Liahona
Safari Yangu kama Mwanafunzi wa Yesu Kristo katika Kanisa Lake Lililorejeshwa
Machi 2024


Makala

Safari Yangu kama Mwanafunzi wa Yesu Kristo katika Kanisa Lake Lililorejeshwa

Nilipomaliza shule ya msingi, baba yangu alinifunza kufanya maamuzi mwenyewe, ilinibidi nisafiri zaidi ya kilomita 150 ili kufika katikati ya jiji la Mweka katika mkoa wa Kasai katika Jamhuri ya Kidemokarsia ya Kongo, ambapo nilianza shule ya upili katika mafunzo ya kibinadamu pamoja na makuhani wa Kikatoliki.

Mara nilipomaliza shule ya upili, ilinibidi nifuate Imani ya Kikatoliki ili kuendelea na mafunzo yangu ya kibinadamu; basi mwaka wa 5 na wa 6 wa mafunzo ya kibinadamu tuliandaliwa kuikumbatia Imani ya Kikatoliki. Baada ya kumaliza mduara wa kibinadamu, tulipata fursa ya kujiandaa wenyewe kama watarajiwa wa makasisi wa Josephite.

Nilipoanza mwaka wangu wa kwanza katika falsafa, kaka yangu mkubwa aliyekuwa mkufunzi wangu alimtaarifu kasisi kwamba sipaswi kuendelea kama mtarajiwa wa makasisi wa Josephite. Bila kukubali upinzani, kasisi wa Josephite, kupitia baba yangu wa ubatizo, aliniomba niachane na njia ya kujiweka wakfu katika Kanisa Katoliki kwa ajili ya kitu kingine.

Ndipo basi nilihamia hadi mji mkuu wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, mji wa Kinshasa, kuanza masomo yangu ya sheria. Mara nilipowasili Kinshasa mnamo mwaka 2007, nilijisajili katika Chuo Kikuu cha Kinshasa. Katika mwaka wangu wa kwanza mnamo mwaka 2008, tulipatwa na mgomo mkubwa wa Chuo Kikuu cha Kinshasa. Wakati wa mgomo, nilihama mtaa wangu nilioishi na kwenda eneo la Masina kuishi na kaka yangu mkubwa.

Na mara nikiwa Masina, wakati wa mgomo, niligundua Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho katika mtaa nilioishi na kaka yangu mkubwa.

Nilifanya uamuzi wa kwenda katika jengo la Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho siku ya Jumapili. Nilipowasili kwenye jengo, kaka mmoja aliniamkia mlangoni na kunialika niingie ndani. Kisha nilishiriki katika ibada ya Jumapili na baadaye nilitambulishwa kwa wamisionari.

Nilipata masomo ya wamisionari kwa wiki 2. Baada ya kufundishwa, nilipata hamu kubwa ya kubatizwa kama muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho.

Hata hivyo, huu ulikuwa mwanzo wa upinzani mkali kutoka miongoni mwa familia yangu na kaka yangu mkubwa ambaye alikuwa mlezi wangu. Alikiambia kijiji kimjulishe kila mtu kwamba ninataka kuwa muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, kwamba ni kanisa baya, kwamba kusiwe na mtu yeyote atakayeniunga mkono wala kuchangia pesa za kunisaidia katika masomo yangu.

Matokeo yake nilisitisha shule yangu ya sheria na kuanza kujiandaa kwa ajili ya misheni. Nashukuru ushauri na maelekezo ya Askofu Mutambay, nilibakia muumini wa Kanisa licha ya upinzani na nikaanza kujiandaa kwa ajili ya misheni yangu. Nilitumikia misheni ya Lubumbashi DR Congo kuanzia Juni mwaka wa 2013 hadi Juni mwaka wa 2015.

Baada ya kutumikia kama mmsisionari nilirudi nyumbani na nilibahatika kupata mradi wenye mwongozo wa kanisa wa Perpetual Education Fund (PEF) ambao uliniwezesha kufikia malengo yangu katika kumaliza masomo yangu ya sheria kupitia mradi ulioanzishwa na rais wa 15 wa kanisa Rais Gordon B. Hinckely.

Leo, mimi ni mwanasheria. Mimi pamoja na Mke wangu Mireille ni wazazi wa watoto wanne: Ross Power Kongo, Ron Cross Kongo Munemeka, Blacke Prestone Kongo Ibula na Brian Lesser Kongo. Nilikubali kupambana na dhiki kwa kutumia Imani yangu bila kujua kile ambacho kingenitokea wakati nilipotelekezwa kwa kuchagua Kanisa Liliorejeshwa.

Mimi najua kwamba Mungu ni Baba yetu wa Mbinguni na licha ya magumu na upinzani Yeye yupo pale kutusaidia. Kamwe sitavunjika moyo kwa sababu ya njia niliyochukua na uamuzi wangu wa kujiunga na kanisa Lake.

Najua huu ulikuwa uamuzi bora ambao nimeshawahi kuufanya.Milele nitakuwa na shukurani. Joseph Smith ni nabii wa Urejesho, na nina shukrani kuwa katika Kanisa la Yesu Kristo, Amina!