2023
Nguvu ya Mfano
Januari 2023


“Nguvu ya Mfano,” Liahona, Jan. 2023.

Taswira za Imani

Nguvu ya Mfano

Nilijua kwamba njia pekee ambayo ningeweza kumleta mke wangu Kanisani ilikuwa kupitia mfano wangu. Nilipobadilisha tabia yangu, alianza kumhisi Roho wa Mungu.

Picha
Mume na mke wakisali

Picha na Cody Bell

Siku moja nikiwa njiani kuelekea kazini niliwaona vijana wawili wakihubiri neno la Mungu barabarani. Walinisimamisha na kuniuliza kama nilitaka kujua zaidi kuhusu Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Wakati ule, sikujua wapi familia yangu ilikuwa ikielekea. Hatukuwa na dira ya kiroho ya kuitafuta njia yetu.

Nilikuwa nimekunywa pombe asubuhi ile, kwa hiyo sikumbuki sana wamisionari waliniambia nini. Lakini walinipa Kitabu cha Mormoni na kipeperushi kuhusu Nabii Joseph Smith, pamoja na nambari yao ya simu. Baadaye siku ile, nilianza kukisoma. Kitu fulani kiligusa nafsi yangu niliposoma kitabu cha Mormoni, na nilishangazwa jinsi kijana wa miaka 14 angeweza kuwa na ufunuo mkubwa kama ule.

Nilikuwa nikitafuta ukweli, kwa hiyo nilianza kukutana na wamisionari. Baada ya kusoma karibu mada zote, nilijua nilihitaji kubatizwa. Lakini jinsi siku ya ubatizo wangu ilivyokaribia, tulikuwa na somo ambalo lilikuwa gumu kwa mimi kusikia. Somo hilo lilikuwa Neno la Hekima.

Somo lile lilikuwa gumu kwangu kwa sababu nilikuwa nakunywa sana pombe. Mazingira ya kazi yangu yalikuwa magumu. Kila mtu niliyefanya naye kazi alikuwa anakunywa pombe, na ndivyo nilivyofanya pia. Mara kwa mara ningekwenda kunywa pombe baada ya kazi na kurudi nyumbani usiku sana.

Lakini wamisionari walifanya kazi kubwa mno. Bado ninawapenda kwa ajili ya hilo. Walinifundisha kwamba Mungu anatutaka sisi kuwa imara na kwamba alitupa sisi Neno la Hekima ili litubariki. Kutii sheria hii kwa kweli ilikuwa vigumu kwangu, lakini polepole, nilianza kuitii. Ninakumbuka kuwapigia simu wamisionari kila siku, nikiwajuza maendeleo yangu na kuwaambia kwamba sikunywa pombe siku ile. Walifurahi sana kwa maendeleo yangu.

Kwa msaada wao, nilibatizwa na kuingia katika kundi la Yesu Kristo. Nilimhisi Roho katika siku ile nzuri! Lakini nilikuwa peke yangu nilipojiunga na Kanisa. Nilitaka familia yangu iwe pamoja nami.

Nilipozungumza na mke wangu, Clirime, kuhusu Kanisa, hakusikiliza hapo mwanzo. Babu yake alikuwa wa dini tofauti na alijiuliza kwa nini Kanisa la Yesu la Watakatifu wa Siku za Mwisho limekuja huku Albania. Nilijua kwamba njia pekee ambayo ningeweza kumleta mke wangu kwenye injili ilikuwa kupitia mfano wangu. Kupitia matendo yetu, watu wanaweza kuona sisi ni nani hasa.

Clirime aliona mabadiliko ndani yangu wakati nilipoacha pombe na kuanza kurudi nyumbani mapema kutokea kazini. Kwa sababu ya mabadiliko niliyokuwa nayafanya, alianza kumhisi Roho wa Mungu pale nilipomweleza kuhusu Kanisa. Siwezi kuielezea hisia ya furaha niliyokuwa nayo wakati aliponieleza kwamba siku moja yeye pia atabatizwa. Punde alianza kuchukuwa masomo ya wamisionari, ambayo niliwasaidia wamisionari kumfundisha. Nilikuwa na furaha hususan alipoweka tarehe kwa ajili ya ubatizo wake, miezi sita baada ya mimi kubatizwa

Kwa ubatizo wake na ubatizo wa watoto wetu wawili walipofikisha umri wa miaka minane kila mmoja, nilihisi kwamba tungeweza kuwa familia ya milele. Lakini ubatizo ulikuwa ni mwanzo tu. Ili kujitayarisha kwenda hekaluni, tulijua kwamba tulipaswa kumfuata Mungu mpaka mwisho wa maisha yetu, kushika amri, kwenda Kanisani, kushiriki sakramenti, kuhudumu katika miito, kusoma maandiko na kujifunza zaidi kuhusu maagano na mpango wa wokovu.

Siku tuliyounganishwa kama familia katika Hekalu la Frankfurt Ujerumani ilikuwa siku nyingine nzuri. Ndani ya hekalu, nilikuja kuelewa zaidi kuhusu mpango wa furaha Mungu alionao kwa ajili yetu, na nilihisi upendo Wake.

Bado nakumbuka ahadi ambazo Clirime na mimi tulizifanya hekaluni. Wakati wowote kitu kinapoharibika au tunapokuwa na wakati mgumu, akili yangu inarudi kwenye ahadi zile.

Kama familia tunajaribu kuishi kwa amani kati yetu kwa sababu hicho ndicho kitu tulichohisi pale hekaluni. Kila wakati ninapofikiria juu ya hekalu, ninajihisi mwenye furaha na aliyebarikiwa. Ninajua kwamba Mungu yupo na kwamba Anatupenda na anatutaka tuwe na furaha.