Mkutano Mkuu
Ngazi ya Imani
Mkutano mkuu wa Aprili 2022


Ngazi ya Imani

Kutoamini kunazuia uwezo wetu wa kuona miujiza, wakati mtazamo wa imani katika Mwokozi unafungua nguvu za mbingu.

Ni jinsi gani changamoto za maisha zinaathiri imani yetu katika Yesu Kristo? Na ni athari ipi imani yetu itakuwa nayo kwenye furaha na amani tunayoipata katika maisha haya?

Mwaka ulikuwa 1977. Simu iliita, na ujumbe ulirarua mioyo yetu. Carolyn na Doug Tebbs walikuwa kwenye mchakato wa kuhamia kwenye nyumba yao mpya baada ya kumaliza mafunzo ya chuo. Akidi ya wazee ilikuwa imekuja kupakia mizigo kwenye gari. Doug, akihakikisha kwamba njia ilikuwa salama kabla ya kurudi nyuma, aliangalia kwa mara ya mwisho. Kile ambacho hakukiona kilikuwa binti yake mdogo, Jennie, akiruka nyuma ya gari kwa wakati ambao haukuwa sahihi. Papo hapo, mpendwa wao Jennie hakuwepo tena.

Nini kingetokea baada ya hapo? Je maumivu makali waliyoyapata na hisia zisizoweza kubebeka za upotevu zingeweza kujenga ufa mkubwa usiozibika kati ya Carolyn na Doug, au zingeweza kuunganisha mioyo yao pamoja na kuimarisha imani yao katika mpango wa Baba wa Mbinguni?

Njia ya kupitia mateso yao imekuwa ndefu na ya maumivu, lakini kutoka sehemu fulani yalikuja malimbikizo ya kiroho ya kutokata tamaa, bali “kushikilia njia [yao].”1 Kwa namna fulani wanandoa hawa wa kupendeza wakawa hata zaidi kama Kristo. Wenye msimamo zaidi. Wenye huruma zaidi. Waliamini kwamba, katika muda Wake, Mungu angeweka wakfu mateso yao kwa ajili ya faida yao.2

Ingawa maumivu na upotevu visingeweza na haviwezi kuondoka kabisa, Carolyn na Doug wamefarajiwa kwa hakikisho kwamba kwa kubaki imara kwenye njia ya agano, mpendwa wao Jennie atakuwa wao milele.3

Mfano wao umeimarisha imani yangu katika mpango wa Bwana. Hatuoni vitu vyote. Yeye anaona. Bwana alimwambia Joseph Smith katika jela ya Liberty kwamba “mambo haya yote yatakupa wewe uzoefu, na yatakuwa kwa faida yako. Mwana wa Mtu amejishusha chini yao wote. Je, wewe u mkuu kuliko yeye?”4

Tunapokubali mapenzi ya Bwana, Yeye anatufundisha jinsi ya kutembea pamoja Naye. Kama mmisionari kijana nikuhudumu Tahiti, niliombwa kumhudumia mtoto mchanga mgonjwa. Tuliweka mikono yetu juu ya kichwa chake na kumbariki apate ahueni. Afya yake ilianza kutengemaa, lakini kisha alianza kuugua tena. Mara ya pili tukambariki lakini matokeo yakawa yale yale. Ombi la tatu likaja. Tulimsihi Bwana kwamba mapenzi yake yafanyike. Muda mfupi baadaye, nafsi hii ndogo ilirudi kwenye nyumba yake ya mbinguni.

Tulikuwa na amani. Tulitaka mtoto mchanga aishi, Lakini Bwana alikuwa na mipango mingine. Kukubali mapenzi Yake badala ya yetu wenyewe ni msingi wa kupata furaha bila kujali hali zetu.

Imani ndogo tuliyonayo katika Yesu Kristo tunapoanza kujifunza kuhusu Yeye inaweza kubaki katika mioyo yetu pale tunapokabiliana na changamoto za maisha. Imani yetu katika Yeye inaweza na itatuongoza kupita magumu ya maisha. Kwa hakika, tutagundua kwamba kuna urahisi kwenye upande mwingine wa magumu ya maisha6 pale tunapobaki “[imara] katika Kristo, tukiwa na mng’aro mkamilifu wa tumaini.”7

Sehemu ya lengo la maisha ni kuruhusu vikwazo hivi muhimu viwe mawe ya kuvukia wakati tunapopanda kile ninachokiita “ngazi ya imani”—ngazi kwa sababu inapendekeza kwamba imani si tuli. Inaweza kwenda juu au chini kulingana na chaguzi tunazozifanya.

Tunapojitahidi kujenga imani katika Mwokozi, yawezekana tusielewe kikamilifu upendo wa Mungu kwa ajili yetu na tunaweza kutii sheria Zake kwa hisia za sharti. Hatia inaweza kuwa hata motisha yetu ya msingi kuliko upendo. Muunganiko wa kweli Kwake unaweza kuwa bado haujafikiwa.

Tunapotafuta kuongeza imani yetu, tunaweza kukanganywa na kile alichofundisha Yakobo. Alitukumbusha kwamba “Imani pasipo matendo imekufa.”8 Tunaweza kujikwaa ikiwa tunafikiri kila kitu kinatutegemea sisi. Utegemezi uliokithiri kwetu sisi wenyewe unaweza kuzuia uwezo wetu wa kufikia nguvu za mbingu.

Bali tunaposonga kuelekea imani ya kweli katika Yesu Kristo mtazamo wetu unaanza kubadilika. Tunatambua kwamba utii na imani katika Mwokozi vinatustahilisha kuwa na Roho Wake pamoja nasi daima.9 Utii unakuwa si tena jambo la kukera, bali la kutafuta.10 Tunatambua kwamba utii kwa amri za Mungu unatuwezesha kuaminika Kwake. Kwa tumaini Lake huja ongezeko la nuru. Nuru hii huongoza safari yetu na inaturuhusu kuona kwa uwazi zaidi njia tunayopaswa kwenda.

Lakini kuna zaidi. Wakati imani yetu kwa mwokozi inapoongezeka, tunaona badiliko kidogo ambalo hujumuisha uelewa wa kiungu wa uhusiano wetu na Mungu—hatua mathubuti kutoka “Nini ninachotaka?” kwenda “Mungu anataka nini?” Kama Mwokozi, tunataka kutenda “si kama nitakavyo mimi, bali kama utakavyo wewe.”11 Tunataka kufanya kazi ya Mungu na kuwa chombo katika mikono Yake.12

Maendeleo yetu yanakuwa ya milele. Rais Russell M. Nelson amefundisha kwamba kuna mengi zaidi ambayo Baba wa Mbinguni anatutaka tuyajue.13 Tunapoendelea, tunaelewa vyema kile Bwana alichomfundisha Joseph Smith: “Kwani ikiwa mnazishika amri zangu mtaupokea utimilifu wake, na kutukuzwa ndani yangu, … ninawaambia, mtapokea neema juu ya neema.”14

Jinsi gani tunapanda juu zaidi ya ngazi ya imani ni uamuzi wetu. Mzee Andersen alifundisha kwamba , “Imani siyo kwa bahati, bali kwa kuchagua.”15 Tunaweza kuchagua kufanya chaguzi zinazohitajika ili kuongeza imani yetu kwa Mwokozi.

Fikiria matokeo ya chaguzi zilizofanywa wakati Lamani na Lemueli waliposhuka ngazi ya imani huku Nefi akipanda juu zaidi. Je, kuna uwakilishi wa wazi kuliko tofauti kati ya jibu la Nefi la “nitakwenda na kufanya”16 dhidi ya Lamani na Lemueli, wakiwa ndio kwanza wamemuona malaika, wakijibu “Vipi itawezekana kwamba Bwana atamkabidhi?”17

Kutoamini kunazuia uwezo wetu wa kuona miujiza, wakati akili za imani katika Mwokozi zinafungua nguvu za mbinguni.

Hata wakati imani yetu ni dhaifu, mkono wa Bwana siku zote utakuwa umenyooshwa kutuinua.18 Miaka mingi iliyopita, nilipokea uteuzi kuratibu kigingi nchini Nigeria. Dakika ya mwisho, kulikuwa na mabadiliko katika tarehe. Kulikuwa na mtu katika kigingi ambaye alikuwa ameamua kuondoka mjini tarehe ya kwanza ya mkutano. Hakutaka kuchukua jukumu la kuitwa kama rais wa kigingi.

Wakati alipokuwa mbali, alipata ajali ya kutisha, lakini hakuumia. Hii ilimsababisha kufikiria kwa nini maisha yake yalikuwa yamenusurika. Alifikiria upya uamuzi alioufanya. Alitubu na kwa unyenyekuvu alihudhuria tarehe mpya ya mkutano. Na ndiyo, aliitwa kuwa rais mpya wa kigingi.

Mzee Neal A. Maxwell alifundisha: “ni kwa kufungamanisha tu mapenzi yetu na ya Mungu ndiyo furaha kamili inapopatikana. Chochote chini ya hapo matokeo yake ni sehemu ndogo zaidi.”1919

Baada ya kufanya “mambo yote yaliyo katika uwezo wetu,” ndipo ni wakati wa “kusimama imara … kuuona wokovu wa Mungu.”20 Nililiona hili wakati nikihudumu kama kaka mhudumiaji kwa familia ya McCormick. Akiwa ameolewa kwa miaka 21, Mary Kay ilihudumu kwa uaminifu katika miito yake. Ken hakuwa muumini wa Kanisa na hakuwa na hamu ya kuwa muumini, lakini kwa kumpenda mkewe, alichagua kuhudhuria Kanisani pamoja naye.

Jumapili moja nilipata msukumo kushiriki ushuhuda wangu kwa Ken. Nilimuuliza kama ningeweza kufanya hivyo. Jibu lake lilikuwa rahisi na wazi: “Hapana asante.”

Nilishangazwa. Nilikuwa nimehisi ushawishi na nilijaribu kuufuata. Ilikuwa ya kushawishi kuamua kwamba nimefanya sehemu yangu. Lakini baada ya sala na tafakari, Niliweza kuona kwamba ingawa dhamira zangu zilikuwa sahihi, nilikuwa nimejitegemea sana mimi mwenyewe na kidogo sana kwa Bwana.

Baadaye, Nilirudi, lakini kwa mtazamo tofauti. Nitakwenda tu kama chombo mikononi mwa Bwana, bila tamanio lingine zaidi ya kumfuata Roho. Nikiwa na mwenzangu mwaminifu, Gerald Cardon, tuliingia nyumbani kwa McCormick.

Punde baadaye, nilihisi kushawishiwa kumwalika Gerald kuimba “Najua Mkombozi Wangu yu Hai.”21 Alinipa mtazamo wa mshangao, lakini kwa kuwa na imani katika imani yangu, alifanya hivyo. Roho wa kupendeza alijaza chumba. Ushawishi ulikuja wa kumwalika Mary Kay na Kristin, binti yao, kushiriki shuhuda zao. Wakati walipofanya hivyo, Roho alikua na nguvu zaidi. Hakika, baada ya ushuhuda wa Kristin, machozi yalikuwa yakitiririka chini ya mashavu ya Ken.22

Mungu alikuwa ameingilia. Mioyo haikuwa tu imeguswa bali ilibadilishwa milele. Miaka ishirini na moja ya kutoamini ilitupiliwa mbali kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Wiki moja baadaye, Ken alibatizwa. Mwaka mmoja baadaye, Ken na Mary Kay waliunganishwa katika nyumba ya Bwana kwa sasa na kwa milele yote.

Kwa pamoja tulipata uzoefu wa nini ilimaanisha kubadilisha mapenzi yetu kwa mapenzi ya Bwana, na imani yetu katika Yeye iliongezeka.

Tafadhali zingatia maswali yafuatayo yaliyotolewa na manabii watakatifu wa Mungu pale unapojitahidi kupanda ngazi yako ya imani:

Je, nimevua kiburi changu?23

Je, ninatoa nafasi moyoni mwangu kwa ajili ya neno la Mungu?24

Je, ninaruhusu mateso yangu kuwekwa wakfu kwa faida yangu?25

Je, nipo tayari kuacha mapenzi yangu yamezwe katika mapenzi ya Baba?26

Kama nimehisi kuimba wimbo wa upendo wa ukombozi, je, ninaweza kuhisi hivyo sasa?27

Je, ninamwacha Mungu ashinde katika maisha yangu?28

Kama unaona kwamba njia yako ya sasa inapingana na imani yako katika Mwokozi, basi tafadhali tafuta njia yako ya kurudi Kwake. Kuinuliwa kwako na kule kwa uzao wako kunategemea juu ya hilo.

Na tupande mbegu za imani ndani zaidi ya mioyo yetu. Na turutubishe mbegu hizi wakati tunapojifunga wenyewe kwa Mwokozi kwa kuheshimu maagano tuliyoyafanya na Yeye. Katika Jina la Yesu Kristo, amina.