2023
Baraka za Ukuhani
Machi 2023


“Baraka za Ukuhani,” Liahona, Machi 2023.

Misingi ya Injili

Baraka za Ukuhani

Picha
Kristo akiwatawaza Mitume Kumi na Wawili

Kristo Akiwatawaza Mitume Kumi na Wawili, na Harry Anderson

Baraka ya ukuhani hutolewa kupitia uvuvio kutoka kwa mwenye Ukuhani wa Melkizedeki. Baraka za Ukuhani hufanya iwezekane kwa watoto wote wa Mungu kupokea nguvu, uponyaji, faraja na mwongozo Wake.

Ukuhani

Ukuhani ni nguvu na mamlaka ya Mungu. Wanaume wenye kustahili walio na Ukuhani wa Melkizedeki hutenda katika jina la Yesu Kristo wakati wanapotoa baraka za ukuhani. Wanapotoa baraka hizi, wanafuata mfano wa Mwokozi wa kuwabariki wengine.

Picha
mikono ikiwa juu ya kichwa

Picha imepigwa na David Winters

Jinsi Baraka Zinavyotolewa

Baraka za ukuhani hutolewa kwa uwekaji mikono. Mwenye Ukuhani wa Melkizedeki anaweka mikono juu ya kichwa cha mtu anayepokea baraka. Kisha hutoa baraka kadiri Roho anavyomwongoza. Wale wanaotoa baraka na wale wanaozipokea huonesha imani katika Mungu na kutumaini katika mapenzi na wakati Wake.

Kuwapa Majina na Kuwabariki Watoto

Baada ya mtoto kuzaliwa, mwenye ukuhani humpatia jina na baraka (ona Mafundisho na Maagano 20:70). Hii mara nyingi hutokea kwenye mkutano wa mfungo na ushuhuda. Kwanza mtoto hupewa jina. Kisha mwenye ukuhani humpa mtoto baraka.

Picha
mvulana mgonjwa akipokea baraka ya ukuhani

Baraka kwa ajili ya Mgonjwa

Mwenye Ukuhani wa Melkidezeki anaweza kutoa baraka kwa watu ambao ni wagonjwa. Aina hii ya baraka ina sehemu mbili: upakaji wa mafuta na ufungaji wa upakaji mafuta. Kwanza, mwenye ukuhani huweka tone la mafuta ambayo yamekwishawekwa wakfu, au yamekwisha barikiwa, juu ya kichwa cha mtu na kutoa sala fupi. Kisha mwenye ukuhani mwingine hufunga upakaji mafuta na humpa mtu baraka kadiri atakavyoongozwa na Roho Mtakatifu.

Baraka za Faraja na Ushauri

Mwenye Ukuhani wa Melkidezeki anaweza kutoa baraka za faraja na ushauri kwa mwanafamilia na wengine ambao wanaziomba. Baba mwenye Ukuhani wa Melkidezeki anaweza kutoa baraka ya baba kwa watoto wake. Hizi zinaweza kuwa zenye msaada hasa wakati watoto wanapokabiliwa na changamoto.

Kuwatenga Waumini ili Watumikie katika Miito

Wakati waumini wa Kanisa wanapopokea miito, wanapewa baraka pale wanapotengwa ili watumikie. Kiongozi mwenye ukuhani huwabariki kwa mamlaka ya kutenda katika wito. Kiongozi mwenye ukuhani huwapa pia baraka ya kuwasaidia katika huduma yao.

Picha
mwanamke akisoma baraka yake ya patriaki

Picha na Shauna Stephenson

Baraka za Patriaki

Kila muumini wa Kanisa mwenye kustahili anaweza kupokea baraka ya patriaki. Baraka hii hutoa ushauri binafsi kutoka kwa Bwana. Inaweza kutoa mwongozo na faraja katika maisha yote ya mtu. Inaonesha pia ukoo wa mtu katika nyumba ya Israeli. Ni patriaki aliyetawazwa pekee ndiye anayeweza kutoa aina hii ya baraka.