2023
“Amani Yangu Nawapa”
Machi 2023


“Amani Yangu Nawapa,” Liahona, Machi 2023.

“Amani Yangu Nawapa”

Maneno yaleyale Yesu aliyoyazungumza kwenye Bahari ya Galilaya usiku ule wa dhoruba, Yeye anatuambia katika dhoruba za maisha yetu: “Nyamaza, utulie.”

Picha
mvua ikinyesha baharini

Picha kupitia Getty Images

Kwangu mimi na familia yangu, majira ya baridi ya 1944 yalikuwa wakati wa hofu na wasiwasi. Baba yangu akiwa mbali katika eneo la western front, mama yangu alipambana kuwalisha watoto wake wanne na kuwapa joto wakati vita ilipotishia nyumba yetu huko Chekoslovakia.

Kila siku hatari ilisonga karibu zaidi. Hatimaye, mama yangu aliamua kukimbilia nyumbani kwa wazazi wake huko mashariki ya Ujerumani. Kwa namna fulani, alifanikiwa kutupandisha kwenye moja ya gari moshi la mwisho la wakimbizi lililoelekea magharibi. Maeneo ya jirani milipuko, nyuso zenye wasiwasi na matumbo yenye njaa vilimkumbusha kila mmoja juu ya gari moshi ambalo tulikuwa tukisafiri nalo kupitia ukanda wa vita.

Usiku mmoja baada ya gari moshi letu kusimama kwa ajili ya watu kupata mahitaji, mama yangu aliharakisha kushuka ili atafute chakula. Aliporejea, kwa mshtuko, gari moshi lililotubeba sisi watoto lilikuwa limeondoka!

Akiwa amejawa wasiwasi, alimgeukia Mungu katika sala ya dhati na kisha kwa hasira alianza kutafuta kwenye kituo chenye giza cha gari moshi. Alikimbia kutoka kituo kimoja hadi kingine na kutoka gari moshi moja hadi lingine. Alifahamu kwamba ikiwa gari moshi lake lingeondoka kabla hajalipata, asingeweza kamwe kutuona tena.

Dhoruba katika Maisha Yetu

Wakati wa huduma ya Mwokozi, wanafunzi Wake walijua kwamba Yeye angeweza kutuliza dhoruba katika maisha yetu. Jioni moja, baada ya siku nzima ya kufundisha kando ya pwani ya bahari, Bwana alipendekeza kwamba “wavuke mpaka ng’ambo ya Bahari ya Galilaya (Marko 4:35).

Baada ya kuwa wameondoka, Yesu alipata mahali pa kupumzika ndani ya chombo na akasinzia. Punde mawingu yakawa meusi, “ikatokea dhoruba kuu ya upepo, mawimbi yakakipiga chombo hata kikaanza kujaa maji” (ona Marko 4:37–38).

Hatujui ni kwa muda gani wanafunzi walipambana kukifanya chombo kiendelee kuelea, lakini hatimaye hawangeweza kusubiri zaidi. Wakiwa hawajui nini cha kufanya, walilia, “Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia?” (Marko 4:38).

Sote tunapitia dhoruba za ghafla. Katika maisha yetu ya duniani ya majaribu na mitihani, tunaweza kuhisi huzuni, kuvunjika moyo na kukata tamaa. Mioyo yetu huvunjika kwa ajili yetu na wale tunaowapenda. Tuna wasiwasi na hofu na nyakati zingine tunapoteza tumaini. Wakati wa nyakati kama hizo, sisi pia tunaweza kulia “Mwalimu, si kitu kwako kuwa mimi ninaangamia?”

Katika ujana wangu moja ya nyimbo zangu pendwa za dini zilikuwa “Bwana Dhoruba Yavuma.”1 Ningeweza kujifikiria mwenyewe ndani ya chombo wakati “mawimbi [yalipokuwa] makali.” Sehemu muhimu na ya kuvutia ya wimbo inaendelea: “Upepo na mawimbi yaitika: Nyamaza, tulia.” Kisha unakuja ujumbe muhimu: “Hakuna maji ya kumdhuru Bwana wa bahari na nchi na mbingu.”

Ikiwa tutamkaribisha Yesu Kristo, Mfalme wa Amani, ndani ya chombo chetu, hatuhitaji kuwa na hofu. Tutajua kwamba tunaweza kupata amani katikati ya dhoruba ambazo huvuma ndani yetu na kutuzunguka. Baada ya wanafunzi Wake kuomba msaada, Yesu “Akaamka, akaukemea upepo, akaiambia bahari, Nyamaza, utulie. Na upepo ukakoma, kukawa shwari kuu” (Marko 4:39).

Maneno yaleyale Yesu aliyoyazungumza kwenye Bahari ya Galilaya usiku ule wa dhoruba, Yeye anatuambia katika dhoruba za maisha yetu: “Nyamaza, utulie.”

“Sivyo kama Ulimwengu Utoavyo”

Pamoja na wanafunzi, tunaweza kuuliza, “Ni nani huyu, basi, hata upepo na bahari humtii?” (Marko 4:41).

Yesu ni mtu tofauti na wengine. Kama Mwana wa Mungu, aliitwa kukamilisha misheni ambayo hakuna mwingine angeweza kuikamilisha.

Kupitia Upatanisho Wake na katika njia ambayo hatuwezi kuelewa kikamilifu, mwokozi alijichukulia juu Yake “maumivu na masumbuko na majaribio ya kila aina” (Alma 7:11) na “uzito wote wa dhambi za wanadamu.”2

Japo hakudaiwa na haki, aliteseka “madai … yote ya haki” (Alma 34:16). Kwa maneno ya Rais Boyd K. Packer (1924–2015), Rais wa Akidi ya Mitume Kumi na Wawili, “Yeye hakutenda kosa lolote. “Hata hivyo, jumla ya hatia zote, huzuni na hofu, maumivu na kufedheheshwa, mateso yote ya kiakili, kihisia na kimwili yanayojulikana kwa mwanadamu—Yeye aliyapitia yote.”3 Na aliyashinda yote.

Alma alitoa unabii kwamba Mwokozi “atajichukulia kifo, ili afungue kamba za kifo ambazo zinafunga watu wake; na atajichukulia unyonge wao, ili moyo wake ujae rehema, kulingana na mwili, ili ajue kulingana na mwili jinsi ya kuwasaidia watu wake kulingana na unyonge wao” (Alma 7:12).

Kupitia nguvu ya kiungu iliyoletwa ili apitie mateso yote na kwa sababu ya upendo kwetu, Yesu Kristo alilipa gharama ili atukomboe, atuimarishe na atuokoe. Ni kupitia upatanisho pekee kwamba tunaweza kupata amani tunayoihitaji sana na tunayoitaka katika maisha haya. Kama Mwokozi alivyoahidi, “Amani nawaachieni, amani yangu nawapa: niwapavyo mimi, sivyo kama ulimwengu utoavyo. Msifadhaike mioyoni mwenu, wala msiwe na woga.” (Yohana 14:27).

Picha
mchoro wa Yesu Kristo

Maisha na mafundisho ya Yesu Kristo vinatupatia njia za kuhisi amani Yake ikiwa tutamgeukia Yeye.

Picha ya Kristo, na Heinrich Hofmann

Njia za kupata Amani

Yesu Kristo, anayedhibiti vipengele, anaweza pia kurahisisha mizigo yetu. Yeye anazo nguvu za kuwaponya watu binafsi na mataifa. Yeye ametuonesha njia kwenye amani ya kweli, kwani Yeye ni “Mfalme wa Amani” (Isaya 9:6). Amani Mwokozi atoayo ingeweza kubadilisha uwepo wote wa mwanadamu ikiwa watoto wa Mungu wangeiruhusu. Maisha na mafundisho Yake vinatupatia njia za kuihisi amani Yake ikiwa tutamgeukia Yeye.

“Jifunze kwangu,” Yeye alisema “na sikiliza maneno yangu; enenda katika unyenyekevu wa Roho yangu, na utapata amani kwangu ” (Mafundisho na Maagano 19:23).

Tunajifunza Kwake pale tunapoinua nafsi zetu katika sala, kujifunza maisha na mafundisho Yake na “kusimama … katika mahali patakatifu,” ikiwa ni pamoja na hekaluni (Mafundisho na Maagano 87:8; ona pia 45:32). Hudhuria nyumba ya Bwana mara nyingi kadiri uwezavyo. Hekalu ni kimbilio lenye amani kutoka kwenye dhoruba zinazoongezeka za siku yetu.

Rafiki yangu mpendwa Rais Thomas S. Monson (1927–2018) alifundisha: “tunapokwenda [hekaluni], tunapokumbuka maagano tuliyofanya huko, tutaweza kuvumilia kila taabu na kushinda kila jaribu. Hekalu hutoa lengo kwenye maisha yetu. Huleta amani kwenye nafsi zetu—si amani itolewayo na wanadamu bali amani iliyoahidiwa na Mwana wa Mungu.”4

Tunasikiliza maneno Yake wakati tunapoyakubali mafundisho Yake katika maandiko matakatifu na kutoka kwa manabii Wake walio hai, tunapofuata mfano Wake na kuja Kanisani Kwake na kulishwa na neno zuri la Mungu.

Tunatembea katika unyenyekevu wa Roho Wake wakati tunapopenda kama vile Yeye alivyopenda, kusamehe kama Yeye alivyosamehe, kutubu na kuzifanya nyumba zetu mahala ambapo tunaweza kumhisi Roho Wake. Tunatembea pia katika unyenyekevu wa Roho Wake wakati tunapowasaidia wengine, tunapomtumikia Mungu kwa shangwe na tunapojitahidi kuwa “wafuasi wa imani ya Kristo” (Moroni 7:3).

Hatua hizi za imani na matendo huongoza kwenye uadilifu, hutubariki katika safari yetu ya ufuasi na hutuletea amani na lengo la kudumu.

“Mpate Kuwa na Amani Ndani Yangu”

Katika usiku wa kiza kwenye kituo cha kuogofya cha barabara ya gari moshi miaka mingi iliyopita, mama yangu alikabiliana na uchaguzi. Angeweza kuketi chini na kuomboleza msiba wa kuwapoteza watoto wake, au angeweza kuweka imani yake na tumaini lake katika matendo. Nina shukrani kwamba imani yake ilishinda hofu yake na kwamba tumaini lake lilishinda kukata kwake tamaa.

Hatimaye, katika eneo la mbali la kituo, aliliona gari moshi letu. Pale, hatimaye, tuliungana tena. Usiku ule na katika mchana na usiku wenye dhoruba uliofuatia, mfano wa mama yangu wa kuweka imani kwenye matendo ulituhimili pale tulipotumainia na kutafuta wakati ujao ulio angavu.

Leo, wengi wa watoto wa Mungu wanakuta kwamba gari moshi lao, pia, limeondoka. Matumaini na ndoto zao kwa ajili ya wakati ujao vimechukuliwa na vita, janga la ulimwengu na kuzorota kwa afya, kupoteza kazi, fursa za elimu na kupoteza wapendwa wao. Wamekata tamaa, ni wapweke, wana ukiwa.

Akina kaka na akina dada, marafiki wapendwa, tunaishi katika nyakati za hatari. Mataifa yamekanganywa, hukumu i juu ya nchi na amani imeondolewa kutoka duniani (ona Mafundisho na Maagano 1:35; 88:79). Lakini amani haipaswi kuondolewa mioyoni mwetu, hata ikiwa lazima tuteseke, tuomboleze na tumgoje Bwana.

Kwa sababu ya Yesu Kristo na Upatanisho Wake, sala zetu zitajibiwa. Ratiba ni ya Mungu, lakini ninashuhudia kwamba matamanio yetu ya haki siku moja yatatambuliwa na kwamba upotevu wetu wote utafidiwa, ikiwa tu tutatumia kipawa cha kiungu cha toba na kubaki waaminifu.5

Tutaponywa—kimwili na kiroho.

Tutasimama tukiwa safi na watakatifu mbele ya kiti cha hukumu.

Tutaungana na wapendwa wetu katika ufufuko mtukufu.

Wakati tukisubiri, na tupate faraja na kutiwa moyo wakati tunapoitegemea ahadi ya Mwokozi: “Mpate kuwa na amani ndani yangu” (Yohana 16:33).

Muhtasari

  1. “Bwana Dhoruba Yavuma,” Nyimbo za Dini, na. 53.

  2. Neal A. Maxwell, “Radhi Kunyenyekea,” Ensign, Mei 1985, 73.

  3. Boyd K. Packer, “Dhabihu Isiyo ya Ubinafsi na Takatifu ya Mwokozi,” Liahona, Apr. 2015, 38.

  4. Thomas S. Monson, “Baraka za Hekaluni,” Liahona, Okt. 2010, 15.

  5. Ona Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith (2007), 51.