Mkutano Mkuu
Furaha ya Juu Zaidi
Mkutano mkuu wa Aprili 2024


Furaha ya Juu Zaidi

Na sote tutafute na kupata furaha ya juu zaidi inayotokana na kuweka wakfu maisha yetu kwa Baba yetu wa Mbinguni na Mwanawe mpendwa.

Nimekuwa na baraka kubwa ya kuongea kwenye mkutano mkuu kwa miongo mitatu sasa. Kwa kipindi hicho, nimeulizwa maswali yahusianayo na jumbe hizi na wengi ulimwenguni kote. Hivi karibuni, swali moja mahsusi limekuwa likija. Huwa linaulizwa kama hivi: “Mzee Uchtdorf, nilisikiliza kwa makini hotuba yako ya mwisho, lakini [anatulia] … sikusikia chochote kuhusu masuala ya ndege?”

Ndio, baada ya leo, huenda nisisikie swali hilo kwa muda.

Kuhusu “Mawingu angavu Yaliyoachana”1

Ni vigumu kuamini ilikuwa miaka 120 iliyopita wakati Wilbur na Orville Wright walipoondoka na kuruka juu ya mchanga wa Kitty Hawk, Carolina ya Kaskazini. Safari nne fupi za ndege siku hiyo ya Desemba zilibadilisha ulimwengu na kufungua mlango wa moja ya uvumbuzi mkubwa zaidi katika historia ya dunia.

Kuruka ilikuwa hatari katika siku hizo za mwanzo. Kaka hao walilijua hili. Na hivyo ndivyo alivyojua baba yao, Milton. Kwa kweli, aliogopa sana kupoteza watoto wake wote wawili katika ajali ya kuruka hivyo walimwahidi kuwa hawataruka pamoja.

Na hawakuwahi kufanya hivyo—hadi siku moja waliporuhusiwa. Miaka saba baada ya siku hiyo ya kihistoria huko Kitty Hawk, Milton Wright hatimaye alitoa idhini yake na kutazama wakati Wilbur na Orville wakiruka pamoja kwa mara ya kwanza. Baada ya kutua, Orville alimshawishi baba yake kupaa kwa mara ya kwanza ili ajionee mwenyewe jinsi ilivyokuwa.

Ndege ilipokuwa ikipaa kutoka ardhini, Milton mwenye umri wa miaka 82 alishangaa kasi yake kwamba hofu yote ilimwacha. Orville alishangilia wakati baba yake akishangilia kwa furaha, “Juu zaidi, Orville, juu zaidi!”2

Huyu alikuwa mtu wa moyo wangu mwenyewe!

Labda sababu ya mimi kuzungumza juu ya anga mara kwa mara ni kwamba najua kitu ambacho akina Wrights walihisi. Mimi pia “nimeteleza katika maeneo ya Dunia na kuzichezea anga kwenye mabawa ya kicheko.”3

Safari ya kwanza ya ndege ya akina Wright, ambayo ilitokea miaka 37 tu kabla ya kuzaliwa kwangu, ilifungua milango ya safari, maajabu na furaha ya kweli katika maisha yangu.

Na bado, kama ilivyo furaha hiyo isiyo na kifani, kuna aina ya furaha hata ya juu zaidi. Leo, katika roho ya kilio cha furaha cha Milton Wright, “Juu zaidi, Orville, juu zaidi,” ningependa kuzungumza juu ya furaha hii ya juu zaidi—ambapo inatoka, jinsi inavyoingia mioyoni mwetu na jinsi tunavyoweza kupata uzoefu kwa kipimo kikubwa zaidi.

Kusudi Lote la Uwepo wa Binadamu

Inajulikana kwamba kila mtu anataka kuwa na furaha.4 Hata hivyo, ni muhimu pia kusema kwamba si kila mtu ana furaha. Cha kusikitisha, inaonekana kwamba, kwa watu wengi, furaha ni ngumu kupata.5

kwa nini? Kama furaha ni kitu pekee ambacho sisi wanadamu tunatamani zaidi, kwa nini hatufanikiwi kuipata? Ili kufafanua wimbo fulani wa country, labda tumekuwa tukitafuta furaha katika maeneo yote yasiyo sahihi.6

Ni Wapi Tunaweza Kupata Furaha?

Kabla ya kujadili jinsi ya kupata furaha, niruhusuni nikiri kwamba msongo wa mawazo na changamoto zingine ngumu za kiakili na kihisia ni za kweli, na jibu sio tu, “Jaribu kuwa na furaha zaidi.” Lengo langu leo si kupunguza au kupuuza matatizo ya afya ya akili. Ikiwa unakabiliwa na changamoto kama hizo, ninaomboleza pamoja nawe na kusimama kando yako. Kwa watu wengine, kupata furaha kunaweza kujumuisha kutafuta msaada kutoka kwa wataalamu wa afya ya akili ambao hujitolea maisha yao kufanya kazi yao ya matibabu. Tunapaswa kushukuru kwa msaada kama huo.

Maisha sio mlolongo usio na mwisho wa viwango vya juu vya kihisia. “Kwani lazima, kuwe na upinzani katika mambo yote.”7 Na kama Mungu Mwenyewe analia, kama maandiko yanavyothibitisha,8 basi bila shaka wewe na mimi tutalia pia. Kuhisi huzuni sio ishara ya kushindwa. Katika maisha haya, angalau, furaha na huzuni ni wenza wasiotenganishwa.9 Kama ninyi nyote, nimehisi sehemu yangu ya kukata tamaa, huzuni, masikitiko na majuto.

Hata hivyo, pia nimejionea mwenyewe mapambazuko ya utukufu ambayo hujaza nafsi kwa furaha kubwa sana kiasi kwamba haiwezi kuzuiwa. Nimegundua mwenyewe kwamba ujasiri huu wa amani unatokana na kumfuata Mwokozi na kutembea katika njia Yake.

Amani anayotupa siyo kama ile itolewayo na ulimwengu.10 “Ni amani bora zaidi. Ni ya juu zaidi na takatifu. Yesu alisema, “Mimi nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.”11

Injili ya Yesu Kristo kwa kweli ni “habari njema ya furaha kuu”!12 Ni ujumbe wa tumaini lisilo na kifani! Ni ujumbe wa nira ya kubeba na kuinua mzigo.13 Injili ya kukusanya nuru. Injili ya neema ya mbinguni, ufahamu wa juu, usalama wa milele na utukufu wa milele!

Furaha ndiyo lengo la mpango wa Mungu kwa ajili ya watoto Wake. Ndiyo sababu uliumbwa—“kwamba [uweze] kuwa na furaha”!14 Ulijengwa kwa ajili hii!

Baba yetu wa Mbinguni hajaificha njia ya furaha. Siyo siri. Inapatikana kwa wote!15

Imeahidiwa kwa wale wanaotembea njia ya ufuasi, kufuata mafundisho na mfano wa Mwokozi, kushika amri zake na kuheshimu maagano wanayofanya pamoja na Mungu. Ni ahadi ya ajabu jinsi gani!

Mungu Ana Kitu Zaidi Cha Kutoa

Sote tunajua watu wanaosema kwamba hawamhitaji Mungu kuwa na furaha, kwamba wana furaha ya kutosha bila dini.

Ninakiri na kuheshimu hisia hizi. Baba yetu mpendwa wa Mbinguni anataka watoto Wake wote wawe na furaha nyingi iwezekanavyo, kwa hivyo amejaza ulimwengu huu na raha za kupendeza, nzuri na za kuvutia, “ili kuridhisha jicho na … kufurahisha moyo.”16 Kwangu mimi, kurusha ndege kulileta furaha kubwa. Wengine huipata katika muziki, sanaa, jambo alipendalo au uoto wa asili.

Kwa kumualika kila mmoja kushiriki habari njema ya Mwokozi ya shangwe kuu, hatupunguzi kwa vyovyote vyanzo hivi vya furaha. Tunasema tu kwamba Mungu ana kitu cha zaidi cha kutupatia. Furaha ya juu na ya kina zaidi—furaha inayopita kitu chochote ambacho ulimwengu huu hutoa. Ni furaha inayovumilia kuvunjika moyo, hupenya kwenye huzuni na hupunguza upweke.

Furaha ya kidunia, kwa upande mwingine, haidumu. Haiwezi. Ni asili ya vitu vyote vya kidunia kuzeeka, kuoza, kuchakaa au kuchacha. Lakini furaha ya Mungu ni ya milele, kwa sababu Mungu ni wa milele. Yesu Kristo alikuja kutuinua kutoka kwenye vya muda na kubadilisha toka kwenye kuharibika kwenda kutoharibika. Ni Yeye tu ndiye mwenye nguvu hiyo na furaha Yake tu ndiyo ya kudumu.

Ikiwa unahisi kunaweza kuwa na furaha zaidi ya aina hii katika maisha yako, ninakualika uanze safari ya kumfuata Yesu Kristo na Njia Yake. Ni safari ya maisha yote—na zaidi. Tafadhali niruhusu nipendekeze hatua chache za mwanzo katika safari hii ya kustahili ya kugundua furaha safi.

Sogeeni karibu na Mungu17

Je, unakumbuka mwanamke katika Agano Jipya ambaye alivumilia ugonjwa wa kutokwa na damu kwa miaka 12?18 Alikuwa ametumia kila kitu alichokuwa nacho kwa madaktari, lakini mambo yalikuwa mabaya zaidi. Alikuwa amesikia habari za Yesu; Nguvu Yake ya kuponya ilikuwa inajulikana sana. Lakini je, angeweza kumponya? Na jinsi gani yeye angeweza kuwa karibu Naye? Ugonjwa wake ulimfanya kuwa “mchafu” kulingana na sheria ya Musa, na kwa hivyo alitakiwa kukaa mbali na wengine.19

Kumkaribia Yeye wazi wazi na kuomba aponywe ilikuwa ni kazi ngumu.

Bado, alifikiria, “Nikiyagusa mavazi yake tu, nitapona.”20

Hatimaye, imani yake ilishinda hofu yake. Alijipa moyo wa kukemea wengine na kushinikiza kwenda kwa Mwokozi.

Mwishowe, alikuwa ndani ya uwezo. Alinyoosha mkono wake.

Na aliponywa.

Je sisi sote hatufanani na mwanamke huyu?

Kunaweza kuwa na sababu nyingi za kwa nini tunasita kumkaribia Mwokozi. Tunaweza kukabiliwa na kejeli au lawama kutoka kwa wengine. Katika kiburi chetu, tunaweza kukataa uwezekano wa kitu rahisi sana kuwa cha thamani sana. Tunaweza kufikiri kwamba hali yetu kwa namna fulani inatuondolea kutoka kwa uponyaji Wake—kwamba umbali ni mkubwa sana au dhambi zetu ni nyingi sana.

Kama mwanamke huyu, nimejifunza kwamba ikiwa tunamkaribia Mungu na kumfikia ili kumgusa, hakika tunaweza kupata uponyaji, amani na furaha.

Itafute

Yesu alifundisha, “Tafuta, na utapata.”21

Ninaamini kifungu hiki rahisi sio tu ahadi ya kiroho; ni kauli ya ukweli.

Tukitafuta sababu za kuwa na hasira, kuwa na mashaka, kuwa na uchungu au peke yetu, tutazipata.

Hata hivyo, tukitafuta furaha—ikiwa tunatafuta sababu za kufurahi na kumfuata Mwokozi kwa furaha, tutazipata.

Ni nadra sana kupata kitu ambacho hatukitafuti.

Je, unatafuta furaha?

Tafuta, na utapata.

Kubebeana Mizigo22

Yesu alifundisha, “Ni heri kutoa kuliko kupokea.”23

Je, inaweza kuwa kwamba, katika kutafuta furaha, njia bora ya kupata ni kuleta furaha kwa wengine?

Akina kaka na akina dada, ninyi mwajua nami najua kuwa ni kweli! Furaha ni kama pipa la unga au mtungi wa mafuta ambao hautaisha kamwe.24 Furaha ya kweli huongezeka wakati inashirikishwa kwa wengine.

Haihitaji kitu kikubwa au kigumu.

Tunaweza kufanya vitu rahisi.

Kama vile kusali kwa ajili ya mtu kwa moyo wetu wote.

Kutoa pongezi ya dhati.

Kumsaidia mtu kuhisi kukaribishwa, kuheshimiwa, kuthaminiwa na kupendwa.

Kushiriki maandiko pendwa na kile inachomaanisha kwetu.

Au hata kwa kusikiliza tu.

“Mnapowatumikia wanadamu wenzenu mnamtumikia tu Mungu,”25 na Mungu atawalipa kwa wema wenu.26 Furaha mnayowapa wengine itawarudieni katika “kipimo cha kujaa, kushindiliwa, na kusukwa sukwa hata kumwagika.”27

“Hivyo Tunapaswa Kufanya Nini?”28

Katika siku zijazo, wiki na miezi, naomba nikualike kwenye:

  • Kutumia muda katika juhudi za dhati na za moyoni za kumkaribia Mungu.

  • Kutafuta kwa bidii kwa nyakati za kila siku za matumaini, amani na furaha.

  • Leta furaha kwa wengine wanaokuzunguka.

Wapendwa akina kaka na dada, wapendwa marafiki, unapotafiti neno la Mungu kwa ajili ya uelewa wa kina wa mpango wa milele wa Mungu, kubali mialiko hii, na jitahidi kutembea katika Njia Yake, utapokea “amani ya Mungu, ipitayo uelewa wote,”29 hata miongoni mwa majonzi. Utahisi kipimo kikubwa cha upendo wa Mungu usioweza kupimika ndani ya moyo wako. Mawio ya mwangaza wa selestia yatapenya vivuli vya matatizo yako, na utaanza kuonja utukufu usioelezeka na maajabu ya mbingu yasiyoonekana, makamilifu. Utahisi roho yako ikinyanyuka kutokana na mvuto wa ulimwengu huu.

Na kama Milton Wright, labda utainua sauti yako kwa kufurahi na kupiga kelele, “Juu zaidi, Baba, juu zaidi!”

Na sote tutafute na kupata furaha ya juu zaidi inayotokana na kuweka wakfu maisha yetu kwa Baba yetu wa Mbinguni na Mwanawe mpendwa. Haya ndiyo maombi yangu ya dhati na baraka katika jina la Yesu Kristo, amina.

Muhtasari

  1. John Gillespie Magee Jr., “High Flight,” poetryfoundation.org.

  2. Ona Christopher Klein, “10 Things You May Not Know about the Wright Brothers,” History, Machi 28, 2023, history.com.

  3. Magee, “High Flight.”

  4. Miaka 2400 iliyopita, Aristotle aliona kwamba furaha ni kitu kimoja ambacho wanadamu wote wanatamani zaidi. Katika kitabu chake cha Nicomachean Ethics, alifundisha kwamba mema makubwa katika maisha ni kitu tunachofuatilia kama matokeo yake (kinyume na mambo hayo tunayofuatilia ambayo ni njia ya mwisho mwingine). Furaha, zaidi ya yote, ni kitu kama hicho. “Siku zote tunatamani furaha,” alisema, “na kamwe si kwa ajili ya kitu kingine” (The Nichomachean Ethics of Aristotle, trans. J. E. C. Weldon [1902], 13–14).

  5. See Harry Enten, “American Happiness Hits Record Lows,” CNN, Feb. 2, 2022, cnn.com; Tamara Lush, “Poll: Americans Are the Unhappiest They’ve Been in 50 Years,” Associated Press, June 16, 2020, apnews.com; “The Great Gloom: In 2023, Employees Are Unhappier Than Ever. Kwa nini?” BambooHR, bamboohr.com.

  6. See Wanda Mallette, Patti Ryan, and Bob Morrison, “Lookin’ for Love (in All the Wrong Places)” (1980).

  7. 2 Nefi 2:11.

  8. Ona Yohana 11:35; Musa 7:28–37.

  9. Ona 2 Nefi 2:11.

  10. Ona Yohana 2:27.

  11. Yohana 10:10.

  12. Luke 2:10, New Revised Standard Version.

  13. Ona Mathayo 11:28–30.

  14. 2 Nefi 2:25.

  15. Kama una wasiwasi wowote kuhusu kama Baba yenu wa mbinguni atakukubali au la na kukuruhusu kupokea furaha yake, ninakualika usome kwa maombi mfano wa Kristo wa mwana mpotevu (see Luka 15:11–32). Katika mfano huo, tunajifunza jinsi Baba yetu wa Mbinguni anavyohisi kuhusu watoto Wake na jinsi Yeye anavyosubiri na kusherehekea kurudi kwetu baada ya kupotea kutoka Kwake! Kuanzia wakati “tunakuja kwetu wenyewe” (ona mstari wa 17) na kuanza safari ya kurudi nyumbani, atatuona, kwa kuwa Yeye anasimama akitazama na kusubiri. Na nini Anakisubiria? Kwa ajili yetu! Tunapomkaribia, Yeye atasherehekea kurudi kwetu na kutuita mtoto Wake.

  16. Mafundisho na Maagano 59:18. Ufunuo huu pia unaelezea, “Imempendeza Mungu kwamba ametoa vitu hivi vyote kwa mwanadamu; kwani ni kwa sababu hii vilifanywa” (mstari wa 20).

  17. Kwa wale wanaomkaribia Mungu, Yeye anatoa ahadi hii kuu: “Nitawakaribia ninyi” (Mafundisho na Maagano 88:63.; ona pia Yakobo 4:8).

  18. Ona Marko 5:24–34.

  19. See Bible Dictionary, “Clean and unclean.”

  20. Marko 5:28.

  21. Mathayo 7:7.

  22. Kwa kubebeana mizigo, sisi “tunatimiza sheria ya Kristo” (Wagalatia 6:2; ona pia Mosiah 18:8).

  23. Matendo ya Mitume 8:35.

  24. Ona 1 Wafalme 17:8–16.

  25. Mosia 2:17.

  26. Katika Waraka wake kwa Warumi, Paulo anasema kwamba Mungu “atampa kila mtu kulingana na matendo yake: kwa wale ambao kwa uvumilivu huendelea katika kufanya vizuri kutafuta utukufu na heshima na kutokufa, uzima wa milele: … utukufu na heshima na amani kwa kila mtu atendaye mema” (Warumi 2:6–7, 10).

  27. Luka 6:38. Wokovu wetu na furaha ya milele inaweza kutegemea huruma na wema wetu kwa wengine (ona Mathayo 25:31–46).

  28. Luka 3:10.

  29. Wafilipi 4:7.