Mkutano Mkuu
Maneno ni Muhimu
Mkutano mkuu wa Aprili 2024


Maneno ni Muhimu

Maneno yanaweka mwelekeo. Yanatoa sauti ya mawazo yetu, hisia na uzoefu wetu, kwa uzuri au ubaya.

Akina Kaka, Dada, na marafiki kote ulimwenguni, ni heshima kuhutubia hii hadhara kubwa, wengi ambao ni waumini wa Kanisa letu na wengi ambao ni marafiki na wasikilizaji wapya wa matangazo haya ya mkutano mkuu. Karibuni!

Jumbe zinazotolewa kutoka kwenye mimbari hii zinawasilishwa kwa maneno. Zinatolewa kwa Kiingereza na kutafsiriwa katika karibia lugha 100 tofauti. Daima msingi ni ule ule. Maneno. Na maneno ni muhimu sana. Acheni niseme hilo tena. Maneno ni muhimu!

Ni kiini cha jinsi tunavyounganika, yanawakilisha imani, maadili na mitazamo yetu. Wakati mwingine tunasema maneno; wakati mwingine tunasikiliza. Maneno yanaweka mwelekeo. Yanatoa sauti ya mawazo yetu, hisia na uzoefu wetu, kwa uzuri au ubaya.

Kwa bahati mbaya, maneno yanaweza kuwa ya kipumbavu, makali na yenye kuumiza. Mara yanaposemwa, hatuwezi kuyarudisha nyuma. Yanaweza kuumiza, kuadhibu, kukatakata, na hata kuongoza kwenye matendo angamizi. Yanaweza kutulemea sisi.

Kwa upande mwingine, maneno yanaweza kusherehekea ushindi, kuwa ya matumaini na kutia moyo. Yanaweza kutuchochea kufikiria tena, kuanza upya na kugeuza tena mwelekeo wetu. Maneno yanaweza kufungua akili zetu kwenye kweli.

Hiyo ndiyo kwa nini, kwanza kabisa, maneno ya Bwana ni muhimu.

Katika Kitabu cha Mormoni, nabii Alma na watu wake katika Amerika ya kale walikabiliwa na vita visivyo na mwisho na wale ambao walipuuza neno la Mungu, walioshupaza mioyo yao na kuharibu utamaduni wao. Wangeweza kupigana, lakini Alma alishauri: “Na sasa, kwa vile kuhubiri kwa neno kulikuwa na maelekezo makubwa ya kuongoza watu kufanya yale ambayo ni haki—ndio, ilikuwa na matokeo ya nguvu zaidi kwa akili za watu kuliko upanga, au kitu chochote kingine, ambacho kiliwahi kufanyika kwao—kwa hivyo Alma alifikiri ilikuwa bora kwamba wangejaribu matokeo ya uwezo wa neno la Mungu.”1

“Neno la Mungu” linashinda maonyesho yote mengine. Imekuwa hivyo tangu Uumbaji wa ulimwengu wakati Bwana aliposema: “Iwe nuru, ikawa nuru.”2

Kutoka kwa Mwokozi ukaja uhakikisho katika Agano Jipya: “Mbingu na dunia zitapita; lakini maneno yangu hayatapita.”3

Na hili: “Mtu akinipenda, atalishika neno langu; na Baba yangu atampenda; nasi tutakuja kwake, na kufanya makao kwake.”4

Na kutoka kwa Mariamu, mama wa Yesu ukaja ushuhuda huu wa unyenyekevu: “Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema.”5

Kuamini na kutilia maanani neno la Mungu kutatuleta karibu na Yeye. Rais Russell M. Nelson ameahidi, “Kama utajifunza maneno Yake, uwezo wako wa kuwa kama Yeye utaongezeka.”6

Je, sisi sote hatutaki kuwa, kama wimbo unavyosema, “nipe utukufu—zaidi, ulivyo Bwana”?7

Ninamwona kijana Joseph Smith amepiga magoti yake akisikiliza maneno ya Baba yake wa Mbinguni: “[Joseph,] Huyu ni Mwanangu Mpendwa. Msikilize Yeye!”8

Sisi “tunamsikiliza Yeye” katika maneno ya maandiko, lakini tunayaacha yakae tu kwenye ukurasa, au tunamtambua Yeye anaposema nasi? Je, tunabadilika?

Sisi “tunamsikiliza Yeye” katika ufunuo wa binafsi na minong’ono kutoka kwa Roho Mtakatifu, katika majibu ya sala, na katika zile nyakati ambazo Yesu Kristo tu, kupitia nguvu za Upatanisho Wake, anaweza kuinua mizigo yetu, kutupatia msamaha na amani, kutukumbatia sisi “katika mikono ya upendo wake.”9

Pili, maneno ya manabii ni muhimu.

Manabii wanashuhudia juu ya uungu wa Yesu Kristo. Wanafundisha injili Yake na kuonyesha upendo Wake kwa wote.10 Ninatoa ushahidi wangu kwamba nabii wetu aliye hai, Rais Russell M. Nelson, husikia na kunena neno la Bwana.

Rais Nelson ana njia ya kunena maneno. Amesema, “Kaa katika njia ya agano,”11 “Kusanya Israeli,”12 “Acha Mungu ashinde,”13 “Jenga daraja za uelewa,”14 “Toa Shukrani,”15 “Ongeza imani katika Yesu Kristo,”16 “Chukua jukumu la ushuhuda wako,”17 na “Kuwa mpatanishi.”18

Hivi karibuni ametuhimiza “fikiria selestia.” “Wakati unapokumbana na mkanganyiko,” alisema “fikiria selestia! Wakati unapojaribiwa na jaribu, fikiria selestia! Wakati maisha au wapendwa wako wanapokuangusha, fikiria selestia! Wakati mtu fulani anapofariki katika umri mdogo, fikiria selestia.Wakati shinikizo za maisha zinapokuzonga, fikiria selestia! … Unapofikiria selestia, moyo wako utabadilika polepole, … utayatazama majaribu na upinzani katika njia mpya, … [na] imani yako itaongezeka.”19

Tunapofikiria selestia, tunaona “mambo jinsi yalivyo na jinsi yatakavyokuwa.”20 Katika ulimwengu huu uliolemewa na mkanganyiko na mabishano, sote tunahitaji mtazamo huo.

Mzee George Albert Smith, kitambo kabla hajawa Rais wa Kanisa, alizungumza juu ya kumkubali nabii na kushika maneno yake Alisema: “Wajibu ambao tunafanya wakati tunapoinua mikono yetu … ni mtakatifu sana. … Inamaanisha … kwamba tutasimama nyuma yake; tutasali kwa ajili yake; … na tutajitahidi kutimiza maelekezo yake kama Bwana atakavyoelekeza.”21 Kwa maneno mengine, tutatenda kwa bidii juu ya maneno ya nabii wetu.

Kama mmoja wa manabii 15, waonaji na wafunuzi waliokubaliwa jana na Kanisa letu la ulimwenguni kote, ninataka kushiriki nawe mojawapo ya uzoefu wangu wa kumkubali nabii na kukumbatia maneno yake. Ilikuwa kwangu kama vile kwa nabii Yakobo, ambaye alikumbuka, “Nilikuwa nimesikia sauti ya Bwana ikizungumza nami katika neno lile.”22

Picha
Mzee na Dada Rasband huko Thailand.

Oktoba iliyopita mimi pamoja na mke wangu, Melanie, tulikuwa Bangkok, Thailand, nilipokuwa nikijiandaa kuweka wakfu lile ambalo lingekuwa hekalu la 185 la Kanisa.23 Kwangu mimi, wajibu huu ulikuwa wa kama ndoto na wa kunyenyekeza. Hili lilikuwa hekalu la kwanza katika rasi ya Asia Kusini Mashariki.24 Iilikuwa limesanifiwa kwa ustadi sana—ghorofa sita, umbo la minara tisa, “iliyowekwa vizuri”25 ili kuwa nyumba ya Bwana. Kwa miezi nilikuwa nimetafakari kuwekwa wakfu huku. Kile kilichokaa ndani ya nafsi yangu na akili ilikuwa kwamba nchi na hekalu vimekuwa vimeshikiliwa katika mikono ya manabii na mitume. Rais Thomas S. Monson alikuwa ametangaza hekalu hili26 na Rais Nelson kutangaza uwekwaji wakfu.27

Picha
Hekalu la Bangkok Thailand.

Nilikuwa nimeandaa sala ya kuweka wakfu miezi kadhaa mapema. Maneno haya matakatifu yalikuwa yametafsiriwa katika lugha 12. Tulikuwa tayari. Au nilifikiria hivyo.

Usiku kabla ya uwekaji wakfu, niliamka kutoka kwenye usingizi wangu nikiwa na hisia ya kutotulia na muhimu kuhusu sala ya kuweka wakfu. Nilijaribu kuweka kando minong’ono hii, nikifikiria sala ilikuwa sawa. Lakini Roho hangeniacha nitulie. Nilihisi maneno fulani yalikuwa hayapo, na kwa mpango wa kiungu yalikuja kwangu katika ufunuo, na niliyaingiza maneno haya katika sala karibu na mwisho: “Na tuweze kufikiria selestia, tukiacha Roho Yako ishinde katika maisha yetu, na tujitahidi daima kuwa wapatanishi.”28 Bwana alikuwa ananikumbusha mimi kutia maanani maneno ya nabii wetu aliye hai: “Fikiria selestia,” “acha Roho ishinde,” “tujitahidi kuwa wapatanishi.” Maneno ya nabii ni muhimu kwa Bwana na kwetu.

Tatu, na ya muhimu sana, ni maneno yetu wenyewe. Amini hili, katika ulimwengu wetu uliojaa emoji29, maneno yetu ni muhimu.

Maneno yetu yanaweza kuwa msaada au kuudhi, ya shangwe au ukatili, huruma au kurushwa kando. Kwa hali ya sasa, maneno yanaweza kung’ata na kuzama kwa kina katika nafsi—na kubakia hapo. Maneno yetu katika intaneti, arafa, mitandao ya kijamii, au twita huchukua mkondo wake binafsi. Kwa hiyo kuwa makini kwa kile unachosema na jinsi unavyokisema. Katika familia zetu, hasa waume, wake, na watoto, maneno yetu yanaweza kutuleta pamoja au kuleta uhasama kati yetu.

Acha nipendekeze virai vitatu rahisi ambavyo tunaweza kutumia ili kuondoa magumu na tofauti, kuinua na kuhakikishiana mmoja kwa mwingine:

“Asante.”

“Pole.”

Na “ninakupenda.”

Usihifadhi virai hivi vya unyenyekevu kwa ajili ya tukio maalumu au janga. Vitumie kila mara na kwa uaminifu, kwani vinaonyesha kuwajali wengine. Kama mazungumzo hayana maana; usiendelee kwenye mwenendo huo.

Tunaweza kusema “asante” kwenye lifti, katika maegesho ya magari, sokoni, ofisini, kwenye foleni au kwa majirani zetu au marafiki. Tunaweza kusema “pole” wakati tumefanya kosa, kukosa mkutano, kusahau siku ya kuzaliwa au kumtembelea mtu aliye kwenye uchungu. Tunaweza kusema “Ninakupenda” na maneno hayo hufikisha ujumbe kama “ninakufikiria wewe,” “ninakujali wewe,” “niko hapa kwa ajili yako,” au “una maana sana kwangu.”

Acha nishiriki mfano wa kibinafsi. Waume, tilieni maanani. Kina Dada, hii itawasaidia pia. Kabla ya jukumu langu katika Kanisa, nilisafiri sana kwa ajili ya kampuni yangu. Nilikuwa nimeenda kwa muda mwingi sehemu za mbali ulimwenguni. Mwishoni wa siku yangu, kila mara nilipiga simu nyumbani. Wakati mke wangu, Melanie, alipochukua simu na kutoa taarifa, mazungumzo yetu daima yalituelekeza kuonyesha “Ninakupenda.” Kila siku, maneno hayo yalikuwa kama nanga kwa nafsi yangu na tabia yangu, yalikuwa ulinzi kutokana na njama za uovu. Maneno “Melanie, ninakupenda” yalitoa tumaini la thamani kati yetu.

Rais Thomas S. Monson alikuwa anapenda kusema, “Kuna miguu ya kuimarisha, mikono ya kushika kwa nguvu, mawazo ya kutia moyo, mioyo ya kutia hamasa na roho za kuokoa.”30 Kusema “asante,” “pole,” “ninakupenda” kutafanya hivyo tu.

Akina Kaka na Dada, maneno ni muhimu.

Ninaahidi kwamba kama “tutasherehekea maneno ya Kristo”31 ambayo huongoza kwenye wokovu, maneno ya nabii wetu ambayo yanatuongoza na kutuhimiza, na maneno yetu wenyewe ambayo yanazungumza sisi ni kina nani na kile tunachopenda sana, nguvu za mbinguni zitatiririka juu yetu. “Maneno ya Kristo yatawaelezea vitu vyote mnavyostahili kutenda.”32 Sisi ni watoto Baba wa Mbinguni na Yeye ni Mungu wetu, na Yeye anatutegemea sisi kuzungumza kwa “ndimi za malaika”33 kwa nguvu za Roho Mtakatifu.34

Ninampenda Bwana Yesu Kristo. Yeye ndiye, katika maneno ya nabii Isaya wa Agano la Kale, “Ajabu, Mshauri, Mwenyezi Mungu, Baba asiye na mwisho, Mwana Mfalme wa Amani.”35 Na kama Mtume Yohana alivyosema wazi, Yesu Kristo Mwenyewe ndiye “Neno.”36

Juu ya haya ninashuhudia kama Mtume aliyeitwa kwenye huduma takatifu ya Bwana—kutangaza neno Lake—na kuitwa kusimama kama shahidi Wake maalumu. Katika jina la Bwana Yesu Kristo, Amina.