Liahona
Nilijua Nilikuwa Ninalindwa
Machi 2024


“Nilijua Nilikuwa Ninalindwa,” Liahona, Machi 2024.

Sauti za Watakatifu wa Siku za Mwisho

Nilijua Nilikuwa Ninalindwa

Vita vilikuwa vimepamba moto huko nje, lakini nilipokuwa nikisoma Kitabu cha Mormoni, nilihisi amani na sikuwa na woga.

Picha
mwanamke akisoma kitabu

Kielelezo na Alex Nabaum

Mnamo mwaka 1992, vita vya Yugoslavia vilikuwa vimepamba moto. Mji wetu wa Mostar ulikuwa ukipigwa mabomu kila siku. Huduma zote za umma zilisimamishwa, ikijumuisha huduma za posta.

Mnamo Aprili 1 hata hivyo, sauti ya kubisha hodi ilisikika mlangoni. Nilipofungua, mwanamume ambaye kamwe sijawahi kumwona alinipa kifurushi kutoka kwa binti yangu, ambaye wakati huo alikuwa anaishi Malaga, Hispania, ambapo alikuwa amejiunga na Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Ndani ya kifurushi kulikuwa na nakala ya Kitabu cha Mormoni.

Nilianza kukisoma siku ile ile. Vita vilikuwa vimepamba moto huko nje, lakini nilipokuwa nikisoma Kitabu cha Mormoni, nilihisi amani na sikuwa na woga. Baadaye, nilijifunza kwamba amani niliyoihisi alikuwa Roho Mtakatifu. Nilijua nilikuwa ninalindwa na sitakufa.

Niliposoma, nilijifunza kuhusu Yesu Kristo na kwamba alikuwa bado yu hai. Nilijifunza kuhusu ubatizo na Kanisa la Mwokozi. Nilihisi kwamba kila kitu nilichosoma kilikuwa kweli. Mara kwa mara, binti yangu angeweza kujibu maswali yangu.

Mume wangu alipofariki mnamo mwaka 2019, niliamua kwenda Marekani, ambapo binti yangu anaishi sasa. Nilitaka kumwona na kujifunza zaidi kuhusu Kanisa lililorejeshwa.

Nilikaa Jiji la Salt Lake, Utah, kwa miezi minne na nusu. Nilienda Kanisani kila wiki na binti yangu. Nilikuwa na hisia ambazo sikuweza kuzielezea. Nilifanya majadiliano ya wamisionari. Nilijua yote yalikuwa ya kweli. Nilipata uzoefu wa siku nzuri sana maishani mwangu wakati nilipoingia ndani ya maji ya ubatizo na nilithibitishwa kuwa muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho mnamo Julai 27, 2019.

Wakati nilipotembea ndani ya chumba ili kuthibitishwa baada ya ubatizo wangu, kila mtu alikuwa analia. Kubatizwa na kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu ni zawadi kubwa kutoka kwa Baba yetu wa Mbinguni Baada ya uthibitisho, nilihisi kwamba mbingu zilikuwa wazi na kwamba tulikuwa wote pamoja huko. Katika baraka zangu za patriaki zilizofuatia, nilipokea ahadi nyingi maalumu za milele.

Kitabu cha Mormoni ni cha kweli. Kwa kusoma na kusali kuhusu kitabu hicho, tunaweza kupata ushuhuda wetu wenyewe juu yake. Pamoja na ushuhuda huo, tutajua kwamba Joseph Smith alikuwa nabii na kwamba kupitia yeye, Kanisa la kweli la Yesu Kristo lilirejeshwa duniani.