2021
‘Anatujua kila mmoja binafsi’: Vijana Wakubwa huko Afrika ya Kati wanashiriki uelewa wao kutoka kwenye ibada ya Mzee Andersen
Julai 2021


SAUTI ZA ENEO

‘Anatujua kila mmoja binafsi’: Vijana Wakubwa huko Afrika ya Kati wanashiriki uelewa wao kutoka kwenye ibada ya Mzee Andersen

“Vijana wakubwa toka pande mbalimbali za eneo walikusanyika kuangalia ujumbe maalum uliotolewa kwa Kifaransa na Mtume wa Bwana, na kushiriki mawazo yao baada ya mkutano.”

Kutoka Cameroon hadi Kongo, vijana wakubwa wanaozungumza Kifaransa kutoka Eneo la Kati la Afrika walikusanyika mnamo Februari kuangalia ibada mubashara iliyotolewa na Mzee na Dada Andersen.

Ilikuwa ni moja ya ibada kadhaa mubashara zilizotolewa na Mitume wa Bwana—sambamba na wake zao na viongozi wengine wenye ushawishi wa Kanisa—pamoja na vijana wakubwa kutoka maeneo yao na kwa lugha zao.

Mzee Andersen, aliyehudumu misheni yake huko Paris, Ufaransa akiwa kijana, alisema kwamba alinoa Kifaransa chake kwa ajili ya tukio hilo.

Ujumbe wake ulijikita kwenye uhalisia wa Baba wa Mbinguni mwenye upendo na Mwanawe Yesu Kristo: kitu ambacho amepata ufahamu wake mkubwa katika miaka 12 aliyohudumu kama Mtume.

Katika nyakati tofauti kwenye miaka hiyo, aliwaambia vijana wakubwa kwamba, alipata “uzoefu usioelezeka na hisia ambazo sikuzitarajia katika maisha yangu, vikinihakikishia uhalisia wa Yeu Kristo.”

Alitoa mialiko sita kwa wasikilizaji wake:

  1. Amini katika Mungu.

  2. Amini kwamba wewe ni mwana au binti wa Mungu, na kwamba Anakujua na Anakupenda.

  3. Amini kwamba unaweza kuzungumza na Baba yako wa Mbinguni na Yeye atamtuma roho wake juu yako.

  4. Amini kwamba ufalme wa Mungu unasonga mbele kote ulimwenguni na kwamba sisi kila mmoja ni sehemu muhimu ya maandalizi ya Ujio wa Pili wa Mwokozi.

  5. Amini kwamba wengine unaowajua wataikubali injili ya Yesu Kristo.

  6. Amini kwamba Yesu Kristo ni Mwokozi wa Ulimwengu.

Mzee Andersen aliwahakikishia vijana wakubwa kwamba “imani yenu katika Yesu Kristo si bure. Mtamwona tena. Ulimwengu wote utajua kwamba Yeye ni Mwana wa Mungu.”

Na kisha, vijana wakubwa toka pande mbalimbali za eneo walishiriki kile walichojifunza kutoka kwenye uzoefu huo.

Kabeya Konji Freddy, mshiriki wa kata ya Kanshi huko Mbuji-Mayi, alisema kwamba ujumbe mkuu kwake ulikuwa ni ule wa kazi ya umisionari. “Kama vijana wakubwa tunapaswa kuwa watiifu na tayari kuhubiri injili,” alisema. “Tunapaswa kumwamini Yeye na kuwa wenye shukrani Kwake wakati tukifanya kazi ya umisionari, ambayo ni maandalizi ya Ujio wa Pili wa Kristo.”

Dieudonné Tshibangu, kutoka kata ya Kanshi alisema, “Sasa ninajua jukumu muhimu tulilonalo katika mpango wa Mungu na kazi Yake ya kukusanya Israeli. Ninajua kwamba Mungu hutusikiliza sana kila mara tunaposali. Yeye yu pamoja nasi na anatupenda sana.”

Robert Banjangi kutoka kata ya Kanshi alisema kwamba “tunapaswa kumweka Kristo kwenye kiini cha matatizo yetu yote.” Kabla ya kujikita kwenye jambo lolote jipya, tunapaswa “kumgeukia Kristo na kutafuta mapenzi ya Bwana. Mara tunapojua mapenzi hayo ni nini, tunapaswa kuwa na ujasiri wa “kutenda kile ambacho roho Wake hutuambia tutende”.

Nzuzi Fallone Alaret, kutoka tawi la New Bell huko Cameroon, alisema alijifunza ujumbe wa imani iliyolenga kwenye shukrani. “Tunapaswa kuwa wenye shukrani kwa baraka za Mungu; tunapaswa kuwa na imani,” alisema. “Pia tunapaswa kusali na kumuuliza Yeye kitu chochote kama vile marafiki,” alisema. Vijana wakubwa wanapaswa “kuwa na imani” kwamba Bwana atajibu sala zetu.

Nathan Ntika, kutoka kata ya Kanshi, alisema alikuwa amejifunza kwamba analo jukumu binafsi katika kujiandaa kwa ajili ya ujio wa Yesu Kristo duniani. “Kwa haraka nimeelewa kwamba mimi ni kipengele muhimu katika kuandaa Ujio wa Pili wa Mwokozi,” alisema.

Vijana wakubwa wanahitaji kuwa na imani “isiyotikisika na kuamini” katika Yesu Kristo, hata ingawa hatumwoni, ndicho ambacho Demnie Idjol, kutoka tawi la New Bell Cameroon alijifunza kutoka kwenye ibada hiyo.

“Pia nimejifunza juu ya nguvu ya sala, na kwamba tunapomwomba Bwana, mara zote Yeye atajibu,” alisema. “Kwa dhati ninaamini katika kweli na Kitabu cha Mormoni ambavyo Baba yetu wa Mbinguni amevituma ili visaidie kutujenga tuwe imara.”

“Imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yasiyoonekana,” alisema Kasongo kutoka kata ya Kanshi, akinukuu Waebrania 11:1. Ukumbusho wa akina Andersen wa andiko hili “umeniimarisha na kunipatia lengo la daima kuwa imara katika mambo yote yahusianayo na Mungu.”

Felicia kutoka Kanshi huko Mbuji-Mayi alisema alijifunza kwamba “ni muhimu kwamba tusizikane imani zetu. Ninajua kwamba mimi ni binti wa Baba yetu wa Mbinguni, na kwamba ninahitaji kumwamini Yeye bila kujali hali niliyonayo,” alisema.

Kwa Balanganayi Badibanga Papy kutoka Pieu de Kananga, moja ya jumbe zilizopenya ilikuwa ni jinsi tunavyopendwa sana na Baba yetu wa Mbinguni. “Anatujua kila mmoja binafsi na anatupenda kikamilifu,” alisema. “Tunaweza kuzungumza na Baba yetu wa Mbinguni, na Yeye atamtuma roho Wake kwetu. Tunapaswa kuamini kwamba sisi ni mabinti na wana wa Mungu.”

Tunapaswa kuamini kwamba watu wengine tunaowajua wataikubali injili ya Yesu Kristo, alisema.

Sehemu ya mchakato huo inatuhitaji sisi kuonyesha imani, ambayo ni kanuni ya matendo na nguvu, alisema Balanganayi. “Imani hutusaidia kujiandaa vyema kwa ajili ya matukio ya Ujio wa Pili wa Yesu Kristo, ambao uko karibu, kulingana na maneno ya nabii.”

Njia moja ya kuonyesha imani ni kwa kukubali wito wa kuwa shahidi wa Mungu na Injili Yake. Kama waumini wa Kanisa Lake, tunahitaji “kuzungumza kuhusu imani yetu katika Yesu Kristo kwa uwazi.”