2023
Mazungumzo Muhimu ya Kifamilia
Januari 2023


“Mazungumzo Muhimu ya Kifamilia,” Liahona,, Jan. 2023

Mazungumzo Muhimu ya Kifamilia

Mazungumzo muhimu yatawasaidia watoto wetu kujua ni kipi wanaamini na kwa nini wanakiamini.

Picha
baba na mwana wakipanda mlima

Vielelezo na Noah Regan

Mwana alimwomba baba yake amfundishe kuhusu upandaji wa mlima. Baba alimfundisha mambo yote muhimu, ikiwa ni pamoja na upangaji, usalama, matayarisho na vifaa. Mwana aliuliza ni lini watakwenda kuzungumza kuhusu nini cha kufanya inapotokea dharura. Baba alisema kwamba hakutaka kumtisha mwanaye na kwamba mazungumzo haya yangeweza kusubiri mpaka yatakapokuja kuwa ya lazima.

Walimaliza mafunzo yao na walikwenda kwenye safari yao ya kwanza ya kupanda Mlima Rainer karibu na Seattle, Washington. Uzoefu na hali vilianza vizuri mpaka pale hali ya hewa ilipobadilika kuwa mbaya sana, na mara walijikuta wakitazama kwenye macho ya maporomoko ya theluji yaliyokuwa yakiwajia.

Hawakujua nini cha kufanya kwa sababu hawakulijadili. Mwana alimwuliza baba yake, “Baba, je, Niko tayari sasa kwa ajili ya mazungumzo juu ya nini cha kufanya kwenye dharura?”

Mazungumzo Muhimu—katika usalama wa nyumba zetu—yanaweza kutusaidia kujitayarisha kwa ajili ya maporomoko ya theluji ya maisha.

Ukweli mkuu wa kwanza katika ulimwengu ni kwamba Mungu anatupenda,” alisema Mzee Jeffrey R. Holland wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili.1 Maneno yake yanatukumbusha kwamba upendo ni msingi kwa milele yote na kwa maisha yetu ya kila siku. Tukiwa na upendo huo kama nguzo, mazungumzo na miunganiko tunayofanya na familia yetu ni muhimu.

Kama mume, baba, mshauri wa shule na mshauri wa afya ya akili mwenye leseni, Nimegundua kwamba mazungumzo ya kifamilia ni muhimu sana na hayapaswi kucheleweshwa. Joy D. Jones, Rais Mkuu wa zamani wa Msingi, alisema: “Hatuwezi kusubiri mazungumzo kutokea yenyewe tu kwa watoto wetu. … Mazungumzo ya kifamilia kuhusu injili ya Yesu Kristo, mazungumzo muhimu, … yanaweza kumwalika Roho.”2

Mazungumzo muhimu ni nini?

Dada Jones alifafanua mazungumzo muhimu kama “mazungumzo rahisi ya kujali [ambayo] yanaweza kuwaongoza watoto [na kila mmoja wetu] kujua siyo tu kile wanachokiamini, lakini muhimu zaidi, kwa nini wanakiamini.”3 Neno moja ninalolipenda kutokana na ufafanuzi huu ni rahisi. Mazungumzo yetu hayahitaji kuwa ya kina au magumu au hata yaliyopangiliwa. Hakika, baadhi ya mazungumzo bora sana tutakayoweza kuwa nayo hayawezi kupangwa, zaidi ya kujitayarisha kwa siku zote kuwa na Roho pamoja nasi ili atusaidie.

Dada Jones alifundisha zaidi: “Kuongoka kwa bahati siyo kanuni ya injili ya Yesu Kristo. Kuwa kama Mwokozi wetu hakutatokea bila mpangilio.”4 Kunatokea mstari juu ya mstari, kwa kusudio la wakati na jitihada.

Mara ngapi mazungumzo muhimu yanapaswa kufanyika?

Tunapaswa kuzungumza na watoto wetu kila siku. Kadiri tunavyokuwa na mazungumzo muhimu mara kwa mara, ndivyo yanavyokuwa ya kawaida zaidi, ya asili na ya kuelimisha.

Njia mbaya kabisa ya kuwa na mazungumzo muhimu ni kutokuwa nayo kabisa! Mara nyingi tunafikiri siyo muda muafaka, ni vigumu mno au watoto wetu hawataelewa. Hatutaki kuwaudhi au kusema kitu kisicho sahihi au kumfanya mtu ahisi vibaya. Hata hivyo, angalau kujaribu kuwa na mazungumzo ni vyema kuliko kutosema chochote.

Jinsi gani tunakuwa na mazungumzo muhimu na watoto wetu?

Mbinu rahisi niliyoigundua kwa ajili ya kuwa na mazungumzo muhimu ni upendo, kusikiliza na kubadilika. Ingawa tunaweza tusiwe wakamilifu kwa yoyote kati ya hayo, tunaweza kujitahidi kufuata mpangilio kwa uthabiti.

Upendo: Bila msingi na matumizi ya upendo, hatuwezi kuwa na mazungumzo muhimu yenye tija. Upendo ndiyo nini, lini, kwa nini na jinsi gani ya kila kitu tunachofanya ndani ya familia zetu. Watoto wetu wanahitaji kuhisi wako salama wanapounganika na sisi, na upendo unatoa mazingira hayo muhimu. Tunaweza siku zote kuonesha upendo. Yesu Kristo alituonesha jinsi ya kufanya hivyo.

Dada Jones alisema: “Kadiri tunavyowalea na kuwaandaa watoto wetu, tunaruhusu haki yao wa kujiamulia, tunawapenda kwa moyo wetu wote, tunawafundisha amri za Mungu na vipawa Vyake vya toba na kamwe, katu, hatutawakatia tamaa. Hata hivyo, je, hii siyo njia ya Bwana kwa kila mmoja wetu?”5

Kusikiliza: Nimejifunza kupitia makosa yangu mwenyewe kwamba kusikiliza kwa makini ni sehemu ya kipeo cha mazungumzo muhimu yoyote. Kusikiliza kunapaswa kuja kwanza na mara ya pili na mara kwa mara. Yesu Kristo ni mfano mzuri mno wa jinsi ya kuwa na mazungumzo muhimu na kusikiliza kwa umakini. Tunajifunza katika Yohana 8 kwamba wakati Mafarisayo walipomletea mwanamke aliyeshikwa akizini, kitu cha kwanza alichosema kwa mwanamke yalikuwa maswali: “Wako wapi wale washitaki wako? je! hakuna mtu aliyekuhukumu kuwa na hatia?”(mstari wa 10). Ili kusaidia mafunzo muhimu yafanyike, Aliuliza maswali na alisikiliza kabla ya kufundisha.

Kubadilika: Mara baada ya kuwa tumependa, tumesikiliza na tumeunganika, tunafanya nini kutokea hapa? Je! tunahitaji kutubu, kufundisha, kusikiliza zaidi, kuhudumu, kuomba radhi, kusamehe? Mazungumzo muhimu yanapaswa kutupatia fursa ya kubadilika. Natumaini siku zote tunajitahidi kuwa, kama Rais Russell M. Nelson alivyosema, “wazuri zaidi kila siku.”6

Picha
baba na mwana wakizungumza pamoja

Jinsi gani tunaweza kuwa na mazungumzo muhimu mara kwa mara?

Utaongozwa na ufunuo kwa ajili ya kile kinachofanya kazi vizuri zaidi kwa ajili ya familia yako. Fikiria mapendekezo haya kutokana na uzoefu wa familia yetu:

Kujifunza maandiko kifamilia: Wakati nilipowauliza watoto wetu ni nini ambacho kinawasaidia zaidi wao kuwa na mazungumzo ya injili, walisema ilikuwa kujifunza maandiko pamoja kila jioni kwa kutumia Njoo,Unifuate.

Mkutano wa familia wa ushuhuda kila Jumapili ya mfungo: Kwa kawaida siyo mkutano rasmi wa ushuhuda lakini ni muda wa kila mtu ndani ya familia yetu kushiriki hisia, imani, jitihada na mafanikio. Mke wangu na mimi siku zote tunajitahidi kutoa ushuhuda juu ya Yesu Kristo. Mkutano huu umekuja kuwa moja ya matukio yenye tija kubwa katika nyumba yetu.

Chakula cha jioni cha familia: Tunaposema, “Ni saa ngapi sasa?” wakati wa chakula cha usiku, watoto wanajua ni muda kwa ajili ya kila mtu kushiriki jambo moja ambalo lilikwenda vizuri na jambo moja ambalo walitamani lingekuwa zuri kuhusu siku hiyo. Hiyo mara kwa mara huongoza kwenye maneno ya shukrani, upendo, wakati mwingine kukatishwa tamaa na mara kwa mara kwenye mazungumzo yaliyojaa injili ambayo yasingeweza kutokea vinginevyo.

Mazungumzo ya mmoja- mmoja: Ninafurahia muda katika kila mwezi siku ya Jumapili ya mfungo kukaa na kila mmoja wa watoto wangu mmoja baada ya mwingine, kusali kwa ajili yao kwa jina, kuwaangalia machoni na kuwauliza maswali. Najaribu kusikiliza na kuunganika na hisia zao na mahitaji yao. Inawezekana ilikuwa jambo geni kwao kwa mara ya kwanza, lakini sasa wanajisikia kulikosa siku tusipolifanya. Natumaini wanajua kwamba muda wangu pamoja nao ni muhimu zaidi kuliko chochote kingine na kwamba ninataka kuwa na mazungumzo muhimu pamoja nao kila siku.

Kupitia upya malengo: Tunatengeneza malengo ya mtu binafsi, ya wana ndoa na malengo ya familia kila Januari. Kisha tunajadiliana kuhusu ukuaji na maendeleo yetu juu ya malengo hayo kila mwezi wakati wa muda wa kujifunza maandiko au jioni ya nyumbani. Hii inatuongoza kwenye mazungumzo muhimu.

Ushirikiano wa wana ndoa au wazazi: Kila usiku wa Jumapili, wakati mke wangu na mimi tunapopitia kalenda zetu za kila wiki, pia tunaulizana kuhusu jinsi tunavyohisi na nini tunapambana nacho au tunahitaji msaada. Tunayo mazungumzo muhimu kuhusu ndoa yetu na kila mmoja wa watoto wetu na nini tunahitaji kufanya ili kuendeleza kuingiza injili ya Yesu Kristo ndani ya mioyo yetu.

Mke wangu ni msikilizaji mzuri zaidi kuliko mimi na mzuri zaidi kwenye kutusaidia sisi tuwe na usawa na tuliofokasi kwenye njia ya agano. Ninajifunza mengi kutoka kwake na nimebarikiwa mno kwamba alinichagua mimi kwa ajili ya milele.

Familia yetu sio kamilifu katika kufanya vitu vyote hivi, lakini tunafanya kwa uwezo wetu wote na tunaendelea kujaribu.

Kuwa tayari kabla maporomoko ya theluji hayajaja

Usingojee mpaka maporomoko ya maisha yaje kwenye ndoa yako, kwa watoto wako au kwenye mahusiano mengine. Siyo jambo la kama bali lini. Mazungumzo muhimu ya injili na mengineyo yanatuandaa sisi vyema kama tu yanatokea kwa makusudi na mara kwa mara.

Kuwa pamoja na mke wangu, watoto na familia milele ndiyo lengo langu kubwa na kusudi la kila kitu ninachokifanya, ikiwa ni pamoja na kila mazungumzo muhimu.

Ninafanya makosa, kama wote tunavyofanya, lakini kupitia nguvu ya Yesu Kristo na toba, ninainuliwa juu. Mwokozi ameahidi kutuimarisha sisi kwa nguvu Zake na mng’aro mkamilifu wa tumaini ambao Yeye hutupatia sisi kupitia Upatanisho Wake. Hatuhitaji kuwa wakamilifu, lakini tunahitaji kuwa tunaojitahidi kuwa bora! Kila mmoja wetu anayo nguvu ile inayopatikana kwetu. Hautashindwa. Mafanikio siku zote yapo kwenye juhudi.

Rais Nelson ameahidi kwamba “kadiri mnavyochagua kuacha Mungu ashinde katika maisha yenu, mtajionea wenyewe kwamba Mungu wetu ni ‘Mungu wa miujiza’ [Mormoni 9:11].”7 Hiyo inaweza kujumuisha kumwacha Mungu ashinde katika mazungumzo yetu muhimu. Mambo yote yanawezekana kupitia Mwokozi wetu, Yesu Kristo, ikijumuisha mazungumzo haya muhimu. Upendo siku zote ndilo jibu Lake!

Mwandishi anaishi Washington, Marekani.