Mkutano Mkuu
Usiwe na Hofu: Amini Tu!
Mkutano mkuu wa Aprili 2022


Usiwe na Hofu: Amini Tu!

Anza kutafuta furaha yako kwa kukumbatia wingi ambao tumekwishapokea kutoka kwa mtoaji wa kila kilicho chema.

Ninaelekeza maneno yangu leo kwa watu wenye umri mdogo Kanisani, nikimaanisha kila mmoja rika la Rais Nelson au mdogo wa hapo. Mara chache natumia vielelezo, lakini siwezi kuacha kushiriki hili.

Picha
Barua kutoka kwa Marin Arnold

Ombi hili maalum linatoka kwa rafiki yangu wa miaka nane Marin Arnold, lililoandikwa wakati akiwa na miaka saba. Nitawatafsiria lugha yake ya Kimisri kilichofanywa upya:

Mpendwa Askofu

a kutano mkuu

haukuwa Mzuri kwa nini

Kwani a zima

Kushiriki? Nambie kwa nini

A dhati, Marin

Arnold.”1

Marin, ujumbe ambao niko karibu kuutoa bila shaka utakuvunja moyo tena. Lakini unapomwandikia askofu wako kulalamika, ni muhimu umwambie kwamba jina langu ni “Kearon. Mzee Patrick Kearon.”

Takribani kwa miaka miwili janga la uwiano wa kibiblia limefunika sayari yetu, na wakati janga hili limefanya takribani kila kitu cha kijamii kusimama, bila shaka, halikufanya ukatili, unyanyasaji na ukali kisiasa—ndani ya taifa au kimataifa kusimama. Kama hayo hayakuwa ya kutosha, bado tunakabiliwa na changamoto nyingi za kijamii na kimila, zinazoanzia kwenye ugumu wa kiuchumi mpaka kwenye uharibifu wa mazingira, ubaguzi wa rangi na zaidi.

Hali ngumu na siku za giza kama hizo zinaweza kuwa za kukatisha tamaa kwa vijana miongoni mwetu, wale tunaowatarajia kwa ajili ya mafanikio na furaha kuhusu kesho yetu. Imesemwa kwamba “nguvu ya vijana ni nyenzo ya thamani kwa ulimwengu mzima. Hawa … vijana … ni nyuso za … kesho yetu.”2 Zaidi, watoto wetu ni washirika ambao katika mikono yao hatima ya Kanisa hili itawekwa.

Kwa hali zetu za sasa, ni ya kueleweka kama mtazamo wa wadogo hawa unapungua kidogo. Dk. Laurie Santos, profesa wa Chuo Kikuu cha Yale, hivi karibuni aliandaa darasa lenye jina Saikolojia na Maisha Mazuri. “Mwaka wa kwanza wa darasa hili, takribani [robo] ya wanafunzi [wote] wa shahada ya kwanza walijiandikisha.”3 Zaidi ya watu milioni 64 walitembelea ukurasa wake wa intanenti. Akiandika kuhusu tukio hili, mwandishi mmoja wa habari alisimulia jinsi inavyouma kuona wanafunzi wengi vijana, wenye akili—na watu wazima—pasipo matumaini “wakitafuta kitu walichokipoteza” au, mbaya zaidi, wakitamani kitu ambacho hawajawahi kuwa nacho.4

Ombi langu kwa vijana, nanyi wazazi na watu wazima mnaowashauri, ni kuanza kutafuta furaha yenu kwa kukumbatia wingi ambao tumekwishapokea kutoka kwa mtoaji wa kila kilicho chema.5 Kwa wakati muafaka wengi ulimwenguni wanauliza maswali ya dhati ya nafsi, tunapaswa kuyajibu kwa “habari njema”6 ya injili ya Yesu Kristo. Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho, ambalo huiinua misheni na ujumbe wa Mwokozi wa ulimwengu, linatoa njia ya msingi ya milele katika kutafuta mema na kutenda mema katika muda kama huo wa mahitaji.

Rais Russell M. Nelson amesema kwamba kizazi hiki cha vijana kina uwezo wa kuwa na “matokeo zaidi [ya mema] ulimwenguni kuliko kizazi kingine kilichopita.”7 Sisi, kati ya watu wote, tunapaswa “kuimba wimbo wa upendo wa ukombozi,”8 lakini hiyo inahitaji nidhamu—“ufuasi,” kama utapenda iwe hivyo—upendo unaotulinda dhidi ya mitazamo hasi na tabia haribifu ambazo hutuondoa kwenye mapigo ya wimbo tunapojaribu kuuimba wimbo huo wa wokovu wa milele.

Hata kama tuna “hali nzuri,”9 tunaweza kumfikia yule mmoja mara kwa mara ambaye amedhamiria kutafuta kitu kitupu na kisicho thamani kwenye kila kitu. Mnajua kauli mbiu yake: “huwa kiza siku zote kabla tu ya kuwa kiza kinene.” Ni mtazamo mbaya ulioje na mwisho wa kutisha! Ndio, wakati mwingine tunataka kupakimbia pale tulipo, lakini hatupaswi kuukimbia utambulisho wetu—watoto wa Mungu aliye hai anayetupenda, ambaye daima yu tayari kutusamehe, na kamwe, kamwe hatatuacha. Wewe ni mtoto Wake wa thamani. Wewe ni mtoto Wake, ambaye amekupatia manabii na ahadi, vipawa vya kiroho na ufunuo, miujiza na jumbe na malaika katika pande zote mbili za pazia.10

Pia amekupatia Kanisa linaloimarisha familia kwa kipindi chote cha maisha na kuyaunganisha milele zote. Lina zaidi ya kata 31,000 na matawi ambako watu hukutana na huimba na hufunga na kusali kwa ajili ya kila mmoja na kutoa walichonacho kwa masikini. Hapa ndiko kila mmoja hupewa jina, hutambuliwa na uhudumiwa na ambako marafiki na majirani wa kawaida kwa kujitolea hutumikiana katika miito ambayo ni kati ya ile ya kikarani mpaka ile ya usimamizi. Vijana watuwazima—pamoja na wanandoa wazee kwa maelfu wanatumikia misheni kwa gharama zao wenyewe bila kujali wapi watapelekwa kutumikia, na waumini wadogo kwa wakubwa hufika hekaluni kufanya ibada takatifu zinazohitajika kuunganisha familia ya mwanadamu pamoja—shughuli shupavu katika ulimwengu uliogawanyika lakini yenye kutangaza kwamba mgawanyiko huo ni wa muda tu. Hizi ni baadhi ya sababu chache tunazozitoa kwa ajili ya “tumaini lililo ndani [yetu].”11

Ni kweli, katika siku zetu za leo, mambo mengi magumu yatamkabili mfuasi yeyote wa Yesu Kristo. Viongozi wa Kanisa hili hujitolea maisha yao ili kutafuta mwongozo wa Bwana katika kutatua changamoto hizi. Kama baadhi hayawezekani kutatulika kumridhisha kila mmoja, basi huenda yamejumuisha sehemu ya msalaba Yesu aliousema itatupasa kuubeba ili kumfuata Yeye.12 Ni dhahiri kwa sababu kutakuwa na siku za giza na mambo magumu ambayo Mungu aliahidi kwamba, kutoka katika wingu la mchana na mwale wa moto usiku, atawaongoza manabii, kutoa fimbo ya chuma, kufungua lango jembamba linaloelekea kwenye njia iliyonyooka, na zaidi ya yote kutujalia nguvu ya kuumaliza mwendo.13

Kwa hiyo tafadhali, tafadhali, bakia mpaka mwisho wa karamu hata kama huna uhakika na chakula chenyewe. Tegemea nuru Yake na weka mshumaa wako kwenye shughuli hii.14 Wimbo huu wa Msingi unaimbwa vizuri: Yesu kwa dhati “[anakuhitaji wewe] kuwa mwale wa nuru.”15

Wakati Yairo kiongozi wa Kiyahudi alipomwomba Yesu kumponya binti yake wa miaka 12, aliyekuwa akikaribia kufariki nyumbani kwake, umati uliozunguka ulimsubiri Mwokozi kwa muda mrefu kiasi kwamba mtumishi wa Yairo alikuja na kumwambia baba huyu mwenye hofu “Binti yako amekwisha kufa; usimsumbue mwalimu.”

“Lakini Yesu aliposikia hayo, alimjibu, Usiwe na hofu, amini tu, naye ataponywa.”16

Na aliponywa. Itakuwa vivyo hivyo kwako pia. “Usiwe na hofu: amini tu.”

Kwa sababu kila mmoja katika umati huu ni wa thamani kwa Mungu na Kanisa hili, ninahitimisha na tangazo hili maalum la kitume. Kabla hujapokea kipawa cha Roho Mtakatifu, ulikuwa na nuru ya Kristo ndani ya nafsi yako,17 hiyo “nuru iliyo ndani ya vitu vyote, … hutoa uhai kwa vitu vyote,”18 na ni chanzo cha mema katika mioyo ya watu wote ambao wamewahi kuishi na watakaoishi. Nuru hiyo ilitolewa kukulinda na kukufundisha. Moja ya jumbe zake kuu ni kwamba maisha ni ya thamani zaidi kuliko zawadi zote, zawadi ambayo hupatikana katika milele pekee kupitia Upatanisho wa Bwana Yesu kristo. Kama Nuru na Uhai wa ulimwengu,19 Mwana Pekee wa Mungu alikuja kutupatia uhai kwa kukishinda kifo.

Lazima tujikite kikamilifu kwenye zawadi hiyo ya maisha na kujitoa kuwasaidia wale walio katika hatari ya kukatisha zawadi hii. Viongozi, washauri, marafiki, familia—tazameni ishara za huzuni, kukata tamaa au chochote kiashiriacho kujidhuru. Jitolee kusaidia. Sikiliza. Chukua hatua ya kuingilia kama inawezekana.

Kwa vijana wetu wowote huko waliko wanaopitia ugumu, bila kujali matatizo au magumu yako, kifo kwa kujiua kwa dhahiri sio suluhisho. Hakitapoza maumivu unayohisi au yale unayodhani umeyasabisha. Katika ulimwengu ambao kwa tabu unahitaji kila nuru unayoweza kuipata, tafadhali acha kupunguza nuru ya milele ambayo Mungu ameiweka nafsini mwako kabla ya ulimwengu huu kuwepo. Zungumza na mtu. Omba msaada. Tafadhali acha kuangamiza uhai ambao ilimgharimu Kristo kuutoa wa Kwake ili kuulinda. Unaweza kukabiliana na changamoto za maisha haya kwa sababu tutakusaidia kukabiliana nayo. Una nguvu sana kuliko unavyofikiria. Msaada unapatikana kutoka kwa wengine na hususan kutoka kwa Mungu. Wewe unapendwa na kuthaminiwa na unahitajika! Tunawahitaji! “Usiwe na hofu: amini tu.”

Mtu fulani aliyekumbana na hali ngumu kuliko zile ambazo wewe na mimi tutazipitia, aliwahi kusema: “Twende mbele [wapendwa marafiki zangu wadogo]. Ujasiri … na mbele, mbele kwenye ushindi! Acheni mioyo yenu ifurahi, na kuwa yenye furaha zaidi.”20 Tunayo mengi sana ya kufurahia. Tuna kila mmoja wetu na tunaye Mungu. Usitukatalie fursa ya kuwa nawe, ninasihi, katika jina takatifu la Bwana Yesu Kristo, Kiongozi wetu, amina.