2021
Tafadhali Rudi
Julai 2021


Sauti za Watakatifu wa Siku za Mwisho

Tafadhali Rudi

Wakati tulipokuwa na watoto watatu, Vanessa alisema, “tunahitaji dini katika nyumba hii.”

Picha
a father helping his son with his shirt sleeve

Nilipokuwa na umri wa miaka 12, kaka yangu mkubwa aliwaleta nyumbani wamisionari, ambao walitutambulisha kwenye Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Hatimaye, mama yangu alianza kuwachukuwa kaka zangu wawili, dada yangu, na mimi kanisani. Haukupita muda mrefu sisi sote tulibatizwa.

Kidogo kidogo, hata hivyo, tuliacha kuhudhuria. Siku zote nililipenda Kanisa, bali nilipokuwa na umri wa miaka 17, mambo katika maisha yangu yaliniongoza kwenye njia tofauti. Nilijaribu kuwa mtu mzuri, na kamwe sikuwa na moyo mbaya. Bali nilipotea na nilianza kuishi njia za ulimwengu. Bila kujijua au kutambua, ulimwengu ulininyakua.

Kisha nilikutana na Vanessa. Siku moja baada ya kuwa pamoja kwa muda, alisema, “tunahitaji dini katika nyumba hii.” Kwa wakati huo tulikuwa na watoto watatu.

Na ulimwengu kama ulivyo, tulikuwa na wasiwasi kuhusu mwelekeo gani wa kiroho tungewapa watoto wetu. Nilifikiria kwamba kama nilikuwa narudi kwenye dini, nitarudi kwenye kanisa langu. Nilikumbuka kwamba palikuwa pahala penye watu wema.

Nilizungumza na muumini wa Kanisa na kumwambia nilikuwa nafikiria kurudi kanisani.

“Tafadhali rudi!” alisema.

Wasiwasi wangu mkubwa sana ulikuwa kwamba watoto wangu watafikiri kanisa lilikuwa linachosha na wasingelipenda, bali walilipenda. Tulipoendelea kwenda kanisani, Vanessa aliamua kwamba hapakuwa na chochote kinachofanana na Kanisa hili ambacho kinasaidia familia kukua pamoja. Kilikuwa hasa kile alichokuwa anakitafuta. Vanessa na mimi tulifunga ndoa, na yeye pamoja na watoto wetu walibatizwa.

Sasa tunaitembea njia ya injili kama familia. Lengo letu ni kuunganishwa pamoja katika hekalu.

Wakati wa ujenzi wa Hekalu la Rio de Janeiro Brazil, nililitembelea karibu nalo karibia kila siku. Ningewaeleza rafiki zangu, “Siku moja, nitakwenda kufunga ndoa katika jengo hili.”

“Ndugu, unasema jambo hilohilo kila siku!” walisema.

Nilisema kila siku kwa sababu nilijua kwamba hekalu lilikuwa linakaribia kumalizika, na nilitaka kujikumbusha kuendelea kufanya vitu sahihi ili kwamba familia yetu iweze kuunganishwa pamoja. Hili ni tamanio la moyo wangu.

Najua kwamba watoto wangu wataanza kujifunza zaidi kuhusu ulimwengu na kupitia baadhi ya vitu vilevile nilivyopitia. Bali ninaposhiriki uzoefu wangu pamoja nao, ninasema, “Tafadhali kamwe usikaribie vitu nilivyofanya kwa sababu havifai.”

Nawatia moyo watoto wangu kujifunza injili ya Yesu Kristo na kulenga kuwa wamisionari sasa ili waweze kubariki wengine. Hawaelewi kila kitu, bali wanajifunza. Hiki ndio ninachotamani kwa ajili yao.