2020
Jinsi Vijana Wakubwa Wanavyoleta Tofauti katika Urejesho Unaoendelea.
Aprili 2020


Vijana Wakubwa

Jinsi Vijana Wakubwa Wanavyoleta Tofauti katika Urejesho Unaoendelea

Vijana wakubwa siku zote wamekuwa na wajibu muhimu katika kazi ya wokovu.

Picha
young adults

Wakati wowote unaposikia mwaliko kutoka kwa kiongozi wa Kanisa kushiriki katika Urejesho unaoendelea au kusaidia katika kukusanya Israeli, je umewahi kufikiria, “Ni nini naweza nikafanya? Mimi ni mtu mmoja tu,” “Mimi nina umri mdogo sana,” “Mimi sina ndoa,” au “Mimi sijui vya kutosha. Ni tofauti gani ninaweza kuleta?”

Kila mmoja wetu ana mawazo kama hayo akilini mara kwa mara. Lakini jaribu kunyamazisha mashaka haya binafsi unaposoma sentensi chache zinazofuata:

  • Joseph Smith alikuwa na umri wa miaka 22 tu wakati alipoanza kutafsiri Kitabu cha Mormoni.

  • Oliver Cowdery alikuwa pia na miaka 22 na John Whitmer alikuwa na miaka 26 (na wote wawili walikuwa waseja!) wakati walipoanza kufanya kazi kama waandishi wa Joseph.

  • Mwaka 1835, wakati Akidi ya kwanza ya Mitume Kumi na Wawili ilipoitwa, walitofautiana kwa umri kuanzia miaka 23 hadi 35.

  • Wengi wa Watakatifu wa mwanzo ambao walijiunga na Kanisa na kueneza injili walikuwa vijana wakubwa.

Kwa jumla, Mungu alifanya kazi kupitia vijana wakubwa katika siku za mapema za Urejesho wa injili ya Yesu Kristo. Watu kama wewe.

Acha hilo lizame ndani yako.

Kanisa halingeweza kuenea kote duniani leo hii kama kila mtu angedhania kwamba hawezi kuleta tofauti. Na wewe—ndio, wewe!—ni sehemu ya kizazi kilichochaguliwa kuendelea kurejesha na kuongoza Kanisa la Yesu Kristo leo hii.

Ulitumwa Hapa. Sasa hivi. Kwa sababu fulani.

Wakati akizungumza kuhusu kizazi chetu, Rais Russell M. Nelson alifundisha, “mnaishi ndani ya ‘saa ya kumi na moja.’ Bwana ametangaza kwamba huu ni wakati wa mwisho ambao Atawaita watumishi katika shamba Lake la mzaibu kuwakusanya wateule kutoka pande zote nne za dunia. (Ona M&M 33:3–6.) Na wewe ulitumwa kushiriki katika ukusanyaji huu.”1

Fikiria kuhusu jeshi la wamisionari 65,000 wanaoshiriki injili siku nzima, kila siku, kote ulimwenguni. Fikiria kiuhusu vijana wakubwa wote ambao wanafanya maagano hekaluni, wakitumia ukuhani uliorejeshwa na baraka za hekaluni na wakiahidi kuwa waaminifu, kuimarisha familia zao, na kuujenga ufalme wa Mungu duniani. Fikiria kuhusu vijana wakubwa wanaohudumu kama viongozi wa Kanisa kote ulimwenguni. Fikiria kuhusu wale ambao wanasonga mbele kumfuata Yesu Kristo licha ya upinzani wote dhidi yao. Vijana Wakubwa wamekuwa sehemu muhimu ya Urejesho toka mwanzo. Na Urejesho unaoendelea umekuwa sehemu muhimu ya maisha ya vijana wakubwa wengi ambao ni waumini wa Kanisa.

Kile Urejesho Unachomaanisha Kwetu

Kwa wengi wetu, kushiriki kwetu katika Urejesho kunatokana na kile ambacho urejesho umetufundisha sisi. Kwa Vennela Vakapalli, kijana mkubwa muongofu kutoka Andhra Pradesh, India, “Urejesho unahusu kutafuta ufunuo. Joseph Smith alitafuta ufunuo msituni. Alishauriana na Bwana, alisubiri apate jibu, alikuwa na subira. Hayo ndiyo ninayopenda.” Vennela anaeleza, “Kabla ya kusikia kuhusu Urejesho, Sikujua mengi kuhusu kutafuta ufunuo. Mojawapo ya vitu vikuu ambavyo hunishangaza mimi ni kiasi cha muda aliotumia kupata ufunuo kutoka kwa Mungu. Hicho ndicho nilichojifunza kutoka kwenye Urejesho.”

Emma na Jacob Roberts, wenza wa umri mdogo kutoka Utah, Marekani, wanakubali kwamba Urejesho unahusu “ufunuo unaoendelea”—kwa ajili yetu na kwa ajili ya ulimwengu—”kwamba tunaweza kuwa na nabii, msemaji hapa duniani kutoka kwa Mungu, kuhakikisha kwamba changamoto zozote ulimwengu unazoleta, tuna mtu ambaye anafanya kazi na kusali na kuzungumza na Mungu kuhakikisha kwamba tuko tayari na tuna uwezo wa kukabiliana na changamoto zozote ulimwengu unazoleta wakati unapobadilika.”

“Ufahamu mwingi ambao huja na urejesho unafanya maisha yangu kuwa rahisi na tulivu,” anasema Jacob. Unakuja na hakikisho “kwamba kuna Mungu anayetupenda na kutulinda,” Emma anasema. “Nia Yake ni tuwe na furaha. Kama vijana wakubwa, tunaweza kumwamini Yeye kikamilifu na kumfuata kwa sababu tunajua lengo Lake ni sisi tuwe na furaha. Tunajua kwamba sisi ni viumbe wa milele, na hilo linanipa matumaini na imani nyingi, kwamba chochote ninachofanya hivi sasa na makosa yoyote ninayofanya hivi sasa, bado naweza kutubu na nina wakati huu wa kuendelea na kujifunza.”

Kutiwa moyo kwa aina hiyo pia kulimsaidia Ramona Morris, kijana mkubwa kutoka Barbados, wakati alipojifunza kuhusu Urejesho kwa mara ya kwanza. Miongoni mwa vitu vingine, alipata ushuhuda kwamba “Baba wa Mbinguni yuko pale kwa ajili yetu. Urejesho huleta amani kwa wale ambao wana maswali kuhusu maisha yao na mpango wa Mungu kwa ajili yao.”

Lakini hata kama kuelewa Urejesho kumeleta uwazi katika maisha yake, anakiri pia “kuwa mbali sana na makao makuu ya Kanisa, ni vigumu kuhusiana na injili, lakini kwa sababu nimekuwa na ushuhuda imara wa injili ya urejesho, ninajua kwamba mbali nilivyo, bado naweza kuhisi kuwa sehemu ya Urejesho, kwamba siko peke yangu.”

Na hayuko peke yake. Vijana wakubwa kote ulimwenguni wanashiriki katika Urejesho kupitia huduma ya hekaluni, historia ya familia, na kazi ya umisionari. Kwa uelewa wa ufunuo binafsi ambao tunapata kutokana na kujifunza kuhusu Ono la Kwanza la Joseph Smith na Urejesho, tunaweza wote tukaendelea kutafuta kujua mapenzi ya Mungu na kile tunachoweza kufanya katika Urejesho unaoendelea.

Picha
world map

Ramani kutoka Getty Images

Vijana Wakubwa Wakiongoza Kanisa

Tunaweza kuwa vijana wakubwa, lakini tunaweza kuwa viongozi katika Kanisa sasa hivi. Licha ya kuwa muumini pekee wa Kanisa katika familia yake, Janka Toronyi kutoka Győr, Hungary, anaimarishwa na kushiriki kwa vijana wakubwa wenzake katika vipengele vingine vya Urejesho: “Marafiki zangu kadhaa wametumikia misheni, na imekuwa vizuri sana kuona maendeleo yao na kisha wanarudi na wanakua kabisa kupitia uzoefu wao. Ni uzoefu mzuri sana kwa ajili yetu sisi wote. Na siku zote ni ajabu kuwaona rafiki zangu vijana wakubwa waseja wakitumikia katika wito wao na wakati mwingine hata nafasi wanazotafuta wenyewe, kama kujitolea kuwa washauri katika mikutano ya FSY (Kwa Ajili ya Nguvu kwa Vijana). Ninahisi kwamba Urejesho hauhusu tu kufundisha watu kuhusu injili—ni kuhusu kuwaimarisha waumini ambao tuko nao.”

Vijana wakubwa kule Hungary wanaelewa kwamba wao ni viongozi wa baadaye wa Kanisa. “Tunahitajika na tunahitaji kuwa tayari kutimiza jukumu, ambalo wakati mwingine linakuwa gumu,” Janka anakiri. “Bwana anaharakisha kazi na sisi ni sehemu yake. Wakati mwingine tunafikiria, ‘Nawezaje kufanya hili?’ Lakini ni vizuri kuona kwamba viongozi wetu wana imani kubwa na sisi. Inatia moyo kwa wale ambao wanapenda Kanisa na wana ushuhuda imara, kwa sababu tunajua kwamba siku moja tutawajibika. Ni lazima tuwajibikie maendeleo yetu ya kiroho sisi wenyewe.”

Sean na Stefany Joseph kutoka Magharibi mwa Australia wanashiriki katika Urejesho kwa kuwashauri vijana katika kata yao. “Kwangu mimi, kushiriki katika Urejesho ni kuvisaidia vizazi vya siku za baadaye kuelewa injili ni nini na jinsi inavyoweza kuwasaidia wao na wengine kwenye maisha yao,” Stefany anasema. “Tunaweza tukasaidia kujenga msingi thabiti kwa ajili ya Kanisa katika nchi yetu baadaye.”

“Tunataka kuwasaidia vijana kupata ushuhuda wa Kitabu cha Mormoni na Joseph Smith na kutambua kwamba wao wenyewe hakika ni watoto wa Mungu,” Sean anaeleza. “Hatutaki kiwe tu ni kitu ambacho waliimba katika Msingi—tunataka wajue hakika kwamba ni kweli.”

Kulingana na Vennela, kuishi injili India si rahisi kila wakati, lakini anajua uwezo wa vijana wakubwa waumini huko utawatia msukumo wengine na kusaidia Urejesho kusonga mbele. “Hapa, vijana wote wakubwa ni waaminifu. Wao hutafuta nafasi za kushiriki ushuhuda wao,” anasema. “Sisi ni kama watangulizi hapa India. Tunahama kutoka sehemu mbalimbali na hata baadhi yetu wanaziacha familia zao. Maisha yanaweza kuwa magumu hapa, lakini bado sisi huchagua kuishi injili. Maandiko yananipa tumaini, nguvu, na ujasiri mwingi.”

Haijalishi mahali tulipo, kama vijana wakubwa, tunaweza kuendelea kuwa na ushawishi wenye nguvu juu ya Urejesho unaoendelea kupitia imani yetu na kujitolea kwenye injili.

Siku za Baadaye za Kanisa: Ni Juu Yetu Sisi

Sisi ni siku za baadaye za Kanisa. Tuko katika vita vya mwisho. Baba wa Mbinguni anatutegemea sisi kumsaidia kufanya kazi Yake—Kazi Yake ya kuleta mabadiliko ya milele. Anajua tuna uwezo wa kutosha kuendelea kusonga mbele na kupigana dhidi ya kila kitu ambacho adui ana nia ya kutumia. Na Shetani anapoteza tumaini. Anajua anapigana katika vita ambavyo atashindwa kwa sababu kazi ya Bwana itashinda.

“Tunajua kwamba Bwana anaharakisha kazi na hakuna anayeweza kuisimamisha,” Janka anasema. “Tunajua itafanyika kwa vyovyote vile. Lakini lazima tuamue kama tutakuwa sehemu yake na kuisaidia kusonga mbele au kutazama kutokea pembeni. Tuna haki ya kujiamulia kuwa sehemu yake, na tuna ushuhuda wa kutuwezesha kuchagua haki na kuchagua kumfuata Kristo. Ni lazima tuwe sehemu yake.”

Kwa hivyo ni juu yetu kuchagua ni upande wa nani tuko.

Ni juu yetu kuwa na ujasiri wa kusimama kwa ajili ya kile tunachoamini.

Ni juu yetu kutafuta ufunuo binafsi kwa ajili ya maisha yetu.

Ni juu yetu kukubali changamoto ngumu tunazokabiliana nazo kuimarisha imani yetu katika Mwokozi.

Ni juu yetu kumfuata Yeye na kufanya kadri ya uwezo wetu kuwaleta wengine Kwake.

Ni juu yetu kuvumilia hadi mwisho vizuri tuwezavyo.

Hakika tuko katika siku za mwisho. Na kuliongoza Kanisa katika kile Rais Nelson anachoita “kipindi chenye ushawishi mkubwa zaidi katika historia ya ulimwengu”2 inaonekana kama jukumu gumu sana. Lakini fikiria kuhusu hilo—Baba wa Mbinguni alituamini vya kutosha na kutuhifadhi sisi ili tuje duniani hasa kwa wakati huu, wakati huu ambapo tunakabiliana na majaribu yasiyohesabika na vivuta mawazo na dhana nyingi zinazopingana.

Kwa kututuma hapa katika kipindi hiki cha maana sana, Baba wa Mbinguni hakuwa anatupangia kufeli. Anajua uwezo wetu, nguvu zetu, ujasiri wetu, na hatimaye, Anajua tunaweza kuleta tofauti katika Urejesho wa Kanisa, bila kujali umri wetu na hali ya ndoa. Bila kujali majaribu yetu ni magumu kiasi gani, au jinsi isivyowezekana kuongoza na kushiriki injili kote ulimwenguni inavyoonekana, pamoja Naye kando yetu, ni nani anaweza kupigana dhidi yetu? Atatuwezesha kutimiza yasiyowezakana.

Muhtasari

  1. Russell M. Nelson, “Simameni kama Wanamilenia wa Kweli,” Liahona, Okt. 2016, 48.

  2. Russell M. Nelson, “Simameni kama Wanamilenia wa Kweli,” Liahona, 46.