa akina kaka na dada, Mungu Baba yetu wa Mbinguni na Mwanawe Mpendwa wanaishi. Wanatoa amani, shangwe na uponyaji kwa kila ukoo na lugha, kwa kila mmoja wetu. Nabii wa Bwana anaongoza njia. Ufunuo wa siku za mwisho unaendelea. Na tumkaribie zaidi Mwokozi wetu katika nyumba takatifu ya Bwana, na Yeye atusogeze karibu zaidi na Mungu na kwa kila mmoja wetu, tunapounganisha mioyo yetu pamoja kwa huruma, ukweli na rehema kama ya Kristo katika vizazi vyetu vyote—kwa wakati huu na milele, furaha daima. Katika Yesu Kristo, inawezekana; katika Yesu Kristo, ni kweli. Ninashuhudia hayo, katika jina Lake tukufu, Yesu Kristo, amina.