Mkutano Mkuu
Ombeni, Yeye Yupo
Mkutano mkuu wa Aprili 2024


Ombeni, Yeye Yupo

Ninakualika usali ili ujue Baba wa Mbinguni yupo, usali ili ukue ili kuwa kama Yeye, na usali ili kuonyesha upendo Wake kwa wengine.

Akina kaka na akina dada, ninahisi shangwe ninapoitikia msukumo wa kuongea na watoto!

Wasichana na wavulana, popote mlipo ulimwenguni, ninataka kushiriki kitu fulani pamoja nanyi.

Baba yetu wa Mbinguni anakupenda! Wewe ni mtoto Wake. Yeye anakujua. Yeye anataka kukubariki. Ninaomba kwa moyo wangu wote kwamba uhisi upendo Wake.

Je, unapenda kupokea zawadi? Ninataka kuongea kuhusu zawadi maalumu sana ambayo Baba wa Mbinguni amekupatia ili kukusaidia. Ni zawadi ya sala. Sala ni baraka iliyoje! Ninaweza kuongea na Baba wa Mbinguni wakati wowote, mahali popote.

Picha
Yesu pamoja na watoto.

Wakati Yesu alipokuwa ulimwenguni, Yeye alitufundisha kusali. Yeye alisema, “Ombeni, nanyi mtapewa.”1

Ni zawadi gani unayoweza kuiombea? Ziko nyingi, lakini leo ninataka kushiriki tatu:

  1. Sali ili ujue.

  2. Sali ili ukue.

  3. Sali ili uonyeshe.

Hebu tuzungumze kuhusu kila moja.

Cha kwanza, Sali ili Ujue

Ni nini unachohitaji kujua?

Kuna wimbo kuhusu sala ambao Darasa la Watoto huimba ulimwenguni kote. Unaanza na swali. “Je, Unajua wimbo huo ni upi?” Kama ningekuwa jasiri kweli, ningeuimba kwa ajili yako?

“Baba wa Mbinguni, je, kweli upo? Na je, unasikia na kujibu sala ya kila mtoto?”2

Je, ni kwa jinsi gani tunaweza kujua kwamba Baba wa Mbinguni kweli yupo, hata kama hatuwezi kumwona?

Rais Russell M. Nelson amekualika “kumimina moyo wako kwa Baba yako wa Mbinguni. … Na kisha sikiliza!”3 Sikiliza kile unachohisi katika moyo wako na mawazo ambayo yanakuja akilini mwako.4

Baba wa Mbinguni ana mwili uliotukuka wa nyama na mifupa na ndiye Baba wa roho yako. Kwa sababu Baba wa Mbinguni ana nguvu zote na anajua vitu vyote, Yeye anaweza kuwaona watoto Wake wote5 na anaweza kusikia na kujibu kila sala. Unaweza kuja kujua mwenyewe kwamba Yeye yupo na kwamba Yeye anakupenda.

Unapojua kwamba Baba wa Mbinguni yupo kweli na kwamba Yeye anakupenda, unaweza kuishi kwa ujasiri na matumaini! “Ombeni, yeye yupo; semeni, yeye anasikiliza.”6

Je, umewahi kujihisi mpweke? Siku moja wakati Ashley mjukuu wetu wa kike alipokuwa na umri wa miaka sita, alikuwa mtoto pekee na hakuwa na rafiki wa kucheza naye kwenye uwanja wa shule. Alipokuwa amesimama pale, akihisi kutokuwa muhimu na kutoonekana, wazo mahususi lilikuja akilini mwake: “Subiri! Mimi siko peke yangu! Mimi ninaye Kristo!” Ashley alipiga magoti saa hiyo katikati ya uwanja, akakunja mikono yake, na akamuomba Baba wa Mbinguni. Wakati alipofumbua macho yake, msichana wa umri wake alikuwa amesimama hapo akimuuliza kama yeye alikuwa anataka kucheza. Ashley alijifunza kwamba, “Sisi ni wa muhimu kwa Bwana, na kamwe hatuko peke yetu.”

Wakati mwingine unaweza kutaka kujua kwa nini kitu fulani kigumu kinatendeka katika maisha yako au kwa nini haukupokea baraka ulizoomba. Mara nyingi swali bora la kumuuliza Baba wa Mbinguni si kwa nini bali ni nini.

Je, unakumbuka wakati Nefi na familia yake walipokuwa na njaa wakati wakisafiri nyikani? Wakati Nefi na kaka zake walipoenda kuwinda kwa ajili ya chakula, Nefi akavunja upinde wake. Lakini hakuuliza kwa nini.

Picha
Nefi alimwuliza Lehi wapi pa kupata chakula.

Nefi alitengeneza upinde mpya na kumuuliza baba yake, Lehi, mahali ambapo angekwenda kupata chakula. Lehi alisali, na Bwana aliwaonyesha mahali ambapo Nefi angeweza kwenda.7 Baba wa Mbinguni atakuongoza wewe wakati ukimuuliza nini unaweza kufanya na nini unaweza kujifunza.

Pili, Sali ili Ukue

Baba wa Mbinguni anataka kukusaidia ukue! Yeye anatupenda sana kiasi kwamba Yeye alimtuma Mwanawe, Yesu Kristo, ili kutuonyesha njia ya kuishi.8 Yesu aliteseka, akafa na akafufuka ili kwamba sisi tuweze kusamehewa dhambi zetu na kukua ili kuwa kama Yeye.

Je, unataka kukua katika subira au katika uaminifu? Je, unataka kukua katika ujuzi? Pengine unaona aibu na unataka kukua katika ujasiri. “Ombeni, yeye yupo”!9 Kupitia Roho Wake, moyo wako unaweza kubadilika na unaweza kupokea nguvu.

Rafiki yangu mpya Jonah aliandika: “Mara nyingi ninahisi uoga nikiwa njiani kwenda shule asubuhi. Ninaogopa kuhusu vitu kama kuchelewa, kusahau kitu fulani na kufanya mitihani. Nilipokuwa na umri wa miaka 10, nilianza kusema sala nikiwa njiani kwenda shule pamoja na mama yangu. Ninaomba kwa ajili ya msaada ninaohitaji, na ninasali kwa ajili ya familia yangu pia. Pia nafikiria kwa ajili ya vitu ninavyoshukuru kwa kuwa navyo. [Kusali kwa Baba wa Mbinguni] kumenisaidia. Wakati mwingine sihisi nafuu mara moja ninapotoka nje ya gari, lakini inapofika wakati nikiwa darasani ninahisi amani.”10

Imani ya Jonah inakua pale anaposali kila siku na kisha kusonga mbele.

Tatu, Sali ili Uonyeshe

Unaweza kusali kwa ajili ya msaada wa kuwaonyesha wengine upendo wa Baba wa Mbinguni.11 Kupitia Roho Wake, Baba wa Mbinguni atakusaidia kutambua mtu ambaye ana huzuni ili wewe uweze kumfariji. Yeye anaweza kukusaidia kuonyesha upendo Wake kwa kumsamehe mtu. Yeye anaweza kukupatia ujasiri wa kumtumikia mtu na kushiriki naye kwamba yeye ni mtoto wa Mungu. Unaweza kuwasaidia wengine kuja kumjua na kumpenda Yesu Kristo na Baba wa Mbinguni kama unavyofanya.12

Kwa maisha yangu yote nilisali kwamba baba yangu angekuja kuwa muumini wa Kanisa la Yesu Kristo la Watakatifu wa Siku za Mwisho. Hata kama msichana mdogo, nilijua ni baraka ngapi yeye angeweza kuzipokea. Familia yetu ingeweza kupokea baraka za kuunganishwa milele. Familia yangu, marafiki zangu na mimi kila mara tulimuombea, lakini hakujiunga na Kanisa. Baba wa Mbinguni hamlazimishi mtu yeyote kufanya uchaguzi.13 Yeye anaweza kututumia majibu ya sala zetu katika njia nyingine.

Picha
Rais Porter pamoja na wazazi na ndugu zake.

Wakati nilipokuwa mkubwa vya kutosha, nilipokea baraka yangu ya kipatriaki. Katika baraka, patriaki aliniambia kuwa kitu kizuri ambacho ningeweza kufanya ili kuisaidia familia yangu kuwa pamoja mbinguni ilikuwa ni kuwa mfano mzuri wa injili ya Yesu Kristo. Hicho ndicho nilichoweza kufanya!

Baba yangu aliishi kufikia umri wa miaka 86. Siku tano baada ya yeye kufariki, nilipokea hisia takatifu ya shangwe. Baba wa Mbinguni alinifanya nijue kupitia Roho Wake kwamba baba yangu alikuwa anataka kupokea baraka za injili ya Yesu Kristo! Kamwe sitasahau siku hiyo, nilipiga magoti kwenye madhabahu hekaluni pamoja na dada yangu na kaka zangu kuunganishwa pamoja na wazazi wangu. Nilianza kusali kwa ajili ya baraka hii wakati nikiwa katika Darasa la Watoto, na niliipokea wakati nilipokuwa bibi.

Labda wewe unaomba baraka kwa ajili ya familia yako na wengine unao wapenda. Usikate Tamaa! Baba wa Mbinguni atakuonyesha nini unachoweza kufanya.

Shiriki na Baba wa Mbinguni kile kilicho ndani ya moyo wako.14 Na kwa dhati unapoomba msaada Wake, utapokea Roho Wake ili akuongoze.15 Kusali kila siku kutakujaza upendo kwa ajili ya Baba wa Mbinguni na Yesu Kristo. Hii itakusaidia wewe kutaka kuwafuata Wao maishani yako yote!

Fikiria kile ambacho kingetokea kama watoto wote katika Afrika, Amerika Kusini, Asia, Ulaya, Amerika Kaskazini na Australia wangesali kila siku Ulimwengu wote ungebarikiwa na upendo zaidi wa Mungu!

Picha
Watoto ulimwenguni kote wakisali.

Ninakualika usali ili ujue Baba wa Mbinguni yupo, usali ili ukue ili uwe kama Yeye, na usali ili kuonyesha upendo Wake kwa wengine. Ninajua kwamba Yeye anaishi na anakupenda wewe. “Sali, Yeye Yupo.” Katika jina takatifu la Yesu Kristo, amina.