Mkutano Mkuu
Uongofu Kwenye Mapenzi ya Mungu
Mkutano mkuu wa Aprili 2022


Uongofu Kwenye Mapenzi ya Mungu

Uongofu wetu binafsi hujumuisha jukumu la kushiriki injili ya Yesu Kristo kwa ulimwengu.

Nashukuru kwa ajili ya wito wa kinabii wenye nguvu wa Rais Russell M. Nelson juu ya huduma ya umisionari na ujumbe wa mwongozo wa Rais M, Russell Ballard asubuhi ya leo.

Jukumu la kimisionari huko Uingereza mwaka jana liliniruhusu kutafakari juu ya matukio ya thamani ya kiroho ambayo yalikuwa ni msingi wa maamuzi yangu kutumikia kama mmisionari.1 Nilipokuwa na umri wa miaka 15 kaka yangu mkubwa mpendwa, Joe, alikuwa na miaka 20—umri wa uliofaa wakati huo wa kutumikia misheni. Marekani, kwa sababu ya mgogoro na Korea, watu wachache waliruhusiwa kutumikia. Kwa mwaka mzima mtu mmoja tu angeitwa kutoka katika kila kata.2 Ilishangaza wakati askofu wetu alipomuomba Joe kuangalia uwezekano huu pamoja na baba yetu. Joe alikuwa akiandaa maombi kwa ajili ya kwenda shule ya utabibu. Baba yetu, ambaye hakuwa mshiriki kikamilifu Kanisani, alikuwa amefanya maandalizi ya kifedha kwa ajili ya kumsaidia na hakupendezwa na Joe kwenda misheni. Baba alipendekeza kwamba Joe angefanya vizuri sana kwa kwenda shule ya utabibu. Hili lilikuwa suala kubwa sana kwenye familia yetu.

Katika majadiliano ya kupendeza na kaka yangu mkubwa mwenye hekima na wa mfano, tulitamatisha kwamba uamuzi wake kama atatumikia misheni na kuhairisha masomo yake ulitegemea maswali matatu: (1) Je, Yesu Kristo ni Mungu? (2) Je, Kitabu cha Mormoni ni neno la Mungu? Na (3) Je, Joseph Smith ni Nabii wa Urejesho? Kama jibu la maswali ni ndio, ilikuwa wazi kwamba Joe angefanya vizuri zaidi kwa kupeleka injili ya Yesu Kristo ulimwenguni kuliko kuwa daktari mapema.3

Usiku ule tuliomba kwa unyenyekevu na kwa nia ya dhati. Roho, katika njia ya nguvu isiyokatalika, alithibitisha kwangu kwamba majibu ya maswali haya matatu yalikuwa ni ndiyo. Hilo lilikuwa tukio la ushawishi mkubwa kwangu. Niligundua kwamba kila uamuzi ambao ningeufanya katika maisha yangu yote ungeshawishiwa na kweli hizi. Pia nilijua kwamba ningetumikia misheni kama ningepatiwa fursa. Katika huduma ya maisha yote na uzoefu wa kiroho, nimeelewa kwamba uongofu wa kweli ni matokeo ya kukubali kwa dhamira mapenzi ya Mungu, na tunaweza kuongozwa katika matendo yetu na Roho Mtakatifu.

Tayari nilikuwa na ushuhuda wa uungu wa Yesu Kristo kama Mwokozi wa ulimwengu. Usiku ule nilipokea ushuhuda wa kiroho wa Kitabu cha Mormoni4 na Nabii Joseph Smith.

Joseph Smith Alikuwa Chombo katika Mikono ya Bwana

Ushuhuda wako utaimarishwa wakati utakapojua katika moyo wako kupitia sala yako kwamba Nabii Joseph Smith alikuwa chombo katika mikono ya Bwana. Katika miaka nane iliyopita mojawapo ya jukumu langu katika Mitume Kumi na Wawili ilikuwa ni kupitia tena na kusoma makala na hati za kupendeza za Joseph Smith na utafiti ambao ungeleta chapisho la juzuu ya Saints. 5 Ushuhuda na kumuenzi kwangu Nabii Joseph Smith kumeimarishwa pakubwa sana na kuongezeka baada ya kusoma kuhusu maisha yake na huduma yake kama nabii kabla ya kuzaliwa.

Tafsiri ya Joseph Smith ya Kitabu cha Mormoni kwa kipawa na uwezo wa Mungu ilikuwa msingi wa Urejesho.6 Kitabu cha Mormoni ki thabiti kiundani, kimeandikwa vizuri, na kina majibu ya maswali makuu ya maisha. Ni ushuhuda mwingine wa Yesu Kristo. Nashuhudia kwamba Joseph Smith alikuwa mwema, aliyejaa imani, na chombo katika mikono ya Mungu kukileta Kitabu cha Mormoni.

Mafunuo na matukio yaliyoandikwa katika Mafundisho na Maagano yanatoa funguo, ibada, na maagano muhimu kwa ajili ya wokovu na kuinuliwa. Yanaanzisha si tu mambo ya msingi yaliyohitajika ili kuanzisha Kanisa lakini pia yanatoa mafundisho ya kina ambayo yanawezesha kuelewa madhumuni ya maisha na kutupa mtazamo wa milele.

Mojawapo ya mifano mingi ya kazi ya kinabii ya Joseph Smith inayopatikana katika sehemu ya 76 ya Mafundisho na Maagano. Ni kumbukumbu dhahiri ya ono kuhusu mbinguni, ikijumuisha falme za utukufu, ambazo Nabii Joseph na Sidney Rigdon walibarikiwa kulipokea mnamo Februari 16, 1832. Wakati huo, makanisa mengi sana yalikuwa yanafundisha kwamba Upatanisho wa Mwokozi usingetoa wokovu kwa sehemu kubwa ya watu. Ilikuwa inaaminika kwamba ni wachache wangeokolewa, na wengi wangeangamia katika jehanamu na kulaaniwa, ikijumuisha mateso yasiyo na mwisho ya ukali wa kuogofya na usioelezeka.7

Ufunuo uliopo katika sehemu ya 76 hutoa ono tukufu la daraja za utukufu pale wengi wa watoto wa Baba wa Mbinguni ambao walikuwa jasiri katika hali zao za kabla kuzaliwa wanabarikiwa sana baada ya hukumu ya mwisho.8 Ono la daraja tatu za utukufu, la chini kuliko yote “lipitayo akili zote,”9 ni ukanushaji wa moja kwa moja wa mafundisho ya nguvu ya wakati huo lakini yaliyo na makosa kwamba wengi wangeangamia katika jehanamu na kulaaniwa.

Unapotambua kwamba Joseph Smith alikuwa na miaka 26 tu, akiwa na elimu ndogo, na akiwa na ufahamu mdogo au bila ufahamu kabisa wa lugha za ufasihi ambazo kwazo Bibilia ilitafsiriwa, yeye kwa kweli alikuwa chombo katika mikono ya Bwana. Katika mstari wa 17 wa sehemu ya 76, yeye alipata mwongozo wa kutumia neno wasio haki badala ya hukumu lililotumiwa katika Injili ya Yohana.10

Inashangaza kwamba miaka 45 baadaye kiongozi wa kanisa Muangilikana na mwanazuoni wa elimu mwenye sifa,11 Frederic W. Farrar, ambaye aliandika The Life of Christ,12 alidai kwamba maelezo ya hukumu katika Toleo la King James la Biblia ilikuwa matokeo ya makosa ya tafsiri kutoka Kiebrania na Kigiriki kwenda Kiingereza.13

Katika siku yetu wengi wamekubali dhana kwamba hakuna matokeo yajayo kutokana na dhambi. Wanaunga mkono kusamehe dhambi bila toba. Mafundisho yetu yaliyofunuliwa sio tu yanakanusha wazo kwamba watu wengi wangehukumiwa milele kwenda jehanamu na kulaaniwa lakini pia huthibitisha kwamba toba binafsi ni sharti lililoamriwa la kupokea Upatanisho wa Mwokozi na kuurithi ufalme wa selestia.14 Nashuhudia kwamba Joseph Smith alikuwa ni chombo katika mikono ya Mungu kuleta Urejesho wa injili Yake!

Kwa sababu ya Urejesho wa injili ya Yesu Kristo, tunaelewa umuhimu wa yote, toba na “kazi za haki.”15 Tunaelewa umuhimu zaidi wa Upatanisho wa Mwokozi na ibada na maagano Yake ya kuokoa, ikijumuisha zile zinazofanywa hekaluni.

“Kazi za haki” zinatokana na ni matunda ya uongofu. Uongofu wa kweli huletwa na dhamira ya kukubali na sharti la kufuata mapenzi ya Mungu.16 Shada la matokeo na baraka ambazo hutiririka kutoka kwenye uongofu ni amani ya kweli na ya kudumu na hakikisho binafsi la furaha ya mwisho17—licha ya dhoruba za maisha haya.

Uongofu kwa Mwokozi humbadilisha mtu wa kawaida kuwa mtu aliyetakaswa, aliyezaliwa tena, kusafishwa—kiumbe kipya katika Kristo Yesu.18

Wengi Wametengwa kutoka kwenye Ukweli kwa Sababu Hawajui pa Kuupata

Je, ni majukumu gani huja kutokana na uongufu? Katika Jela ya Liberty, Nabii Joseph alisema kwamba wengi “wametengwa kutoka kwenye ukweli kwa sababu hawajui pa kuupata.”19

Utangulizi wa Bwana wa Mafundisho na Maagano, taswira kuu ya tamko la madhumuni ya Bwana kwetu sisi yalianzishwa. Yeye alitamka “Hivyo basi, Mimi Bwana, nikijua majanga yajayo juu ya wakazi wa dunia, nimemwita mtumishi wangu Joseph Smith, Mdogo, na kusema naye kutoka mbinguni, na nikampa yeye amri.” Yeye akatoa maelezo zaidi “Kwamba utimilifu wa injili yangu uweze kutangazwa na watu walio dhaifu na wa kawaida hata mwisho wa dunia.”20 Hiyo hujumuisha wamisionari. Hiyo hujumuisha kila mmoja wetu. Hii inapaswa kuwa fokasi ya leza kwa kila mmoja ambaye amebarikiwa na uongofu kwenye mapenzi ya Mungu. Yesu Kristo anatualika tuwe sauti Yake na mikono Yake.21 Upendo wa Mwokozi utakuwa nuru yetu ya kuongoza. Mwokozi aliwafundisha wanafunzi Wake, “Enendeni, na mfundishe mataifa yote.”22 Na kwa Joseph Smith, Yeye alitamka, “kuihubiri injili yangu kwa kila kiumbe ambacho bado hakijaipokea.”23

Wiki moja baada ya kuwekwa wakfu Hekalu la Kirtland mnamo Aprili 3, 1836, ambayo ilikuwa Jumapili na pia Pasaka, Bwana alitokea katika ono kuu kwa Joseph na Oliver Cowdery. Bwana alilikubali hekalu na kutangaza, “Huu ni mwanzo wa baraka ambazo zitamwagwa juu ya vichwa vya watu wangu.”24

Baada ya hili ono kufungwa, Musa alitokea “na kutukabidhi … funguo za kukusanywa kwa Israeli kutoka pande nne za dunia, na kuongozwa kwa makabila kumi kutoka nchi ya kaskazini.”25

Rais Russell M. Nelson, nabii wetu mpendwa leo ambaye anashikilia funguo zile zile, aliwafundisha asubuhi: “Ninyi wavulana mmehifadhiwa kwa ajili ya wakati huu ambapo ahadi ya kukusanywa kwa Israeli inafanyika. Mnapotumikia misheni, mnashiriki katika jukumu muhimu katika tukio hili ambalo halijawahi tokea!26

Ili agizo la Mwokozi la kushiriki injili kuwa sehemu ya sisi, tunahitaji kuwa waongofu kwenye mapenzi ya Mungu; tunahitaji kuwapenda majirani zetu, kushiriki injili iliyorejeshwa ya Yesu Kristo, na kuwaalika wote waje na kuona. Kama waumini wa Kanisa, tunaenzi jibu la Nabii Joseph kwa John Wentworth, mhariri wa Chicago Democrat, mnamo 1842. Alikuwa akiomba habari kuhusu Kanisa. Joseph alihitimisha jibu lake kwa kutumia “Kiwango cha Ukweli” kama utangulizi wa Makala ya Imani ya kumi na tatu. Kiwango hiki kinaelezea, kwa njia ya muhtasari, kile ambacho hatuna budi kukitimiza.

“Hakuna mkono usio wekwa wakfu unaweza kusimamisha kazi isiendelee; mateso yanaweza kuja, makundi maovu yanaweza kuungana, majeshi yanaweza kukusanyika, uzushi unaweza kukashifu, lakini ukweli wa Mungu utaendelea kwa ujasiri, kwa uadilifu, na kwa uhuru, mpaka upenye kila bara, ufike kwenye kila tabia ya nchi, ufikie kila nchi na kusikika katika kila sikio; mpaka makusudi ya Mungu yatatimizwa, na Yehova Mkuu atasema kazi imekamilika.”27

Hii imekuwa kauli mbiu kwa vizazi vya Watakatifu wa Siku za Mwisho, hasa wamisionari. Katika roho ya Kiwango cha Ukweli, tuna shukrani kwamba miongoni mwa janga la ulimwengu kote wamisionari waaminifu wameshiriki injili. Wamisionari, tunawapenda! Bwana anamuamuru kila mmoja wetu kushiriki injili Yake katika neno na tendo. Uongofu wetu binafsi hujumuisha jukumu la kushiriki injili ya Yesu Kristo kwa ulimwengu.

Baraka za kushiriki injili zinajumuisha kuongeza uongofu wetu kwenye mapenzi ya Mungu na kumuacha Mungu ashinde katika maisha yetu.28 Tunawabariki wengine kupata “badiliko kuu” la moyo.”29 Kuna shangwe ya kweli ya milele katika kusaidia kuleta nafsi kwa Kristo.30 Kufanyia kazi uongofu wa mtu binafsi na wengine ni kazi ya uadilifu.31 Ninashuhudia hivyo katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. Nilitumikia katika Misheni huko Uingereza kutoka Septemba 1, 1960, hadi Septemba 1, 1962.

  2. Wavulana wengine ilibidi waewepo ili wasajiliwe jeshini.

  3. Baada ya kurudi kutoka misheni yake, alihitimu shule ya utabibu na kuhudumu kama daktari mashuhuri. Misheni yake ilimuandaa yeye kuwa askofu, rais wa kigingi, mwakilishi wa eneo, na rais wa misheni.

  4. Ona Moroni 10:4. Tayari nilikuwa nimesoma Kitabu cha Mormoni. Kwa uzito wa jambo hili katika familia yetu, nilikuwa ninasali kwa nia ya dhati.

  5. Ona Saints: The Story of the Church of Jesus Christ in the Latter Days, vol. 1, The Standard of Truth, 1815–1846 (2018), na vol. 2, No Unhallowed Hand, 1846–1893 (2020).

  6. Tafsiri ilianza Aprili 7, 1829, na ilimalizika karibia mwanzo wa Julai 1829. Imekuwa ajabu kujifunza kweli zihusuzo tafsiri. Mimi hasa ninathamini kusoma mswada wa mpiga chapa na mswaada wa asili wa Kitabu cha Mormoni uliochapishwa kama juzuu ya 3 na ya 5 katika mfululizo wa Revelations and Translations wa The Joseph Smith Papers. Zote ni juzuu maharufu.

  7. Frederic W. Farrar, Eternal Hope: Five Sermons Preached in Westminster Abbey, November, and December 1877 (1892), xxii.

  8. Ono linajumuisha wale ambao hawakujua kuhusu Kristo katika maisha haya, watoto ambao hufa kabla ya umri wa kuwajibika, na wale ambao hawana uelewa.

  9. Mafundisho na Maagano 76:89.

  10. Ona Yohana 5:29.

  11. Farrar alipata elimu kutoka King’s College, London, na Trinity College, Cambridge. Alikuwa kasisi wa Church of England (Anglikana), Kasisi mkuu wa Westminister Abbey, Paroko wa Canterbury Cathedral, na Kasisi wa Royal Household.

  12. Ona Frederic W. Farrar, The Life of Christ (1874).

  13. Ona Farrar, Eternal Hope, xxxvi–xxxvii. Frederic Farrar alihisi kulazimika kurekebisha mafundishokuhusu hukumu na jehanamu. Kwa nguvu alitangaza kile alichokiita “mambo rahisi, yasiyo weza kataliwa, na kukanushwa. … Kitenzi ‘kuhukumu’ na mizizi yake haitokea hata mara moja katika Agano la Kale. Hakuna neno linaloleta maana yoyote kama hiyo katika Kigiriki cha Agano Jipya. Anaendelea kueleza kwamba neno hukumu ni “kosa kubwa la tafsiri … [na] linapotosha na kuficha maana halisi ya usemi wa Bwana wetu” (Eternal Hope, xxxvii). Farrar pia alitaja kwamba onyesho la kuzidi la upendo wa Baba aliye Mbinguni kote katika Biblia kama ushahidi wa ziada kwamba maelezo ya jehanamu na hukumu yaliyotumiwa katika tafsiri ya Kiingereza ni makosa (ona Eternal Hope, xiv–xv, xxxiv, 93; ona pia Quentin L. Cook, “Our Father’s Plan—Big Enough for All His Children,” Liahona, May 2009, 36).

  14. Uhusiano kati ya toba na Upatanisho unawekwa wazi katika Mafundisho na Maagano 19:15–18, 20. Kama nyongeza, adhabu isiyo na mwisho imefafanuliwa katika Mafundisho na Maagano 19:10–12.

  15. Mafundisho na Maagano 59:23.

  16. Ona Mosia 27:25; Mafundisho na Maagano 112:13; ona pia Dale E. Miller, “Bringing Peace and Healing to Your Soul,” Liahona, Nov. 2004.

  17. Ona Mosia 2:41.

  18. Ona Dallin H. Oaks, “The Challenge to Become,” Ensign, Nov. 2000, 33; Liahona, Jan. 2001, 41; ona pia 2 Wakorintho 5:17; Kamusi ya Biblia, “Uongofu.”

  19. Mafundisho na Maagano 123:12.

  20. Mafundisho na Maagano 1:17, 23.

  21. Kama ni hamu yetu, sisi “tunaitwa kwenye kazi” (Mafundisho na Maagano 4:3; ona pia Thomas S. Monson, “Kuitwa katika Kazi,” Liahona, Juni 2017, 4–5).

  22. Mathayo 28:19

  23. Mafundisho na Maagano 112:28.

  24. Mafundisho na Maagano 110:10.

  25. Mafundisho na Maagano 110:11.

  26. Ona Russell M. Nelson, “Kuhubiri Injili ya Amani,” Liahona, Mei 2022, 6–7; ona pia Russell M. Nelson, “Hope of Israel” (worldwide youth devotional, June 3, 2018), HopeofIsrael.ChurchofJesusChrist.org.

  27. Teachings of Presidents of the Church: Joseph Smith (2007), 444.

  28. Ona Russell M. Nelson, “Acha Mungu Ashinde,” Liahona, Nov. 2020, 92–95.

  29. Alma 5:14.

  30. Ona Madundisho na Maagano 18:15; ona pia Yakobo 5:19–20.

  31. Ona Alma 26:22; Mafundisho na Maagano 18:13–16; ona pia Kamusi ya Biblia, “Uongofu.”