Mkutano Mkuu
Nao Wakataka Kumwona Yesu Yeye ni Nani
mkutano mkuu wa Oktoba 2022


Nao Wakataka Kumwona Yesu Yeye ni Nani

Ninatoa ushahidi kwamba Yesu yu hai, kwamba anatujua, na kwamba ana uwezo wa kuponya, kubadilisha, na kusamehe.

Akina kaka, akina dada, na marafiki, mnamo 2013 mimi na mke wangu, Laurel, tuliitwa kuhudumu kama viongozi wa misheni katika Misheni ya Czech/Slovak. Watoto wetu wanne walihudumu pamoja nasi.1 Tulibarikiwa kama familia kuwa na wamisionari mahiri na Watakatifu wa ajabu wa Czech na Slovakia. Tunawapenda.

Familia yetu ilipoingia katika uwanja wa misheni, jambo ambalo Mzee Joseph B. Wirthlin alifundisha lilienda nasi. Katika hotuba yenye kichwa cha habari “Amri Kuu” Mzee Wirthlin aliuliza, “Je, unampenda Bwana?” Ushauri wake kwetu sisi ambao tungejibu “ndiyo” ulikuwa rahisi na wa kina: “Tumieni muda pamoja Naye. Tafakarini maneno Yake. Jitieni nira Yake. Tafuteni kuelewa na kutii.”2 Mzee Wirthlin kisha aliahidi baraka za kuleta mabadiliko kwa wale walio tayari kutoa muda na nafasi kwa Yesu Kristo.3

Tulichukua ushauri na ahadi ya Mzee Wirthlin moyoni. Pamoja na wamisionari wetu, tulitumia muda mrefu pamoja na Yesu tukijifunza Mathayo, Marko, Luka, na Yohana kutoka Agano Jipya na 3 Nefi kutoka Kitabu cha Mormoni. Mwishoni mwa kila mkutano wa wamisionari, tulijikuta tumerudi katika kile tulichotaja kama “Injili Tano”4 kusoma, kujadili, kuzingatia na kujifunza kuhusu Yesu.

Kwangu mimi, kwa Laurel, na kwa wamisionari wetu, kutumia muda na Yesu katika maandiko kulibadilisha kila kitu. Tulipata shukrani ya kina ya kile Yeye alichokuwa na kile kilicho muhimu Kwake. Kwa pamoja tulizingatia jinsi Yeye alivyofundisha, kile Alichofundisha, jinsi alivyoonesha upendo, kile alichofanya ili kubariki na kuhudumu, miujiza Yake, jinsi alivyojibu usaliti, kile alichofanya kwenye hisia ngumu za kibinadamu, vyeo na majina Yake, jinsi alivyosikiliza, jinsi Alivyosuluhisha mzozo, ulimwengu Alimoishi, mifano Yake, jinsi Alivyohimiza umoja na ukarimu, uwezo Wake wa kusamehe na kuponya, mahubiri Yake, maombi Yake, dhabihu Yake ya kulipia dhambi, Ufufuko Wake, injili Yake.

Mara nyingi tulijihisi kama yule mtu “[mfupi] kwa kimo” Zakayo akikimbia kupanda mkuyu Yesu alipokuwa akipitia Yeriko kwa sababu, kama Luka alivyoeleza, ‘tulitafuta kumwona Yesu alikuwa nani.5 Haikuwa Yesu kwa jinsi tulivyotaka au tulivyotamani awe, bali Yesu jinsi alivyokuwa na alivyo.6 Kama vile Mzee Wirthlin alivyoahidi, tulijifunza kwa njia ya kweli kwamba “injili ya Yesu Kristo ni injili ya mabadiliko. Inatuchukulia sisi kama wanaume na wanawake wa dunia na inatusafisha kuwa wanaume na wanawake wa milele.”7

Hizo zilikuwa siku maalum. Tulikuja kuamini kwamba “kwa Mungu hakuna lisilowezekana.”8 Alasiri takatifu huko Prague, Bratislava, au Brno, tukipata uzoefu wa nguvu na uhalisia wa Yesu, huendelea kuvuma katika maisha yetu yote.

Mara nyingi tulisoma Marko 2:1–12. Hadithi hapo inavutia. Ninataka kusoma sehemu yake moja kwa moja kutoka kwa Marko, na kisha nishiriki jinsi nilivyoielewa baada ya kujifunza kwa kina na majadiliano na wamisionari wetu na wengine.9

“[Yesu] akaingia Kapernaumu tena baada ya siku kadha wa kadha; na ikasikika kwamba yumo nyumbani.

“Wakakusanyika watu wengi, isibaki nafasi hata mlangoni, akawa akisema nao neno lake.

“Wakaja watu wakimleta mtu mwenye kupooza, anachukuliwa na watu wanne.

“Na walipokuwa hawawezi kumkaribia kwa sababu ya makutano, waliitoboa dari pale alipokuwapo: na wakiisha kuivunja wakaliteremsha godoro alilolilalia yule mwenye kupooza.

“Naye Yesu, alipoiona imani yao, akamwambia yule mwenye kupooza, Mwanangu, umesamehewa dhambi zako.”

Baada ya mazungumzo na baadhi ya watu katika umati,10 Yesu anamtazama mtu aliyepooza na kumponya kimwili, akisema:

“Nakuambia, Ondoka, ujitwike godoro lako uende nyumbani kwako.

“Mara akaondoka, akajitwika godoro lake, akatoka mbele yao wote; hata wakastaajabu wote, wakamtukuza Mungu, wakisema, namna hii hatujapata kuiona kamwe.”11

Sasa hadithi kama nilivyokuja kuielewa: mapema katika huduma Yake, Yesu alirudi Kapernaumu, kijiji kidogo cha wavuvi kilichoko kwenye ufuko wa kaskazini wa Bahari ya Galilaya.12 Yeye hivi karibuni alikuwa amefanya mfululizo wa miujiza kwa kuponya wagonjwa na kutoa pepo wabaya.13 Wakiwa na shauku ya kumsikia na kumwona mtu anayeitwa Yesu, wanakijiji walikusanyika kwenye nyumba ambayo ilisemekana kuwa anakaa.14 Walipofanya hivyo, Yesu alianza kufundisha.15

Nyumba za wakati huo katika Kapernaumu zilikuwa na paa tambarare, za orofa moja, zikiwa zimepangwa pamoja.16 Paa na kuta zilikuwa mchanganyiko wa mawe, mbao, udongo, na nyasi, zilizofikiwa kwa seti ya hatua rahisi kando ya nyumba.17 Umati wa watu ukaongezeka upesi katika ile nyumba, wakajaza chumba ambacho Yesu alikuwa akifundisha, wakaenea hata njiani.18

Hadithi hiyo inamlenga mtu “mgonjwa wa kupooza” na marafiki zake wanne.19 Kupooza ni aina ya kiharusi, mara nyingi huambatana na udhaifu na kutetemeka.20 Ninawaza kwamba mmoja wa wale wanne akiwaambia wengine, “Yesu yuko kijijini kwetu. Sote tunajua miujiza aliyofanya na wale aliowaponya. Ikiwa tunaweza kumfikisha tu rafiki yetu kwa Yesu, pengine na yeye pia anaweza kuponywa.”

Kwa hiyo, kila mmoja wao anachukua kona ya mkeka au kitanda ambacho rafiki yao amelazwa na kuanza kumbeba kupitia njia za vichochoroni, nyembamba, zisizo na lami za Kapernaumu.21 Misuli ikiwa inauma wanapinda kona ya mwisho na kugundua kwamba umati au, kama maandiko yanavyouita, “msongamano” wa watu waliokusanyika kusikiliza ni mkubwa sana kiasi kwamba haiwezekani kufika kwa Yesu.22 Kwa upendo na imani, wanne hawa hawakati tamaa. Badala yake, wanapanda ngazi hadi juu ya paa tambarare, kwa uangalifu wakimwinua rafiki yao na kitanda chake, wanavunja dari ya chumba ambamo Yesu anafundisha, na kumshusha rafiki yao.23

Fikiria kwamba katikati ya kile ambacho lazima kilikuwa kipindi kigumu cha kufundisha, Yesu anasikia kelele ya kukwaruza, anatazama juu, na kuona shimo linaloongezeka kwenye dari huku vumbi na nyasi zikianguka ndani ya chumba. Mtu aliyepooza kitandani kisha anashushwa chini. Inashangaza kwamba Yesu anatambua kwamba huku si kukatiza bali badala yake ni jambo muhimu. Anamtazama mtu yule kitandani, anamsamehe dhambi zake hadharani, na kumponya kimwili.24

Kwa maelezo hayo ya Marko 2 akilini, kweli kadhaa muhimu zinakuwa wazi kuhusu Yesu kama Kristo. Kwanza, tunapojaribu kumsaidia mtu tunayempenda kuja kwa Kristo, tunaweza kufanya hivyo kwa kujiamini kwamba Yeye anao uwezo wa kuinua mzigo wa dhambi na kusamehe. Pili, tunapoleta magonjwa ya kimwili, kihisia, au mengine kwa Kristo, tunaweza kufanya hivyo tukijua kwamba anao uwezo wa kuponya na kufariji. Tatu, tunapofanya bidii kama wale wanne kuwaleta wengine kwa Kristo, tunaweza kufanya hivyo kwa uhakika kwamba Yeye huona nia zetu za kweli na ataziheshimu ipasavyo.

Kumbuka, mafundisho ya Yesu yalivurugwa na kutokea kwa shimo kwenye paa. Badala ya kuwaadhibu au kuwafukuza wale wanne waliotoboa shimo darini kwa kuvuruga somo, maandiko yanatuambia kwamba “Yesu aliiona imani yao.”25 Wale walioshuhudia muujiza kisha “wakastaajabu, wakamtukuza Mungu, ambaye amewapa wanadamu uwezo wa namna hii.”26

Akina kaka na akina dada, wacha nimalizie kwa mambo mawili ya ziada. Iwe kama wamisionari, watumishi, marais wa Muungano wa Usaidizi, maaskofu, walimu, wazazi, ndugu, au marafiki, sisi sote tunahusika kama wanafunzi Watakatifu wa Siku za Mwisho katika kazi ya kuwaleta wengine kwa Kristo. Hivyo, sifa zilizoonyeshwa na marafiki wanne zafaa kuzingatiwa na kuigwa.27 Wao ni wajasiri, wenye kubadilika, wastahimilivu, wabunifu, wenye uwezo mwingi, wenye matumaini, wenye kudhamiria, waaminifu, wenye matumaini, wanyenyekevu, na wenye kuvumilia.

Zaidi ya hayo, marafiki wanne wanasisitiza umuhimu wa kiroho wa kuwa na jumuiya na ushirika.28 Ili kumleta rafiki yao kwa Kristo, kila mmoja wa wanne lazima ashikilie kona yake. Kama mmoja ataachia, mambo yanakuwa magumu zaidi. Ikiwa wawili watakata tamaa, kazi hiyo inakuwa haiwezekani kabisa. Kila mmoja wetu ana jukumu la kufanya katika ufalme wa Mungu.29 Tunapotimiza jukumu hilo na kufanya sehemu yetu, tunabeba kona yetu. Iwe huko Argentina au Vietnam, Accra au Brisbane, tawi au kata, familia au wenzi wa mmisionari, kila mmoja wetu anayo kona ya kubeba. Tunapofanya hivyo, na iwapo tutafanya, Bwana hutubariki sote. Jinsi alivyoona imani yao, ndivyo atakavyoiona imani yetu na kutubariki sisi kama watu.

Kwa nyakati tofauti nimeshikilia kona ya kitanda na nyakati zingine nimekuwa mtu niliyebebwa. Sehemu ya nguvu ya hadithi hii ya ajabu ya Yesu ni kwamba inatukumbusha tu jinsi tunavyohitajiana, kama kaka na dada, ili kuja kwa Kristo na kubadilishwa.

Haya ni baadhi ya mambo machache niliyojifunza kwa kutumia muda pamoja na Yesu katika Marko 2.

“Mungu na atujalie tuwe na uwezo wa [kubeba kona yetu], ili tusikwepe, tusiogope, bali tuwe na nguvu katika imani yetu, na kudhamiria katika kazi yetu, ili kutimiza makusudio ya Bwana.”28

Ninatoa ushahidi kwamba Yesu yu hai, kwamba anatujua, na kwamba ana uwezo wa kuponya, kubadilisha, na kusamehe. Katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Evie, Wilson, Hyrum, and George.

  2. Joseph B. Wirthlin, “Amri Kuu,” Liahona, Nov. 2007, 30.

  3. Baraka zilizotambuliwa na Mzee Wirthlin inajumuisha ongezeko la uwezo wa upendo, nia ya kuwa mtiifu na kuitikia amri za Mungu, hamu ya kuwahudumia wengine, na tabia ya kufanya mema daima.

  4. “Injili … ni maonyesho manne chini ya majina ya wainjilisti wanne tofauti au waandishi wa Injili wa maisha na mafundisho ya Yesu, na mateso, kifo na ufufuko wake” (Anders Bergquist, “Bible,” in John Bowden, ed., Encyclopedia of Christianity [2005], 141). Kamusi ya Biblia inaongeza kwamba “neno injili humaanisha ‘habari njema.’ Habari njema ni kwamba Yesu Kristo amefanya upatanisho mkamilifu kwa ajili ya wanadamu ambao utawakomboa wanadamu wote. … Kumbukumbu za maisha Yake ya duniani na matukio yanayohusiana na huduma Yake inaitwa Injili” (Kamusi ya Biblia, “Injili”).Injili”). 3 Nefi , iliyorekodiwa na Nefi, mjukuu wa Helamani, ina kumbukumbu ya kutokea na mafundisho ya Yesu Kristo aliyefufuka katika Amerika mara tu baada ya kusulubiwa Kwake na, kwa hivyo, inaweza pia kujulikana kama “Injili.” Injili ni za kuvutia hasa kwa sababu zinarekodi matukio na mazingira ambayo Yesu Mwenyewe anafundisha na kushiriki kikamilifu. Ni sehemu muhimu ya kuanzia kwa ajili ya kumwelewa Yesu kama Kristo, uhusiano wetu Kwake, na injili Yake.

  5. Ona Luka 19:1–4; ona pia Yakobo 4:13 (ikifafanua kwamba Roho “hunena juu ya mambo jinsi yalivyo, na juu ya mambo jinsi yatakavyokuwa”) na Mafundisho na Maagano 93:2493:24 (ikifafanua ukweli kama “maarifa ya mambo jinsi yalivyo, na kama yalivyokuwa, na kama watakavyokuja”).

  6. Rais J. Reuben Clark vile vile alihimiza kujifunza “maisha ya Mwokozi kama utu halisi.” Aliwaalika wengine wawe katika masimulizi ya kimaandiko ya maisha ya Yesu Kristo, wajaribu na “kwenda pamoja na Mwokozi, wakaishi naye, awe mtu halisi, nusu kimungu, bila shaka, lakini akisogea jinsi mtu anavyosogea katika hizo siku.” Zaidi ya hayo aliahidi kwamba juhudi kama hiyo “itakupa mtazamo kama huo juu yake, urafiki kama huo naye kama ninavyofikiri huwezi kupata kwa njia nyingine. … Jifunze alichofanya, alichofikiri, alichofundisha. Fanya kama Alivyofanya Ishi kama alivyoishi, kadiri tuwezavyo. Alikuwa mtu mkamilifu” (Tazama Mwana Kondoo wa Mungu [1962], 8, 11). Kwa maarifa kuhusu thamani na sababu za kumsoma Yesu katika muktadha wa historia, ona N. T. Wright na Michael F. Bird., Agano Jipya katika Ulimwengu wake (2019), 172–87.

  7. Joseph B. Wirthlin, “Amri Kuu,” 30.

  8. Luka 1:37.

  9. Pamoja na majadiliano ya . mara kwa mara na marefu ya Marko 2:1-2 pamoja na wamisionari wa Misioni ya Czech Slovak, ninashukuru pia kwa masomo niliyojifunza kwa kuzingatia kifungu hiki pamoja na vijana wa kiume na wa kike wa darasa la maandalizi ya umisionari wa Kigingi cha Salt Lake Highland na viongozi na washiriki wa Kigingi cha Salt Lake Pioneer YSA

  10. Ona Marko 2:6-10.

  11. Marko 2:11–12.

  12. Ona Bruce M. Metzger and Michael D. Coogan, eds., The Oxford Companion to the Bible (1993), 104; James Martin, Jesus: A Pilgrimage (2014), 183–84.

  13. Ona Marko 1:21–45.

  14. Ona Marko 2:1–2.

  15. Ona Marko 2:2.

  16. Ona Metzger and Coogan, The Oxford Companion to the Bible, 104; William Barclay, The Gospel of Mark (2001), 53.

  17. Ona Barclay, The Gospel of Mark (2001), 53; ona pia Martin, Jesus: A Pilgrimage, 184.

  18. Ona Marko 2:2, 4; ona pia Barclay, The Gospel of Mark, 52–53. Barclay anaeleza kwamba “maisha katika Palestina yalikuwa ya umma sana. Asubuhi mlango wa nyumba ulifunguliwa na yeyote aliyetaka anaweza kutoka na kuingia. Mlango haukufungwa kamwe isipokuwa mtu angetaka faragha kwa makusudi; mlango ulio funguliwa ulimaanisha mwaliko wazi kwa wote kuingia. Katika nyumba duni kama vile [ile iliyotambuliwa katika Marko 2] lazima iwe kulikuwa, hakukuwa na ukumbi wa kuingilia; mlango ulifunguliwa moja kwa moja … kwenda barabarani. Kwa hiyo, kwa muda mfupi, umati ulikuwa umejaza nyumba kwa wingi na kujaza barabara kuzunguka ule mlango; na wote walikuwa wakisikiliza kwa hamu maneno ya Yesu.

  19. Marko 2:3.

  20. Ona Medical Dictionary of Health Terms, “palsy,” health.harvard.edu.

  21. Ona Martin, Jesus: A Pilgrimage, 184–183.

  22. Marko 2:4.

  23. Ona Marko 2:4; ona pia Julie M. Smith, “The Gospel according to Mark,” BYU Studies (2018), 155–71.

  24. Ona Marko 2:5-12.

  25. Marko 2:5; mkazo umeongezwa.

  26. Mathayo 9:8; ona pia Marko 2: 12; Luka 5:26

  27. Mafundisho na Maagano 62:3 inaeleza kwamba watumishi wa Bwana “wamebarikiwa, kwa kuwa ushuhuda ambao mmetoa umeandikwa mbinguni … na dhambi zenu zimesamehewa.

  28. Ona M. Russell Ballard, “Tumaini katika Kristo,” Liahona, Mei 2021, 55–56. Rais Ballard anabainisha kwamba “hisia ya kuhusika” ni muhimu kwa afya ya kimwili na kiroho, na anasisitiza kwamba “kila mshiriki katika akidi zetu, vikundi, kata, na vigingi, ana zawadi na talanta alizopewa na Mungu ambazo zinaweza kusaidia kujenga ufalme Wake sasa.” Ona pia David F. Holland, Moroni: A Brief Theological Introduction (2020), 61–65. Holland anajadili Moroni 6 na njia ambazo ushiriki na ushirika katika jumuiya ya imani husaidia kuwezesha aina ya uzoefu wa kibinafsi wa kiroho unaotuunganisha kwa karibu zaidi na Mbingu.

  29. Ona Dieter F. Uchtdorf, “Lift Where You Stand,” Liahona, Nov. 2008, 56. Mzee Uchtdorf anaeleza kwamba “hakuna hata mmoja wetu anayeweza au anayepaswa kusogeza kazi ya Bwana peke yake. Lakini kama sisi sote tutasimama pamoja kwa karibu katika mahali ambapo Bwana ameweka na kuinua pale tunaposimama, hakuna kitu kinachoweza kuzuia kazi hii takatifu kusonga mbele na kwenda juu.” Ona pia Chi Hong (Sam) Wong, “Rescue in Unity,” Liahona, Nov. 2014, 15. Mzee Wong anarejelea Marko 2:1–5 na anafundisha kwamba “ili kumsaidia Mwokozi, inatubidi kufanya kazi kwa pamoja katika umoja na maelewano. Kila mmoja, kila nafasi, na kila wito ni muhimu.”

  30. Oscar W. McConkie, katika ripoti ya Mkutano, Oct. 1952, 57.