2022
“Misheni Yangu Haikuwa Kitu Nilichotarajia—na Hiki Ndicho Nilichojifunza”
Machi 2022


SAUTI ZA WAUMINI

“Misheni Yangu Haikuwa Kitu Nilichotarajia—na Hiki Ndicho Nilichojifunza”

Christiana Ogunbote alimaliza misheni yake wakati wa janga la ulimwengu. Kupitia matukio kadhaa yasiyotarajiwa, anashiriki jinsi alivyojifunza na kukua.

Miezi minne kwenye misheni yake huko Lusaka Zambia, Dada Christiana Ogunbote aliambiwa kwamba alipaswa kurejea nyumbani. Mwanzo wa janga la ulimwengu ulimaanisha kwamba wamisionari wengi kote ulimwenguni wangehitajika kurejea kwenye nchi zao. Hivyo, Dada Ogunbote alirejea kwenye nchi yake ya Uingereza. Mabadiliko yaliendelea: alipangiwa upya kuhudumu Misheni ya Uskochi/Ireland, na kisha kuitwa tena Zambia mnamo October 2020. Alipoulizwa kuhusu masomo ya maisha aliyokuwa amejifunza wakati akitumikia misheni wakati wa janga la ulimwengu, alishiriki yafuatayo kwa maneno yake mwenyewe:

“Kumekuwa na mafunzo mengi na masomo mengi ya maisha. Moja kubwa ni kwamba tunapoitwa kutumikia kama wamisionari, hatuchagui mazingira ya wito wetu. Tunaamua kwamba tunakwenda kumtumikia Bwana kwa vyote tulivyo navyo, bila kujali ni wapi au lugha ipi, iwe ni ndani ya nyumba za wamisionari au nje barabarani. Hatupati nafasi ya kuchagua mazingira hayo.

Lakini tunapata nafasi ya kuchagua jinsi tunavyoitikia. Tunapata nafasi ya kuchagua ikiwa tunataka kutumikia kwa shangwe na kwa moyo wote, au ikiwa tunataka kuona mabaya na kuzidiwa kwa mambo ambayo hatuwezi kufanya. Hilo ndilo jambo ambalo nilijifunza hasa na kukumbushwa kwamba uzoefu wa misheni ni moja ya shangwe kubwa. Hakuna shangwe kubwa kuliko kufanya kazi ya Bwana.

Kuwa Zambia ilikuwa wakati wa kupendeza wa maisha yangu. Kuwepo Uskochi kulifanya misheni yangu iwe kubwa kuliko nilivyowahi kupanga. Kuweza kuwa mmisionari nyumbani pamoja na wazazi wangu na kujaribu kuwa mmisionari katikati ya maisha yao ya kila siku ulikuwa uzoefu wa kuvutia kwangu na kwa wamisionari wengine wengi ambao walifanya jambo sawa na hilo. Nadhani yalikuwa mafunzo tuliyoyahitaji ili kuelewa kwa nini tulihitaji kuwa wamisionari.

Ingawa nilienda kutoka bara moja hadi lingine na kutumikia kwa muda nyumbani na kuwa nyumbani pamoja na wazazi wangu, kupitia yote, ninajua kwamba ilikuwa sehemu ya uzoefu ambao ulinisaidia kuelewa hasa kwamba Baba wa Mbinguni yu katika vipengele vya maisha yetu. Anamfahamu kila mmoja wetu na anataka sisi tuweze kufanya mambo kulingana na usanifu wake.

Nina mtazamo mzuri zaidi wa milele, nikifahamu kwamba si kila jambo litakuwa la furaha. Lakini kuwa na mtazamo huo wa milele ndivyo Bwana anavyotupatia nguvu ya kustahimili changamoto na majaribu yanayotukabili.”