Mkutano Mkuu
Uanafunzi wa Ujasiri katika Siku za Mwisho
Mkutano mkuu wa Aprili 2022


Uanafunzi wa Ujasiri katika Siku za Mwisho

Acha tuwe wa kujiamini, wala si watetezi, wala wepesi wa kutishwa, wala si waoga tunaposhikilia nuru ya Bwana katika hizi siku za mwisho.

Maadili ya haki ya kujiamulia ni kipawa cha thamani cha Mungu kwa kila mmoja wa watoto Wake.1 Sisi “tuko huru kuchagua uhuru na uzima wa milele, kupitia yule Mpatanishi mkuu wa wanadamu wote, au kuchagua utumwa na kifo, kulingana na utumwa na nguvu za ibilisi.”2 Mungu hatatulazimisha kutenda mema, na ibilisi hatatulazimisha kutenda maovu.3 Ingawa wengine wanaweza kufikiria kwamba maisha ya duniani ni mashindano kati ya Mungu na adui, neno kutoka kwa Mwokozi “na Shetani amenyamazishwa na kufukuzwa. … Ni nguvu [zetu] ambazo zinapimwa—wala si Mungu.”4

Mwisho wa siku sisi ndio tunaovuna kile ambacho chaguzi zetu za maisha yote tulikipanda.5 Kwani jumla ya mawazo yetu, hamu, maneno, na kazi zetu vinasema nini kuhusu upendo wetu kwa Mwokozi, kwa watumishi Wake wateule, na kwa Kanisa Lake lililorejeshwa? Je, ubatizo wetu, ukuhani, na maagano yetu ya hekaluni yana maana zaidi kwetu kuliko sifa za ulimwengu au idadi ya “likes” kwenye mtandao wa kijamii? Je, upendo wetu kwa Bwana na amri Zake vina nguvu zaidi kuliko upendo wetu kwa ajili ya kitu cho chote au mtu ye yote katika maisha haya?

Adui na wafuasi wake daima wametafuta kuangamiza kazi za Kristo na manabii Wake. Amri za Mwokozi, kama hazijapuuzwa kabisa, zimeraziniwa kuwa bure na wengi katika ulimwengu wa leo. Wajumbe wa Mungu ambao wanafundisha kweli “sumbufu” mara nyingi wamepuuzwa. Hata Mwokozi Mwenyewe aliitwa “Mlafi huyu, na mlevi,”6 akatuhumiwa kuvuruga mawazo ya umma na kuwa mtu wa kutenganisha. Nafsi dhaifu na zenye kula njama “wakafanya shauri, jinsi ya kumtega kwa maneno,”7 na “dhehebu” Lake la Wakristo wa kale “walikuwa kila mahali … walinenwa dhidi yao.”8

Mwokozi na wafuasi Wake wa mwanzoni walikabiliana na upinzani mkali wa ndani na nje, nasi tunapitia hali kama hiyo. Leo ni vigumu kabisa kuishi imani yetu kwa ujasiri bila mara kwa mara kusababisha vidole vichache halisi na vya kufikirika vya dharau kutoka kwa walimwengu. Kumfuata Mwokozi kwa kujiamini kuna lipa, lakini wakati mwingine tunaweza kujikuta katika kupingana na wale wanaotetea falsafa ya “ule, unywe, ufurahi,”9 pale imani katika Kristo, utiifu, na toba vinapobadilishwa na dhana kwamba Mungu atahalalisha dhambi ndogo kwa sababu Yeye anatupenda sana.

Akisema “kwa sauti [Yake] mwenyewe au kwa sauti ya watumishi [Wake],”10 kwani Mwokozi hakusema kuhusu siku yetu kwamba “utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao wenyewe watajipatia waalimu” na kwamba wengi “watajiepusha wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo”?11 Yeye hakuomboleza kwamba “nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu”?12 Yeye hakuonya kwamba “katika ninyi wenyewe watainuka watu wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao,”13 Yeye hakutabiri kwamba “uovu [ungeitwa] wema, na kwamba wema ni uovu,”14 na kwamba “na adui za mtu ni wale wa nyumbani mwake”?15

Kwa hiyo kuhusu sisi je? Je, yatupasa tutishike au kuogopa? Je, yatupasa tuishi dini yetu kwa kina cha nyambizi? Kwa hakika sivyo! Kwa imani katika Kristo, hatuna haja ya kuogopa lawama za wanadamu au kuogopa shutuma zao.16 Na Mwokozi akiwa kwenye usukani na manabii hai wakituelekeza na kutuongoza, “ni nani aliye juu yetu?”17 Acha tuwe wenye kujiamini, wala si watetezi, majasiri wala si wepesi wa kutishwa, waaminifu wala si waoga tunaposhikilia nuru ya Bwana katika hizi siku za mwisho.18

Mwokozi aliweka hili wazi kwamba “basi, kila mtu atakayenikiri mbele ya watu, nami nitamkiri mbele za Baba yangu. … Bali mtu ye yote atakayenikana mbele ya watu, nami nitamkana mbele za Baba yangu.”19

Kama matokeo yake, hali wengine wangependa Mungu ambaye huwa hana amri, acha kwa ushupavu tushuhudie katika maneno ya Mzee D. Todd Christofferson kwamba “Mungu ambaye hatoi masharti ni kisawe cha nadharia ya Mungu ambaye hayupo.”20

Hali wengine wangependa kuwa wachaguzi katika amri watakazofuata, acha kwa shangwe tukubali mwaliko wa Mwokozi wa “kuishi kwa kila neno litokalo kinywani mwa Mungu.”21

Hali wengine wanaamini Bwana na Kanisa Lake wanakubali “fanya cho chote ambacho moyo wako unapenda,”22 acheni kwa ushupavu tutangaze kwamba ni makosa “kuandamana na makutano ili kutenda uovu,”23 kwa sababu “umati hauwezi kufanya kitu kuwa sahihi kile ambacho Mungu ametangaza kuwa ni kosa.”24

“Ee kumbuka, kumbuka … vile amri za Mungu ni kali [bado zinaokoa].”25 Kuwafundisha wao ni wazi wakati mwingine kunaweza kuonekana kama tendo la kutovumilika. Acha kwa hivyo kwa heshima tuonyeshe kwamba sio tu inawezekana bali ni muhimu kumpenda mtoto wa Mungu ambaye anakumbatia imani zilizo tofauti na zetu.

Tunaweza kuwakubali na kuwaheshimu wengine bila kuunga mkono imani yao au vitendo vyao ambavyo haviwiani na mapenzi ya Mungu. Hakuna haja ya kutoa dhabihu ukweli kwenye madhabahu ya makubaliano na upendeleo wa kijamii.

Sayuni na Babeli hazipatani. “Hakuna mtu ambaye anaweza kutumikia mabwana wawili.”26 Acha sote tukumbuke swali lenye kuchoma la Mwokozi, “Na kwa nini mnaniita, Bwana, Bwana, walakini hamyatendi nisemayo?”27

Tunadhihirisha upendo wetu kwa Bwana kupitia utiifu kwa moyo mkunjufu, kwa hiari.

Kama utahisi kubanwa kati uanafunzi wako na ulimwengu, tafadhali kumbuka kwamba Mwokozi wako mwenye upendo “huwatumia mwaliko … , kwani mikono ya huruma imenyoshwa kwao, na anasema: Tubuni, na nitawapokea.”28

Rais Russell M. Nelson alifundisha kwamba “Yesu Kristo, atafanya baadhi ya kazi Zake kubwa kati ya sasa na wakati atakapokuja tena.”29 Lakini pia alifundisha kwamba “wale wanaochagua njia ya Bwana kuna uwezekano wa kustahimili mateso.”30 “Wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya jina lake”31 wanaweza wakati mwingine kuwa wetu tunapo “ruhusu sauti Yake kuchukua kipaumbele juu ya kingine cho chote.”32

“Naye heri,” Mwokozi alisema, “awaye yote asiye chukizwa nami.”33 Mahali pengine tunajifunza kwamba “amani nyingi waipendao sheria yako: Wala hawana la kuwakwaza.”34 Hawana! Kwa hiyo acha tujiulize, “Mimi hudumu kwa muda; ikitukia dhiki au udhia kwa ajili ya lile neno, mara huchukizwa?35 Je, nimejengwa kwa uthabiti juu ya mwamba wa Yesu Kristo na watumishi Wake?

Wenye imani kwamba maadili ni mambo ya mpito wanatetea kwamba ukweli ni dhana tu ya kijamii, kwamba hakuna masharti wala mipaka ya maadili. Kile wanachosema kweli ni kwamba hakuna dhambi,36 kwamba “cho chote mtu alichofanya sio kosa,”37 falsafa ambayo kwayo adui anadai utunzi mashuhuri! Acha sisi kwa hivyo tujihadhari na mbwa-mwitu waliovaa mavazi ya kondoo ambao daima wanawasajili na “kila mara wanatumia vizuizi vya akili ili kuficha upotovu wao [wenyewe] wa tabia.”38

Ikiwa tunataka kweli kuwa wanafunzi jasiri wa Kristo, tutapata njia. Vinginevyo, adui anatoa mbadala wa kuvutia. Lakini kama wanafunzi waaminifu, “hatuhitaji kuomba msamaha kwa ajili ya imani yetu wala kurudi nyuma kutokana na kile tunachojua kuwa ni cha kweli.”39

Katika hitimisho, neno kuhusu watumishi 15 wa Mungu walioketi nyuma yangu. Wakati walimwengu “wawaambiao waonaji, Msione; na kwa manabii, Msitoe unabii,”40 waaminifu “watavikwa taji la baraka kutoka juu, ndiyo, na amri zisizo haba, na pamoja na mafunuo katika wakati wao.”41

Haishangazi, watu hawa kila mara wanakuwa fimbo umeme kwa wale wasiofurahia neno la Mungu manabii wanapolitangaza. Wale waliowakataa manabii hawatambui kwamba “hakuna unabii katika maandiko [upatao] kufasiriwa kama apendavyo mtu fulani tu,” au matokeo ya mapenzi ya mwanadamu, “bali [kwamba] wanadamu walinena yaliyotoka kwa Mungu, wakiongozwa na Roho Mtakatifu.”42

Kama Paulo, hawa watu wa Mungu “hawauonei haya ushuhuda wa Bwana wetu” nao ni “ [wafungwa]” Wake43 katika hali ambayo mafundisho wanayofundisha si yao bali ni Yake ambaye aliyewaita. Kama Petro, wao “hawawezi kuacha kuyanena mambo [wao] waliyoyaona na kuyasikia.”44 Nashuhudia kwamba Urais wa Kwanza na Akidi ya Mitume Kumi na Wawili ni watu wazuri na waaminifu ambao wanampenda Mungu na watoto Wake na ambao wanapendwa Naye. Maneno yao tunapaswa kuyapokea kama vile yanatoka kinywani mwa Bwana mwenyewe, “katika uvumilivu wote na imani yote. Kwani kwa kufanya mambo haya milango ya jehanamu haitatushinda [sisi] … na Bwana Mungu atazitawanya nguvu za giza kutoka mbele [yetu].”45

“Hakuna mkono usio mtakatifu unaoweza kusitisha kazi kusonga mbele”;46 itasonga mbele kwa ushindi tukiwemo au tusipokuwemo kwa hiyo “chagueni hivi leo mtakayemtumikia.”47 Usipumbazwe au kutishwa na kelele kubwa za adui zinazotoka kwenye lile jumba kubwa na pana. Sauti zao za kukata tamaa haiwezi kulinganishwa na ushawishi mpole wa ile sauti tulivu, ndogo juu ya mioyo iliyovunjka na roho zilizopondeka.

Nashuhudia kwamba Kristo yu hai, kwamba Yeye ni Mwokozi wetu na Mkombozi wetu, na kwamba Yeye huongoza Kanisa Lake kupitia Urais wa Kwanza na wale Mitume Kumi na Wawili, hivyo akihakikisha kwamba sisi “hatutatupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu.“48

“Wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo” Rais Nelson alifundisha, “wako tayari kujitokeza, kusema kwa ukakamavu, na kuwa tofauti na watu wa ulimwengu. Hawana woga, wamejitolea na ni wajasiri.”49

Akina kaka na akina dada, ni siku nzuri ya kuwa wazuri! Katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.