2020
Kupata Furaha katika Kufanya Kazi ya Bwana
Aprili 2020


Kidijitali Pekee: Vijana Wakubwa

Kupata Furaha katika Kufanya Kazi ya Bwana

Kama vijana wakubwa, maisha yana hekaheka. Kuna mambo mengi sana tungeweza kufanya: kuendeleza elimu yetu, kutafuta wenza wetu wa milele, kufanya maamuzi ya kazi, kuanzisha familia. Na pamoja na hayo yote mazuri, pia tumehamasishwa “daima tupatikane tukifanya kazi ya Bwana.”1

“Ni muda kwetu sote kuelewa kwa uwazi zaidi jukumu letu katika kuharakisha kazi ya wokovu. Tunapofanya kazi ya muumini mmisionari,… kazi ya hekalu na historia ya familia na kufundisha injili kuwa sehemu asilia ya maisha yetu, tutapata uzoefu wa furaha kuu na kufunikwa na vipawa vya kiroho tunavyohitaji ili kuimarisha Kanisa.”2

Hapa ni vijana wakubwa wachache wanaopata furaha kwa kutenga muda kwa ajili ya kazi ya Bwana.

Historia ya Familia: Anza Tu Sasa

“Urejesho umenifanyia mengi kibinafsi kwa sababu nimekuja kujua kwamba familia zinaweza kuwa pamoja daima,” anasema Itumeleng Tlebere kutoka Maseru, Lesotho. “Ninaweza kuwaona babu na bibi zangu ambao wamekwisha fariki. Hiyo ndiyo maana ninapenda sana historia ya familia. kwa sababu mimi ni kizazi cha kwanza Kanisani, nina kazi kubwa ya kufanya kwa ajili yao.”

Itumeleng anajua kutokana na uzoefu kwamba kutunza kumbukumbu na taarifa inaweza kuwa changamoto, lakini anawahimiza vijana wakubwa wengine kutafiti historia ya familia zao: “Anza tu kuifanya. … Historia ya familia imenifanya niwe na shukrani kwa kila kitu nilichonacho.” Inaweza kufanya hivyo hivyo kwako.

Kuhudumu: Kuwa Mikono ya Mungu

Lucy Fergeson kutoka Utah, USA, anashiriki jinsi kuhudumu kulivyomsaidia kupita wiki mbaya ya maisha yake—lakini katika njia isiyotarajiwa. Ilikuwa wiki ya mtihani wa mwisho shuleni, wiki yenye shughuli nyingi, na rafiki yake wa kiume alikuwa amevunja mahusiano naye. Na kisha, anasema, “ningesahau, lakini mimi na mwenza wangu mhudumiaji tulipanga kutengeneza keki kwa ajili ya dada tuliyepangwa kumhudumia.”

Walipooka pamoja, mwenza mhudumiaji wa Lucy alisikiliza, alionesha huruma na alitoa ushauri. “Kutengeneza na kupeleka keki haikuwa kitu ambacho kingekuwa muhimu sana au kuleta tofauti kubwa,” Lucy anakumbuka. “Lakini baada ya mwenza wangu kunishusha nyumbani, niligundua kwamba ilikuwa hasa kile nilichohitaji ili kuhisi vizuri na kwamba nyakati zingine Mungu hutuma watu wengine kuwa mikono Yake. Kile kilichokuwa kizuri kwangu ilikuwa kwamba msaada ulikuja kutoka kwa mwenza wangu mhudumiaji badala ya akina dada waliopangwa kunihudumia. Ninashukuru alinisaidia kuhisi sikuwa peke yangu na kwamba nilipendwa.”

Kazi ya umisionari: Ishi Kuwa Mfano

Huitaji kuwa mmisionari wa muda wote ili kueneza injili. Vennela Vakapalli, kutoka Andhra Pradesh, India, anaeleza, “Ninapokuwa kwenye mabasi, ninapokuwa kwenye magari moshi, ninafungua Kitabu cha Mormoni na kukisoma. Na watu wengi wananiuliza kukihusu.”

Ashlee Dillon kutoka Utah, USA, anashiriki: “Kwa vile tu sikutumikia misheni haimaanishi mimi siyo mmisionari. Badala ya kuiacha familia yangu kwenda kumtumikia Bwana, ninamtumikia Bwana pamoja na familia yangu. Ninawatumikia wengine, na ninaishi kuwa mfano wa mfuasi wa Yesu Kristo.”

Uzazi: Wafunze Watoto Injili

Ingrid de Bastian Ortiz, kutoka Veracruz, Mexico, ni mama wa miaka 26 wa watoto watatu. Anaeleza, “Wakati wazazi vijana wa watoto wadogo, kuna siku zinazochosha, zenye kazi za nyumbani zisizoisha vilevile umakini ambao watoto wanahitaji. Hata hivyo, tunahisi jukumu kubwa kufundisha injili kwa watoto wetu ili wajue kwamba wao ni watoto wa Mungu.

“Jukumu langu kama mama ni kuwasaidia kutambua wao wenyewe kwamba Baba yetu wa Mbinguni ana mpango kwa ajili yao.”

Hata kama bado hujawa mzazi, bado unaweza kuwa sehemu katika kusaidia kufundisha watoto. “Ni muhimu kwamba watoto wafahamu kuhusu kanuni na mafundisho haya,” anasema Ingrid, “kwamba tuweze kwa hakika kuchangia kama vijana wakubwa waseja au wenye ndoa kwenye baadhi ya miito ya Msingi na chekechea.”

Sisi sote tu vijana wakubwa wenye shughuli nyingi. Lakini bila kujali hali yako, unaweza kutafuta njia rahisi za kufanya kazi ya Bwana katika nyanja zote za maisha yako—zote kubwa na ndogo.

Muhtasari

  1. Rais Thomas S. Monson, “Mpaka Tutakapokutana Pamoja Tena,” Liahona, Nov. 2013, 110.

  2. “Kuharakisha Kazi ya Bwana,” Liahona, Okt. 2013, 33.