2020
Yenye Thamani Kuliko Bangili ya Fedha
Aprili 2020


Yenye Thamani Kuliko Bangili ya Fedha

Sylvie Houmeau

Quebec, Kanada

Picha
bracelet

Kielelezo na Emily Lui

Wakati nilipoombwa kuongoza mjadala katika Muungano wa Usaidizi wa Akina Mama kuhusu mwaliko wa Mwokozi kulisha kondoo Wake, niliamua kwamba kama nilitaka kuwatia moyo akina dada, ni sharti nifanye jambo kwa ajili ya mmoja wa kondoo Wake.

Nilitafuta ujasiri na kumwalika dada asiyeshiriki kikamilifu kuhudhuria shughuli ya Muungano wa Usaidizi wa Akina Mama pamoja nami. Alikubali mwaliko wangu na tulikuwa na wakati mzuri. Nilihisi kuwa huu ulikuwa mfano mwema, na nilikuwa na hamu ya kushiriki uzoefu wangu. Lakini Bwana alikuwa na mengi ya kunifundisha.

Asubuhi moja nilipokuwa nikijiandaa, niligundua kwamba bangili yangu ya fedha ilikuwa imepotea. Nilikuwa nimepewa bangili hii kama zawadi kwenye siku ya kuzaliwa nilipokuwa nazuru Ufaransa, kwa hivyo ilikuwa na maana maalum kwangu. Nilianza kuitafuta mahali ambapo palikuwa na uwezekano mkubwa kupatikana, lakini sikuipata. Kisha nilijiambia kwamba kama ningesali tu, ningeweza kuipata bangili yangu kwa haraka.

Baada ya kusali, nilitafuta kila mahali. Kwa muda wa siku mbili nilisali kwa dhati na kutafuta kwa bidii. Nilimlilia Baba wa Mbinguni anisaidie kuipata, lakini sikuipata. Moyo wangu ulikuwa na huzuni kwa sababu bangili hii ilikuwa ya thamani kwangu.

Jioni moja mwanangu alisali pamoja nami kando ya kitanda changu. Baada ya sala yetu, aliokota kitu fulani na kunipa. Ilikuwa bangili yangu! Alikuwa ameipata chini ya kitanda. Kwa namna fulani sikuiona nilipoitafuta. Nililia kwa furaha kuipata tena.

Ghafla, wazo lilinijia: “Je, wewe unasali kwa dhati namna hii kwa niaba ya dada zako wa Kanisani? Je, wao ni wa thamani kwako kama bangili yako? Vipi kuhusu dada zako nje ya Kanisa? Unasali kwa niaba yao pia?”

Wakati niliposhiriki uzoefu wangu wa bangili yangu iliyokuwa imepotea katika Muungano wa Usaidizi wa Akina Mama, tulikuwa na mjadala mzuri. Niliwaambia akina dada kwamba wakati Mwokozi anapotuomba tuwalishe kondoo Wake, ni lazima tukumbuke kwamba “thamani ya nafsi ni kubwa mbele za Mungu” (Mafundisho na Maagano 18:10). Anatutaka tuwajali wale walio karibu na sisi na kupenda, kujali, na kusali kwa nguvu zetu zote kwa ajili yao. Wakati tunapofanya hivyo, tutagundua kwamba kila mtu ana thamani kubwa zaidi kuliko bangili ya fedha.