2010–2019
Njoo Uone
Oktoba 2014


Njoo Uone

Kanisa la Yesu Kristo mara yote limekuwa na litaendelea kuwa kanisa la umisionari.

Ujumbe wangu unawalenga zaidi watu wasio waumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Nitanena juu ya swali la kimsingi ambalo wengi wenu mmekuwa mkijiuliza: “Kwa nini Watakatifu wa Siku za Mwisho wanashauku ya kunieleza juu ya yale wanayoyaamini na kunikaribisha kujifunza kuhusu Kanisa lao?”

Ninaomba Roho wa Bwana aweze kunisaidia ili niwasiliane nanyi vizuri, nanyi muweze kuelewa vizuri, jibu langu kwa swali hili muhimu.

Jukumu Takatifu

Wafuasi waliojitolea wa Yesu Kristo kila mara wamekuwa na kila mara watakuwa wamisionari washupavu. Mmisionari ni mfuasi wa Kristo anayemshuhudia Yeye kama ni Mkombozi na kutangaza kweli za injili Yake.

Kanisa la Yesu Kristo daima limekuwa na litaendelea kuwa kanisa la umisionari. Kila mshiriki wa Kanisa la Kristo amekubali jukumu takatifu ya kusaidia katika kutimiza wajibu mtakatifu uliotolewa na Bwana kwa Mitume Wake, kama ilivyoandika katika agano Jipya.

“Enendeni, na mkayafundishe mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba, na la Mwana, na la Roho Mtakatifu:

“Mkiwafundisha kuyashika yale yote Niliyo waamuru nyinyi: na lo, Nipo pamoja nanyi daima, hata mwisho wa ulimwengu. Amina” (Mathayo 28:19–20).

Watakatifu wa Siku za Mwisho wanayachukulia kwa makini majukumu haya ya kuwafundisha watu katika mataifa yote juu ya Bwana Yesu Kristo na injili Yake iliyorejeshwa. Tunaamini kanisa lile lile lililoanzishwa na Mwokozi hapo kale kwamba limeanzishwa hapa duniani Naye katika siku za mwisho. Mafundisho, kanuni, mamlaka ya ukuhani, ibada, na maagano ya injili Yake yapo hivi leo katika Kanisa Lake.

Tunapowakaribisheni kuhudhuria kanisa pamoja nasi au kujifunza kutoka kwa wamisionari, hatujaribu kuwauzieni bidhaa. Kama washiriki wa Kanisa, hatupokei tuzo au bonasi katika shindano la mbinguni. Hatuhitaji tu kuongeza idadi ya tarakimu za Kanisa. Na muhimu zaidi, hatujaribu kukulazimisha kuamini tunavyoamini. Tunakualika kusikiliza ukweli uliorejeshwa wa injili ya Yesu Kristo ili uweze kujifunza, kutafakari, kuomba, na uje kujijulia wewe mwenyewe kama mambo tunayoshiriki nawe ni ya kweli.

Baadhi yenu mnaweza kujibu, “Lakini tayari ninamwamini Yesu na kufuata mafundisho Yake,” au “Sina uhakika kama kweli Mungu anaishi.” Mwaliko wetu kwako si jaribio la kudidimiza desturi za dini yako au mwenendo wa maisha yako. Yalete yote unayoyajua kuwa ni ya kweli, yaliyo mema, na yenye thamani – kisha uonje ujumbe wetu. Kama vile Yesu alivyowaalika wafuasi wake wawili “njoo uone” (Yohana 1:39), hivyo tunakuomba uje uone kama injili iliyorejeshwa ya Yesu Kristo itakuza na kurutubisha kila ambacho tayari unaamini kuwa cha kweli.

Hakika, tunahisi wajibu huu mtakatifu wa kuupeleka ujumbe kwa kila taifa, lugha, ndimi na watu. Na kwa uangalifu huu ndipo tunapofanya tukiwa na kundi la vijana 88,000 la wamisionari wakihudumu katika nchi zaidi ya 150 duniani kote. Vijana hawa wa ajabu wa kiume na kike na wale wazee huwasidia washiriki wa Kanisa letu kutimiza wajibu uliowekwa na majukumu ya kibinafsi ambayo kila mmoja wetu anayo ya kuitangaza injili ya milele ya Yesu Kristo (ona M&M 68:1).

Ni Zaidi ya Wajibu wa Kiroho

Lakini shauku yetu ya kuutangaza ujumbe huu siyo tu kuwa ni matokeo ya wajibu wa kiroho. Badala yake, hamu yetu kushiriki injili ya Yesu Kristo pamoja nanyi ni kuonyesha umuhimu wa ukweli huu kwetu. Ninaamini ninaweza kuelezea vizuri kwa nini tunakabili moja kwa moja tukitaka kuelezea imani yetu kwenu kwa kupitia uzoefu wa maisha ya mke wangu nami tuliokuwa nao miaka mingi iliyopita tukiwa na wana wetu wawili.

Jioni moja Susan nami tulisimama karibu na dirisha ndani ya nyumba yetu tukiwatazama wana wetu wadogo wakicheza nje. Wakati wa michezo yao, mdogo wa wale wavulana wawili aliumia kidogo kwa ajali. Tuligundua mara moja kwamba hakuumia sana, na tukaamua tusitoe msaada wa haraka. Tulitaka kutazama na kuona kama mazungumzo yetu ya kifamilia juu ya undugu mwema yatakuwa yamewaingia akilini. Kilichotokea baadaye ni cha kufurahisha na kuelimisha.

Kaka mkubwa alimfariji na kwa uangalifu alimsaidia mdogo wake kurudi ndani. Susan nami tulikaa karibu na jiko ili tuweze kuona kitakachofuata baada ya hapo, na tulijiandaa kutoa msaada wa haraka kama tungeona hatari ya kudhuru mwili ingetokea au ajali ya mbaya ingetokea.

Kaka mkubwa alivuta kiti kukipeleka kwenye sinki jikoni. Alipanda juu ya kiti, akamsaidia mdogo wake kukaa kwenye kiti, akafungulia maji, na kuendelea kutia sabuni nyingi ya vyombo kwenye mkono uliochubuka wa kaka yake mdogo. Alijitahidi kusafisha uchafu. Kitendo cha kaka mdogo katika utaratibu huu kinaweza tu kuelezewa kwa usahihi kwa kutumia lugha kutoka katika maandiko matakatifu: “na watakuwa na sababu ya kupiga makelele, na kulia, na kuomboleza, na kusaga meno yao” (Mosia 16:2). Na hivyo ndivyo alivyopiga kelele yule kijana mdogo!

Baada ya kumaliza kusafisha, mkono ulikaushwa kwa taulo. Hatimaye mayowe yakakoma. Kaka mkubwa kisha akapanda kwenye meza ya jikoni, akafungua kabati, na akaiona tyubu ya dawa ya kupaka. Ijapokuwa kidonda cha mdogo wake hakikuwa kikubwa au cha kutisha, kaka yake alimpaka karibu dawa yote kwenye tyubu katika mkono ulioumia. Mayowe hayakurejea tena, kaka mtu yaonekana alipendelea utulivu wa maumivu uliokuwa ukiletwa na dawa iliyokuwa kuliko kitendo cha kusafishwa kwa sabuni.

Kaka mkubwa akarudi tena kwenye kabati aliloipata dawa na akaliona boksi jipya la bandeji safi. Kisha akaifungua bandeji na kuufunga mkono wa mdogo wake–kutoka kwenye kifundo cha mkono hadi kwenye kiwiko. Dharura ikiwa imetatuliwa, na huku mapofu ya sabuni, dawa na maganda ya bandeji vikiwa vimetapakaa jikoni kote, vijana wadogo wawili walishuka chini ya kiti wakiwa na tabasamu na nyuso zenye furaha.

Kilichotokea baada ya hapo ndicho muhimu zaidi. Kaka aliyeumia alikusanya mabaki yote ya bandeji, na ile tyubu ya dawa iliyokaribia kwisha, na akaenda nje. Haraka akawatafuta rafiki zake na kuanza kuwapaka dawa na kuwafunga bandeji kwenye mikono yao. Sote Susan na mimi tulishangazwa kwa upendo, shauku, na uharaka wa matendo yake.

Ni kwa nini mvulana yule mdogo alifanya alichokifanya? Tafadhali tambua kwamba kwa haraka na uhalisia alitaka kuwapa rafiki zake kitu kile kile kilichomsaidia yeye pale alipoumia. Yule mvulana mdogo hakuhitaji kuambiwa, kutia changamoto, kuongozwa, au kulazimishwa kutenda. Shauku yake ya kutaka kushiriki na matokeo halisi ya msaada na uzoefu wa mtu aliyepata faida.

Wengi wetu kama watu wazima tunatenda vivyo hivyo tunapopata tiba au dawa ambayo inatuliza maumivu ambayo tumekuwa nayo kwa muda mrefu, au tunapopewa ushauri ambao unatusaidia kupambana na changamoto tukiwa na ujasiri na mchanganyiko wa uvumilivu. Kushiriki na watu wengine vitu vyenye maana kwetu au vilivyotusaidia si kitu kisicho cha kawaida kabisa.

Mfumo huo huo hasa unadhihirika katika mambo makubwa ya kiroho yenye umuhimu na matokeo. Kwa mfano, maelezo katika maandiko yajulikanayo kama Kitabu cha Mormoni yanaelezea maono yaliyopokelewa na nabii wa kale – kiongozi aliyeitwa Lehi. Kiini cha habari ya ono la Lehi ni juu ya mti wa uzima – ambao unawakilisha “upendo wa Mungu” ambao ni “wakutamanisha kuliko vitu vyote” na “wenye kuleta furaha katika nafsi” (1 Nefi 11:22–23; ona pia 1 Nefi 8:12, 15).

Lehi alielezea:

“Na ikawa kwamba nilienda na nikala matunda yake; na nikagundua kwamba yalikuwa matamu, zaidi ya yote ambayo nilikuwa nimeonja. Ndio, na nikaona kwamba tunda lilikuwa leupe, kushinda weupe wote ambao nilikuwa nimeuona.

Na nilipokula tunda lile lilijaza nafsi yangu na shangwe tele; kwa hivyo, nikaanza kutaka jamii yangu na wao pia wale” (1 Nefi 8:11–12; msisitizo umeongezwa).

Onyesho kuu la upendo wa Mungu kwa watoto Wake ni huduma ya maisha haya ya duniani, dhabihu ya kujitoa, na Ufufuko wa Bwana Yesu Kristo. Tunda katika mti linaweza kuwa ishara kwa baraka za Upatanisho wa Mwokozi.

Mjibizo wa haraka wa Lehi wa kula tunda la mti na kupata furaha kubwa ulileta matamanio ya kushiriki na wenzake na kuitumikia familia yake. Hivyo, alipomgeukia Kristo, pia akawageukia wengine katika upendo na huduma.

Na tukio jingine katika Kitabu cha Mormoni linaelezea kilichotokea kwa mtu aitwaye Enoshi baada ya sala yake ya dhati na yenye maombi ilisikika na kujibiwa na Mungu.

Alisema:

“Na nafsi yangu ikapata njaa; na nikapiga magoti mbele ya Muumba wangu, na nikamlilia kwa sala kuu na nikamsihi kwa nafsi yangu; na kwa siku nzima nikamlilia; ndiyo, na wakati usiku ulipofika bado nilipaza sauti yangu na hata ikafika mbinguni.

“Na sauti ikamjia, ikasema: Enoshi, umesamehewa dhambi zako, na wewe utabarikiwa.

“Na mimi, Enoshi, nilijua kwamba Mungu hawezi kusema uongo; kwa hivyo, hatia yangu iliondolewa mbali.

“Nami nikasema: Bwana, je, inafanywa vipi?

“Na akaniambia: Kwa sababu ya imani yako katika Kristo, ambaye wewe hujamwona kamwe wala kumsikia …. Kwa hivyo, nenda, imani yako imekufanya mkamilifu.

“Sasa, ikawa kwamba baada ya kusikia maneno haya nilianza kushughulika na ustawi wa ndugu zangu, Wanefi; kwa hivyo, nilimlilia Mungu kwa roho yangu yote na kwa niaba yao” (Enoshi 1:4–9; msisitizo umeongezwa)

Wakati Enoshi alipomgeukia Bwana “akiwa na moyo wenye nia ya dhati” (2 Nefi 31:13), wasiwasi wake kwa ajili ya mahitaji ya familia yake, marafiki, na watu wa karibu uliongezeka zaidi.

Somo la kuendelea tunalojifunza kutoka katika habari hizi mbili ni umuhimu unaojitokeza katika maisha yetu binafsi na ni baraka za Upatanisho wa Yesu Kristo kabla hatujatoa huduma iliyo ya dhati na halisi. Kama ilivyokuwa kwa Lehi, Enoshi, na mvulana wetu mdogo katika simulizi niliyoitoa, sisi kama washiriki wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho tumehisi maumivu yatokanayo na wasiwasi wa kiroho na dhambi. Pia tumeshuhudia kusafishwa, amani ya dhamira, uponywaji wa kiroho na kufanywa upya, na mwongozo unaopatikana tu kwa kujifunza na kuishi kanuni za injili ya Mwokozi.

Upatanisho wa Yesu Kristo unatoa utakaso unaowezesha kuwa safi na bila doa, kutoa maumivu unasaidia kuponya vidonda vya kiroho na kuondoa hatia, na ulinzi unaotuwezesha sisi kuwa waaminifu katika nyakati zote nzuri na mbaya.

Ukweli Mkamilifu Upo

Kwenu ninyi wanafamilia na marafiki ambao si washiriki wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, nimejaribu kuelezea sababu za msingi kwa nini sisi ni wamisionari.

Ukweli mkamilifu upo katika dunia inayozidi kubeza na kupuuzilia mbali ukweli. Katika siku za usoni, kila goti litapigwa na kila ndimi zitakiri kwamba Yesu ndiye Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba” (Wafilipi 2:10–11). Yesu ndiye Kristo wa kweli ndiye Mwana Pekee wa Baba wa Milele. Kama washiriki wa Kanisa hili, tunashuhudia Anaishi na kwamba Kanisa Lake limerejeshwa kwa ukamilifu wake katika hizi siku za mwisho.

Mialiko tunayoitoa kwenu ya kujifunza na kuonja ujumbe wetu ni matokeo chanya ya injili ya Yesu Kristo katika maisha yetu. Wakati mwingine kuwa wagumu kueleweka au wepesi au hata wenye mzingatio tukijaribu kuongea nanyi, lakini matamanio yetu ni kushiriki nanyi ukweli ambao una thamani kubwa kwetu.

Nikiwa mmoja wa Mitume wa Bwana, na kwa nguvu zote za nafsi yangu, ninatoa ushuhuda wa utukufu na uhalisi wake. Nami ninawalika “njoo na uone” (Yohana 1:39), katika jina takatifu la Bwana Yesu Kristo, amina.