2023
Unyenyekevu wa Mwanamke Mkananayo
Septemba 2023


“Unyenyekevu wa Mwanamke Mkananayo,” Liahona, Sept. 2023.

Miujiza ya Yesu

Unyenyekevu wa Wanamke Mkananayo

Ni ipi nafasi ya imani na unyenyekevu katika kutafuta miujiza tunayoihitaji?

Picha
Yesu na mwanamke Mkananayo

Mwanamke Mkananayo, na Harold Copping, Bridgeman Images

Miongoni mwa michangamano mingi sana ambayo Yesu Kristo lazima alikuwa ameipata wakati wa huduma Yake duniani, kulikuwa na mmoja ambao ni rahisi kuuruka kwa sababu ulikuwa mfupi na wakati mwingine haueleweki vizuri: mwanamke Mkananayo aliyeelezwa katika Mathayo 15:21–28.

Kwa baadhi ya muktadha wa ziada, hata hivyo, tunajifunza kweli nzuri kuhusu subira na huruma ya Yesu Kristo wakati tunapopata kumjua mwanamke huyu wa mfano wa imani na unyenyekevu anayetajwa mara chache.

Muktadha

Katika Mathayo 14, tunajifunza kwamba Mwokozi alikuwa anajua kuhusu kifo cha Yohana Mbatizaji, ambaye alikuwa amekatwa kichwa kutokana na uchochezi wa Herodia. Baada ya kujua kifo cha binamu Yake, Yesu aliondoka huko katika chombo, akaenda “mahali pasipo watu,” labda kuomboleza, lakini makutano walimfuata kwa miguu (ona Mathayo 14:13). Katika onyesho la huruma nyingi, Kristo alitumia siku na watu na hata akatenda mojawapo ya miujiza Yake mikuu, kuwalisha umati wa maelfu kwa vipande vitano vya mikate na samaki wawili (ona Mathayo 14:15–21).

Usiku ule Mwokozi alitenda muujiza wa pili mkubwa. Yeye alikuwa ameenda mlimani, “mbali” na wanafunzi Wake, ili kusali. Wanafunzi Wake walipanda chomboni, ambapo wakati huo kilikuwa katikati ya Bahari ya Galilaya, kikitaabika kwa mawimbi na upepo. “Hata … Yesu akawaendea, akienda kwa miguu juu ya bahari” ikisababisha wanafunzi kusema, “Hakika wewe u Mwana wa Mungu.” (ona Mathayo 14:23–25, 33).

Yesu kisha akasafiri kwenda kaskazini kutoka Galilaya hadi pwani ya Tiro na Sidoni, ambayo wakati huu ndiyo Lebanoni. Yeye hakika alikuwa akitafuta “pumziko, faragha, au nafasi ya kutosha ya kuwaelekeza wale Kumi na Wawili” fursa ambazo zilikuwa zimempita.1 Ilikuwa hapo ambapo “mwanamke Mkananayo wa mipaka ile akatokea, akampazia sauti akisema, Unirehemu, Bwana, Mwana wa Daudi; binti yangu amepagawa sana na pepo” (Mathayo 15:22).

Picha
ramani na picha za Sidoni na Tiro

Uponyaji wa binti wa mwanamke Mkananayo ulitokea mahali fulani katika mkoa kati ya Sidoni na Tiro, kaskazini mwa Galilaya.

Sidoni (ona kielelezo hapo juu): Pia ijulikana kama Sidoni Nyakati za kale, uchuuzi wa kibiashara uliufanya kuwa mojawapo ya miji muhimu ya Fonesia.

Tiro (ona picha hapo juu): Mji mwingine muhimu wa kibiashara, uliopo karibu maili 22 kusini mwa Sidoni. Wakati wa huduma Yake, Mtume Paulo aliwatembelea waumini wa Kanisa (ona Matendo ya Mitume 21:3–7.)

Kielelezo cha Sidoni na Balage Balogh

Mwanamke Mkananayo

Ilikuwa ya kushangaza sana kwamba mwanamke huyu alimwendea Yesu. Alikuwa Mkananayo, wa uzao wa mpagani au mataifa,” Wakananayo walikuwa wakidharauliwa na Wayaudi.”2 Na bado imani yake katika nguvu za Yesu Kristo na upendo wake kwa ajili ya binti yake ulipelekea yeye kuomba msaada kwa Mwokozi. Mzee James E. Talmage (1862–1933) wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili aliandika, “Ukweli kwamba yeye alimwita Yesu kama Mwana wa Daudi ilionyesha imani yake kwamba Yeye alikuwa Masiya wa Israeli.”3

Ingawa sisi tunajua kidogo sana kuhusu huyu mama Myunani, tunaweza kudhani kwamba imani yake ilikuwa kama ya wanawake wengine waliotajwa katika Agano Jipya. Kama yule mwanamke aliyekuwa “mwenye kutokwa na damu” (Marko 5:25), Mariamu na Martha wa Bethania, na Mariamu Magdalena, mwanamke Mkananayo aliweka tumaini lake lote katika Mwokozi. Alikuwa na uelewa makini na wa imani wa Yeye alikuwa nani.

Hapo mwanzo, Yesu hakumjibu. Wanafunzi walimhimiza amfukuze kwa sababu alikuwa anawasumbua, na wakadhani kwamba alikuwa akimsumbua katika hali ya ukimya.4

Hatimaye, Yesu alijibu. Akieleza ukimya Wake hapo awali, Yeye alisema, “Sikutumwa ila kwa kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli” (Mathayo 15:24).

Kauli ya Mwokozi hufanya ishangaze hata zaidi kuhusu mwanamke Myunani aliyekuja kutafuta baraka kwa ajili ya binti yake. Hakuwa mwanamke wa Israeli, lakini kwa njia fulani alijua kwamba Yesu Kristo alikuwa Masiya, Mfalme. Na ingawa Yeye alisema wazi kwamba misheni Yake ilikuwa kwa Wayahudi katika Israeli, yule mwanamke alikuwa na imani kwamba Yeye angemponya binti yake. Kwa upole, mwanamke alianguka miguuni kwake katika kutambua ufalme wake na nguvu zake (ona Marko 7:25), “akamsujudia,” na tena akisema, “Bwana, unisaidie” (Mathayo 15:25).

Unyenyekevu na Miujiza

Katika jibu ambalo lilionekana kuwa ukali kwa wafuasi wa sasa, Yesu alijibu, “Si vema kukitwaa chakula cha watoto na kuwatupia mbwa” (Mathayo 15:26). Wasomi wa Biblia wameeleza kwamba katika analojia hii “watoto” ni Wayahudi na “mbwa” ni Wayunani.

Kwa maneno mengine, wajibu wa msingi wa Kristo ulikuwa ni kwa Wayahudi. Yeye alikuwa awalishe wao—au kuwapa wao injili kwanza—na kisha wangewalisha au kuufundisha ulimwengu wote. Mzee Talmage alieleza: “Maneno, makali kama yanavyoweza kusikika kwetu, yalieleweka kwa mwanamke katika roho ya nia ya Bwana. … Kwa kweli yule mwanamke hakukasirishwa na mfananisho huo.”5

Tena, mjibizo wa mwanamke mwema unagusa na ni wa ajabu na unyenyekevu: “Bwana, lakini hata mbwa hula makombo yaangukayo mezani pa bwana zao. (Mathayo 15:27).

Huyu mwanamke aliyejaa imani hakukata tamaa. Badala ya kuchagua kuudhika, alichagua imani. Jibu lake lilikuwa onesho la tumaini hata kwenye makombo. Ni imani jinsi gani kuamini kwamba makombo kutoka kwenye meza ya Mwokozi yangeweza kuwa ya kutosha kushinda chochote kilichokuwa kinamuumiza binti yake. Jibu la mwanamke huyu mwaminifu linaonesha unyenyekevu na upole.

Mzee David A. Bednar wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili alielezea unyenyekevu kama “enye nguvu, si dhaifu, hai, si baridi; jasiri, si muoga.”6 Mwanamke Mkananayo kwa kweli alikuwa mwenye nguvu, hai, na jasiri katika kutangaza imani yake kwamba hata chembe moja ya nguvu ya Mwokozi ingekuwa ya kutosha.

Picha
sahani iliyo na makombo

Mwanamke Mkananayo alikuwa mwenye nguvu, hai, na jasiri katika kutangaza imani yake kwamba hata chembe moja ya nguvu ya Mwokozi ingekuwa ya kutosha.

Hatimaye, Yesu Kristo alijibu kwa jibu la uwezeshaji na linalojulikana: “Mama, imani yako ni kubwa; na iwe kwako kama utakavyo.” Kielelezo hiki kwamba Yeye humthamini na humkumbatia kila mmoja wetu katika safari yetu ya kuja Kwake kinafuatiwa katika kumbukumbu ya kimaandiko na hakikisho kwamba “binti yake alipona tangu saa ile” (Mathayo 15:28).

Je, Tunaweza Kujifunza Nini?

Mzee Talmage alisema, “Ushikiliaji wa kupongezwa wa mwanamke huyu wenye msingi wa imani ambayo hushinda vizuizi dhahiri na huvumilia hata katika kuvunjwa moyo.”7

Aina hiyo ya imani endelevu katika Yesu Kristo ni kile hasa ambacho nabii wetu mpendwa, Rais Russell M. Nelson, ametushauri sisi tukuze: “Imani katika Yesu Kristo ni nguvu kuu inayopatikana kwetu katika maisha haya. Vitu vyote vinawezekana kwa wale waaminio.”8

Mimi namsherekea mwanamke Mkananyo ambaye alikuwa mwenye nguvu, hai, na mshikiliaji katika kudai imani yake katika Yesu Kristo kama Mwokozi, Masiya, na Mfalme. Ni mfano wa Agano Jipya wa imani na unyenyekevu unaohitajika kwa wafuasi wote wa Yesu Kristo. Bila kukata tamaa, acha tutafute daima aina hiyo ya imani katika “kuhani wetu mkuu wa mambo mema yatakayokuwapo” (Waebrania 9:11).

Muhtasari

  1. Ona James E. Talmage, Jesus the Christ (1916), 354.

  2. James E. Talmage, Jesus the Christ, 354.

  3. James E. Talmage, Jesus the Christ, 354.

  4. Ona James E. Talmage, Jesus the Christ, 355.

  5. James E. Talmage, Jesus the Christ, 355.

  6. David A. Bednar, “Unyenyekevu na Upole wa Moyo,” Liahona, Nov. 2018, 32.

  7. James E. Talmage, Jesus the Christ, 356.

  8. Russell M. Nelson, “Kristo Amefufuka; Imani Kwake Itahamisha Milima,” Liahona, Mei 2021, 104.